Thursday, June 25, 2026

MAWAKALA WAITWA KUCHANGAMKIA VIPAJI TUMBI KIBAHA

MAWAKALA wa michezo ikiwemo soka wametakiwa kujitokeza kushuhudia vipaji vya wacehzaji chini ya miaka 17 na 22 kwenye mashindano ya Compassion ili kuwa na timu bora zitakazozalisha wachezaji wakulitumikia Taifa ambapo moja zao la wachezaji hao ni Dickson Job anayechezea timu ya Yanga.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Lucas Kiluwasha ambaye ni mwenyekiti wa Mashindano ya Compassion Kanda ya Mashariki kwenye Viwanja vya Shirika la Elimu Kibaha Tumbi.

Mashindano hayo ambayo ni ya nne kufanyika yameweza kuwatoa wachezaji wengi akiwemo Dickson Job wa Yanga, Paschal Msindo wa timu ya Azam na Haji Abdala kipa wa timu ya Serengeti Boys chini ya miaka 17 iliyoshika nafasi ya pili kwenye michuano ya Afcon ya vijana iliyofanyika Morocco hivi karibuni.

Mbali ya kuzalisha wachezaji hao ambao wanatambulika pia imezalisha wachezaji wengine ambao wako timu za Yanga B, Azam na Fountain Gate pamoja na msanii wa muziki wa kisasa Dogo Janja na wasanii mbalimbali hapa nchini.

Kiluwasha amesema kuwa mashindano hayo ambayo hufanyika kila mwaka yanashirikisha jumla ya mikoa mitatu ya Pwani, Dar es Salaam na Morogoro ambapo kuna wachezaji zaidi ya 430 kauli mbiu ya mwaka huu inasema “Kipaji Changu Mtaji Wangu”.

“Michezo inayoshindaniwa ni pamoja na soka, mpira wa pete, riadha na michezo ya ndani ikiwa ni pamoja na kupiga vyombo vya muziki, ubunifu wa mavi na sanaa mbalimbali lengo ni kuinua na kuibua vipaji kwa vijana,”alisema Kiluwasha.

Alisema kuwa kwa sasa mara wanapopatikana vijana wa michezo husika huwapeleka ili wakaendeleze vipaji vyao ambapo wa soka huwapeleka kwenye timu zenye Academy ili waweze kukuza vipaji vyao na kujipatia ajira kupitia michezo.

“Changamoto kubwa ni ushiriki mdogo wa wadau kujitokeza kuhudhuria mashindano yao pia baadhi ya wachezaji kwenda kushiriki michezo ya Umisseta na Umitashumta kwani nao hufanya kipindi cha likizo hivyo kuwa na mwingiliano,”alisema Kiluwasha.

Aidha alisem akuwa malengo yao ya baadaye ni kuanzisha timu ya mipra wa miguu ili ishiriki ligi mbalimbali na hatimaye kufika ligi kuu pia wanazikaribisha timu mbalimbali kama zinahitaji wachezaji kuona nao ili kukubalina na kuwachukua ili wakaendeleze vipaji vyao.

Wachezaji hao wanatoka kwenye vituo vya huduma ya mtoto na kijana kwenye makanisa ya Kiinjili na Kipentekoste kwenye mikoa hiyo na wachezaji watakaofanya vizuri watachaguliwa kwenda kushiriki mashindano hayo kitaifa.

Tuesday, June 23, 2026

WAZO BORA LA KIJANA KUNYAKUA MILIONI 50

KIJANA mwenye wazo bora kati ya vijana 100 watakaowania kinyanganyiro cha Vijana Uchumi Challenge anatarajiwa kujinyakulia kitita cha shilingi milioni 50.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Dk Kedmon Mapana wakati akizungumza na vijana hao 100 watakaokuwa kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere iliyopo Kibaha Mkoani Pwani.

Mapana amesema kuwa wapili akijinyakulia shilingi milioni 20 na watatu milioni 10 ambapo vijana wanaoshiriki ni wenye umri chini ya miaka 35 kutoka nchi nzima.

"Wizara ilitoa shindano la vijana kutoa wazo la kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia mawazo ya vijana kukuza ubunifu na Ujasiriamali na kuwapa vijana fursa ya kuonyesha mawazo yao ya kibiashara na miradi ya kibunifu inayoweza kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi,"amesema Mapana.

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya Vijana Uchumi Challenge Joseph Malecela amesema kuwa jumla ya mawazo zaidi ya 7,000 ya vijana kote nchini yaliwasilishwa na kuchujwa na kubaki 100 ambayo yatashindanishwa kupata mshindi.

Malecela amesema kuwa washiriki hao 100 ambao wameingia kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere watachujwa na majaji wabobezi wa masuala ya uchumi na fedha na kubaki 30 na baadaye 10.

Kilele kinatarajiwa kufanyika Jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi atakuwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan.

VIJANA 100 KUWANIA MILIONI 50 VIJANA UCHUMI CHALLANGE

NAIBU Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Dk Kedmon Mapana amesema vijana kuwa na ujuzi na mtaji ni suluhisho la kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050.

Ameyasema hayo Mjini Kibaha kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere wakati akifungua Jukwaa la Vijana Uchumi Challenge.

Mapana amesema kuwa Waziri wa Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Joel Nanauka alizindua shindano la vijana kwa ajili ya kuwawezesha vijana nchini Tanzania kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na ubunifu. 

"Lengo kuu la mpango huu ni kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia mawazo ya vijana kukuza ubunifu na Ujasiriamali na kuwapa vijana fursa ya kuonyesha mawazo yao ya kibiashara na miradi ya kibunifu inayoweza kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi,"amesema Mapana.

Amesema kuwa pia ni kuongeza ajira kwa kusaidia miradi ya vijana kuanzishwa au kukua ambapo shindano linakusudia kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa kuwezesha vijana kujiajiri na kuajiri wengine.

"Kwa wale ambao hawatafanikiwa kushinda mawazo yao yatachukuliwa na kufanyiwa kazi kwa kupewa mafunzo kutokana na mawazo yao ya bunifu zao kupitia sekta mbalimbali zikiwemo za kilimo uvuvi mifugo tehama na ujasiamali,"amesema Mapana.

Aidha amesema vijana wasilalamike bali watoe mawazo na suluhisho nini kifanyike hata ikitokea changamoto kama za kupanda bei ya mafuta ili uchumi wa nchi uwe stahimilivu

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya Vijana Uchumi Challenge Joseph Malecela amesema kuwa jumla ya mawazo zaidi ya 7,000 ya vijana kote nchini yaliwasilishwa na kuchujwa na kubaki 100 ambayo yatashindanishwa kupata mshindi.

Malecela amesema kuwa washiriki hao 100 ambao wameingia kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere watachujwa na majaji wabobezi wa masuala ya uchumi na fedha na kubaki 30 na baadaye 10.

Amesema kuwa washindi 10 watakwenda kwenye kilele kitakachofanyika Jijini Dar es Salam Julai 6 ambapo mshindi atapata kiasi cha shilingi milioni 50 huku wapili akijinyakulia shilingi milioni 20 na watatu milioni 10 ambapo vijana wanaoshiriki ni wenye umri chini ya miaka 35.

Kilele kinatarajiwa kufanyika Jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi atakuwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan.

PWANI YAKUSANYA BILIONI 266

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani imefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 266 katika kipindi cha miaka 10 iliyopita na kuvuka malengo yaliyowekwa ya kukusanya shilingi bilioni 235 katika kipindi hicho.

