Wednesday, May 27, 2026

WATAKIWA KUWA NA UTII KAMA WA IBRAHIM

WATANZANIA wametakiwa kufuata maandiko ya vitabu vya dini vinavyoelezea juu ya utii wa Ibrahim ambaye alimuamini Mungu na kumbariki katika maisha yake.

Hayo yalisemwa na Ustaadh Mahamudu Lipambila ambaye ni katibu wa Msikiti wa Masjid Hadharaj Mzimuni Maili Kibaha Mkoani Pwani wakati wa Maadhimisho ya Sikukuu ya Kuchinja (EIDY L ADHUHAA) inayoadhimishwa ulimwenguni kote.

Lipambila alisema kuwa hadhithi ya Ibrahim ambayo ilimtaka amchinjie mwanae ili awe sadaka ambapo ndiyo chimbuko la sikukuu hiyo kubwa kwa imani ya Kiislamu.

"Ibrahim alionyesha utii kwa Mungu kwa kutaka kumtoa mwanae wa pekee ili awe sadaka ya kuchinjwa na alipokubali Mungu kwa kupitia Malaika alimletea kondoo na ndiyo akachinjwa kuwa sadaka,"alisema Lipambila.

Alisema kuwa hadithi hiyo inafundisha jinsi gani watu wanapaswa kuwa na utii juu ya imani zao na kufuata mafundisho ya Mwenyezi Mungu ambayo yatafanya watu waishi kwa kuthaminiana.

"Pia hadithi inafundisha wazazi kuwa na kiasi katika upendo juu ya watoto wao ambapo wengine wamekuwa chanzo cha mmomonyoko wa maadili kwa kutaka kuwafurahisha badala ya kumpenda zaidi Mungu kwa kufuata mafundisho yake,"alisema Lipambila.

Aidha alisema kuwa sikukuu hiyo ni ya furaha kwa kuhakikisha jamii yote inakuwa na furaha kwa kuwa na utii juu ya Mwenyezi Mungu na wanapaswa kumpenda Mungu zaidi.

"Watu waishi kama ilivyokuwa makusudio ya Mungu kutuumba na wakizingatia hayo wataishi kwa amani na upendo na hakutakuwa na tofauti za kimitazamo hasi ya kimaendeleo,"alisema Lipambila.

Aliongeza kuwa viongozi wanapaswa kuwa na hekima na utii kama aliokuwa nao Ibrahim ambaye dini zote zinamuona kama kielelezo cha imani zao kwa Mwenyezi Mungu.

Tuesday, May 26, 2026

WATENDAJI KATA WATAKIWA KUPAMBANA KUONGEZA MAPATO

WATENDAJI wa Kata Mkoani Pwani wametakiwa kumsadia Rais kwenye suala la ukusanyaji wa mapato ili yaweze kuleta maendeleo kwa wananchi ili kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge wakati wa Kikao kazi cha watendaji wa Kata wa Mkoa huo kilichofanyika Kibaha.

Kunenge alisema kuwa Mkoa kwa sasa unafanya vizuri kwenye suala la ukusanyaji wa mapato hapa nchini kutokana na kuweka mazingira mazuri kwa kwenye maeneo ya vyanzo vya mapato.

"Nyie ni watu muhimu sana na serikali ingependa kuona mnaendana na Dira ya Maendeleo ya Taifa ambayo inataka pato la mtu lifikie dola 7,000 kwa mwaka na la nchi trilioni 1 hadi ifikapo mwaka 2050,"alisema Kunenge.

Alisema wakati anafika kwenye Mkoa huo ulikuwa ni moja ya mikoa iliyokuwa chini kimapato ikiwa ni Mkoa wa 23 lakini kwa sasa umeweza kuinuka kimapato.

"Mnapofanya shughuli zenu mhakikishe mnazingatia Dira ya Maendeleo ya Taifa inaweka mazingira mazuri kwa sekta binafsi ili iendeshe uchumi kuzalisha ajira kuongeza thamani ya mazao na kuuza nje ya nchi,"alisema Kunenge.

Alisema kuwa sekta binafsi ni ya kimageuzi ili kuwe na mabadiliko ambapo asilimia 70 ya maendeleo inatokana na sekta binafsi hivyo lazima kuweka mazingira mazuri hasa ikizingatiwa Mkoa wa Pwani ni moja ya mikoa yenye viwanda vingi.

