Tuesday, June 9, 2026

LULU YA WAJANE KUANZISHA MRADI WA MINOFU YA KUKU

KIKUNDI cha Lulu ya Wajane kilichopo Kongowe Wilayani Kibaha Mkoani Pwani kinatarajia kuanzisha mradi wa uuzaji wa minofu ya kuku.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa kikundi hicho Kanyenda Mweri wakati akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea kikundi hicho ambacho kinajihusisha na ufugaji wa kuku.

Mweri amesema kuwa kikundi chao kinaundwa na wanachama watano kiliwezeshwa na Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha mkopo wa asilimia 10 kiasi cha shilingi milioni 46 ambapo tayari wameshazirejesha.

"Tumeomba mkopo mwingine wa fedha nyingi kidogo ambapo tutanunua mashine ya kuchakata minofu, mashine ya kunyonyolea kuku, mashine ya kutotolesha na kuuza vifaranga, mashine ya kusaga vyakula vya kuku na kufufua mashine ya kusaga unga,"amesema Mweri.

Amesema kuwa tayari wameshafanya utafiti juu ya soko la minofu ambapo mbali ya minofu watauza kuku na viungo vyake ikiwemo miguu, vichwa na vyote vitokanavyo na kuku.

"Uwezo wa kurejesha mkopo tutakaokopeshwa tunao kwani mkopo uliopita tulikopeshwa milioni 46 tukazirejesha mapema kabla ya muda kwani tulipewa miaka mitatu kurejesha lakini tulirejesha kwa miezi 11 tu na kupewa cheti cha wajasiriamali bora,"amesema Mweri.

Aidha amesema kuwa kutokana na mradi wa ufugaji kuku unaoendelea kila mwezi wanajilipa kiasi cha shilingi  100,000 pia wameweza kuwaajiri mabinti wa wawili ambao ni wahitimu wa vyuo wakiwa na diploma ya mifugo ambao ndiyo wanafanya shughuli za kitaalamu na kijana mmoja wa kiume.

"Tunamshukuru Mungu kwani ameweza kutuunganisha na kutupa mshikamano ambao ndiyo siri ya mafanikio yetu na ushirikiano tunaoupata kutoka kwa wataalamu wa Halmashauri na Mkurugenzi,"amesema Mweri..

Amesema kuwa walianzisha kikundi hicho kwa malengo ya kusaidiana kutatua changamoto na kutafuta fursa mbalimbali za ujasiriamali na kûwa na miradi ya kiuchumi endelevu kwani wanawake wanapofiwa na waume zao ndugu huwanyanyasa naa kuwanyanganya mali. 

"Matarajio yetu ni kuwa kikundi imara na hodari ambapo kwa sasa tayari wameanzisha kikundi cha vijana wanawake wanaojulikana kama Lulu Nazi wanaozalisha bidhaa zitokanazo na nazi,"amesema Mweri.

Ameongeza kuwa wanaiomba Halmashauri wawapatie mikopo kutokana na maombi kwani malengo wanakuwa wameshayaweka hivyo kuwakopesha chini ya walichoomba husababisha kufanya malengo yasifikiwe ya kile walichokiombea.

"Pia watoe mikopo kwa muda uliopangwa ambapo wao wanasubiri awamu ya pili tangu Desemba mwaka jana hadi leo bado hawajapata mkopo waliouomba ambapo gharama zinaongezeka za mahitaji mfano chakula cha kuku bei imeongezeka na mkopo hesabu zilizopigwa tayari zinakuwa chini,"amesema Mweri.

Amewataka wanawake wajane kutokata tamaa katika kupambania maisha yafamilia zao kwani wao ndiyo walezi wa familia na kulinda maadili ya watoto wao na kikundi hicho kilianzishwa mwaka 2022 na kimesajiliwa.

mwisho.







