MKUU wa Mkoa wa Pwani Stanslaus Nyongo amesema Wilaya za Mkoa huo zimetenga maeneo kwa ajili ya wananchi watakaokumbwa na changamoto zitakazotokana na mvua za Elnino.
Aidha aliwataka wananchi waishio mabondeni waondoke na kuhamia kwenye maeneo ya miinuko ili kuepuka madhara wakati wa mvua hizo zitakazonyesha hivi karibuni.
Nyongo aliyasema hayo ofisini kwake Mjini Kibaha wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake juu ya tahadhari ya ujio wa mvua za Elnino zinazotarajiwa kunyesha hivi karibuni.
Alisema kuwa maeneo yaliyotengwa ni pamoja na shule na maeneo mbalimbali yanayotoa huduma za kijamii hivyo wananchi wanapaswa kukaa sehemu zisizo hatarishi ili kupunguza madhara ya mvua hizo kwa wananchi kuchukua tahadhari ili kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza.
"Wananchi waishio mabondeni na sehemu hatarishi wanapaswa kuhama na kuishi sehemu salama wasisubiri hadi madhara yatokee,"alisema Nyongo.
Alibainisha kuwa suala la kutoa tahadhari kwa wananchi linapaswa kufanywa na watu wote wakiwemo viongozi wa dini na viongozi mbalimbali wa jamii.
"Tunapaswa kuwapa elimu wananchi ya kusafisha mazingira kwa kusafisha mitaro na njia za maji sehemu za biashara na kwenye makazi ili kuepusha maji kutuama bali yapate njia,"alisema Nyongo.
Pia aliwataka wananchi kuhifadhi chakula, madawa, tochi, madawa na vifaa mbalimbali kwani yawezekana kukawa na changamoto ya barabara katika kupata mahitaji.





