Saturday, March 7, 2026

KIKUNDI CHA LULU YA WAJANE WAISHUKURU MANISPAA YA KIBAHA KWA MKOPO WA MILIONI 46

KIKUNDI cha wanawake cha Lulu ya Wajane kilichopo  Kongowe, Manispaa ya Kibaha mkoani Pwani, kimeishukuru Manispaa ya Kibaha kwa kuwapatia mkopo wa shilingi milioni 46 uliowawezesha kuendesha na kukuza shughuli zao za kiuchumi.

Akizungumza kwa niaba ya wanakikundi, Mwenyekiti wa kikundi hicho Kanyenda Mweri amesema mkopo huo waliupata kupitia mpango wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri kwa makundi maalum, na wamefanikiwa kuurejesha ndani ya kipindi cha miezi 11.

Amesema kikundi chao kinajishughulisha na ufugaji wa kuku wa aina mbalimbali, ambapo huuza kuku hao kwa jumla na rejareja na hivyo kuwa chanzo kikuu cha kipato kwa wanachama wake.

Aidha, amesema baada ya mafanikio waliyoyapata, kwa sasa wanatarajia kuomba mkopo mwingine ambao utawawezesha kununua mashine ya kutotolea vifaranga ili kupanua zaidi shughuli zao za ufugaji na kuongeza uzalishaji.

Kikundi hicho kimebainisha kuwa mkopo huo umewasaidia kujikwamua kiuchumi na kuboresha maisha yao, sambamba na kutoa ajira kwa baadhi ya wananchi katika eneo lao.

PANGANI SEKONDARI WAPANDA MITI 344

SHULE ya Sekondari Pangani, Manispaa ya Kibaha imefanya zoezi la kupanda miti zaidi ya 344 katika mazingira ya shule hiyo ikiwa ni sehemu ya kutekeleza agizo la Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan la kuhimiza taasisi za elimu kuhifadhi mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Zoezi hilo limehusisha wanafunzi, walimu pamoja na viongozi wa Serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kata ya Pangani kwa lengo la kuboresha mazingira ya shule hiyo.

Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Tatu Mwambala amefafanua miti hiyo ni ya kivuli na mbao ambapo miti 220 imetolewa na kitalu cha Manispaa, miti 110 kutoka Wakala wa Misitu kupitia Shule ya Sekondari Msangani II na miti 14 ya matunda imenunuliwa na shule.

Amesema miti hiyo itasaidia kukuza stadi za utunzaji wa mazingira kwa wanafunzi pamoja na kuboresha mazingira ya shule.

Diwani wa Kata ya Pangani, John Katele amebainisha zoezi hilo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM pamoja na mikakati ya kupanda miti milioni 1.5 katika mkoa huo.

Kwa upande wake Ofisa Kilimo wa kata hiyo, Omary Ngulengule ameeleza kuwa, wanafunzi wamepata elimu ya vitendo kuhusu uchimbaji mashimo na upandaji sahihi wa miti ili wawe mabalozi wa utunzaji wa mazingira katika jamii.

Mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule hiyo, Stanley Amos ameeleza elimu waliyoipata itawasaidia kuhamasisha familia na jamii kupanda miti na kutunza mazingira.

MUHIMILI WA MAHAKAMA KUTATUA CHANGAMOTO ZA WANAWAKE KWA WAKATI


MWENYEKITI wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii Hawa Mchafu amesema mhimili wa Mahakama unatakiwa kuangalia uwezekano wa kushughulikia kwa karibu changamoto za Wanawake ili ziweze kutatuliwa kwa wakati.

Mchafu ambaue pia ni Mbunge Vitimaalumu Mkoa wa Pwani amesema Serikali inatakiwa kuweka madawati ya jinsia na dawati la msaada wa kisheria katika Halmashauri ili Wanawake wanufaike kwa kupata ushauri wa kisaikolojia utakaosaidia kujikwamua kiuchumi kwa kushirikiana na wenza wao ili kupata kipato kwa ajili ya kujikimu na familia zao.

Ametoa angalizo hilo Machi 6 alipokuwa akihutubia wakazi wa Manispaa ya Kibaha walioshiriki kwenye maadhimisho ya siku ya Wanawake duniani ambapo Manispaa hiyo ilifanya maadhimisho yake mjini Mailimoja.

Katika hotuba yake Mchafu amebainisha kwamba dawati la jinsia Polisi ambalo lina kazi ya kusikiliza na kutoa ushauri kwa matatizo yanayowasilishwa wanawake waliofanyiwa ukatili wa kijinsia, mashauri 461 yalipokelewa na kati ya hayo  63 yamepelekwa Mahakamani kwa ajili ya maamuzi zaidi. 