 

Akizungumza kwenye Kongamano la Mamlaka hiyo ya kutimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake Meneja wa TRA Mkoa wa Pwani Peter Jackson alisema kuwa mafanikio hayo ni ongezeko la asilimia 113 ya makusanyo kwa kipindi hicho.

 

Jackson alisema kuwa mafanikio hayo yametokana na ushirikiano ulioonyeshwa na wafanyabiashara na wadau wote wa kodi ambapo katika kipindi hicho malaengo ya makusanyo yalikuwa ni bilioni 23 lakini zilikusanywa kiasi cha shilingi bilioni 27.

 

“Kwa wastani makusanyo kwa kipindi cha miaka 10 ni ongezeko la asilimia 10 ambapo yamekuwa yakiongezeka hadi kufikia kiasi hicho na kuonyesha jinsi gani mamlaka hiyo inavyopiga hatua katika kuleta maendeleo ya nchi,”alisema Jackson.

 

Alisema kuwa makusanyo yana faida kubwa kwani yanatumika kwa ajili ya kufanya shughuli za kimaendeleo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ikiwemo ya barabara ujenzi wa reli ya kisasa SGR huduma za afya, huduma za elimu na masuala mbalimbali.

 

Aidha alisema kuwa ukusanyaji wa mapato makubwa ndiyo njia ya kukuza uchumi wa nchi ambapo walipa kodi wanapaswa kulipa kwa hiyari na kwa wakati ili kuondoa changamoto za kupewa adhabu ambayo inawarudisha nyuma.

 

“Kwa sasa tumeweka mifumo madhubuti ya ukusanyaji na namna ya kuwafikia kwa urahisi walipa kodi na kuwaondolea usumbufu wa kufika ofisini badala yake wanauwezo wa kulipa au kufanya shughuli zote wakiwa maeneo yao jambo ambalo limerahisisha utendaji kazi,”alisema Jackson.

 

Akizungumzia kuhusu changamoto alisema kuwa ukuaji wa uchumi usio rasmi umekuwa ni tatizo kwani unakuwa nje ya mfumo rasmi hivyo kusababisha kukosekana kwa mapato kutokana na kukwepa au kupunguza kodi kuongezeka kwa biashara mtandaoni biashara haramu na za magendo ambazo huathiri ushindani wa kibiashara..

 

Kwa upande wake mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT) Mkoa wa Pwani Abdala Ndauka alisema kuwa baadhi ya wafanyabiashara hawana uelewa juu ya masuala ya ulipaji kodi hivyo kuna haja ya kutolewa elimu ya kutosha.

 

Ndauka alisema kuwa ulipaji kodi unapaswa kuwa rafiki na si kama adhabu bali uwe rafiki hata hivyo malalamiko kwa sasa yamepungua kwani kwa sasa kumekuwa na majadiliano juu ya changamoto zinazowakumba walipa kodi na watengeneze walipa kodi wapya.

 

Mwenyekiti wa Chemba ya wafanyabiashara Mkoa wa Pwani Said Mfinanga alisema kuwa matumizi ya teknolojia yamesaidia kuwapunguzia muda walipa kodi kwenda ofisini ili kufanya kufanya taratibu mbalimbali juu ya masuala ya ya biashara zao.

 

Mfinanga alisema kuwa mfumo wa teknolojia pia utumike kutoa elimu juu ya masuala ya ulipaji kodi na taratibu zote zihusikanazo na masula ya kodi ili kujenga uelewa wa pamoja kwa walipa kodi na mamlaka hiyo ambayo inajuhusisha na ukusanyaji wa mapato ya serikali.   

 

Naye mwenyekiti wa Shirikisho la Umoja wa Machinga (SHIUMA) Mkoa wa Pwani Philemon Maliga alisema kuwa ili kuboresha ukusanyaji wa mapato Mamlaka inapaswa kuwa na mahusiano bora na mazuri na walipakodi kwnai kundi lao ni kubwa na lina uwezo wa kuchangia pato la serikali.

 

Maliga alisema kuwa TRA iatoe limu kuanzia mashuleni na sehemu mbalimbali ili kuwajengea walipa kodi utamaduni wa kulipa mapato ili kuonyesha uzalendo wa nchi yao kwani kodi ndiyo msingi mkubwa wa maendeleo.

 

Monday, June 15, 2026

TAARIFA KWA UMMA


Ofisi ya Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, inapinga na kukanusha vikali taarifa ya uongo na upotoshaji inayosambaa mitandaoni, ikidai kuwa Dkt. Kikwete anahusishwa na mradi unaodaiwa kuwa wa uwekezaji unaowaahidi Watanzania kipato cha uhakika kupitia jukwaa la kifedha linalotumia teknolojia ya akili mnemba

Taarifa hiyo inadai kuwa maelfu ya Watanzania tayari wamenufaika na mradi huo baada ya kuwekeza kiasi cha shilingi 653,000, huku wakiahidiwa kupata zaidi ya shilingi 9,200,000 kwa mwezi. Madai hayo si ya kweli hata kidogo.

Ofisi ya Rais Mstaafu inapenda kuweka wazi kwamba Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete hajawahi kushiriki, kuidhinisha, kutangaza, kuunga mkono, wala kuhusika kwa namna yoyote ile na mpango huo wa kifedha. 

Ofisi yake haijawahi kuruhusu matumizi ya jina, picha, au heshima yake kuhusishwa na mradi huo unaodaiwa, na haitajihusisha na shughuli za aina hiyo.

Wananchi wanashauriwa kupuuza taarifa hiyo ya uongo na kuwa makini dhidi ya miradi ya kitapeli na vitendo haramu vya aina hiyo. 

Mtu yeyote atakayekutana na taarifa kama hizo za upotoshaji anapaswa kuzichukulia kama habari za uongo, kuepuka kuzisambaza, kujisajili, au kutuma fedha kwa mtu au jukwaa lolote linalohusishwa nazo.

Sunday, June 14, 2026

PWANI YAENDELEA KUHAMASISHA UCHANGIAJI DAMU KUOKOA MAISHA YA WATU

MKOA wa Pwani umekusanya jumla ya chupa za damu 1,129 kwa ajili ya Hospitali na Vituo vya Afya.

Hayo yamesemwa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani Kusirye Ukio wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mchangiaji Damu wa Dunia kimkoa ambapo maadhimisho hayo yamefanyika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani Tumbi.

Kwa upande wake Msimamizi wa Huduma kwa Mteja na Wachangiaji Damu Salama Makao Makuu Kaito Tamba amesema kuwa kwa sasa mpango ni kukusanya chupa 600,000 kwa mwaka 

Akisoma risala ya siku hiyo Mkuu wa Idara ya Maabara Hospitali ya Tumbi Simon Lupatu amesema kuwa kauli mbiu ya mwaka huu inasema "Changia Damu Okoa Maisha" ambapo wanahitaji mashine kwa ajili ya uzalishaji mazao ya damu.

Naye Mkuu wa Idara ya Kinamama na Uzazi wa Hospitali ya Tumbi Dk Alfonce Moyo amesema kuwa takwimu zinaonyesha vifo vilivyotokea kwa mwezi Januari hadi Juni mwaka huu asilimia 80 vilitokana na kupoteza damu nyingi.