 



 

POLISI PWANI KUFANYA UCHUNGUZI KISAYANSI KUCHUNGUZA MADAI MZAZI KUBADILISHIWA MTOTO

JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani linafanya uchunguzi wa kitaalamu na kisayansi ili kubaini ukweli juu ya lalamiko la mwanamke aitwaye Filomena Mataris (36) Mkazi wa Gongo la Mboto Dar es Salaam kudai kubadilishiwa mtoto baada ya kujifungua katika Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo.

Uchunguzi huo unafanyika baada ya mlalamikaji kudai kuambiwa mtoto wake aliyejifungua amefariki na kuzikwa pasipo yeye na mume wake kushiriki mazishi ya mtoto wake ambapo alizikwa na ndugu zake.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani Salim Morcase alisema kuwa Juni 5 mwaka huu Filomena Mataris akiwa na mume wake Caros Kapata walifika kituo cha Polisi Bagamoyo wakilalamika kubadilishiwa mtoto kwenye Hospitali ya Bagamoyo. 

Morcase alisema kuwa walipofika polisi walieleza kuwa Aprili 14 mwaka huu Filomena Mataris alihamia Kerege Wilayani Bagamoyo kwa mtoto wa dada yake aitwaye Avetha Mabadiliko kwa ajili ya uangalizi wa karibu akitokea Gongo la Mboto Dar es Salaam.

"Mnamo Mei 17 mwaka huu majira ya saa 3:000 asubuhi Mataris alipata uchungu wa kujifungua hivyo aliongozana na ndugu yake huyo Mabadiliko kwenda Hospitali ya Kerege kwa ajili ya kujifungua,"alisema Morcase.

Alisema kuwa baada ya kufika hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo daktari alibaini Mataris ana dalili ya uzazi pingamizi hivyo alielekeza apelekwe Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji.

"Iipofika Mei 18 mwaka huu majira ya saa 8:00 usiku Mataris alihamishiwa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo ambapo saa 8:30 usiku alijifungua mtoto wa kiume kwa njia ya upasuaji na alieleza kuwa alimuona mtoto wake na kumbeba akiwa mzima wa afya,"alisema Morcase.

Aidha alisema Mataris alisema kuwa baada ya kupewa huduma na kwenda wodini alioneshwa picha za mtoto kwenye simu ya daktari na kuambiwa ndiye mtoto wake na ameshafariki. 

"Mtoto aliyeonyeshwa kwenye picha alikuwa na changamoto kama vile kichwa kubonyea na kuwa na uvimbe kifuani tofauti na mtoto wake aliyembeba baada ya kujifungua,"alisema Morcase.

Aliongeza kuwa baada ya kuonyeshwa picha hizo aliambiwa na daktari kuwa mwili umekabidhiwa kwa ndugu zake ambao ni Mabadiliko na shangazi
yake aitwaye Adora Mathias kwa ajili ya mazishi. 

"Mtoto huyo alizikwa bila uwepo wa Mataris ambaye ni mama wa mtoto wala baba wa
mtoto hakufahamishwa kuhusu mazishi hayo na mara baada ya kupata taarifa hiyo kutoka kwa familia hiyo Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani lilifungua jalada la uchunguzi lenye
namba BAG/PE/33/2026,"alisema Morcase.

Aliongeza kuwa Polisi walianza ufuatiliaji ulianza ambapo walimhoji Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo Dk. Mariam Ngwele aliyeeleza kuwa baada ya kumpokea Mataris.

Alisema kuwa Dk Ngwele alieleza kuwa Mataris  alijifungua kwa njia ya upasuaji lakini mtoto hakuwa wa kawaida kwani alikuwa na kichwa kilichobonyea na uvimbe sehemu ya kifuani na changamoto ya upumuaji hivyo alifariki muda mfupi baada ya kuzaliwa.

Kamanda Morcase alisema kuwa kutokana na changamoto hiyo Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani linaendelea na uchunguzi zaidi wa kitaalamu
na kisayansi ili kubaini ukweli wa taarifa hiyo.