"Watendaji wa kata ni muhimu kwani ni sehemu muhimu ya maendeleo na mabadiliko hivyo hawapaswi kufanya kazi kwa mazoea kwani dunia inabadilika,"alisema Kunenge.

Aidha alisema kuwa wasiamini kwenye kushindwa bali waamini kwenye kushinda kwani wanatakiwa kuongeza thamani na  hawapaswi kulala kama anavyofanya Rais Dk Samia Suluhu Hassan ambaye halali ili kuhakikisha wananchi wanapata maendeleo.

Alibainisha kuwa watendaji hao wanapaswa kupunguza kero na rasilimali zinazopatikana zitumike kwa kuzingatia vipaumbele vya eneo husika na waongeze mapato ya ndani ili nchi iweze kujitegemea.

Nao watendaji hao walisema kuwa watahakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa kushirikiana na viongozi wao na wadau ili kufikia malengo hayo yaliyowekwa ili kuleta maendeleo.

Monday, May 25, 2026

PWANI YAONGEZA MAPATO YA MKOA

MKOA wa Pwani umeongeza ukusanyaji wa mapato kutoka asilimia 87.9 Juni kwa mwaka 2025 na kufikia asilimia 106 Machi mwaka 2026.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge wakati wa Kikao kazi cha watendaji wa Kata wa Mkoa huo.

Kunenge amesema kuwa Mkoa unafanya vizuri kwenye suala la ukusanyaji wa mapato hapa nchini kutokana na kuweka mazingira mazuri.

"Nyie ni watu muhimu sana na serikali ingependa kuona mnaendana na Dira ya Maendeleo ya Taifa ambayo inataka pato la mtu lifikie dola 7,000 kwa mwaka na la nchi trilioni 1 hadi ifikapo mwaka 2050,"amesema Kunenge.

Amesema wakati anafika kwenye Mkoa huo ulikuwa ni moja ya mikoa iliyokuwa chini kimapato ikiwa ni Mkoa wa 23 lakini kwa sasa umeweza kuinuka kimapato.

"Mnapofanya shughuli zenu mhakikishe mnazingatia Dira ya Maendeleo ya Taifa inaweka mazingira mazuri kwa sekta binafsi ili iendeshe uchumi kuzalisha ajira kuongeza thamani ya mazao na kuuza nje ya nchi,"amesema Kunenge.

Amesema kuwa sekta binafsi ni ya kimageuzi ili kuwe na mabadiliko ambapo asilimia 70 ya maendeleo inatokana na sekta binafsi hivyo lazima kuweka mazingira mazuri hasa ikizingatiwa Mkoa wa Pwani ni moja ya mikoa yenye viwanda vingi.

"Watendaji wa kata ni muhimu kwani ni sehemu muhimu ya maendeleo na mabadiliko hivyo hawapaswi kufanya kazi kwa mazoea kwani dunia inabadilika,"amesema Kunenge.

Aidha amesema kuwa wasiamini kwenye kushindwa bali waamini kwenye kushinda kwani wanatakiwa kuongeza thamani na  hawapaswi kulala kama anavyofanya Rais Dk Samia Suluhu Hassan ambaye halali ili kuhakikisha wananchi wanapata maendeleo.

Alibainisha kuwa watendaji hao wanapaswa kupunguza kero na rasilimali zinazopatikana zitumike kwa kuzingatia vipaumbele vya eneo husika na waongeze mapato ya ndani ili nchi iweze kujitegemea.

Sunday, May 24, 2026

MTAA WA MWENDAPOLE B MBIONI KUANZA ULINZI SHIRIKISH KUKABILI UHALIFUI

WANANCHI wa Mtaa wa Mwendapole B Wilayani Kibaha wamekubaliana kuanza kufanya ulinzi shirikishi ili kukabiliana na vitendo vya kihalifu ndani ya Mtaa huo..

Akizungumza na wananchi wakati wa kikao cha Mtaa kilichofanyika kwenye ofisi za Mtaa huo Mwenyekiti wa Mtaa Abubakar Matumla alisema kuwa kabla ya kuanza kamati itakaa ili kuangalia namna ya kufanya ulinzi huo.