Saturday, June 13, 2026

*SERIKALI YADHAMIRIA KUWAENDELEZA WACHIMBAJI WADOGO NCHINI*

▪️Taarifa ya mapendekezo ya kuwaendeleza Wachimbaji wadogo yawasilishwa

▪️Prof Mkumbo aeleza umuhimu wa sekta ya madini kufikia Dira 2050

Lengo ni Kuongeza Ajira, Kupunguza Umaskini na Kukuza Uchumi

▪️Mfuko wa Dhamana  kutatua changamoto ya mitaji kwa wachimbaji

▪️Serikali yaanzisha mfuko wa Madini kwa ajili ya Utafiti wa Madini

📍 Dar Es Salaam

Serikali imesisitiza kufanyia kazi kwa haraka Mapendekezo yaliyotolewa na Timu ya Wataalamu iliyoundwa Kuishauri Wizara ya Madini kuhusu namna ya Kuwaendeleza Wachimbaji Wadogo Kiuchumi na kueleza kuwa, utatuzi wa changamoto za Mitaji, Teknolojia na upatikanaji wa taarifa sahihi za Kijiolojia kwa Wachimbaji Wadogo wa Madini ni hatua muhimu ya kuongeza ajira kwa watanzania, kupunguza umaskini na kukuza uchumi wa Taifa kuelekea Dira 2050.

Hayo yamebainishwa Juni 13, 2026 jijini Dar Es Salaam  na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, wakati wa hafla ya Kupokea Mapendekezo ya Kuwaendeleza Wachimbaji Wadogo Nchini na kusisitiza kwamba, maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha mipango ya maendeleo inajibu changamoto tatu kuu za taifa ambazo ni kuongeza mitaji kwa wananchi, kuzalisha ajira na kupunguza umaskini.

Amesema kuwawezesha wachimbaji wadogo kupata mitaji na teknolojia, kunafungua fursa za kuongeza uzalishaji, ajira na kipato cha wananchi na kuongeza kuwa hiyo ndiyo njia mojawapo ya kupambana na umaskini.

‘’Kazi kubwa ya Waziri ni kutoa mwelekeo wa kisera wa taasisi au wizara anayoiongoza. Kwa muda niliokaa kwenye Wizara yangu, Mhe. Mavunde amekua akijua kipaumbele anachokitaka na jinsi ya kukipata,’’amesisitiza Prof. Mkumbo.

Ameongeza kwamba, hali ya umaskini nchini  bado ipo kwa kiwango cha juu na kutolea mfano wa Mkoa wa Geita ambao unaoongoza kwa shughuli za uchimbaji madini ya dhahabu nchini ambapo  hali ya umaskini inafikia asilimia 38 na kusisitiza kwamba, wachimbaji wadogo wanapowezeshwa wanasaida kutatua changamoto kama hizo na kuongeza kuwa, Sekta ya Madini imewekwa kama moja ya sekta muhimu za kimageuzi  inayotarajiwa kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi na ajira ambapo awali haikuwa ikibeba watu wengi.

Naye, Waziri wa Madini Anthony Mavunde akizungumza katika halfa hiyo, amesema Serikali iliamua kuunda kamati hiyo kutokana na mchango mkubwa unaotolewa na wachimbaji wadogo katika Sekta ya Madini, licha ya kukabiliwa na changamoto za mitaji, teknolojia na upatikanaji wa huduma za kifedha , hivi sasa wanachangia asilimia 40 ya makusnyo ya maduhuli ya Serikali.

Ameongeza kwamba, kuwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika Sekta ya Madini ndani ya miaka ya hivi karibuni yanaonyesha umuhimu wa kuwawezesha zaidi wachimbaji wadogo ili waongeze mchango wao katika uchumi wa taifa.

Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, Mwaka wa Fedha  2015/16 Sekta ya Madini katika mwaka mmoja iliingiza shilingi bilioni 161 pekee katika Mfuko Mkuu wa Serikali. 

Hata hivyo, kufuatia mageuzi mbalimbali yaliyofanyika ikiwemo mabadiliko ya sheria, kuanzishwa kwa masoko ya madini na udhibiti wa biashara haramu ya madini, makusanyo yameongezeka kwa kiwango kikubwa kufikia Shilingi trilioni 1.107 mwaka 204/25 na mpaka kufikia  tarehe 13, Juni, tayari Serikali imekusanya shilingi trilioni 1.3.

Amesisitiza kuwa jukumu la Serikali yoyote duniani ni kuwawezesha wananchi wake kufanya shughuli za uzalishaji kwa tija zaidi sababu ambayo ilipelekea  Serikali kuweka mkakati maalum wa kuwawezesha wachimbaji wadogo ili waweze kukua na kuwa wachimbaji wa kati na baadaye wakubwa.

Kuhusu changamoto ya mitaji, Waziri Mavunde  amesema Serikali imeanza utekelezaji wa Kampuni ya dhamana ya mikopo (Credit Guarantee Corporation) itakayosaidia  wachimbaji kupata mikopo kutoka taasisi za fedha mbalimbali.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo  Dkt. Victor Tesha  amesema suluhu ya changamoto hizo ni kujenga mfumo jumuishi wa kuwawezesha wachimbaji wadogo kupitia upatikanaji wa mitaji, teknolojia za kisasa, taarifa za kijiolojia na uratibu wa taasisi zinazohusika na sekta hiyo huku akipendekeza kuanzishwa kwa Mfuko wa Madini Tanzania utakaowezesha miradi yenye sifa kupata fedha za kuendeleza uzalishaji, kununua mitambo na kuboresha shughuli za uchimbaji, na kuongeza kwamba, mfuko huo utasaidia kugharamia tafiti na taarifa za kijiolojia kwa wachimbaji.

Ameongeza kuwa, baada ya mfuko huo kukua na kuimarika, hatua itakayofuata itakuwa ni kuanzisha Benki ya Wachimbaji itakayotoa huduma maalumu za kifedha kwa sekta ya madini kwa masharti yanayoendana na mazingira ya wachimbaji.

‘’Kamati pia imependekeza mikopo ielekezwe zaidi katika ununuzi wa mitambo na teknolojia badala ya fedha taslimu pekee, ili kuongeza tija, uzalishaji na usalama katika shughuli za uchimbaji,’’ amesema Tesha.


 Naye, rais wa Shirikisho la Vyama Vya Wachimbaji Wadogo John Bina, ameipongeza Serikali kwa ripoti hiyo na kueleza imetokana  na Serikali kusikiliza na kuyafanyia kazi maoni na changamoto za wachimbaji wadogo, pamoja na kuipongeza kwa kutenga asilimia 10 ya mapato yanayotokana na shughuli za madini kwa ajili ya utafiti.

Wednesday, June 10, 2026

HALMASHAURI YA MANISPAA YA KIBAHA YATOA MIKOPO YA SHILINGI MILIONI 991.5 KWA VIKUNDI

HALMASHAURI ya Manispaa ya Kibaha Mkoani Pwani imetoa mikopo ya jumla ya shilingi milioni 991.5 kwa vikundi 51 vya ujasiriamali.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dk Rogers Shemwelekwa wakati wa hafla ya utoaji mikopo ya robo ya tatu.

Shemwelekwa amesema kuwa fedha hizo kiasi cha shilingi milioni 359 ni kwa vikundi 17 vya wanawake shilingi milioni 557 kwa vikundi 25 vya Vijana.

"Kiasi cha shilingi milioni 75.5 kilitolewa kwa watu wenye ulemavu 17 ambapo fedha hizo zimetokana na asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha,"amesema Shemwelekwa.

Amesema kuwa miradi iliyokopeshwa kwa vikundi hivyo ni pamoja na mradi wa usafirishaji ambapo pikipiki 25 zimetolewa na TOYO moja, Bajaji nne, pia miradi ya ufugaji kuku, uchomeleaji ,ushonaji na hardware.

