Thursday, March 5, 2026

MAOFISA USAFIRISHAJI WATAKIWA KUUNDA VIKUNDI WAKOPE HALMASHAURI





MAOFISA Usafirishaji maarufu kama Bodaboda kwenye Mtaa wa Mwendapole B wametakiwa kuunda vikundi ili waweze kukopa vyombo vya usafiri vinavyotolewa na Halmashauri kuachana na mikopo ya taasisi za watu binafsi ambazo zina gharama kubwa.

Aidha alisema kuwa gharama za mikopo ya Halmashauri ni ndogo na marejesho yake ni madogo tofauti na mikopo ya vyombo hivyo kwenye taasisi au watu binafsi.

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti wa Mtaa huo Abubakar Matumla wakati wa kikao na waendesha pikipiki wa Mtaa huo na kuwa wanashindwa kufanikiwa kwa kukopa pikipiki kwa riba kubwa.

Matumla alisema kuwa gharama za kukopa pikipiki kwa watu binafsi imekuwa ikiwafanya wasifanikiwe kutokana na gharama kuwa kubwa za mikopo hiyo hivyo hujikuta wanashindwa kujiongezea kipato.

"Serikali imewawekea mazingira mazuri ya mikopo yake kwani mnauwezo wa kukopa pikipiki, bajaji na Toyo kwa gharama nafuu na unarejesha kiasi kilekile ulichokopa na hakuna riba ya mkopo unaokopa hivyo ni wakati wenu wa kujiunga na kuwa na vikundi na mtumie fursa ya mikopo pale Halmashauri fedha zipo za kutosha na vyombo vya moto vipo,"alisema Matumla.

Alisema kuwa yuko tayari kuwasimamia kuhakikisha wanapata mikopo hiyo kwani hapendi kuona waendesha pikipiki wakitaabika ili hali kuna sehemu wanaweza kukopa bila ya kuwa na marejesho makubwa pia aliwataka kutoa taarifa kwa wale wanaojihusisha na vitendo vya kiuhalifu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa waendesha pikipiki hao Abdulatif Mbonganga alisema kuwa tayari wameshaanzisha kikundi kimoja na tayari kimeshasajiliwa kikiwa kinasubiri wakati ukifika waende kukopa.

Mboganga alisema kuwa changamoto kubwa kwao ni kukosa vyombo vya usafiri hali inayowabidi kukopa vyombo hivyo kwenye taasisi za watu binafsi ambazo zinagharama kubwa na kujikuta wakitumia nguvu kubwa kwenye marejesho.

Moja ya maofisa usafirishaji Salum Msaku alisema kuwa changamoto ya uhalifu inatokana na baadhi yao kuwapa ma "day worker" hasa nyakati za usiku ambapo wanawaletea sifa mbaya.

Msaku alisema kuwa ili kudhibiti hali hiyo kila mwendesha pikpiki aendeshe pikipiki yake na siyo kumpa mtu mwingine pia wahakikishe wanavaa riflector ambazo zitawatambua kwa namba zinazoandikwa mgongoni inakuwa rahisi katika ufuatiliaji.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mtaa wa Miembe Saba B Nuru Awadh alisema kuwa wanapaswa kuwa na ushirikiano na kuunda vikundi vya bodaboda ili wapate mikopo nafauu.

Awadh aliwataka wajiheshimu na wasijiunge na makundi mabaya kwani Rais amewapa kipaumbele vijana katika uongozi na sehemu mbalimbali ili wawe vinara kwa utendaji kazi.

Tuesday, March 3, 2026

KAMBI SAMIA ARDHI KLINIKI YAANZA PWANI

HALMASHAURI ya Manispaa Kibaha kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeweka kambi ya Samia Ardhi Kliniki ikiwa ni maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani.

Akizungumza kuhusu huduma zinazotolewa katika kambi hiyo ya siku sita, Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Pwani Rugambwa Banyika alisema kuwa kliniki hiyo inalenga kutoa ushauri wa kisheria kuhusu masuala ya ardhi.

Banyika alisema kuwa shughuli nyingine zitakuwa ni kufanya makadirio ya pango la ardhi, kuandaa nyaraka za umiliki, kujibu changamoto za upimaji, urasimishaji, upangaji miji na michoro pamoja na kutoa hati za umiliki.

"Wananchi wote wanakaribishwa ili kupata huduma zote zihusiananazo na masuala ya ardhi ambapo huduma zimesogezwa ili kila mwananchi apate fursa katika kipindi hichi kuanzia Machi 2 hadi 7 kuelekea kilele cha siku ya Wanawake Duniani Machi 8,"alisema Banyika. 