Mwenyekiti huyo wa Kamati ya Kudimu ya Bunge amesema kauli mbiu ya Siku ya Wanawake Duniani kitaifa kwa Mwaka 2026 ni Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050 inahimiza kujenga uelewa kwa jamii na wadau, kuwekeza kwenye Maendeleo Jumuishi ikiwemo kutambua Haki za Wanawake na Wasichana.

Amesema lengo lingine ni kuhakikisha Haki za Wanawake na Wasichana  zinafanyiwa kazi kwa vitendo na kuleta mabadiliko ya kweli kama ilivyoainishwa kwenye nguzo za Dira 2050 . 

Akizungumza katika Maadhimisho hayo Ofisa Maendeleo ya Jamii Manispaa ya Kibaha Lea Lwanji amesema kwasasa wanaendelea kuratibu shughuli za wamachinga kwa kuwatambua na kuwasajili kwenye mfumo ambapo tayari wamachinga 1,112 kati yao wakes 732 wanaume 380.

Akielezea kuhusiana na uwezeshwaji kiuchumi Lwanji amesema katika mwaka wa fedha 2025/2026 Halmashauri imetenga sh. Biln 1.1 na kwamba mikopo yenye thamani ya sh.Billion 2.1 imetolewa kwa vikundi 436 na watu binafsi 21 kati ya vikundi hivyo 275 ni vya Wanawake ambao wamepata zaidi ya sh. Billion 1.

Ofisa Maendeleo huyo amebainisha kwamba Wajasiriamali wengi wamekuwa na mwamko wa kufanya biashara na wengi wanajitokeza kutafuta fursa za mitaji katika taasisi wezeshi.

Wakati huo huo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dk Rogers Shemwelekwa amewapongeza watumishi wanawake katika Manispaa hiyo kwa mchango wao katika ukusanyaji wa mapato uliowezesha Manispaa hiyo kushika nafasi ya pili kitaifa miongoni mwa Halmashauri 184 nchini Tanzania.

Dkt. Shemwelekwa amesema Manispaa ya Kibaha imefanikiwa kushika nafasi ya pili kitaifa katika ukusanyaji wa mapato baada ya kukusanya shilingi bilioni 17, huku idara ya Uhasibu na Mapato ikiongozwa na mwanamke.

Ameongeza kuwa Halmashauri hiyo inaendelea kuimarisha ukusanyaji wa mapato ambapo kwa sasa imefikia shilingi bilioni 18, ikilinganishwa na awali ambapo ilikuwa ikikusanya shilingi bilioni 7.3.

WANANCHI WAMIMINIKA KLINIKI YA ARDHI KIBAHA WAOMBA SIKU ZIONGEZWE

 

WANANCHI wa Manispaa ya Kibaha wameendelea kujitokeza kwa wingi kupata huduma katika Kliniki ya Ardhi ijulikanayo kama Samia Ardhi Kliniki, huku baadhi yao wakiomba muda wa utoaji wa huduma hizo uongezwe kutokana na umuhimu wake.

Wananchi hao pia wameishukuru Serikali kwa kusogeza huduma hizo karibu yao na kueleza kuridhishwa na namna wanavyohudumiwa katika kliniki hiyo.

Maoni hayo yametolewa Machi 4, 2026, wakati kambi maalum ya kushughulikia masuala ya ardhi ikiendelea kwa siku ya tatu katika viwanja vya Maili Moja, Stendi ya Zamani, Manispaa ya Kibaha, ambapo wananchi wengi wameendelea kumiminika kupata huduma mbalimbali.

Mkazi wa Kibaha, Ester Joel, aliyefika katika kliniki hiyo kupata huduma ya hati, amesema ameridhishwa na huduma aliyoipata na kuomba muda wa kliniki hiyo uongezwe ili wananchi wengi zaidi wapate fursa ya kuhudumiwa.

“Nimeridhika na huduma niliyoipata hapa. Kwanza nimepokelewa vizuri na nimeelekezwa namna ya kutatua changamoto yangu. Hata hivyo, kutokana na umuhimu wa huduma hii, ningependa siku ziongezwe hata kufikia wiki mbili,” amesema Ester Joel.

Kwa upande wake Coletha Nombo, ambaye pia alifika kupata huduma ya hati, amepongeza juhudi za Serikali kwa kuwaletea wananchi huduma hiyo karibu na maeneo yao.