"Viwanda vidogo vya utengenezaji batiki, sabuni, kilimo cha umwagiliaji, kiwanda na stationery miradi hiyo yote inatokana na vikundi hivyo ambavyo ni vya wajasiriamali,"amesema Shemwelekwa.

Aidha amesema kuwa kwa mwaka wa fedha wa 2024/25 ambapo mikopo ilianza kutolewa mwezi Disemba 2024 kwa kanuni mpya hali ya urejeshaji kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu imefikia asilimia 52. 

"Pia mikopo ya mwaka huu wa 2025/26 ambayo imetolewa kuanzia mwezi Novemba 2025 marejesho yamefikia asilimia 26 ambapo inaashiria marejesho yapo vizuri,"amesema Shemwelekwa.

Kwa upande wake Mgeni rasmi Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka amesema kuwa kutolewa mikopo hiyo ni jitihada kubwa zinazofanywa katika ukusanyaji wa mapato.

Koka amesema kuwa Halmashauri imeendelea kuimarika kwenye upande wa mapato hali ambayo inaongeza utoaji wa mikopo kutokana na asilimia 10 ya mapato.

Naye Mwenyekiti wa Kikundi cha Lulu ya Wajane Kanyenda Mweri alisema kuwa fedha hizo zitawasaidia wao kama wajane kukuza mtaji wao wa ufugaji wa kuku.

Mweri alisema wanaishukuru Halmashauri na Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kurejesha mikopo hiyo ya asilimia 10 baada ya kusitishwa  kwa muda na kuwekwa utaratibu mpya.

Tuesday, June 9, 2026

LULU YA WAJANE KUANZISHA MRADI WA MINOFU YA KUKU

KIKUNDI cha Lulu ya Wajane kilichopo Kongowe Wilayani Kibaha Mkoani Pwani kinatarajia kuanzisha mradi wa uuzaji wa minofu ya kuku.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa kikundi hicho Kanyenda Mweri wakati akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea kikundi hicho ambacho kinajihusisha na ufugaji wa kuku.

Mweri amesema kuwa kikundi chao kinaundwa na wanachama watano kiliwezeshwa na Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha mkopo wa asilimia 10 kiasi cha shilingi milioni 46 ambapo tayari wameshazirejesha.

"Tumeomba mkopo mwingine wa fedha nyingi kidogo ambapo tutanunua mashine ya kuchakata minofu, mashine ya kunyonyolea kuku, mashine ya kutotolesha na kuuza vifaranga, mashine ya kusaga vyakula vya kuku na kufufua mashine ya kusaga unga,"amesema Mweri.

Amesema kuwa tayari wameshafanya utafiti juu ya soko la minofu ambapo mbali ya minofu watauza kuku na viungo vyake ikiwemo miguu, vichwa na vyote vitokanavyo na kuku.

"Uwezo wa kurejesha mkopo tutakaokopeshwa tunao kwani mkopo uliopita tulikopeshwa milioni 46 tukazirejesha mapema kabla ya muda kwani tulipewa miaka mitatu kurejesha lakini tulirejesha kwa miezi 11 tu na kupewa cheti cha wajasiriamali bora,"amesema Mweri.

Aidha amesema kuwa kutokana na mradi wa ufugaji kuku unaoendelea kila mwezi wanajilipa kiasi cha shilingi  100,000 pia wameweza kuwaajiri mabinti wa wawili ambao ni wahitimu wa vyuo wakiwa na diploma ya mifugo ambao ndiyo wanafanya shughuli za kitaalamu na kijana mmoja wa kiume.

"Tunamshukuru Mungu kwani ameweza kutuunganisha na kutupa mshikamano ambao ndiyo siri ya mafanikio yetu na ushirikiano tunaoupata kutoka kwa wataalamu wa Halmashauri na Mkurugenzi,"amesema Mweri..

Amesema kuwa walianzisha kikundi hicho kwa malengo ya kusaidiana kutatua changamoto na kutafuta fursa mbalimbali za ujasiriamali na kûwa na miradi ya kiuchumi endelevu kwani wanawake wanapofiwa na waume zao ndugu huwanyanyasa naa kuwanyanganya mali. 

"Matarajio yetu ni kuwa kikundi imara na hodari ambapo kwa sasa tayari wameanzisha kikundi cha vijana wanawake wanaojulikana kama Lulu Nazi wanaozalisha bidhaa zitokanazo na nazi,"amesema Mweri.

Ameongeza kuwa wanaiomba Halmashauri wawapatie mikopo kutokana na maombi kwani malengo wanakuwa wameshayaweka hivyo kuwakopesha chini ya walichoomba husababisha kufanya malengo yasifikiwe ya kile walichokiombea.

"Pia watoe mikopo kwa muda uliopangwa ambapo wao wanasubiri awamu ya pili tangu Desemba mwaka jana hadi leo bado hawajapata mkopo waliouomba ambapo gharama zinaongezeka za mahitaji mfano chakula cha kuku bei imeongezeka na mkopo hesabu zilizopigwa tayari zinakuwa chini,"amesema Mweri.

Amewataka wanawake wajane kutokata tamaa katika kupambania maisha yafamilia zao kwani wao ndiyo walezi wa familia na kulinda maadili ya watoto wao na kikundi hicho kilianzishwa mwaka 2022 na kimesajiliwa.

mwisho.







 



 

POLISI PWANI KUFANYA UCHUNGUZI KISAYANSI KUCHUNGUZA MADAI MZAZI KUBADILISHIWA MTOTO

JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani linafanya uchunguzi wa kitaalamu na kisayansi ili kubaini ukweli juu ya lalamiko la mwanamke aitwaye Filomena Mataris (36) Mkazi wa Gongo la Mboto Dar es Salaam kudai kubadilishiwa mtoto baada ya kujifungua katika Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo.

Uchunguzi huo unafanyika baada ya mlalamikaji kudai kuambiwa mtoto wake aliyejifungua amefariki na kuzikwa pasipo yeye na mume wake kushiriki mazishi ya mtoto wake ambapo alizikwa na ndugu zake.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani Salim Morcase alisema kuwa Juni 5 mwaka huu Filomena Mataris akiwa na mume wake Caros Kapata walifika kituo cha Polisi Bagamoyo wakilalamika kubadilishiwa mtoto kwenye Hospitali ya Bagamoyo. 

Morcase alisema kuwa walipofika polisi walieleza kuwa Aprili 14 mwaka huu Filomena Mataris alihamia Kerege Wilayani Bagamoyo kwa mtoto wa dada yake aitwaye Avetha Mabadiliko kwa ajili ya uangalizi wa karibu akitokea Gongo la Mboto Dar es Salaam.

"Mnamo Mei 17 mwaka huu majira ya saa 3:000 asubuhi Mataris alipata uchungu wa kujifungua hivyo aliongozana na ndugu yake huyo Mabadiliko kwenda Hospitali ya Kerege kwa ajili ya kujifungua,"alisema Morcase.

Alisema kuwa baada ya kufika hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo daktari alibaini Mataris ana dalili ya uzazi pingamizi hivyo alielekeza apelekwe Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji.

"Iipofika Mei 18 mwaka huu majira ya saa 8:00 usiku Mataris alihamishiwa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo ambapo saa 8:30 usiku alijifungua mtoto wa kiume kwa njia ya upasuaji na alieleza kuwa alimuona mtoto wake na kumbeba akiwa mzima wa afya,"alisema Morcase.

Aidha alisema Mataris alisema kuwa baada ya kupewa huduma na kwenda wodini alioneshwa picha za mtoto kwenye simu ya daktari na kuambiwa ndiye mtoto wake na ameshafariki. 

