Saturday, April 4, 2026

MKIMBIZA MWENGE KITAIFA AIPONGEZA STAMICO KWA KUIBEBA AGENDA YA KITAIFA YA NISHATI SAFI


*STAMICO YASHIRIKI UZINDUZI WA MWENGE WA UHURU KITAIFA PEMBA.* 

▪️Mkimbiza Mwenge Kitaifa aipongeza STAMICO kwa kuibeba ajenda ya kitaifa ya Nishati Safi.

▪️Atoa msisitizo kwa Taasisi na Shule Mkoani Kusini Pemba kutumia Nishati ya Rafiki Briquettes 

▪️Nishati Safi ya Rafiki Briquettes  kuanza kuuzwa Kisiwani Pemba

▪️Dkt. Mwasse: STAMICO kuwawezesha kontena wanawake na Samia Mkoa wa Kusini Pemba 

Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) limeshiriki katika uzinduzi wa Mbio za Mwenge ambazo umefanyika katika viwanja vya Gombani Kisiwani Pemba.

Mgeni Rasmi katika Uzinduzi huo alikuwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Tukio hilo pia lilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

STAMICO imewakilishwa na Dkt Venance Mwasse, Mkurugenzi  Mtendaji ambaye aliambatana na baadhi ya maafisa kutoka kitengo cha Masoko na Mahusiano.

Katika mbio za mwaka huu za Mwenge wa Uhuru, kauli mbiu ni: “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Maendeleo.” Kauli mbiu hiyo inalenga kuhamasisha umoja, ushirikiano na mshikamano wa Watanzania katika kuchangia maendeleo ya Taifa. Mbio hizi zinatarajiwa kuendelea katika mikoa mbalimbali ya nchi, Tanzania Bara na Visiwani.

Sambamba na uzinduzi huo, pia kumefanyika maonesho ya Taasisi mbalimbali za Serikali na sekta binafsi yaliyolenga kutoa elimu na kuonesha huduma mbalimbali kwa wananchi.

 Katika maonesho hayo, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) nalo limeshiriki kwa kuonesha bidhaa na huduma zake kwa Wananchi.

Awali, Mwenyekiti wa Kikundi cha Wanawake na Samia Mkoani Kusini Pemba Bi Sabra Masoud Ally alimpongeza Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO  kwa ulezi na ushirikiano unaotolewa na STAMICO katika kuwawezesha kushiriki katika shughuli mbalimbali za kiuchumi na usambazaji wa nishati safi ya Rafiki briquettes.

Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Mwasse aliahidi kuendelea kusaidia kikundi hicho kwa kuwapatia kontena  mwezi huu wa nne, ili yaweze kutumika kama vituo vya kuuzia nishati safi ya kupikia ya Rafiki Briquettes. Aidha, alisisitiza kuwa STAMICO itaendelea kufanya uhamasishaji mkubwa wa matumizi ya nishati hii safi katika mikoa ya Kaskazini na Kusini  Pemba, kwa lengo la kulinda mazingira na kupunguza matumizi ya kuni na mkaa wa kawaida.

Akitembelea banda la STAMICO,Mkimbiza Mwenge kitaifa,Ndugu Wazo Mwangonda aliipongeza STAMICO kwa kubeba kikamilifu ajenda ya Kitaifa ya nishati safi na Kusisitiza taasisi na Shule za Mkoa wa Kusini Pemba kutumia Nishati ya Rafiki Briquettes.

STAMICO  inaendelea na azma yake ya kuwa kinara katika kuhamasisha matumizi  ya Nishati Safi kwa kutekeleza kwa vitendo ajenda muhimu za Serikali.

Thursday, April 2, 2026

CCM PWANI YAISHUKURU SERIKALI YA DK SAMIA SULUHU HASSAN FEDHA MIRADI YA MAENDELEO

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Pwani umeishukuru serikali inayoongozwa na Dk Samia Suluhu Hassan kwa kuuongezea Mkoa bajeti ya fedha za miradi ya maendeleo na kufikia kiasi cha shilingi bilioni 497.1 mwaka 2026/2027.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Katibu wa Siasa Uenezi na Mafunzo wa CCM Mkoa wa Pwani Dk David Mramba alisema kuwa hiyo inaonyesha jinsi gani serikali inavyojali maendeleo ya wananchi.