Sunday, June 7, 2026

MAFANIKIO YA GLOBAL PARTNERSHIP FOR EDUCATION CHINI YA UENYEKITI WA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE

Na Albert Kawogo 

TANGU Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete ateuliwe kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Global Partnership for Education mwezi Septemba 2021, taasisi hiyo imeendelea kuimarisha juhudi za kuboresha elimu katika nchi zinazoendelea duniani. 

Dkt. Kikwete akiwa kiongozi wa kwanza kutoka Afrika kushika nafasi hiyo muhimu katika historia ya shirika hilo,chini ya uongozi wake, GPE imeongeza juhudi za kuhakikisha watoto wengi zaidi wanapata elimu bora, hususan wale wanaotoka katika mazingira magumu, maeneo yenye migogoro, wakimbizi na watoto wenye ulemavu.

Taasisi hiyo imeendelea kushirikiana na serikali mbalimbali duniani kuboresha mifumo ya elimu na kuongeza uwekezaji katika sekta hiyo ambapo ufanisi mkubwa umeonekana.

Moja ya mafanikio makubwa yaliyoshuhudiwa ni kuongezeka kwa ufadhili wa miradi ya elimu katika nchi wanachama. Katika kipindi cha mkakati wa GPE 2025, mamia ya mamilioni ya watoto wamefikiwa kupitia programu za kuboresha upatikanaji wa elimu, mafunzo kwa walimu, usambazaji wa vitabu na ujenzi wa miundombinu ya shule.

Kufikia mwaka 2024, GPE iliripoti kuwafikia watoto milioni 253, kutoa mafunzo kwa walimu milioni 1.9, kusambaza vitabu milioni 169 na kujenga au kukarabati zaidi ya madarasa 36,000.

Aidha, chini ya uenyekiti wa Dkt. Kikwete, GPE imepanua ushirikiano wake kwa kuongeza nchi wanachama na wadau wapya wa maendeleo.

Mwaka 2024, nchi za Jordan na Lebanon zilijiunga rasmi na ushirikiano huo, huku Saudi Arabia ikitangaza mchango mkubwa wa kifedha kwa ajili ya kuboresha elimu katika nchi zenye kipato cha chini.

Katika eneo la usawa wa kijinsia, GPE imeongeza juhudi za kuhakikisha wasichana wanapata fursa sawa za elimu ambapo pia shirika hilo limeimarisha programu za kuwajumuisha watoto wenye ulemavu, wakimbizi na makundi mengine yaliyokuwa yakibaki nyuma katika upatikanaji wa elimu.

Dkt. Kikwete ambaye ni Rais mstaafu wa Tanzania ameongoza juhudi za kuhamasisha ufadhili zaidi wa elimu duniani, akisisitiza kuwa elimu ni msingi wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii

 Kupitia  mikutano yake mbalimbali ya kimataifa, Dkt Kikwete amekuwa mstari wa mbele kwenye kutetea uwekezaji mkubwa katika elimu ili kukabiliana na changamoto zilizotokana na athari za COVID-19, migogoro ya kimataifa na mabadiliko ya tabianchi.

Kwa ujumla, kipindi cha uenyekiti wa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete  GPE 

imeonyesha mafanikio makubwa hasa katika kupanua fursa za elimu, kuimarisha ubora wa kujifunza, kuongeza ushirikiano wa kimataifa na kuhakikisha watoto walio katika mazingira magumu wanapata haki yao ya msingi ya elimu bora.

Wednesday, June 3, 2026

RAIS DK SAMIA SULUHU HASSAN AWEKA SHADA LA MAUA KABURI ASKARI ASIYEFAHAMIKA

Na Mwandishi Wetu, TBN, Moscow

KENGELE kubwa iliyogongwa mara tisa, bendi ya jeshi ikiongoza nyimbo za maombolezo Rais Dk Samia Suluhu Hasan majira ya saa tano na dakika 23 aliweka shada la maua kwa kaburi la askari asiyefahamika, mjini hapa.

Aidha Baada ya shughuli la uwekaji wa taji hilo katika eneo ambalo moto huwaka daima ikiwa ni kumbukumbu ya wapiganaji wa Urusi waliopoteza maisha katika vita kuu ya pili, gadi tatu zilipita kwa mwendo wa haraka na kutoa heshima kwa Rais Samia baada ya kupigwa kwa wimbo wa taifa la Tanzania.

Hali ya  askari katika uwanja huo walioonesha nidhamu ya hali ya juu ya kusimama tisti katika maeneo yao bila kutikisika , ubadilishanaji wa gadi za ulinzi na pia mwendo wa pole ambao ulimsindikiza Rais Samia kwenda kwenye tukio la uwekeaji wa shahada. Vilikuwa vitu vinavyovutia kuangalia.

Rais Samia ambaye yupo katika ziara ya kiserikali nchini hapa  baadaye alienda kukutana na mwenyeji wake Rais Vladmir Putin 

Zaidi ya maofisa 300 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania JWTZ wamepata nafasi ya masomo katika nchi ya Urusi kwa ajili ya shahada ya kwanza na ya pili.

Askari hao wameenda kujifunza masuala ya kupambana na ugaidi, sayansi na teknolojia,mafunzo ya kijeshi, ulinzi wa amani, ununuzi na uhifadhi wa silaha,namna ya kukabiliana na majanga.

Tanzania na Urusi zina ushirikiano wa kijeshi kwa kuzingatia makubaliano ya ushirikiano wa kijeshi yaliyosainiwa mwaka 2016  na makubaliano ya mwaka 2018 ya ushirikiano wa kifundi wa kijeshi.

Tanzania yenye ukuaji wa uchumi wa asilimia 5.5 kwa mwaka 2024 na ikikadiriwa kufikia asilimia 6 mwaka huu na ikiwa na mkakati wa kuhakikisha kwamba Dira ya maendeleo ya mwaka2050 inatekelezwa ziara ya Rais Samia nchini Urusi inatarajiwa kuzaa matunda yanayotarajiwa  ya kuinua sekta ya ajira kukuza biashara na kuimarisha uwekezaji.

DK SAMIA SULUHU HASSAN KUTUNUKIWA SHAHADA YA UZAMIVU YA CHUO KIKUU CHA RUDIN URUSI

Na Mwandishi Wetu ,TBN, Moscow

Rais Dkt  Samia Suluhu Hassan ambaye yupo hapa shirikisho la Urusi kwa ziara ya kitaifa anatarajiwa kutunukiwa shahada ya uzamivu na Chuo Kikuu cha Rudin nchini hapa.

Tuzo hiyo inatokana na kutambua kazi yake na mchango wake katika jami ya Tanzania na dunia katika masuala ya msingi yanayohusu Maisha ya binadamu.

Chuo cha RUDIN chenye wanafunzi wa kitanzania 570 kufikia mwaka 2025 katika miaka zaidi ya 65 ya RUDIN, watanzania 1,132 wamepitia chuo hicho.

RUDIN kimesomesha zaidi ya wataalamu 200,000 duniani na sasa ina watu 44,000 kutoka nchi 160 duniani.

Chuo hiki ni cha 367 kwa ubora duniani kwa mujibu wa QS World University Ranking ya mwaka 2025.

Rais Dkt Samia ambaye amepokelewa jana na Waziri wa maendeleo ya Uchumi wa Russia Maxim Reshetnikov anatarajiwa kukutana na mwenyeji wake Rais Vladimir Putin na kufanya mazungumzo ya ana kwa ana kwa ajili ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi.

Aidha akiwa nchini hapa, akiwa kiongozi wa pili wa Tanzania kutembelea Urusi, ziara ya kwanza ikiwa imefanywa na baba wa taifa Mwalimu Julius Nyerere, atashiriki Jukwaa la uchumi la St Petersburg ambapo tanzania itanadi fursa za uwekezaji, na diplomasia ya Uchumi  kwa viongozi, wawekezaji na watunga sera wa kimataifa.