Naye Ruth Kadema, mkazi wa Pangani, amesema ameridhishwa na huduma aliyoipata na kueleza kuwa amepewa maelekezo ya kufika tena siku ya Jumamosi kwa ajili ya kukamilisha taratibu za kupata hati yake.

“Huduma hii ni nzuri sana. Nimeridhika na nimeambiwa nije Jumamosi kuchukua hati yangu baada ya kuwasilisha taarifa zangu leo,” amefafanua Ruth.

Kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambayo huadhimishwa Machi 8 kila mwaka, Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeandaa kambi hiyo maalum ya huduma za ardhi kwa lengo la kusikiliza na kutatua kero mbalimbali za wananchi zinazohusu masuala ya ardhi, hususan umilikishwaji wa ardhi na upatikanaji wa hati.

Kambi hiyo maalum ya siku sita ijulikanayo kama Samia Ardhi Kliniki ilianza rasmi Machi 2 na inatarajiwa kuhitimishwa Machi 7, 2026.

Friday, March 6, 2026

UMILIKI RASILIMALI KWA WANAWAKE WAPUNGUZA VITENDO VYA UKATILI

SERIKALI imeweka mazingira wezeshi ikiwa ni pamoja na umiliki rasilimali ili kupunguza vitendo vya ukatili kwa wanawake kuelekea Dira ya Maendeleo ya mwaka 2050.

Akizungumza wakati wa sherehe za Siku ya Wanawake Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Pwani Hawa Mchafu amesema uwepo wa mazingira hayo unaondoa ukatili wa kijinsia.

Mchafu amesema kuwa uwepo wa usawa na kulinda kulinda haki za wanawake kuna mchango mkubwa katika suala la maendeleo.

"Usawa wezeshi hiyo ni nyenzo muhimu ili kuketa utandaji wa pamoja wa kufikia malengo ya dira ya maendeleo na kuongeza ushiriki wanawake kwenye masuala muhimu yakiwemo ya uongozi,"amesema Mchafu.

Amesema kuwa dhumuni la kuwarudisha wasichana waliopata mimba wakiwa shuleni ni kutimiza ndoto zao kwani siyo wote waliopata ujauzito kwa kupenda au tamaa bali ni kutokana na mazingira wanayoishi na wengine wamepewa na ndugu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dk Rogers Shemwelekwa aesma kuwa asilimia 70 ya watumishi ni wanawake menejimenti idara tano zinaongozwa na wanawake ambapo wanafanya kazi nzuri ikiwemo kwenye zoezi la ukusanyaji mapato.

Shemwelekwa amesema kuwa wamewawezesha wanawake wenye biashara ndogo ndogo kuunda vikundi ambapo walikuwa hawakopesheki lakini sasa wamekopeshwa bilioni 2 na wanarejesha vizuri.

Naye Mkuu wa Divisheni ya Maendeleo ya Jamii Leah Lwanji amesema kuwa vikundi 275 vya wanawake vimekopeshwa zaidi ya bilioni 1 ikiwa ni asilimia 94. 

Lwanji amesema kuwa majukwaa yamehamasishwa kuanzishwa miradi ya kiuchumi ili waweze kujikwamua na mpaka sasa zimekopeshwa milioni 70 kwa akinamama wa majukwaa.

Moja ya kikundi ambacho ni cha mfano cha Lulu ya Wajane mwaka jana kilipata mkopo wa shilingi milioni 46 ambapo walipaswa kurejesha mkopo huo kwa miaka mitatu lakini kimeweza kurejesha ndani ya miezi 11.

Kiongozi wa kikundi hicho Kanyenda Mweri amesema kuwa fedha hizo za mikopo isiyokuwa na riba zimewasaidia kuwakwamua kiuchumi na kuweza kutoa ajira kwa wanawake wenzao.

Thursday, March 5, 2026

MAOFISA USAFIRISHAJI WATAKIWA KUUNDA VIKUNDI WAKOPE HALMASHAURI





MAOFISA Usafirishaji maarufu kama Bodaboda kwenye Mtaa wa Mwendapole B wametakiwa kuunda vikundi ili waweze kukopa vyombo vya usafiri vinavyotolewa na Halmashauri kuachana na mikopo ya taasisi za watu binafsi ambazo zina gharama kubwa.

Aidha alisema kuwa gharama za mikopo ya Halmashauri ni ndogo na marejesho yake ni madogo tofauti na mikopo ya vyombo hivyo kwenye taasisi au watu binafsi.

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti wa Mtaa huo Abubakar Matumla wakati wa kikao na waendesha pikipiki wa Mtaa huo na kuwa wanashindwa kufanikiwa kwa kukopa pikipiki kwa riba kubwa.