"Mtoto aliyeonyeshwa kwenye picha alikuwa na changamoto kama vile kichwa kubonyea na kuwa na uvimbe kifuani tofauti na mtoto wake aliyembeba baada ya kujifungua,"alisema Morcase.

Aliongeza kuwa baada ya kuonyeshwa picha hizo aliambiwa na daktari kuwa mwili umekabidhiwa kwa ndugu zake ambao ni Mabadiliko na shangazi
yake aitwaye Adora Mathias kwa ajili ya mazishi. 

"Mtoto huyo alizikwa bila uwepo wa Mataris ambaye ni mama wa mtoto wala baba wa
mtoto hakufahamishwa kuhusu mazishi hayo na mara baada ya kupata taarifa hiyo kutoka kwa familia hiyo Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani lilifungua jalada la uchunguzi lenye
namba BAG/PE/33/2026,"alisema Morcase.

Aliongeza kuwa Polisi walianza ufuatiliaji ulianza ambapo walimhoji Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo Dk. Mariam Ngwele aliyeeleza kuwa baada ya kumpokea Mataris.

Alisema kuwa Dk Ngwele alieleza kuwa Mataris  alijifungua kwa njia ya upasuaji lakini mtoto hakuwa wa kawaida kwani alikuwa na kichwa kilichobonyea na uvimbe sehemu ya kifuani na changamoto ya upumuaji hivyo alifariki muda mfupi baada ya kuzaliwa.

Kamanda Morcase alisema kuwa kutokana na changamoto hiyo Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani linaendelea na uchunguzi zaidi wa kitaalamu
na kisayansi ili kubaini ukweli wa taarifa hiyo.

Sunday, June 7, 2026

MAFANIKIO YA GLOBAL PARTNERSHIP FOR EDUCATION CHINI YA UENYEKITI WA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE

Na Albert Kawogo 

TANGU Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete ateuliwe kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Global Partnership for Education mwezi Septemba 2021, taasisi hiyo imeendelea kuimarisha juhudi za kuboresha elimu katika nchi zinazoendelea duniani. 

Dkt. Kikwete akiwa kiongozi wa kwanza kutoka Afrika kushika nafasi hiyo muhimu katika historia ya shirika hilo,chini ya uongozi wake, GPE imeongeza juhudi za kuhakikisha watoto wengi zaidi wanapata elimu bora, hususan wale wanaotoka katika mazingira magumu, maeneo yenye migogoro, wakimbizi na watoto wenye ulemavu.

Taasisi hiyo imeendelea kushirikiana na serikali mbalimbali duniani kuboresha mifumo ya elimu na kuongeza uwekezaji katika sekta hiyo ambapo ufanisi mkubwa umeonekana.

Moja ya mafanikio makubwa yaliyoshuhudiwa ni kuongezeka kwa ufadhili wa miradi ya elimu katika nchi wanachama. Katika kipindi cha mkakati wa GPE 2025, mamia ya mamilioni ya watoto wamefikiwa kupitia programu za kuboresha upatikanaji wa elimu, mafunzo kwa walimu, usambazaji wa vitabu na ujenzi wa miundombinu ya shule.

Kufikia mwaka 2024, GPE iliripoti kuwafikia watoto milioni 253, kutoa mafunzo kwa walimu milioni 1.9, kusambaza vitabu milioni 169 na kujenga au kukarabati zaidi ya madarasa 36,000.

Aidha, chini ya uenyekiti wa Dkt. Kikwete, GPE imepanua ushirikiano wake kwa kuongeza nchi wanachama na wadau wapya wa maendeleo.

Mwaka 2024, nchi za Jordan na Lebanon zilijiunga rasmi na ushirikiano huo, huku Saudi Arabia ikitangaza mchango mkubwa wa kifedha kwa ajili ya kuboresha elimu katika nchi zenye kipato cha chini.

Katika eneo la usawa wa kijinsia, GPE imeongeza juhudi za kuhakikisha wasichana wanapata fursa sawa za elimu ambapo pia shirika hilo limeimarisha programu za kuwajumuisha watoto wenye ulemavu, wakimbizi na makundi mengine yaliyokuwa yakibaki nyuma katika upatikanaji wa elimu.

Dkt. Kikwete ambaye ni Rais mstaafu wa Tanzania ameongoza juhudi za kuhamasisha ufadhili zaidi wa elimu duniani, akisisitiza kuwa elimu ni msingi wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii

 Kupitia  mikutano yake mbalimbali ya kimataifa, Dkt Kikwete amekuwa mstari wa mbele kwenye kutetea uwekezaji mkubwa katika elimu ili kukabiliana na changamoto zilizotokana na athari za COVID-19, migogoro ya kimataifa na mabadiliko ya tabianchi.

Kwa ujumla, kipindi cha uenyekiti wa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete  GPE 

imeonyesha mafanikio makubwa hasa katika kupanua fursa za elimu, kuimarisha ubora wa kujifunza, kuongeza ushirikiano wa kimataifa na kuhakikisha watoto walio katika mazingira magumu wanapata haki yao ya msingi ya elimu bora.

Wednesday, June 3, 2026

RAIS DK SAMIA SULUHU HASSAN AWEKA SHADA LA MAUA KABURI ASKARI ASIYEFAHAMIKA

Na Mwandishi Wetu, TBN, Moscow

KENGELE kubwa iliyogongwa mara tisa, bendi ya jeshi ikiongoza nyimbo za maombolezo Rais Dk Samia Suluhu Hasan majira ya saa tano na dakika 23 aliweka shada la maua kwa kaburi la askari asiyefahamika, mjini hapa.

Aidha Baada ya shughuli la uwekaji wa taji hilo katika eneo ambalo moto huwaka daima ikiwa ni kumbukumbu ya wapiganaji wa Urusi waliopoteza maisha katika vita kuu ya pili, gadi tatu zilipita kwa mwendo wa haraka na kutoa heshima kwa Rais Samia baada ya kupigwa kwa wimbo wa taifa la Tanzania.

Hali ya  askari katika uwanja huo walioonesha nidhamu ya hali ya juu ya kusimama tisti katika maeneo yao bila kutikisika , ubadilishanaji wa gadi za ulinzi na pia mwendo wa pole ambao ulimsindikiza Rais Samia kwenda kwenye tukio la uwekeaji wa shahada. Vilikuwa vitu vinavyovutia kuangalia.

Rais Samia ambaye yupo katika ziara ya kiserikali nchini hapa  baadaye alienda kukutana na mwenyeji wake Rais Vladmir Putin 

Zaidi ya maofisa 300 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania JWTZ wamepata nafasi ya masomo katika nchi ya Urusi kwa ajili ya shahada ya kwanza na ya pili.

Askari hao wameenda kujifunza masuala ya kupambana na ugaidi, sayansi na teknolojia,mafunzo ya kijeshi, ulinzi wa amani, ununuzi na uhifadhi wa silaha,namna ya kukabiliana na majanga.

Tanzania na Urusi zina ushirikiano wa kijeshi kwa kuzingatia makubaliano ya ushirikiano wa kijeshi yaliyosainiwa mwaka 2016  na makubaliano ya mwaka 2018 ya ushirikiano wa kifundi wa kijeshi.

Tanzania yenye ukuaji wa uchumi wa asilimia 5.5 kwa mwaka 2024 na ikikadiriwa kufikia asilimia 6 mwaka huu na ikiwa na mkakati wa kuhakikisha kwamba Dira ya maendeleo ya mwaka2050 inatekelezwa ziara ya Rais Samia nchini Urusi inatarajiwa kuzaa matunda yanayotarajiwa  ya kuinua sekta ya ajira kukuza biashara na kuimarisha uwekezaji.