Alisema kuwa fedha hizo zimeongezeka kutoka kiasi cha shilingi bilioni 473 bajeti ya mwaka 2025/2026 hivyo kufanya Mkoa kupiga mbele hatua za maendeleo.

"Fedha hizi zinakwenda kukabili changamoto mbalimbali ambazo zinawakabili wananchi kwenye huduma muhimu za kijamii ambapo zinatoa majawabu,"alisema Mramba.

Alisema kuwa baadhi ya miradi ikiwemo huduma za maji zimeboreshwa ambapo wananchi wanapata maji safi na salama ikilinganishwa na miaka ya nyuma.

"Kwa upande wa elimu madarasa mengi yamejengwa, maabara za kutosha ili kuinua masomo ya sayansi, ujenzi wa vyoo, mabweni, nyumba za walimu na madawati,"alisema Mramba.

Aidha alisema kuwa kwa upande wa huduma za afya nazo zimeboreshwa kwani Hospitali za Rufaa, Hospitali, Zahanati na huduma za kibingwa zinatolewa hapa hapa nchini badala ya kwenda nje ya nchi.

"Kuhusu miundombinu barabara nyingi zimejengwa na kurahisisha shughuli za kiuchumi huku mazao na bidhaa zikisafirishwa kwa urahisi ambapo mikoa na wilaya zinaingiliana kwa urahisi,"alisema Mramba.

Aliongeza kuwa kuna baadhi ya changamoto ambazo zinafanyiwa kazi kwa kuendelea kutengewa bajeti ili kuhakikisha huduma za msingi kwa wananchi zinapatikana kwa urahisi.

Sunday, March 29, 2026

KITUO CHA WANAWAKE WAJASIRIAMALI MANISPAA YA KIBAHA KUJENGA KIWANDA CHA KUTENGENEZEA BATIKI

NGUO za Batiki zimekifanya Kituo cha Wanawake Wajasiriamali Manispaa ya Kibaha kuitangaza Tanzania kwenye soko la Kimataifa ambapo ziliongoza kwa kununuliwa kwenye maonyesho nchi jirani. 

Akizungumza ofisini kwake Mjini Kibaha Mwenyekiti wa Kituo hicho Dk Magdalena Mangi alisema kuwa walishirki maonyesho kwenye nchi za Sudan, Kenya na Burundi miaka ya hivi karibuni ambapo zilinunuliwa kwa wingi.

Mangi alisema kufuatia batiki zao kuwa na soko kubwa wamejipanga kuanzisha kiwanda cha utengenezaji wa batiki ili kuongeza ubora wa bidhaa hiyo ili kuendelea kuitangaza nchi wanapokwenda kwenye maonyesho kama hayo siku za baadaye kwani wamedhamiria kuzalisha bidhaa zenye ubora.

Mangi alisema kuwa kwa sasa wanazalisha batiki kwa kutumia mikono hali inayofanya ubora kupungua lakini wanaamini wakitumia mashine wataongeza ubora.

"Batiki tunazozalisha ni nzuri kwani tunatumia vitamba vizito ambavyo havichuji tofauti na wazalishaji wengine hali ambayo inatufanya tupate soko maeneo mbalimbali ambapo ushiriki kwenye nchi Burundi mwaka 2023, Sudan Kusini 2024, na Kenya 2025  tulipata mafanikio makubwa,"alisema Mangi.

Alisema kuwa wamekuwa wakipata masoko maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na watu binafsi na taasisi zikiwemo za watu binafsi na za serikali.

"Tuna soko japo siyo kubwa sana lakini tunataka tujitanue kwa kujitangaza kwa kutumia vyombo vya habari pamoja na mitandao ya kijamii ili kuwafikia wateja wengi,"alisema Mangi.

Aidha alisema kuwa changamoto inayowakabili ni mtaji ambapo wakipata fedha watahakikisha wanajenga kiwanda ili kuongeza ubora wa batiki zao.

"Tulikopa Halmashauri kiasi cha shilingi milioni 40 ambapo bado tunaendelea na marejesho na tunahitaji sehemu ya kutengenezea batiki kwani hapa eneo ni dogo hali inayofanya tutengenezee nyumbani,"alisema Mangi.

Aliongeza kuwa wanaishukuru serikali kwa kuendelea kuwawezesha ili waweze kufanya shughuli zao katika mazingira mazuri na kuwawezesha hata kwa mikopo ya asilimia 10 ili kukuza biashara zao.

Naye Simon Kiondo mkufunzi wa masuala ya fedha na ujasiriamali alisema kuwa alikipatia elimu ya biashara mtandaoni ili kupata masoko zaidi kwani hiyo ni moja ya njia za kuongeza wateja.

Kiondo alisema kuwa baadhi ya changamoto ya vikundi vya ujasiriamali ni kukosa mipango na malengo na utunzaji wa kumbukumbu na ukosefu wa elimu ya fedha.

Alisema kuwa wajasiriamali wanapaswa kujitangaza na kwenda na wakati kwa kutumia teknolojia ya kisasa kupitia mitandao ya kijamii kuvutia masoko.

Kituo hicho kina jumla ya wanachama 10 na kinajohusisha na uzalishaji wa batiki, sabuni, mafuta mbalimbali, urembo, ushonaji nguo na khanga.

Thursday, March 26, 2026

PROGRAM YA MALEZI MAKUZI NA MAENDELEO YA AWALI YA MTOTO YAPATA MAFANIKIO






PROGRAM ya Malezi Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto imeleta manufaa makubwa kwa kuanzishwa kadi ya alama kwa watoto inayorahisisha ufuatiliaji.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Mkurugenzi wa Shirika lisilo kuwa la Kiserikali la Anjita Child Development Foundation Janeth Malela wakati wa kikao cha wadau wa Program hiyo Mkoa wa Pwani.

Malela amesema kuwa kuanzishwa kwa kadi hiyo kwa watoto ni mafanikio makubwa ya Program hiyo katika kuhakikisha ustawi wa watoto katika makuzi yake.

Amesema kuwa kikao hicho kiliweza kujadili masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na kufanya uchechemuzi wa umuhimu wa kuwekeza kwenye Program hiyo na kusaidia serikali kutekeleza Program za malezi.

"Kuendelea kushirikiana na wadau wa nje katika kuwekeza katika malezi kuhamasisha jamii na serikali katika kuanzisha vituo vya kulea watoto wadogo mchana vya jamii,"amesema Malela.

Msajili wa mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali Elia Kabora amesema kuwa uwekezaji kwa watoto ni moja ya vipaumbele ili kuhakikisha makuzi ya watoto yanazingatia upatikanaji wa huduma muhimu.

Kabora amesema kuwa Programu hiyo inalenga kuimarisha utoaji huduma bora za Afya, Lishe, Malezi yenye Mwitikio, ujifunzaji wa Awali na Ulinzi na Usalama kwa watoto wa miaka 0 hadi 8 na kuimarisha ushirikiano wa wadau wa sekta mbalimbali.

Makamu Mwenyekiti wa Mtandao wa Mashirika yasiyo kuwa ya Kiserikali Kibaha Mjini (KITAN) Dk Rose Mkonyi amesema kuwa jamii kwa kushirikiana wadau wengine wanapaswa kuhakikisha watoto wanapata mahitaji muhimu ili waweze kupata huduma muhimu.

Mkonyi amesema kuwa wadau wanapaswa kuungana kufanikisha Program hiyo ili kuweza kufanikisha ukuaji na maendeleo ya mtoto kikamilifu kimwili, kiakili, kukuza lugha, mawasiliano kijamii na kihisia. 