Matumla alisema kuwa gharama za kukopa pikipiki kwa watu binafsi imekuwa ikiwafanya wasifanikiwe kutokana na gharama kuwa kubwa za mikopo hiyo hivyo hujikuta wanashindwa kujiongezea kipato.

"Serikali imewawekea mazingira mazuri ya mikopo yake kwani mnauwezo wa kukopa pikipiki, bajaji na Toyo kwa gharama nafuu na unarejesha kiasi kilekile ulichokopa na hakuna riba ya mkopo unaokopa hivyo ni wakati wenu wa kujiunga na kuwa na vikundi na mtumie fursa ya mikopo pale Halmashauri fedha zipo za kutosha na vyombo vya moto vipo,"alisema Matumla.

Alisema kuwa yuko tayari kuwasimamia kuhakikisha wanapata mikopo hiyo kwani hapendi kuona waendesha pikipiki wakitaabika ili hali kuna sehemu wanaweza kukopa bila ya kuwa na marejesho makubwa pia aliwataka kutoa taarifa kwa wale wanaojihusisha na vitendo vya kiuhalifu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa waendesha pikipiki hao Abdulatif Mbonganga alisema kuwa tayari wameshaanzisha kikundi kimoja na tayari kimeshasajiliwa kikiwa kinasubiri wakati ukifika waende kukopa.

Mboganga alisema kuwa changamoto kubwa kwao ni kukosa vyombo vya usafiri hali inayowabidi kukopa vyombo hivyo kwenye taasisi za watu binafsi ambazo zinagharama kubwa na kujikuta wakitumia nguvu kubwa kwenye marejesho.

Moja ya maofisa usafirishaji Salum Msaku alisema kuwa changamoto ya uhalifu inatokana na baadhi yao kuwapa ma "day worker" hasa nyakati za usiku ambapo wanawaletea sifa mbaya.

Msaku alisema kuwa ili kudhibiti hali hiyo kila mwendesha pikpiki aendeshe pikipiki yake na siyo kumpa mtu mwingine pia wahakikishe wanavaa riflector ambazo zitawatambua kwa namba zinazoandikwa mgongoni inakuwa rahisi katika ufuatiliaji.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mtaa wa Miembe Saba B Nuru Awadh alisema kuwa wanapaswa kuwa na ushirikiano na kuunda vikundi vya bodaboda ili wapate mikopo nafauu.

Awadh aliwataka wajiheshimu na wasijiunge na makundi mabaya kwani Rais amewapa kipaumbele vijana katika uongozi na sehemu mbalimbali ili wawe vinara kwa utendaji kazi.

Tuesday, March 3, 2026

KAMBI SAMIA ARDHI KLINIKI YAANZA PWANI

HALMASHAURI ya Manispaa Kibaha kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeweka kambi ya Samia Ardhi Kliniki ikiwa ni maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani.

Akizungumza kuhusu huduma zinazotolewa katika kambi hiyo ya siku sita, Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Pwani Rugambwa Banyika alisema kuwa kliniki hiyo inalenga kutoa ushauri wa kisheria kuhusu masuala ya ardhi.

Banyika alisema kuwa shughuli nyingine zitakuwa ni kufanya makadirio ya pango la ardhi, kuandaa nyaraka za umiliki, kujibu changamoto za upimaji, urasimishaji, upangaji miji na michoro pamoja na kutoa hati za umiliki.

"Wananchi wote wanakaribishwa ili kupata huduma zote zihusiananazo na masuala ya ardhi ambapo huduma zimesogezwa ili kila mwananchi apate fursa katika kipindi hichi kuanzia Machi 2 hadi 7 kuelekea kilele cha siku ya Wanawake Duniani Machi 8,"alisema Banyika. 

Alisema kuwa kambi hiyo maalum ina lengo la kushughulikia changamoto mbalimbali za ardhi kwa wananchi hususan wanawake na wasichana katika masuala yanayohusiana na ardhi.

Baadhi ya wananchi Mariam Juma na Ahmed Abdala wameishukuru Serikali kwa kusogeza huduma hizo karibu yao na kueleza kuridhishwa na namna wanavyohudumiwa na wataalamu wa ardhi kwani wanatoa elimu ya kujitosheleza.

Kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani kimkoa kinatarajiwa kufanyika Machi 8 2026 katika Uwanja wa Ujamaa Kata ya Umwe Tarafa ya Ikwiriri Halmashauri ya Mji wa Rufiji ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge.