Tuesday, June 23, 2026

WAZO BORA LA KIJANA KUNYAKUA MILIONI 50

KIJANA mwenye wazo bora kati ya vijana 100 watakaowania kinyanganyiro cha Vijana Uchumi Challenge anatarajiwa kujinyakulia kitita cha shilingi milioni 50.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Dk Kedmon Mapana wakati akizungumza na vijana hao 100 watakaokuwa kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere iliyopo Kibaha Mkoani Pwani.

Mapana amesema kuwa wapili akijinyakulia shilingi milioni 20 na watatu milioni 10 ambapo vijana wanaoshiriki ni wenye umri chini ya miaka 35 kutoka nchi nzima.

"Wizara ilitoa shindano la vijana kutoa wazo la kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia mawazo ya vijana kukuza ubunifu na Ujasiriamali na kuwapa vijana fursa ya kuonyesha mawazo yao ya kibiashara na miradi ya kibunifu inayoweza kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi,"amesema Mapana.

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya Vijana Uchumi Challenge Joseph Malecela amesema kuwa jumla ya mawazo zaidi ya 7,000 ya vijana kote nchini yaliwasilishwa na kuchujwa na kubaki 100 ambayo yatashindanishwa kupata mshindi.

Malecela amesema kuwa washiriki hao 100 ambao wameingia kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere watachujwa na majaji wabobezi wa masuala ya uchumi na fedha na kubaki 30 na baadaye 10.

Kilele kinatarajiwa kufanyika Jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi atakuwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan.

VIJANA 100 KUWANIA MILIONI 50 VIJANA UCHUMI CHALLANGE

NAIBU Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Dk Kedmon Mapana amesema vijana kuwa na ujuzi na mtaji ni suluhisho la kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050.

Ameyasema hayo Mjini Kibaha kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere wakati akifungua Jukwaa la Vijana Uchumi Challenge.

Mapana amesema kuwa Waziri wa Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Joel Nanauka alizindua shindano la vijana kwa ajili ya kuwawezesha vijana nchini Tanzania kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na ubunifu. 

"Lengo kuu la mpango huu ni kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia mawazo ya vijana kukuza ubunifu na Ujasiriamali na kuwapa vijana fursa ya kuonyesha mawazo yao ya kibiashara na miradi ya kibunifu inayoweza kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi,"amesema Mapana.

Amesema kuwa pia ni kuongeza ajira kwa kusaidia miradi ya vijana kuanzishwa au kukua ambapo shindano linakusudia kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa kuwezesha vijana kujiajiri na kuajiri wengine.

"Kwa wale ambao hawatafanikiwa kushinda mawazo yao yatachukuliwa na kufanyiwa kazi kwa kupewa mafunzo kutokana na mawazo yao ya bunifu zao kupitia sekta mbalimbali zikiwemo za kilimo uvuvi mifugo tehama na ujasiamali,"amesema Mapana.

Aidha amesema vijana wasilalamike bali watoe mawazo na suluhisho nini kifanyike hata ikitokea changamoto kama za kupanda bei ya mafuta ili uchumi wa nchi uwe stahimilivu

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya Vijana Uchumi Challenge Joseph Malecela amesema kuwa jumla ya mawazo zaidi ya 7,000 ya vijana kote nchini yaliwasilishwa na kuchujwa na kubaki 100 ambayo yatashindanishwa kupata mshindi.

Malecela amesema kuwa washiriki hao 100 ambao wameingia kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere watachujwa na majaji wabobezi wa masuala ya uchumi na fedha na kubaki 30 na baadaye 10.

Amesema kuwa washindi 10 watakwenda kwenye kilele kitakachofanyika Jijini Dar es Salam Julai 6 ambapo mshindi atapata kiasi cha shilingi milioni 50 huku wapili akijinyakulia shilingi milioni 20 na watatu milioni 10 ambapo vijana wanaoshiriki ni wenye umri chini ya miaka 35.

Kilele kinatarajiwa kufanyika Jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi atakuwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan.

PWANI YAKUSANYA BILIONI 266

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani imefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 266 katika kipindi cha miaka 10 iliyopita na kuvuka malengo yaliyowekwa ya kukusanya shilingi bilioni 235 katika kipindi hicho.