Walengwa wa mradi huo walioshiriki kikao hicho ni pamoja na wazazi, walezi, mashirika yasiyokuwa ya kiserikali, viongozi wa dini na wataalam wa ngazi ya serikali.

mwisho.

Sunday, March 22, 2026

UKUWAWAVI WATOA MISAADA KITUO CHA YATIMA BULOMA


UMOJA wa Kusaidiana Wanajeshi Wastaafu wa Vifaru (UKUWAWAVI) wametoa msaada wa vitu mbalimbali kwenye Kituo cha Kulea Yatima cha Buloma.
Wametoa misaada hiyo ikiwa ni sehemu ya kusherehekea Sikukuu ya Iddi el Fitri na Mfungo wa Kwaresma.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukabidhi misaada hiyo Mwenyekiti wa (UKUWAWAVI) SSGT Omari Makore amesema kuwa wameguswa kuwasaidia watoto hao ili nao waweze kufurahi kama walivyo watoto wanaoishi na familia zao.

Makore amesema wanajua kuwa watoto hao wana mahitaji mengi lakini wameona
waanze na kidogo walichojaliwa na hiyo ni sadaka na wataendelea kusaidia pale watakapojaliwa wakati mwingine.

"Tutarudi tena kwani watoto hawa wametuonyesha mapenzi makubwa na huu ni mfano na vikundi na watu mbalimbali nao wajitokeze kuwasaidia watoto hawa,"amesema Makore.

Kwa upande wake Mlezi wa (UKUWAWAVI) Brigedia Jenerali Rajabu Hanti (Mstaafu) amesema kuwa watoto hao ni Taifa la kesho wanahitaji malezi ya watu.

Hanti amesema kuwa watoto hao wanapaswa kupelekewa furaha kwa kuwashika mkono kwa misaada mbalimbali ambayo ni mahitaji yao ya msingi.

Naye Mchungaji Jackson Bukelebe amesema kuwa umoja huo umechukua jukumu la kidini kwani dini bora ni ile inayojali yatima watu wanapaswa kujotolea kuwasaidia watoto hao.

Mwasisi wa kituo hicho Anna Kyando amesema kuwa wanashukuru kwa misaada hiyo kwani wadau ndiyo wamekuwa wakiendesha kituo hicho kwani bila wao peke yake asingeweza.

Kyando amesema kuwa changamoto kubwa ni chakula kwani ndicho kinachohitajika muda wote uzio wa ukufa, vifaa vya shule, ada kwa wanafunzi walioko vyuoni kutoka kituo hicho.

Moja ya watoto wa kituo hicho Yohana Almas amesema kuwa wanashukuru kwa misaada hiyo na kuahidi kufanya vizuri kwenye masomo yao na kuomba watu waendelee kuwasaidia.

Baadhi ya vitu vilivyotolewa ni pamoja na mchele kilo 100, unga wa sembe kilo 50, maharage kilo 50, mafuta lita 20, madaftari 100, juisi katoni 5, maji katoni 10, doti 5 za khanga, sabuni za unga, taulo za kike na biskuti.

Saturday, March 21, 2026

DA ARUL ARQAM LEARNING CENTRE (DAALC) KUJENGA HOSPITALI YA KISASA.

TAASISI ya DA ARUL ARQAM LEARNING CENTRE (DAALC) ya Kibaha Mkoani Pwani inatarajia kujenga kituo cha taasisi chenye huduma mbalimbali za kijamii kikiwa ni pamoja Hospitali ya kisasa kwa gharama za shilingi bilioni 5.5.


Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mwalimu wa Taasisi hiyo Karume Amri Abeid amesema kuwa kituo hicho kitajengwa eneo la Boko Wilaya ya Kibaha.

Abeid amesema kuwa eneo hilo ndilo litakalokuwa makao makuu ya Taasisi ambalo lina ukubwa wa hekari 11 na tayari nyumba ya mlinzi tayari imejengwa kwa ajili ya maandalizi ya ujenzi.