Matumla alisema tayari wameshapata kibali cha kuwa na ulinzi shirikishi na kinachofuata ni kupanga namna ya kufanya zoezi hilo na namna wananchi watakavyo changia watu watakaokuwa wakilinda.

"Tunamshukuru Mkuu wa Wilaya tayari katoa kibali cha Mtaa kuwa na ulinzi shirikishi ili kukabiliana na vitendo vya uhalifu ambavyo vimekuwa vikijitokeza nyakati tofauti tofauti,"alisema Matumla.

Alisema kuwa watakaa na kamati ya Mtaa wiki hii ili kupanga utaratibu mzuri wa kuanza zoezi hilo na kiwango cha kila kaya kuchangia ili kuwalipa walinzi hasa ikizingatiwa michongo ya ulinzi shirikishi ni hayari.

Aidha alisema kuwa wenye nyumba nao wsnapaswa kuwa makini kwa kuwa na taarifa za kutosha za wapangaji wao kwani baadhi yao wanaweza kuwa wanajihusisha na uhalifu.

Naye Diwani wa Kata ya Kibaha Omary Bulla alisema kuwa ulinzi shirikishi ni muhimu sana kwani baadhi ya vijana ambao siyo waaminifu wamekuwa wakiiba vitu kwenye nyumba au kukaba watu.

Bulla alisema kuwa ili kufanikiwa wananchi wanapaswa kushiriki kikamilifu kwa kutoa michango ili iwezeshe walinzi waweze kufanya kazi zao bila ya vikwazo na kukabili uhalifu ndani ya Mtaa huo.

Kwa upande wake mmoja wa wananchi wa Mtaa huo Dago Mwombeki alisema kuwa baadhi ya vijana wamekuwa wakiwapora watu wanaokuwa wanakwenda kazini alfajiri au wanapokuwa wanatoka kazini.

Mwombeki alisema kuwa ulinzi shirikishi utasaidia kukabili changamoto hiyo ya uhalifu ndani ya Mtaa kwani wanasababisha watu wasiishi kwa amani na kurudisha nyuma maendeleo ya watu.

Saturday, May 23, 2026

NG'OMBE 28 WA WIZI WAKAMATWA

JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani kupitia Kikosi cha Kuzuia Wizi wa Mifugo (STPU) linashikiliwa watu wanne tuhuma za wizi wa ng'ombe 28.

Akizungumza na Waandishi wa Habari ofisini kwake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani  Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Salim Morcase alisema kuwa mara baada ya upelelezi kukamilika watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani.

Morcase alisema kuwa tukio hilo lilitokea Mei 22 mwaka huu huko maeneo ya Tungutungu Mapinga Wilayani Bagamoyo ambapo kati yao ng’ombe 13 ni mali ya Fadhili Ngabilo mkazi wa Kwa Makocho Kata ya Mandela Chalinze

"Mlalamikaji Fadhili Ngabilo aliripoti katika kituo cha Polisi Chalinze kuibiwa  jumla ya ng’ombe 18 na mbuzi watano ambapo Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani kupitia Kikosi cha Kuzuia Wizi wa Mifugo(STPU) walianza ufuatiliaji,"alisema Morcase.

Alisema kuwa katika ufuatiliaji ilipofika Mei 22 majira ya saa 3:00 asubuhi walifanikiwa kuwapata ng’ombe 28 wakiwemo ng’ombe 13 kati ya 18 walioibiwa Chalinze wakiwa kwenye zizi la mfanyabiashara mmoja wa nyama.

"Kati ya ng’ombe 15 waliokutwa nyumbani kwa mtuhumiwa ng’ombe watano walitambulika na ng’ombe wanne mahojiano yanaendelea,"alisema Morcase.

Aidha alisema kuwa mtuhumiwa huyo huwa anachinja ng’ombe wa wizi nyumbani kwake kisha kuuza nyama kwenye bucha yake.

"Hadi sasa jumla ya watuhumiwa wanne wanashikiliwa na mara baada ya upelelezi kukamilika watafikishwa mahakamani kuhusiana na tukio hilo,"alisema Morcase.

Alitoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa sahihi kwa kadri operesheni za kudhibiti uhalifu zinavyofanyika maeneo mbalimbali ndani ya Mkoa wa Pwani.

Sunday, May 17, 2026

MBUNGE SUBIRA MGALU ATOA MSAADA KWA VITONGOJI VILIVYOKUMBWA NA MAFURIKO BAGAMOYO


MBUNGE wa Jimbo la Bagamoyo Subira Mgalu ametoa kiasi cha shilingi milioni 2 kwa Vitongoji vya kata ya Nianjema vilivyokumbwa na mafuriko.

Mgalu amesema vitongoji hivyo vilivyokumbwa na mafuriko yaliyosababisha kuharibika kwa Miundombinu ya barabara na maji kuzingira makazi na taasisi za Umma. 

Nimewapa pole , na nimewaahidi ntaendelea kuwasemea kero hii Bungeni na kwenye Mamlaka mbalimbali .

 Tangu 2018 mafuriko yalipoanza nimekuwa Kiongozi wa kwanza kuwafikia na kuwafariji # Mbunge wa Jimbo Kazini

UMOJA WA WANAUME MKOMBOZI (UWWM) KUNUNUA MABASI MAWILI

UMOJA wa Wanaume Mkombozi (UWWM) wanatarajia kununua mabasi madogo mawili ya abiria ili kukabiliana na changamoto ya usafiri kutoka na kuingia kwenye Mtaa wa Mkombozi uliyopo Wilayani Kibaha Mkoani Pwani.

Hayo yalisemwa na Katibu wa (UWWM) Mwinjilisti Williama Wami wakati wa uzinduzi wa umoja huo na Mfuko wa umoja ambapo changamoto ya usafiri ni kubwa kwani kuna basi moja tu linalofanya safari zake kati ya Mkombozi na Mbezi Jijini Dar es Salaam.

Wami alisema Mtaa huo umepakana na Wilaya ya Ubungo ambapo wanapata mahitaji yao eneo la Kibamba Njia Panda Shule kutokana na ukaribu tofauti na Kibaha ambako ni mbali.

"Wakazi huku ni wengi sana lakini tatizo kubwa ni usafiri ambapo kutokana na ubovu wa barabara magari mengi hayawezi kufika kwani kuna basi moja tu ambalo linatoa huduma lakini sisi malengo yetu ni kununua mabasi madogo mawili ili kurahisisha usafiri,"alisema Wami 

Alisema kuwa kwa sasa wanatumia usafiri wa pikipiki ili kufika majumbani au kutoka kwenda kwenye shughuli zao za kila siku kujiletea kipato lakini usafiri huo ni gharama kubwa sana.

"Kupitia umoja wetu tulihamadisha kupatikana kwa basi hilo lakini bado halikidhi mahitaji kwani uhitaji ni mkubwa sana kwani uwezo wa baadhi ya watu kupanda pikipiki kwao ni mzigo mkubwa lakini kupitia daladala gharama inakuwa nafuu,"alisema Wami.

Aidha alisema kuwa malengo yao mengine ni kujenga ukumbi mkubwa kwa ajili ya shughuli mbalimbali ikiwemo mikutano na sherehe utakaogharimu kiasi cha shilingi milioni 500 ambapo kwa sasa huwabidi kufanya shughuli hizo nje ya mtaa huo pia kuanzisha Chama Akiba na Mikopo ili kukopeshana kwa riba nafuu.

"Vitu tulivyofanya ni kuvuta maji na kujenga vyoo vya kisasa kwenye soko jipya na tunatarajia hapo kuwa na stendi tunaishukuru Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha kwa kutuanzishia soko tunaomba watupe kibali ili watu waanze kufanya biashara,"alisema Wami.

Aliongeza kuwa miradi hiyo mbali ya kutoa huduma itakuwa ni vyanzo vya mapato ya umoja kwani lengo ni kuleta maendeleo ya Mtaa na kwa mwananchi mmoja mmoja pia ni kusaidiana katika shida na raha na kauli mbiu ni Baba kichwa cha Familia.

Umoja huo ulianzishwa mwaka jana na una wanachama 265 huku wanachama hai ni 205 hadi sasa wana kiasi cha shilingi milioni 10 benki ambapo kila mwezi mwanachama huchanga shilingi 5,000.