 

Akizungumza kwenye Kongamano la Mamlaka hiyo ya kutimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake Meneja wa TRA Mkoa wa Pwani Peter Jackson alisema kuwa mafanikio hayo ni ongezeko la asilimia 113 ya makusanyo kwa kipindi hicho.

 

Jackson alisema kuwa mafanikio hayo yametokana na ushirikiano ulioonyeshwa na wafanyabiashara na wadau wote wa kodi ambapo katika kipindi hicho malaengo ya makusanyo yalikuwa ni bilioni 23 lakini zilikusanywa kiasi cha shilingi bilioni 27.

 

“Kwa wastani makusanyo kwa kipindi cha miaka 10 ni ongezeko la asilimia 10 ambapo yamekuwa yakiongezeka hadi kufikia kiasi hicho na kuonyesha jinsi gani mamlaka hiyo inavyopiga hatua katika kuleta maendeleo ya nchi,”alisema Jackson.

 

Alisema kuwa makusanyo yana faida kubwa kwani yanatumika kwa ajili ya kufanya shughuli za kimaendeleo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ikiwemo ya barabara ujenzi wa reli ya kisasa SGR huduma za afya, huduma za elimu na masuala mbalimbali.

 

Aidha alisema kuwa ukusanyaji wa mapato makubwa ndiyo njia ya kukuza uchumi wa nchi ambapo walipa kodi wanapaswa kulipa kwa hiyari na kwa wakati ili kuondoa changamoto za kupewa adhabu ambayo inawarudisha nyuma.

 

“Kwa sasa tumeweka mifumo madhubuti ya ukusanyaji na namna ya kuwafikia kwa urahisi walipa kodi na kuwaondolea usumbufu wa kufika ofisini badala yake wanauwezo wa kulipa au kufanya shughuli zote wakiwa maeneo yao jambo ambalo limerahisisha utendaji kazi,”alisema Jackson.

 

Akizungumzia kuhusu changamoto alisema kuwa ukuaji wa uchumi usio rasmi umekuwa ni tatizo kwani unakuwa nje ya mfumo rasmi hivyo kusababisha kukosekana kwa mapato kutokana na kukwepa au kupunguza kodi kuongezeka kwa biashara mtandaoni biashara haramu na za magendo ambazo huathiri ushindani wa kibiashara..

 

Kwa upande wake mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT) Mkoa wa Pwani Abdala Ndauka alisema kuwa baadhi ya wafanyabiashara hawana uelewa juu ya masuala ya ulipaji kodi hivyo kuna haja ya kutolewa elimu ya kutosha.

 

Ndauka alisema kuwa ulipaji kodi unapaswa kuwa rafiki na si kama adhabu bali uwe rafiki hata hivyo malalamiko kwa sasa yamepungua kwani kwa sasa kumekuwa na majadiliano juu ya changamoto zinazowakumba walipa kodi na watengeneze walipa kodi wapya.

 

Mwenyekiti wa Chemba ya wafanyabiashara Mkoa wa Pwani Said Mfinanga alisema kuwa matumizi ya teknolojia yamesaidia kuwapunguzia muda walipa kodi kwenda ofisini ili kufanya kufanya taratibu mbalimbali juu ya masuala ya ya biashara zao.

 

Mfinanga alisema kuwa mfumo wa teknolojia pia utumike kutoa elimu juu ya masuala ya ulipaji kodi na taratibu zote zihusikanazo na masula ya kodi ili kujenga uelewa wa pamoja kwa walipa kodi na mamlaka hiyo ambayo inajuhusisha na ukusanyaji wa mapato ya serikali.   

 

Naye mwenyekiti wa Shirikisho la Umoja wa Machinga (SHIUMA) Mkoa wa Pwani Philemon Maliga alisema kuwa ili kuboresha ukusanyaji wa mapato Mamlaka inapaswa kuwa na mahusiano bora na mazuri na walipakodi kwnai kundi lao ni kubwa na lina uwezo wa kuchangia pato la serikali.

 

Maliga alisema kuwa TRA iatoe limu kuanzia mashuleni na sehemu mbalimbali ili kuwajengea walipa kodi utamaduni wa kulipa mapato ili kuonyesha uzalendo wa nchi yao kwani kodi ndiyo msingi mkubwa wa maendeleo.