DK SAMIA SULUHU HASSAN KUTUNUKIWA SHAHADA YA UZAMIVU YA CHUO KIKUU CHA RUDIN URUSI

Na Mwandishi Wetu ,TBN, Moscow

Rais Dkt  Samia Suluhu Hassan ambaye yupo hapa shirikisho la Urusi kwa ziara ya kitaifa anatarajiwa kutunukiwa shahada ya uzamivu na Chuo Kikuu cha Rudin nchini hapa.

Tuzo hiyo inatokana na kutambua kazi yake na mchango wake katika jami ya Tanzania na dunia katika masuala ya msingi yanayohusu Maisha ya binadamu.

Chuo cha RUDIN chenye wanafunzi wa kitanzania 570 kufikia mwaka 2025 katika miaka zaidi ya 65 ya RUDIN, watanzania 1,132 wamepitia chuo hicho.

RUDIN kimesomesha zaidi ya wataalamu 200,000 duniani na sasa ina watu 44,000 kutoka nchi 160 duniani.

Chuo hiki ni cha 367 kwa ubora duniani kwa mujibu wa QS World University Ranking ya mwaka 2025.

Rais Dkt Samia ambaye amepokelewa jana na Waziri wa maendeleo ya Uchumi wa Russia Maxim Reshetnikov anatarajiwa kukutana na mwenyeji wake Rais Vladimir Putin na kufanya mazungumzo ya ana kwa ana kwa ajili ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi.

Aidha akiwa nchini hapa, akiwa kiongozi wa pili wa Tanzania kutembelea Urusi, ziara ya kwanza ikiwa imefanywa na baba wa taifa Mwalimu Julius Nyerere, atashiriki Jukwaa la uchumi la St Petersburg ambapo tanzania itanadi fursa za uwekezaji, na diplomasia ya Uchumi  kwa viongozi, wawekezaji na watunga sera wa kimataifa.

Katika kufanikisha dira ya Maendeleo 2050 ziara hii ni kikolezo cha utekelezaji kwa mafanikio ya dira hiyo ambayo inahitaji raslimali watu wenye utaalamu na upeo mkubwa kusimamia na kuendesha miradi ya kimkakati itakayopelekea ajira, viwanda na biashara zitakazoingiza dola trilioni moja na kuwa katika uchumi wa kati wa juu.

Katika WhatsApp yake Rais Samia amesema Ziara hiyo ni muhimu hasa taifa linapoelekea kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 ambayo inataka ushiriki mkubwa wa sekta binafsi.

 "Tutafanya mazungumzo na wenyeji wetu yanayolenga kuimarisha ushirikiano katika sekta za kimkakati zinazogusa maisha ya wananchi." 

"Aidha, tutashiriki majukwaa ya biashara na uwekezaji na kutatangaza fursa zilizopo nchini, pamoja na kufungua zaidi fursa za masoko kwa bidhaa za Tanzania nchini Urusi."

RAIS DK SAMIA SULUHU HASSAN AWASILI URUSI


Na Mwandishi Wetu, TBN, Moscow

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, uliopo Jijini Moscow kwa ajili ya Ziara ya Kitaifa, nchini Urusi

Katika ziara hii ya kihistoria ikifanywa kwa mara ya pili katika historia ya uhusiano wa Tanzania na Urusi, ya kwanza ilikuwa ni miaka ya 1960 iliyofanywa na baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Rais Samia anaendeleza kampeni kubwa ya kuhakikisha Tanzania inanufaika pia kiuchumi na uhusiano mzuri na mataifa mbalimbali

Kwa mujibu wa shughuli atakazofanya Rais Samia akiwa hapa nchini kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa Kidiplomasia, kisiasa, kiuchumi na kihistoria baina ya Tanzania na Urusi,Rais amekuja kuiweka Tanzania katika ramani ya uwekezaji kwa ushiriki wake katika mkutano mkubwa wa uwekezaji jijini St Petersburg na pia kuona namna ya kutengeneza raslimali watu ambayo taifa inahitaji sana katika kufanikisha utekelezaji wa dira ya maendeleo ya 2050. 

Alipowasili nchini hapa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, Jijini Moscow  majira ya saa mbili na dakika 25 usiku , japo jua bado lilikuwa linawaka,  Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alipokea heshima ya wimbo wa Taifa pamoja na gwaride.

Rais Samia alipokewa uwanjani na Waziri wa Maendeleo ya Uchumi wa Shirikisho la Urusi Mhe. Maxim Reshetnikov. 

Kwa mujibu wa ratiba leo asubuhi ataanza na kuweka shada ka maua kwa kaburila askari asiyejulikana kabla ya kwenda Ikuku ya Kremlin kwa mazungumzo na Rais Vladmir Putin.

Sunday, May 31, 2026

WAZIRI KAPINGA AITAKA TBPL KUZALISHA MBOLEA HAI YENYE UBORA

WAZIRI wa Viwanda na Biashara Judith Kapinga ametaka kiwanda cha Tanzania Biotech Production Ltd (TBPL) kuzalisha Mbolea hai kwa kuzingatia ubora.

Kapinga aliyasema hayo Mjini Kibaha wakati wa hafla ya utiaji saini za makubaliano baina ya TPBL kampuni tanzu ya NDC na TFC, TARI, TFRA na TPHPA juu ya ushirikiano wa pamoja.

Alisema kuwa mbolea hiyo inasoko kubwa kwani haina kemikali na pia inatunza mazingira hivyo ni salama kwa afya za binadamu hivyo izingatiwe ubora wake.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji Mwendeshaji wa Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) ambayo ndiyo wasimamizi wa kiwanda hicho Nicolaus Shombe alisema kuwa uzalishaji wa mbolea hiyo utaleta mapinduzi ya kilimo.

Mkurugenzi Mkuu wa TBPL Mhandisi Rafael Moya alisema kuwa mbolea itasaidia wakulima kutumua kemikali kwani kiupaumbele cha Taifa ni kulinda afya za watu.


Wednesday, May 27, 2026

WATAKIWA KUWA NA UTII KAMA WA IBRAHIM

WATANZANIA wametakiwa kufuata maandiko ya vitabu vya dini vinavyoelezea juu ya utii wa Ibrahim ambaye alimuamini Mungu na kumbariki katika maisha yake.

Hayo yalisemwa na Ustaadh Mahamudu Lipambila ambaye ni katibu wa Msikiti wa Masjid Hadharaj Mzimuni Maili Kibaha Mkoani Pwani wakati wa Maadhimisho ya Sikukuu ya Kuchinja (EIDY L ADHUHAA) inayoadhimishwa ulimwenguni kote.

Lipambila alisema kuwa hadhithi ya Ibrahim ambayo ilimtaka amchinjie mwanae ili awe sadaka ambapo ndiyo chimbuko la sikukuu hiyo kubwa kwa imani ya Kiislamu.

"Ibrahim alionyesha utii kwa Mungu kwa kutaka kumtoa mwanae wa pekee ili awe sadaka ya kuchinjwa na alipokubali Mungu kwa kupitia Malaika alimletea kondoo na ndiyo akachinjwa kuwa sadaka,"alisema Lipambila.

Alisema kuwa hadithi hiyo inafundisha jinsi gani watu wanapaswa kuwa na utii juu ya imani zao na kufuata mafundisho ya Mwenyezi Mungu ambayo yatafanya watu waishi kwa kuthaminiana.

