Saturday, September 5, 2026

MJUMBE WA HALMASHAURI KUU MKOA WA PWANI ALHAJ MUSSA MANSOUR AJITOLEA KUJENGA OFISI YA CCM KATA YA MKUZA

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Pwani Mussa Mansour ametoa vifaa vya ujenzi wa ofisi ya CCM Kata ya Mkuza Wilaya ya Kibaha Mjini.

Akizindua ujenzi wa ofisi hiyo na kuhudhuria Mkutano Maalum wa Kata hiyo Mansour amesema kuwa alipewa ombi na Kata hiyo ambayo inatumia ofisi za tawi kwa ajili ya shughuli zake.

Mansour amesema kuwa lengo la kutoa vifaa hivyo vya ujenzi ni kufanikisha Kata hiyo kuwa na ofisi ili kuwa na ofisi badala ya kutegemea ofisi ambazo siyo zao.

"Nimejitolea ili kuimarisha chama na ningetamani uchaguzi wa ndani ya chama mwakani ufanyike kwenye ofisi hizo kikubwa ni uongozi kufuata taratibu ili tuweze kufikia lengo la kuzikamilisha,"amesema Mansour.

Amesema kuwa aliahidi mchanga, simenti, kokoto nondo na matofali anashukuru kwani vyote amevitoa kilichobaki ni ujenzi tu kuanza na uzinduzi uliifanyika ndiyo ishara ya kazi kuanza.

Naye Mwenyekiti wa Kata ya Mkuza Matata Ngollo amesema kuwa wanamshukuru Mjumbe huyo wa Halmashauri ya Mkoa kwa kujitoa kwake kusaidia ujenzi huo.

Ngollo amesema kuwa wanamshukuru kwani vifaa hivyo vitafanya ujenzi kwa asilimia 80 na itabaki umaliziaji tu hivyo kuifanya Kata nayo kumiliki ofisi yake.

Mjumbe huyo alikuwa mgeni rasmi kwenye Mkutano Maalum wa Kata ambapo alizungumza na viongozi mbalimbali wa ngazi za matawi, alizindua tawi la CCM la waendesha bodaboda tawi la Barckyard, alitembelea kijiwe cha draft na kutoa fedha kwa makundi maalum wakiwemo wajane, wazee, bodaboda  na watu wenye ulemavu na vijana na alitembelea soko la Mkuza.

Wednesday, September 2, 2026

WAMACHINGA WAISHUKURU SERIKALI KUWATENGEA ENEO LA BIASHARA

WAFANYABIASHARA wadogo Mkoani Pwani maarufu kama Wamachinga wameishukuru serikali kwa kuwatengea eneo maalum kwa ajili ya kufanyabiashara.

Hayo yemesemwa Mjini Kibaha na Mwenyekiti wa Wamachinga Mkoani humo Filemon Maliga alipokuwa akizungumzia kuhusu zoezi la kusajili wafanyabiashara wanaofanya shughuli zao kwenye eneo la hifadhi ya barabara eneo la Maili Moja.

Maliga amesema kuwa wafanyabiashara hao wametengewa eneo lingine kwa ajili ya kufanya biashara mara utaratibu wa eneo jipya utakapokamilika watahamishiwa hapo ili kuendelea na biashara zao.

"Kama unavyoona zoezi linaloendelea na kuwasajili kutegemeana na biashara wanazofanya wakiwemo wauza mitumba, mama lishe, wauza matunda, chips na biashara nyingine,"amesema Maliga.

Amesema kuwa kutokana na uhaba wa ajira watu wengi wameingia kwenye mfumo wa kujiajiri kwa kufanya biashara hivyo hiyo ni ajira kwa kundi hilo kwani watu wanaendesha maisha yao kupitia biashara zao.

"Tunamshukuru Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kutaka wafanyabiashara wadogo nao watengewe mazingira mazuri kwa ajili ya kufanya biashara zao wakiwa kwenye mazingira rafiki hivyo kufanya biashara zao kwa uhuru,"amesema Maliga.

Aidha amesema kuwa kupitia biashara hizo wafanyabiashara hao wanaendesha maisha yao kw kujenga nyumba kusomesha watoto na kuongeza kipato na kujiletea maendeleo.

Naye moja ya wafanyabiashara wa eneo hilo Wilielmina Lazaro amesema kuwa mpango huo ni mzuri kwani walikuwa hawana eneo maalum na hapo walikuwa wakifanya kwenye eneo la hifadhi ya barabara ambapo maandalizi ya ujenzi yataanza wakati wowote. 

Lazaro amesema kuwa wanatunza familia zao pia baadhi wanakopa fedha kupitia biashara zao hivyo kuweza kukuza biashara na kujiletea maendeleo wao na familia zao.

RAIS DK SAMIA SULUHU HASSAN AMWAPISHA NYONGO KUWA MKUU WA MKOA WA PWANI

Dk Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akimuapisha Stanslaus Haroon Nyongo kuwa Mkuu wa Mkoa wa Pwani kwenye hafla ya uapisho iliyofanyika Ikulu Ndogo ya Tunguu, Zanzibar leo tarehe 02 Septemba, 2026.