 

Monday, June 15, 2026

TAARIFA KWA UMMA


Ofisi ya Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, inapinga na kukanusha vikali taarifa ya uongo na upotoshaji inayosambaa mitandaoni, ikidai kuwa Dkt. Kikwete anahusishwa na mradi unaodaiwa kuwa wa uwekezaji unaowaahidi Watanzania kipato cha uhakika kupitia jukwaa la kifedha linalotumia teknolojia ya akili mnemba

Taarifa hiyo inadai kuwa maelfu ya Watanzania tayari wamenufaika na mradi huo baada ya kuwekeza kiasi cha shilingi 653,000, huku wakiahidiwa kupata zaidi ya shilingi 9,200,000 kwa mwezi. Madai hayo si ya kweli hata kidogo.

Ofisi ya Rais Mstaafu inapenda kuweka wazi kwamba Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete hajawahi kushiriki, kuidhinisha, kutangaza, kuunga mkono, wala kuhusika kwa namna yoyote ile na mpango huo wa kifedha. 

Ofisi yake haijawahi kuruhusu matumizi ya jina, picha, au heshima yake kuhusishwa na mradi huo unaodaiwa, na haitajihusisha na shughuli za aina hiyo.

Wananchi wanashauriwa kupuuza taarifa hiyo ya uongo na kuwa makini dhidi ya miradi ya kitapeli na vitendo haramu vya aina hiyo. 

Mtu yeyote atakayekutana na taarifa kama hizo za upotoshaji anapaswa kuzichukulia kama habari za uongo, kuepuka kuzisambaza, kujisajili, au kutuma fedha kwa mtu au jukwaa lolote linalohusishwa nazo.

Sunday, June 14, 2026

PWANI YAENDELEA KUHAMASISHA UCHANGIAJI DAMU KUOKOA MAISHA YA WATU

MKOA wa Pwani umekusanya jumla ya chupa za damu 1,129 kwa ajili ya Hospitali na Vituo vya Afya.

Hayo yamesemwa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani Kusirye Ukio wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mchangiaji Damu wa Dunia kimkoa ambapo maadhimisho hayo yamefanyika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani Tumbi.

Kwa upande wake Msimamizi wa Huduma kwa Mteja na Wachangiaji Damu Salama Makao Makuu Kaito Tamba amesema kuwa kwa sasa mpango ni kukusanya chupa 600,000 kwa mwaka 

Akisoma risala ya siku hiyo Mkuu wa Idara ya Maabara Hospitali ya Tumbi Simon Lupatu amesema kuwa kauli mbiu ya mwaka huu inasema "Changia Damu Okoa Maisha" ambapo wanahitaji mashine kwa ajili ya uzalishaji mazao ya damu.

Naye Mkuu wa Idara ya Kinamama na Uzazi wa Hospitali ya Tumbi Dk Alfonce Moyo amesema kuwa takwimu zinaonyesha vifo vilivyotokea kwa mwezi Januari hadi Juni mwaka huu asilimia 80 vilitokana na kupoteza damu nyingi.

Saturday, June 13, 2026

*SERIKALI YADHAMIRIA KUWAENDELEZA WACHIMBAJI WADOGO NCHINI*

▪️Taarifa ya mapendekezo ya kuwaendeleza Wachimbaji wadogo yawasilishwa

▪️Prof Mkumbo aeleza umuhimu wa sekta ya madini kufikia Dira 2050

Lengo ni Kuongeza Ajira, Kupunguza Umaskini na Kukuza Uchumi

▪️Mfuko wa Dhamana  kutatua changamoto ya mitaji kwa wachimbaji

▪️Serikali yaanzisha mfuko wa Madini kwa ajili ya Utafiti wa Madini

📍 Dar Es Salaam

Serikali imesisitiza kufanyia kazi kwa haraka Mapendekezo yaliyotolewa na Timu ya Wataalamu iliyoundwa Kuishauri Wizara ya Madini kuhusu namna ya Kuwaendeleza Wachimbaji Wadogo Kiuchumi na kueleza kuwa, utatuzi wa changamoto za Mitaji, Teknolojia na upatikanaji wa taarifa sahihi za Kijiolojia kwa Wachimbaji Wadogo wa Madini ni hatua muhimu ya kuongeza ajira kwa watanzania, kupunguza umaskini na kukuza uchumi wa Taifa kuelekea Dira 2050.

Hayo yamebainishwa Juni 13, 2026 jijini Dar Es Salaam  na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, wakati wa hafla ya Kupokea Mapendekezo ya Kuwaendeleza Wachimbaji Wadogo Nchini na kusisitiza kwamba, maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha mipango ya maendeleo inajibu changamoto tatu kuu za taifa ambazo ni kuongeza mitaji kwa wananchi, kuzalisha ajira na kupunguza umaskini.

Amesema kuwawezesha wachimbaji wadogo kupata mitaji na teknolojia, kunafungua fursa za kuongeza uzalishaji, ajira na kipato cha wananchi na kuongeza kuwa hiyo ndiyo njia mojawapo ya kupambana na umaskini.

‘’Kazi kubwa ya Waziri ni kutoa mwelekeo wa kisera wa taasisi au wizara anayoiongoza. Kwa muda niliokaa kwenye Wizara yangu, Mhe. Mavunde amekua akijua kipaumbele anachokitaka na jinsi ya kukipata,’’amesisitiza Prof. Mkumbo.

Ameongeza kwamba, hali ya umaskini nchini  bado ipo kwa kiwango cha juu na kutolea mfano wa Mkoa wa Geita ambao unaoongoza kwa shughuli za uchimbaji madini ya dhahabu nchini ambapo  hali ya umaskini inafikia asilimia 38 na kusisitiza kwamba, wachimbaji wadogo wanapowezeshwa wanasaida kutatua changamoto kama hizo na kuongeza kuwa, Sekta ya Madini imewekwa kama moja ya sekta muhimu za kimageuzi  inayotarajiwa kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi na ajira ambapo awali haikuwa ikibeba watu wengi.

Naye, Waziri wa Madini Anthony Mavunde akizungumza katika halfa hiyo, amesema Serikali iliamua kuunda kamati hiyo kutokana na mchango mkubwa unaotolewa na wachimbaji wadogo katika Sekta ya Madini, licha ya kukabiliwa na changamoto za mitaji, teknolojia na upatikanaji wa huduma za kifedha , hivi sasa wanachangia asilimia 40 ya makusnyo ya maduhuli ya Serikali.

Ameongeza kwamba, kuwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika Sekta ya Madini ndani ya miaka ya hivi karibuni yanaonyesha umuhimu wa kuwawezesha zaidi wachimbaji wadogo ili waongeze mchango wao katika uchumi wa taifa.

Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, Mwaka wa Fedha  2015/16 Sekta ya Madini katika mwaka mmoja iliingiza shilingi bilioni 161 pekee katika Mfuko Mkuu wa Serikali. 

Hata hivyo, kufuatia mageuzi mbalimbali yaliyofanyika ikiwemo mabadiliko ya sheria, kuanzishwa kwa masoko ya madini na udhibiti wa biashara haramu ya madini, makusanyo yameongezeka kwa kiwango kikubwa kufikia Shilingi trilioni 1.107 mwaka 204/25 na mpaka kufikia  tarehe 13, Juni, tayari Serikali imekusanya shilingi trilioni 1.3.

Amesisitiza kuwa jukumu la Serikali yoyote duniani ni kuwawezesha wananchi wake kufanya shughuli za uzalishaji kwa tija zaidi sababu ambayo ilipelekea  Serikali kuweka mkakati maalum wa kuwawezesha wachimbaji wadogo ili waweze kukua na kuwa wachimbaji wa kati na baadaye wakubwa.

Kuhusu changamoto ya mitaji, Waziri Mavunde  amesema Serikali imeanza utekelezaji wa Kampuni ya dhamana ya mikopo (Credit Guarantee Corporation) itakayosaidia  wachimbaji kupata mikopo kutoka taasisi za fedha mbalimbali.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo  Dkt. Victor Tesha  amesema suluhu ya changamoto hizo ni kujenga mfumo jumuishi wa kuwawezesha wachimbaji wadogo kupitia upatikanaji wa mitaji, teknolojia za kisasa, taarifa za kijiolojia na uratibu wa taasisi zinazohusika na sekta hiyo huku akipendekeza kuanzishwa kwa Mfuko wa Madini Tanzania utakaowezesha miradi yenye sifa kupata fedha za kuendeleza uzalishaji, kununua mitambo na kuboresha shughuli za uchimbaji, na kuongeza kwamba, mfuko huo utasaidia kugharamia tafiti na taarifa za kijiolojia kwa wachimbaji.

