Thursday, May 12, 2016

NOAH KUTOSAJILIWA KUBEBA ABIRIA BARABARA KUU

Na John Gagarini, Kibaha
MAGARI ya kusafirisha abiria aina ya Noah Hiace pamoja na pikipiki yamesababisha vifo vya watu 102 huku 246 wakijeruhiwa katika kipindi cha kuanzia 2015 hadi Machi 2016.
Kutokana na kukithiri kwa ajali za vyombo hivyo Mamlaka ya Udhibiti  wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA) mkoa wa Pwani imesitisha utoaji wa lesseni mpya kwa magari aina ya Noah maarufu kwa jina la ‘Mchomoko’, na Hiace  kwenye barabara zote kuu ikiwamo barabara ya Morogoro.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha ofisa mfawidhi wa SUMATRA mkoa wa Pwani Nashon Iroga alisema kuwa kwa mujibu wa waraka walioupata kutoka makao makuu magari  hayo yote madogo  ya abiria yanayokwenda masafa  marefu kupitia barabara kuu hayatapewa leseni ya kubeba abiria.
“Barabara kuu kuna vyombo vikubwa vya  usafiri hivyo hayataruhusiwa kupata leseni mpya badala yake yaliyokwisha pata leseni yataendelea hadi hapo muongozo mwingine utakapo toka tena,” alisema Iroga.
Alisema kuwa agizo hilo limetolewa baada ya ongezeko kubwa la magari madogo ya kubeba abiria hasa magari  aina ya noah, kufanya safari ndefu huku baadhi  yakiwa yamebeba abiria na mizigo  bila kuangalia usalama wa abiria  na matokeo yake ni kusababisha ajali za mara kwa mara na msongamano katika barabara kuu.
“Ukiangalia kwa hali ya kawaida magari aina ya Noah yanabeba abiria wachache lakini ili wapate faida inabidi watoze viwango vikubwa vya nauli, kubeba abiria kuliko uwezo wake na kwenda mwendo kasi  ili wafanye safari nyingi na kupata faida, matokeo yake wanahatarisha usalama wa maisha ya abiria,” alisema Iroga.
Aidha alisema kuwa  magari hayo madogo yakiwamo Noah na Hiace yanayobeba abiria yatapewa lesseni mpya za kufanya biashara kutumia ruti za barabara  za ndani na sio barabara kuu.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment