Na Allan Kitwe, Sikonge
RAIS wa Awamu ya Sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan amepeleka tabasamu kwa wakazi wa Wilaya ya Sikonge Mkoani Tabora baada ya maji safi na salama kutoka Ziwa Viktoria kufika Wilayani humo.
Shangwe na furaha za wananchi zimelipuka kwenye hafla ya kufungulia maji hayo iliyofanyika juzi katika Kata ya Misheni Mjini Sikonge kwenye eneo lilipojengwa tanki kubwa la kupokelea maji hayo ili yaanze kusambazwa kwa wananchi.
Akizungumza na mamia ya wananchi, wadau wa maendeleo na viongozi mbalimbali wa chama na serikali kwenye hafla hiyo, Waziri wa Maji Mheshimiwa Jumaa Aweso ameeleza kufurahishwa na kazi nzuri ya utekelezaji mradi huo.
Amesema kuwa mradi huo ambao unatekelezwa na Mkandarasi kutoka China kwa gharama ya shilingi bilioni 143 umelenga kufikisha huduma ya maji safi na salama katika Wilaya tatu za Urambo, Kaliua na Sikonge yenyewe.
‘Ndugu zangu wana Sikonge, Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ameleta tabasamu kwenu, alipoingia madarakani, aliahidi kumaliza kero yenu ya maji ili akinamama wasitembee na ndoo kichwani umbali mrefu na leo hii maji yamefika’, amesema.
‘Kazi iliyobakia sasa ni kuyasambaza kwa wananchi, katika hili Wataalamu ongezeni kasi, na kila wananchi atakayetaka kuunganishiwa maji nyumbani kwake hakikisheni ndani ya siku 7 awe amepata maji, si vinginevyo’, ameonya.
Aidha Waziri Aweso amemwagiza Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Mhandisi Mwajuma Waziri kuleta timu ya Wataalamu katika Wilaya hiyo ili kushughulikia mradi wa Bwawa la Utyatya ili uanze kufanya kazi ili kusaidiana na mradi huo.
Ameongeza kuwa kila Mtendaji wa Wizara hiyo anapaswa kuwa mwadilifu na mchapa kazi, Mtendaji mbabaishaji hana nafasi, hivi karibuni tutafanya tathmini ya Utendaji wa kila mmoja na kuchukua hatua kwa wanaozembea.
Amempongeza Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Tabora (TUWASA) Mhandisi Mayunga Kashilimu, RUWASA Mhandisi Hatari Kapufi, Mkuu wa Wilaya Thomas Myinga na Mbunge Amos Maganga kwa kusimamia vizuri utekelezaji mradi huo.