"Pia hadithi inafundisha wazazi kuwa na kiasi katika upendo juu ya watoto wao ambapo wengine wamekuwa chanzo cha mmomonyoko wa maadili kwa kutaka kuwafurahisha badala ya kumpenda zaidi Mungu kwa kufuata mafundisho yake,"alisema Lipambila.

Aidha alisema kuwa sikukuu hiyo ni ya furaha kwa kuhakikisha jamii yote inakuwa na furaha kwa kuwa na utii juu ya Mwenyezi Mungu na wanapaswa kumpenda Mungu zaidi.

"Watu waishi kama ilivyokuwa makusudio ya Mungu kutuumba na wakizingatia hayo wataishi kwa amani na upendo na hakutakuwa na tofauti za kimitazamo hasi ya kimaendeleo,"alisema Lipambila.

Aliongeza kuwa viongozi wanapaswa kuwa na hekima na utii kama aliokuwa nao Ibrahim ambaye dini zote zinamuona kama kielelezo cha imani zao kwa Mwenyezi Mungu.

Tuesday, May 26, 2026

WATENDAJI KATA WATAKIWA KUPAMBANA KUONGEZA MAPATO

WATENDAJI wa Kata Mkoani Pwani wametakiwa kumsadia Rais kwenye suala la ukusanyaji wa mapato ili yaweze kuleta maendeleo kwa wananchi ili kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge wakati wa Kikao kazi cha watendaji wa Kata wa Mkoa huo kilichofanyika Kibaha.

Kunenge alisema kuwa Mkoa kwa sasa unafanya vizuri kwenye suala la ukusanyaji wa mapato hapa nchini kutokana na kuweka mazingira mazuri kwa kwenye maeneo ya vyanzo vya mapato.

"Nyie ni watu muhimu sana na serikali ingependa kuona mnaendana na Dira ya Maendeleo ya Taifa ambayo inataka pato la mtu lifikie dola 7,000 kwa mwaka na la nchi trilioni 1 hadi ifikapo mwaka 2050,"alisema Kunenge.

Alisema wakati anafika kwenye Mkoa huo ulikuwa ni moja ya mikoa iliyokuwa chini kimapato ikiwa ni Mkoa wa 23 lakini kwa sasa umeweza kuinuka kimapato.

"Mnapofanya shughuli zenu mhakikishe mnazingatia Dira ya Maendeleo ya Taifa inaweka mazingira mazuri kwa sekta binafsi ili iendeshe uchumi kuzalisha ajira kuongeza thamani ya mazao na kuuza nje ya nchi,"alisema Kunenge.

Alisema kuwa sekta binafsi ni ya kimageuzi ili kuwe na mabadiliko ambapo asilimia 70 ya maendeleo inatokana na sekta binafsi hivyo lazima kuweka mazingira mazuri hasa ikizingatiwa Mkoa wa Pwani ni moja ya mikoa yenye viwanda vingi.

"Watendaji wa kata ni muhimu kwani ni sehemu muhimu ya maendeleo na mabadiliko hivyo hawapaswi kufanya kazi kwa mazoea kwani dunia inabadilika,"alisema Kunenge.

Aidha alisema kuwa wasiamini kwenye kushindwa bali waamini kwenye kushinda kwani wanatakiwa kuongeza thamani na  hawapaswi kulala kama anavyofanya Rais Dk Samia Suluhu Hassan ambaye halali ili kuhakikisha wananchi wanapata maendeleo.

Alibainisha kuwa watendaji hao wanapaswa kupunguza kero na rasilimali zinazopatikana zitumike kwa kuzingatia vipaumbele vya eneo husika na waongeze mapato ya ndani ili nchi iweze kujitegemea.

Nao watendaji hao walisema kuwa watahakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa kushirikiana na viongozi wao na wadau ili kufikia malengo hayo yaliyowekwa ili kuleta maendeleo.

Monday, May 25, 2026

PWANI YAONGEZA MAPATO YA MKOA

MKOA wa Pwani umeongeza ukusanyaji wa mapato kutoka asilimia 87.9 Juni kwa mwaka 2025 na kufikia asilimia 106 Machi mwaka 2026.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge wakati wa Kikao kazi cha watendaji wa Kata wa Mkoa huo.

Kunenge amesema kuwa Mkoa unafanya vizuri kwenye suala la ukusanyaji wa mapato hapa nchini kutokana na kuweka mazingira mazuri.

"Nyie ni watu muhimu sana na serikali ingependa kuona mnaendana na Dira ya Maendeleo ya Taifa ambayo inataka pato la mtu lifikie dola 7,000 kwa mwaka na la nchi trilioni 1 hadi ifikapo mwaka 2050,"amesema Kunenge.

Amesema wakati anafika kwenye Mkoa huo ulikuwa ni moja ya mikoa iliyokuwa chini kimapato ikiwa ni Mkoa wa 23 lakini kwa sasa umeweza kuinuka kimapato.

"Mnapofanya shughuli zenu mhakikishe mnazingatia Dira ya Maendeleo ya Taifa inaweka mazingira mazuri kwa sekta binafsi ili iendeshe uchumi kuzalisha ajira kuongeza thamani ya mazao na kuuza nje ya nchi,"amesema Kunenge.

Amesema kuwa sekta binafsi ni ya kimageuzi ili kuwe na mabadiliko ambapo asilimia 70 ya maendeleo inatokana na sekta binafsi hivyo lazima kuweka mazingira mazuri hasa ikizingatiwa Mkoa wa Pwani ni moja ya mikoa yenye viwanda vingi.

"Watendaji wa kata ni muhimu kwani ni sehemu muhimu ya maendeleo na mabadiliko hivyo hawapaswi kufanya kazi kwa mazoea kwani dunia inabadilika,"amesema Kunenge.

Aidha amesema kuwa wasiamini kwenye kushindwa bali waamini kwenye kushinda kwani wanatakiwa kuongeza thamani na  hawapaswi kulala kama anavyofanya Rais Dk Samia Suluhu Hassan ambaye halali ili kuhakikisha wananchi wanapata maendeleo.

Alibainisha kuwa watendaji hao wanapaswa kupunguza kero na rasilimali zinazopatikana zitumike kwa kuzingatia vipaumbele vya eneo husika na waongeze mapato ya ndani ili nchi iweze kujitegemea.

Sunday, May 24, 2026

MTAA WA MWENDAPOLE B MBIONI KUANZA ULINZI SHIRIKISH KUKABILI UHALIFUI

WANANCHI wa Mtaa wa Mwendapole B Wilayani Kibaha wamekubaliana kuanza kufanya ulinzi shirikishi ili kukabiliana na vitendo vya kihalifu ndani ya Mtaa huo..

Akizungumza na wananchi wakati wa kikao cha Mtaa kilichofanyika kwenye ofisi za Mtaa huo Mwenyekiti wa Mtaa Abubakar Matumla alisema kuwa kabla ya kuanza kamati itakaa ili kuangalia namna ya kufanya ulinzi huo.

Matumla alisema tayari wameshapata kibali cha kuwa na ulinzi shirikishi na kinachofuata ni kupanga namna ya kufanya zoezi hilo na namna wananchi watakavyo changia watu watakaokuwa wakilinda.

"Tunamshukuru Mkuu wa Wilaya tayari katoa kibali cha Mtaa kuwa na ulinzi shirikishi ili kukabiliana na vitendo vya uhalifu ambavyo vimekuwa vikijitokeza nyakati tofauti tofauti,"alisema Matumla.

Alisema kuwa watakaa na kamati ya Mtaa wiki hii ili kupanga utaratibu mzuri wa kuanza zoezi hilo na kiwango cha kila kaya kuchangia ili kuwalipa walinzi hasa ikizingatiwa michongo ya ulinzi shirikishi ni hayari.