"Eneo hilo pia kutajengwa ofisi, Msikiti, shule ya awali hadi elimu ya juu yaani kidato cha sita, chuo cha elimu ya dini Ibtidai mpaka Thanawi, kituo cha kuhifadhisha Quran kwa watoto kuanzia miaka 5 na kuendelea,"amesema Abeid.

Amesema kuwa njia watakayoitumia kupata fedha ni michango mbalimbali toka kwa wadau, waumini na kufanya harambee ambapo hadi sasa wamekusanya kiasi cha shilingi milioni 2.

"Huduma zikiwemo za afya zitatolewa kulingana na jinsi badala ya huduma kutolewa na jinsi tofauti na wanufaika kwenye sekta ya afya na ajira haitajali dini bali ni kwa dini zote kwani lengo ni kutoa huduma bora na za kisasa,"amesema Abeid.

Aidha amesema kuwa matarajio ni kuanza ujenzi Januari mwakani mara fedha zitakapopatikana na kikubwa wadau mbalimbali wajitokeze kuchangia fedha ili kufanikisha ujenzi huo kwani watu wajitoe kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na kujenga ahera yetu.

Akizungumzia kuhusu sikukuu ya Iddi amesema kuwa siyo kuvaa vizuri na kupendeza bali ni kwa yule mwenye kumuogopa Mwenyezi Mungu na kukumbuka siku ya hesabu (Kiyama) ndiyo maana ya Iddi.

Ameongeza kuwa watu wamwabudu Mwenyezi Mungu na kuacha kumkasirisha na waishi maisha haya na si wakati wa mfungo peke yake ili wasimkosee.

DA ARUL ARQAM LEARNING CENTRE (DAALC) KUJENGA HOSPITALI YA KISASA.

TAASISI ya DA ARUL ARQAM LEARNING CENTRE (DAALC) ya Kibaha Mkoani Pwani inatarajia kujenga kituo cha taasisi chenye huduma mbalimbali za kijamii kikiwa ni pamoja Hospitali ya kisasa kwa gharama za shilingi bilioni 5.5.


Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mwalimu wa Taasisi hiyo Karume Amri Abeid amesema kuwa kituo hicho kitajengwa eneo la Boko Wilaya ya Kibaha.

Abeid amesema kuwa eneo hilo ndilo litakalokuwa makao makuu ya Taasisi ambalo lina ukubwa wa hekari 11 na tayari nyumba ya mlinzi tayari imejengwa kwa ajili ya maandalizi ya ujenzi.

"Eneo hilo pia kutajengwa ofisi, Msikiti, shule ya awali hadi elimu ya juu yaani kidato cha sita, chuo cha elimu ya dini Ibtidai mpaka Thanawi, kituo cha kuhifadhisha Quran kwa watoto kuanzia miaka 5 na kuendelea,"amesema Abeid.

Amesema kuwa njia watakayoitumia kupata fedha ni michango mbalimbali toka kwa wadau, waumini na kufanya harambee ambapo hadi sasa wamekusanya kiasi cha shilingi milioni 2.

"Huduma zikiwemo za afya zitatolewa kulingana na jinsi badala ya huduma kutolewa na jinsi tofauti na wanufaika kwenye sekta ya afya na ajira haitajali dini bali ni kwa dini zote kwani lengo ni kutoa huduma bora na za kisasa,"amesema Abeid.

Aidha amesema kuwa matarajio ni kuanza ujenzi Januari mwakani mara fedha zitakapopatikana na kikubwa wadau mbalimbali wajitokeze kuchangia fedha ili kufanikisha ujenzi huo kwani watu wajitoe kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na kujenga ahera yetu.

Akizungumzia kuhusu sikukuu ya Iddi amesema kuwa siyo kuvaa vizuri na kupendeza bali ni kwa yule mwenye kumuogopa Mwenyezi Mungu na kukumbuka siku ya hesabu (Kiyama) ndiyo maana ya Iddi.

Ameongeza kuwa watu wamwabudu Mwenyezi Mungu na kuacha kumkasirisha na waishi maisha haya na si wakati wa mfungo peke yake ili wasimkosee.