Alisema kuwa kambi hiyo maalum ina lengo la kushughulikia changamoto mbalimbali za ardhi kwa wananchi hususan wanawake na wasichana katika masuala yanayohusiana na ardhi.

Baadhi ya wananchi Mariam Juma na Ahmed Abdala wameishukuru Serikali kwa kusogeza huduma hizo karibu yao na kueleza kuridhishwa na namna wanavyohudumiwa na wataalamu wa ardhi kwani wanatoa elimu ya kujitosheleza.

Kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani kimkoa kinatarajiwa kufanyika Machi 8 2026 katika Uwanja wa Ujamaa Kata ya Umwe Tarafa ya Ikwiriri Halmashauri ya Mji wa Rufiji ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge.

Sunday, March 1, 2026

PWANI YAANZA MAANDALIZI MAADHIMISHO SIKU YA WANAWAKE DUNIANI

MKOA wa Pwani umeanza maandalizi ya Siku ya Wanawake Duniani ambapo kilele cha maadhimisho kimkoa yatafanyika Machi 8, 2026 katika Uwanja wa Ujamaa, Kata ya Umwe, Tarafa ya Ikwiriri, Halmashauri ya Mji Rufiji. 

Mratibu wa maadhimisho hayo, Roseline Kimaro, amesema mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge.

Akizungumza kuhusu maandalizi, Kimaro amesema maadhimisho ya mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu isemayo, “Haki kwa Wanawake na Wasichana: Msingi wa Maendeleo Jumuishi Dira 2050,” ikisisitiza umuhimu wa usawa wa kijinsia na haki kama nguzo ya maendeleo endelevu. 

Amesema lengo ni kutambua na kuenzi mchango wa wanawake katika nyanja za kijamii, kisiasa na kiuchumi, sambamba na kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia.

Amebainisha kuwa kuanzia Machi 1 hadi 7 kutafanyika shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo utoaji wa elimu kwa umma na kampeni za uhamasishaji kuhusu usawa wa kijinsia,  kilele cha maadhimisho Machi 8. 

Ameongeza kuwa maandalizi yanaendelea vizuri na kutoa wito kwa wananchi na wadau wa maendeleo kujitokeza kwa wingi kushiriki na kuunga mkono jitihada za kulinda na kuimarisha haki za wanawake na wasichana.

Friday, February 27, 2026

TRA PWANI KUBADILI UTARATIBU UKUSANYAJI KODI BANDARI YA BAGAMOYO

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani kuanza utaratibu mpya ukusanyaji mapato Bandari ya Bagamoyo Machi Mosi mwaka huu.

Akizungumza na wafanyabiashara wa mafuta ya kula kwenye Bandari hiyo Meneja wa TRA Mkoa huo Masawa Masawa alisema kuwa changamoto iliyopo ni malalamiko ya wafanyabiashara kulalamikia bei ya kodi ya mafuta yanayotoka Zanzibar.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo Shaibu Ndemanga alisema kuwa wananchi wengi wanategemea biashara ya mafuta na kuna wadau wengi wanategemea shughuli zinazohusiana na biashara ya mafuta.

Naye Diwani wa Kata ya Dunda Amiry Mpwimbwi alisema kuwa eneo hilo la Bandari linatoa ajira zaidi ya 8,000 hivyo kutokana na shughuli kutofanyika kumesababisha serikali kukosa mapato.

Mwenyekiti wa wafanyabiashara wa Mafuta kwenye Bandari hiyo Shaban Hamsini alisema kuwa hali imeshakuwa mbaya kwani wanategemea shughuli hizo kuendeshea maisha yao.

Saturday, February 21, 2026

MATUMLA AWATAKA WANANCHI KUSHIRIKIANA NA SERIKALI ILI KUTATUA CHANGAMOTO


MWENYEKITI wa Mtaa wa Mwendapole B Manispaa ya Kibaha Abubakar Matumla ameendelea na ziara ya kutafutia majawabu changamoto zinazowakabili wananchi wa Mtaa huo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Matumla amesema ziara hiyo inaifanya kwa kutembelea Balozi zote zilizopo kwenye Mtaa huo ili kubaini changamoto ili kupeleka sehemu husika kwa utatuzi.

Changamoto ambazo zimekuwa zikijirudia ni pamoja na miundombinu ya barabara, uhalifu, uvutaji wa bhangi, maji, elimu ya msingi.