Ameongeza kuwa, baada ya mfuko huo kukua na kuimarika, hatua itakayofuata itakuwa ni kuanzisha Benki ya Wachimbaji itakayotoa huduma maalumu za kifedha kwa sekta ya madini kwa masharti yanayoendana na mazingira ya wachimbaji.

‘’Kamati pia imependekeza mikopo ielekezwe zaidi katika ununuzi wa mitambo na teknolojia badala ya fedha taslimu pekee, ili kuongeza tija, uzalishaji na usalama katika shughuli za uchimbaji,’’ amesema Tesha.


 Naye, rais wa Shirikisho la Vyama Vya Wachimbaji Wadogo John Bina, ameipongeza Serikali kwa ripoti hiyo na kueleza imetokana  na Serikali kusikiliza na kuyafanyia kazi maoni na changamoto za wachimbaji wadogo, pamoja na kuipongeza kwa kutenga asilimia 10 ya mapato yanayotokana na shughuli za madini kwa ajili ya utafiti.

Wednesday, June 10, 2026

HALMASHAURI YA MANISPAA YA KIBAHA YATOA MIKOPO YA SHILINGI MILIONI 991.5 KWA VIKUNDI

HALMASHAURI ya Manispaa ya Kibaha Mkoani Pwani imetoa mikopo ya jumla ya shilingi milioni 991.5 kwa vikundi 51 vya ujasiriamali.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dk Rogers Shemwelekwa wakati wa hafla ya utoaji mikopo ya robo ya tatu.

Shemwelekwa amesema kuwa fedha hizo kiasi cha shilingi milioni 359 ni kwa vikundi 17 vya wanawake shilingi milioni 557 kwa vikundi 25 vya Vijana.

"Kiasi cha shilingi milioni 75.5 kilitolewa kwa watu wenye ulemavu 17 ambapo fedha hizo zimetokana na asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha,"amesema Shemwelekwa.

Amesema kuwa miradi iliyokopeshwa kwa vikundi hivyo ni pamoja na mradi wa usafirishaji ambapo pikipiki 25 zimetolewa na TOYO moja, Bajaji nne, pia miradi ya ufugaji kuku, uchomeleaji ,ushonaji na hardware.

"Viwanda vidogo vya utengenezaji batiki, sabuni, kilimo cha umwagiliaji, kiwanda na stationery miradi hiyo yote inatokana na vikundi hivyo ambavyo ni vya wajasiriamali,"amesema Shemwelekwa.

Aidha amesema kuwa kwa mwaka wa fedha wa 2024/25 ambapo mikopo ilianza kutolewa mwezi Disemba 2024 kwa kanuni mpya hali ya urejeshaji kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu imefikia asilimia 52. 

"Pia mikopo ya mwaka huu wa 2025/26 ambayo imetolewa kuanzia mwezi Novemba 2025 marejesho yamefikia asilimia 26 ambapo inaashiria marejesho yapo vizuri,"amesema Shemwelekwa.

Kwa upande wake Mgeni rasmi Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka amesema kuwa kutolewa mikopo hiyo ni jitihada kubwa zinazofanywa katika ukusanyaji wa mapato.

Koka amesema kuwa Halmashauri imeendelea kuimarika kwenye upande wa mapato hali ambayo inaongeza utoaji wa mikopo kutokana na asilimia 10 ya mapato.

Naye Mwenyekiti wa Kikundi cha Lulu ya Wajane Kanyenda Mweri alisema kuwa fedha hizo zitawasaidia wao kama wajane kukuza mtaji wao wa ufugaji wa kuku.

Mweri alisema wanaishukuru Halmashauri na Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kurejesha mikopo hiyo ya asilimia 10 baada ya kusitishwa  kwa muda na kuwekwa utaratibu mpya.