Aidha alisema kuwa wenye nyumba nao wsnapaswa kuwa makini kwa kuwa na taarifa za kutosha za wapangaji wao kwani baadhi yao wanaweza kuwa wanajihusisha na uhalifu.

Naye Diwani wa Kata ya Kibaha Omary Bulla alisema kuwa ulinzi shirikishi ni muhimu sana kwani baadhi ya vijana ambao siyo waaminifu wamekuwa wakiiba vitu kwenye nyumba au kukaba watu.

Bulla alisema kuwa ili kufanikiwa wananchi wanapaswa kushiriki kikamilifu kwa kutoa michango ili iwezeshe walinzi waweze kufanya kazi zao bila ya vikwazo na kukabili uhalifu ndani ya Mtaa huo.

Kwa upande wake mmoja wa wananchi wa Mtaa huo Dago Mwombeki alisema kuwa baadhi ya vijana wamekuwa wakiwapora watu wanaokuwa wanakwenda kazini alfajiri au wanapokuwa wanatoka kazini.

Mwombeki alisema kuwa ulinzi shirikishi utasaidia kukabili changamoto hiyo ya uhalifu ndani ya Mtaa kwani wanasababisha watu wasiishi kwa amani na kurudisha nyuma maendeleo ya watu.

Saturday, May 23, 2026

NG'OMBE 28 WA WIZI WAKAMATWA

JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani kupitia Kikosi cha Kuzuia Wizi wa Mifugo (STPU) linashikiliwa watu wanne tuhuma za wizi wa ng'ombe 28.

Akizungumza na Waandishi wa Habari ofisini kwake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani  Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Salim Morcase alisema kuwa mara baada ya upelelezi kukamilika watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani.

Morcase alisema kuwa tukio hilo lilitokea Mei 22 mwaka huu huko maeneo ya Tungutungu Mapinga Wilayani Bagamoyo ambapo kati yao ng’ombe 13 ni mali ya Fadhili Ngabilo mkazi wa Kwa Makocho Kata ya Mandela Chalinze

"Mlalamikaji Fadhili Ngabilo aliripoti katika kituo cha Polisi Chalinze kuibiwa  jumla ya ng’ombe 18 na mbuzi watano ambapo Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani kupitia Kikosi cha Kuzuia Wizi wa Mifugo(STPU) walianza ufuatiliaji,"alisema Morcase.

Alisema kuwa katika ufuatiliaji ilipofika Mei 22 majira ya saa 3:00 asubuhi walifanikiwa kuwapata ng’ombe 28 wakiwemo ng’ombe 13 kati ya 18 walioibiwa Chalinze wakiwa kwenye zizi la mfanyabiashara mmoja wa nyama.

"Kati ya ng’ombe 15 waliokutwa nyumbani kwa mtuhumiwa ng’ombe watano walitambulika na ng’ombe wanne mahojiano yanaendelea,"alisema Morcase.

Aidha alisema kuwa mtuhumiwa huyo huwa anachinja ng’ombe wa wizi nyumbani kwake kisha kuuza nyama kwenye bucha yake.

"Hadi sasa jumla ya watuhumiwa wanne wanashikiliwa na mara baada ya upelelezi kukamilika watafikishwa mahakamani kuhusiana na tukio hilo,"alisema Morcase.

Alitoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa sahihi kwa kadri operesheni za kudhibiti uhalifu zinavyofanyika maeneo mbalimbali ndani ya Mkoa wa Pwani.

Sunday, May 17, 2026

MBUNGE SUBIRA MGALU ATOA MSAADA KWA VITONGOJI VILIVYOKUMBWA NA MAFURIKO BAGAMOYO


MBUNGE wa Jimbo la Bagamoyo Subira Mgalu ametoa kiasi cha shilingi milioni 2 kwa Vitongoji vya kata ya Nianjema vilivyokumbwa na mafuriko.

Mgalu amesema vitongoji hivyo vilivyokumbwa na mafuriko yaliyosababisha kuharibika kwa Miundombinu ya barabara na maji kuzingira makazi na taasisi za Umma. 

Nimewapa pole , na nimewaahidi ntaendelea kuwasemea kero hii Bungeni na kwenye Mamlaka mbalimbali .

 Tangu 2018 mafuriko yalipoanza nimekuwa Kiongozi wa kwanza kuwafikia na kuwafariji # Mbunge wa Jimbo Kazini

UMOJA WA WANAUME MKOMBOZI (UWWM) KUNUNUA MABASI MAWILI

UMOJA wa Wanaume Mkombozi (UWWM) wanatarajia kununua mabasi madogo mawili ya abiria ili kukabiliana na changamoto ya usafiri kutoka na kuingia kwenye Mtaa wa Mkombozi uliyopo Wilayani Kibaha Mkoani Pwani.

Hayo yalisemwa na Katibu wa (UWWM) Mwinjilisti Williama Wami wakati wa uzinduzi wa umoja huo na Mfuko wa umoja ambapo changamoto ya usafiri ni kubwa kwani kuna basi moja tu linalofanya safari zake kati ya Mkombozi na Mbezi Jijini Dar es Salaam.

Wami alisema Mtaa huo umepakana na Wilaya ya Ubungo ambapo wanapata mahitaji yao eneo la Kibamba Njia Panda Shule kutokana na ukaribu tofauti na Kibaha ambako ni mbali.

"Wakazi huku ni wengi sana lakini tatizo kubwa ni usafiri ambapo kutokana na ubovu wa barabara magari mengi hayawezi kufika kwani kuna basi moja tu ambalo linatoa huduma lakini sisi malengo yetu ni kununua mabasi madogo mawili ili kurahisisha usafiri,"alisema Wami 

Alisema kuwa kwa sasa wanatumia usafiri wa pikipiki ili kufika majumbani au kutoka kwenda kwenye shughuli zao za kila siku kujiletea kipato lakini usafiri huo ni gharama kubwa sana.

"Kupitia umoja wetu tulihamadisha kupatikana kwa basi hilo lakini bado halikidhi mahitaji kwani uhitaji ni mkubwa sana kwani uwezo wa baadhi ya watu kupanda pikipiki kwao ni mzigo mkubwa lakini kupitia daladala gharama inakuwa nafuu,"alisema Wami.

Aidha alisema kuwa malengo yao mengine ni kujenga ukumbi mkubwa kwa ajili ya shughuli mbalimbali ikiwemo mikutano na sherehe utakaogharimu kiasi cha shilingi milioni 500 ambapo kwa sasa huwabidi kufanya shughuli hizo nje ya mtaa huo pia kuanzisha Chama Akiba na Mikopo ili kukopeshana kwa riba nafuu.

"Vitu tulivyofanya ni kuvuta maji na kujenga vyoo vya kisasa kwenye soko jipya na tunatarajia hapo kuwa na stendi tunaishukuru Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha kwa kutuanzishia soko tunaomba watupe kibali ili watu waanze kufanya biashara,"alisema Wami.

Aliongeza kuwa miradi hiyo mbali ya kutoa huduma itakuwa ni vyanzo vya mapato ya umoja kwani lengo ni kuleta maendeleo ya Mtaa na kwa mwananchi mmoja mmoja pia ni kusaidiana katika shida na raha na kauli mbiu ni Baba kichwa cha Familia.

Umoja huo ulianzishwa mwaka jana na una wanachama 265 huku wanachama hai ni 205 hadi sasa wana kiasi cha shilingi milioni 10 benki ambapo kila mwezi mwanachama huchanga shilingi 5,000.