Matumla amesema kuwa kutokana na changamoto hizo watawasiliana na mamlaka husika ili wazifanyie kazi changamoto hizo ili ziweze kupatiwa majawabu.

Akizingumzia uhalifu amesema kuwa tayari baadhi ya maeneo yameainishwa kuwa ni kitovu cha uhalifu pamoja na matumizi ya dawa za kulevya aina ya bhangi.

"Tayari tumeshaweka mikakati ya kudhibiti uhalifu kwa kushirikiana na Polisi Kata ili kuwakama wahalifu hao pia ni kufanya doria za kushtukiza ambapo baadhi ya wahalifu wanajificha kwenye Bodaboda ambapo tayari mipango ya kuwatambua inafanyika,"amesema Matumla.

Amesema baadhi ya maeneo kuna changamoto ya upatikanaji wa maji, miundombinu ya barabara imeharibika lakini hata hivyo Mtaa huo umepata barabara moja ambayo itajengwa lami.

"Kwa upande wa elimu ya Msingi changamoto kubwa ni uhaba wa madawati na vyumba vya madarasa ambapo Manispaa ya Kibaha imetoa madawati 20 ambayo yatasaidia kukabiliana na changamoto ya upungufu wa madawati,"amesema Matumla.




DIWANI TANGINI ATOA POLE MTOTO ALIYENUSURIKA KIFO KWA KUSOMBWA NA MAJI NA WALIOEZULIWA PAA ZA NYUMBA ZAO

DIWANI wa Kata ya Tangini Antony Milao ametoa pole kwa wananchi waliokumbwa na kadhia ya mvua ikiwemo ya mwanafunzi Morhat Abdala (9) kunusurika kifo baada ya kusombwa na maji akitoka shuleni.

Mvua hiyo iliyonyesha jana jioni ilileta athari kwa baadhi ya wakazi wa Mtaa wa Machinjioni Kata ya Tangini ambapo nyumba mbili na Machinjio ya mbuzi ambapo mapaa yaliezuliwa baada mvua kubwa kunyesha ikiambatana na upepo mkali kwenye Mtaa huo.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kutokea matukio hayo Milao amesema kuwa mwanafunzi huyo ambaye amepumzishwa kwenye Kituo cha Afya Mkoani akipatiwa matibabu anaendelea vizuri.

Milao amesema anamshukuru Mungu kumnusuru mtoto huyo ambaye anasoma darasa la nne Shule ya Msingi Maendeleo akiwa anatoka shule akiwa na mwenzake waliteleza wakati wakivuka kalavati na kusombwa na maji kabla ya wasamaria wema kuwaokoa.

"Pia nilimtembelea Mzee Boniface Mpanda ambaye nyumba yake imeezuliwa paa na nyumba ya Jackson Sellu ambaye hakuwepo nitawasiliana naye pamoja na sehemu ya paa la Machinjio jambo la kushukuru hakuna madhara kwa binadamu zaidi ya mapaa kungoka nimewashika mkono wale waliopata athari hizo ili waweze kutengeneza nyumba zao ili waendelee na maisha yao,"amesema Milao.

Mama wa mwanafunzi aliyesombwa na maji Fatuma Juma amesema kuwa alipata taarifa toka kwa wasamaria wema kuwa mwanae yuko Hospitali baada ya kusombwa na maji baada ya mvua kubwa kunyesha.

Juma amesema anamshukuru Mungu kwani mwanae kwa sasa anaendelea vizuri baada ya kupatiwa matibabu na anawashukuru wasamaria wema kumuokoa mwanae na kumuwaisha hospitali.

Naye Mzee Boniface Mpanda ambaye nyumba yake imeezuliwa paa amesema kuwa alikuwa ndani wakati mvua inanyesha mara akashtukia paa linarushwa na upepo mkali na vitu vyake vyote kulowa.

Mpanda anasema majirani walimsaidia kutoa vitu vyake na kuviweka kwenye mazingira salama wanatoa shukrani zao kwa majirani kwa kutoa msaada na diwani jinsi alivyojitoa kuwasaidia.

Kwa upande wake jirani ambapo nyumba hizo mbili zilizoezuliwa paa Remminister Komanga amesema kuwa mvua hiyo ilinyesha na ilikuwa na upepo mkali na kuezua mapaa hayo pamoja na kuangusha sehemu ya ukuta wake uliozungushiwa kwenye nyumba yake.