Katika kufanikisha dira ya Maendeleo 2050 ziara hii ni kikolezo cha utekelezaji kwa mafanikio ya dira hiyo ambayo inahitaji raslimali watu wenye utaalamu na upeo mkubwa kusimamia na kuendesha miradi ya kimkakati itakayopelekea ajira, viwanda na biashara zitakazoingiza dola trilioni moja na kuwa katika uchumi wa kati wa juu.

Katika WhatsApp yake Rais Samia amesema Ziara hiyo ni muhimu hasa taifa linapoelekea kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 ambayo inataka ushiriki mkubwa wa sekta binafsi.

 "Tutafanya mazungumzo na wenyeji wetu yanayolenga kuimarisha ushirikiano katika sekta za kimkakati zinazogusa maisha ya wananchi." 

"Aidha, tutashiriki majukwaa ya biashara na uwekezaji na kutatangaza fursa zilizopo nchini, pamoja na kufungua zaidi fursa za masoko kwa bidhaa za Tanzania nchini Urusi."

RAIS DK SAMIA SULUHU HASSAN AWASILI URUSI


Na Mwandishi Wetu, TBN, Moscow

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, uliopo Jijini Moscow kwa ajili ya Ziara ya Kitaifa, nchini Urusi

Katika ziara hii ya kihistoria ikifanywa kwa mara ya pili katika historia ya uhusiano wa Tanzania na Urusi, ya kwanza ilikuwa ni miaka ya 1960 iliyofanywa na baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Rais Samia anaendeleza kampeni kubwa ya kuhakikisha Tanzania inanufaika pia kiuchumi na uhusiano mzuri na mataifa mbalimbali

Kwa mujibu wa shughuli atakazofanya Rais Samia akiwa hapa nchini kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa Kidiplomasia, kisiasa, kiuchumi na kihistoria baina ya Tanzania na Urusi,Rais amekuja kuiweka Tanzania katika ramani ya uwekezaji kwa ushiriki wake katika mkutano mkubwa wa uwekezaji jijini St Petersburg na pia kuona namna ya kutengeneza raslimali watu ambayo taifa inahitaji sana katika kufanikisha utekelezaji wa dira ya maendeleo ya 2050. 

Alipowasili nchini hapa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, Jijini Moscow  majira ya saa mbili na dakika 25 usiku , japo jua bado lilikuwa linawaka,  Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alipokea heshima ya wimbo wa Taifa pamoja na gwaride.

Rais Samia alipokewa uwanjani na Waziri wa Maendeleo ya Uchumi wa Shirikisho la Urusi Mhe. Maxim Reshetnikov. 

Kwa mujibu wa ratiba leo asubuhi ataanza na kuweka shada ka maua kwa kaburila askari asiyejulikana kabla ya kwenda Ikuku ya Kremlin kwa mazungumzo na Rais Vladmir Putin.

Sunday, May 31, 2026

WAZIRI KAPINGA AITAKA TBPL KUZALISHA MBOLEA HAI YENYE UBORA

WAZIRI wa Viwanda na Biashara Judith Kapinga ametaka kiwanda cha Tanzania Biotech Production Ltd (TBPL) kuzalisha Mbolea hai kwa kuzingatia ubora.

Kapinga aliyasema hayo Mjini Kibaha wakati wa hafla ya utiaji saini za makubaliano baina ya TPBL kampuni tanzu ya NDC na TFC, TARI, TFRA na TPHPA juu ya ushirikiano wa pamoja.

Alisema kuwa mbolea hiyo inasoko kubwa kwani haina kemikali na pia inatunza mazingira hivyo ni salama kwa afya za binadamu hivyo izingatiwe ubora wake.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji Mwendeshaji wa Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) ambayo ndiyo wasimamizi wa kiwanda hicho Nicolaus Shombe alisema kuwa uzalishaji wa mbolea hiyo utaleta mapinduzi ya kilimo.

Mkurugenzi Mkuu wa TBPL Mhandisi Rafael Moya alisema kuwa mbolea itasaidia wakulima kutumua kemikali kwani kiupaumbele cha Taifa ni kulinda afya za watu.