BENKI ya NMB imeingia mkataba wa udhamini wa maonyesho ya mifugo ya (Tri-Nations Livestock Expo) kwa kiasi cha shilingi milioni 300 kwa kipindi cha miaka mitatu.
Mkataba huo umeshuhudiwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dk Fabian Madele kwenye Shamba la Mifugo la Mbogo lililopo Ubena Halmashauri ya Chalinze Wilaya ya Bagamoyo ambapo maonyesho hayo mwaka huu yatafanyika Juni 19 hadi 21.
Madele alisema kuwa maonyesho hayo ni muhimu kwani kwani yanaleta tija kwenye ufugaji kuimarisha ushirikiano kukuza teknolojia kwenye sekta ya ufugaji kukuza masoko ya ndani na nje kwani soko la nje ni kubwa sana.
"Malengo ifikapo 2030 kufikia uuzaji wa tani 50 kwa soko la nje ambalo ni kubwa sana hasa la Mshariki ya Kati na China hivyo lazima tutumie fursa kama hizi kuboresha ufugaji wetu ili uakisi uwingi wa mifugo yetu,"alisema Madele.
Alisema kuwa Tanzania ni ya pili kwa kuwa na mifugo mingi ikiwa na ngombe zaidi ya milioni 35 ma mbuzi milioni 28 hivyo lazima tafsiri ya idadi iendane na mapato.
"Tuwavutie vijana ili wajikite kwenye ufugaji kwani endapo nguvu itawekezwa itainua uchumi wa nchi na ili kufika huko ni kufuga kwa utaalamu kwani maofisa mifugo wamesambazwa kila mahali kikubwa ni kujenga mahusiano mazuri,"alisema Madele.
Kwa upande wake mwakilishi wa benki hiyo kupitia Mkuu wa Idara ya Kilimo Biashara wa Benki ya NMB Nsolo Mlozi alisema kuwa mwaka jana walidhamini maonyesho hayo kwa kiasi cha milioni 30 ambayo hufanyika kila mwaka.
Mlozi alisema kuwa udhamini huo ni wa miaka mitatu na ni sehemu ya kuboresha sekta hiyo ya ufugaji ambapo pia hutoa fursa za mikopo kwa wafugaji ambapo hadi sasa imetoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 130.
Alisema kuwa mbali ya kutoa mikopo pia inatoa elimu ya fedha, ushauri na masoko kwa wafugaji ili kuweza kukabiliana na changamoto mbalimbali ambapo imeweka mameneja mahusiano wanaoshughulikia wafugaji.
Naye Mkurugenzi wa Shamba la Mifugo la Mbogo Naweed Mulla alisema kuwa maonyesho hayo yamekuwa na mafanikio makubwa ambapo wafugaji wengi walijitokeza kushiriki na mwaka huu wataongezeka zaidi wakiwemo wafugaji toka nchi mbili jirani.
Mulla alisema kuwa mwaka huu wameongeza kipengele cha ufugaji wa kuku kwa upande wa wanawake ambapo kutakuwa na mshindi ambaye atatambulika kama Malkia wa ufugaji.
Mwenyekiti wa Chama Cha Wafugaji Mrida Maroche alisema kuwa wanapongeza uwekezaji unaofanyika kwenye mifugo kwani unapandisha thamani ya mifugo yao na watatumia fursa mbalimbali ili kuongeza uzalishaji kwa kuzingatia viwango ili kukabili soko la nje.
Maroche alisema kuwa mfano mzuri ni baadhi ya ngombe waliopo kwenye Shamba la Mbogo ngombe wa miaka miwili ana uzito wa kilogramu 350 na ndama wa miezi mitano ana uzito wa kilogramu 180 ambapo hayo ni mabadiliko makubwa.