Komanga amesema upepo huo ulikuwa ni kama kimbunga na ulikuwa ni sehemu hiyo tu kwani maeneo mengine hakukuwa na upepo zaidi ya mvua kuwa tu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Machinjioni Aidan Saimon amesema kuwa baada ya kutokea madhara hayo waliwasiliana na diwani ili waangalie namna ya kuwasaidia wananchi hao.

Simon amesema kuwa alipewa maagizo na diwani kuhakikisha vifaa vyote vya upauaji atakavyovitoa vinatumika kwa haraka ili nyumba ya Mzee Mpanda ipauliwe upya na atawasiliana na Sellu kuona atamsaidiaje ambapo vyumba vyake viwili vimeezuliwa na upepo.


 

Thursday, February 19, 2026

ATAKA MASLAHI KWA WAFANYAKAZI WA MAJUMBANI

JAMII imetakiwa kuheshimu ajira ya wafanyakazi wa majumbani kwani nitaaluma kama zilivyo taaluma zingine kwa kuifanya kuwa yenye staha kwani ni sehemu ya ustawi wa jamii na ukuzaji wa uchumi.

Hayo yalisemwa Jijini Dar es Salaam kwenye ukumbi wa Confucius wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Rashid Ally Salim Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Kazi na Uwekezaji Zanzibar wakati akifungua mkutano wa mradi wa Urasimishaji wa kitaaluma kwa wafanyakazi wa majumbani Tanzania.

Salim alisema kuwa jamii inapaswa kuona kazi za nyumbani ni taaluma kwa kuzingatia maslahi na haki za msingi za mfanyakazi kwani anaiendeleza jamii.

"Hawa ni watu muhimu sana kwani wanatunza familia zetu pale tunapokuwa kazini au kwenye majukumu mengine ya kimaendeleo hivyo tuwape heshima yao,"alisema Salim.

Alisema kupatiwa mafunzo ya ujuzi kupitia vituo vya VETA ni moja ya vitu vitavyoweza kuwasaidia katika maisha yao kwani ujuzi huo utakuwa ni mkombozi kwao na utawasaidia kujitambua na kujiamini.

Naye mwakilishi kutoka Veta Abdala Ulomi alisema kuwa tayari wametoa mafunzo ya ujuzi kwa wafanyakazi wa majumbani 1,280 kwenye vyuo sita vya Bara na vitatu vya Zanzibar na mtaala wao tayari umeshaandaliwa.

Ulomi alisema kuwa wanarasimisha mafunzo kwa wafanyakazi wa majumbani kwani mahitaji yao ni makubwa ndani na nje ya nchi na hiyo itakuwa taaluma kama taaluma zingine.

Kwa upande wake Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Profesa Rose Upor alisema kuwa asilimia 95 ya wafanyakazi wa majumbani ni wanawake ambapo kuna umuhimu wa kuboresha mazingira ya hali za kijinsia.

Upor alisema kuwa suluhisho ni kukuza utu na mazingira bora ya kazi ambapo kuna haja ya kushughulikia tafiti zinazofanywa ili kuleta usawa na kuepukana na vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Mkurugenzi wa Shirika la CVM Tanzania Magesa Nathaniel alisema kuwa wamekuwa wakitekeleza mradi wa miaka mitatu ambao umefika mwisho wa kukuza kazi za staha na haki kwa wafanyakazi kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na wadau mbalimbali wa ndani na nje.

Nathaniel alisema kuwa baadhi ya kazi walizokuwa wakifanya ni kuwajengea uelewa na kuwajengea uwezo kuwaunganisha na chama cha wafanyakazi wa majumbani CHODAWU katika utetezi wa haki zao.

Asteria Gerald mwakilishi wa CHODAWU alisema kuwa kutambuliwa kwa kazi zao kutasababisha kupata heshima ulinzi na stahiki nyingine kwani bado wananyanyaswa wanafanyiwa ukatili na wanafanya kazi kwa muda mrefu.

Gerald alisema kuwa wanaomba kuridhiwa kwa mkataba namba 189 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) ambayo inalinda haki hadhi usalama wa wafanyakazi wa majumbani.

Mkurugenzi wa Taasisi za Taaluma za Kijinsia Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Dk Sara Kisanga alisema kuwa wafanyakazi wa nyumbani wanapaswa kutambuliwa na kulindwa na kuendelezwa kiujuzi.

Kisanga alisema kuwa wataalamu wanaotoka chuoni hapo wanawezesha jamii ili kuleta mabadiliko chanya ili kuwa kazi ambazo zina staha na kuzingatia haki za binadamu.