MPANGO WA KUJIANDAA NA KUKABILIANA NA MVUA ZA EL NINO

Nimeongoza Kikao cha Kamati ya Wataalam Wilaya ya Gairo kupokea taarifa ya Taasisi na Idara mbalimbali namna tulivyojiandaa na kukabiliana na Mvua za El Nino  Kabla ya Mvua, Wakati wa Mvua na Baada ya Mvua.

KIKAO hiki MUHIMU kimehusisha Taasisi za TARURA, RUWASA, GAUWASA, TANESCO, JESHI LA UOKOAJI ZIMAMOTO, JESHI LA POLICE, Udhibiti Ubora wa Elimu na Idara zote zilizopo chini ya Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri.  

KAZI NA UTU, TUNASONGA MBELE.

Monday, August 24, 2026

MJUMBE HALMASHAURI KUU CCM MKOA WA PWANI KUSAIDIA UKAMILISHAJI OFISI UVCCM KATA YA TANGINI

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCMNEC) Mkoa wa Pwani Alhaji Hussein Chuma ameahidi kufanikisha umaliziaji wa ofisi ya Umoja wa Vijana wa (UVCCM) Kata ya Tangini Wilayani Kibaha.

Akifungua Kikao cha Baraza la Umoja huo lililofanyika kwenye Kata hiyo mwakilishi wa Mjumbe huyo Nassoro Shomvi amesema mchango wake ni kwa ajili ya kuhakikisha ofisi hiyo inaanza kutumika.

 Shomvi amesema kuwa UVCCM ni tanuru la kupika vijana ambao ni viongozi wa baadaye wa chama hivyo lazima wawekewe mazingira mazuri ya kufanyia shughuli zao za kila siku.

"Vijana mnapaswa kukitumikia chama ili kiweze kuhudumia wananchi kwani nyie ndiyo nguvu ya chama na chachu ya jumuiya zote za chama hivyo lazima mpambanie chama wakati wote,"amesema Shomvi.

Kwa upande wake Katibu wa UVCCM Kata ya Tangini Lazaro Benjamin amesema kuwa ili kukamilika ofisi hiyo inahitaji baadhi ya vitu ili kukamilika.

Benjamin amesema mojawapo ni samani za ofisi pamoja na kumalizia vitu vidogo vilivyobakia ili iweze kuanza kutumika pia ukosefu wa mashine kwa ajili ya mradi wa uoshaji wa magari.

MBUNGE WA JIMBO LA KIBAHA MJINI SILVESTRY KOKA ATOA MILIONI 1 KWA (UWB)

MBUNGE wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka ametoa kiasi cha shilingi milioni moja kwa Shina la Wakereketwa wa Umoja wa Bodaboda Nida (UWB)  Kata ya Tangini Wilayani Kibaha.

Alikabidhi kiasi hicho cha fedha wakati alipokuwa akitembelea miradi ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Kata ya hiyo kwenye Baraza la kawaida la Kata.

Koka amesema kuwa wao kama wabunge wamekuwa wakiwatetea madereva wa bodaboda bungeni ili kuhakikisha wanarasimishwa na kunufaika na fursa mbalimbali za kiuchumi.

"Hata Halmashauri imetenga fedha kwa ajili ya kuwakopesha madereva wa bodaboda ili nao wanufaike na asilimia 10 zinazotokana na mapato ya ndani,"amesema Koka.

Amewataka madereva wa bodaboda kuhakikisha wanafanya kazi zao kwa kuzingatia taratibu ili waweze kufanikiwa na kuepukana na utendaji kazi ambao haifuati sheria.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Tangini Antony Millao amesema kuwa amekuwa akikisaidia kikundi hicho ili kuhakikisha kinafuata taratibu.

Millao amesema kuwa moja ya changamoto waliyonayo ni ukosefu wa leseni lakini wanaendelea kuitatua changamoto hiyo kwa kuwatafutia madarasa ya kupata elimu ya udereva.

Naye Katibu wa UVCCM Kata ya Tangini Lazaro Benjamin amesema kuwa wameanzisha mradi wa kuosha magari ambapo wanahitaji kupata vifaa kwa ajili ya mradi huo.

Benjamin amesema lengo la kusnzisha mradi huo ni kujiongezea kipato badala ya kuomba fedha kutoka kwa wadau kwa ajili ya kuendeshea shughuli zao.

Thursday, August 20, 2026

RAIS DK SAMIA SULUHU HASSAN KUZINDUA MRADI BWAWA LA KUFUA UMEME LA MWALIMU JULIUS NYERERE RUFIJI

KUELEKEA uzinduzi wa mradi wa Bwawa la kufua umeme la la Mwalimu Julius Nyerere Rufiji unaotarajiwa kufanywa na Rais Dk Samia Suluhu Hassan Agosti 22 Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge amebainisha mafanikio yaliyotokana na mradi huo.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mjini Kibaha kuhusu uzinduzi huo alisema kuwa tukio hilo ni la kihistoria na unatimiza ndoto za Watanzania.

Kunenge alitaja baadhi ya faida ya mradi huo kuwa ni pamoja na Mkoa hadi kufika Julai kupata megawati 356 kutoka megawati 118 za umeme mwaka 2022.

"Kwa sasa umeme umeingizwa kwenye gridi ya umeme ya Taifa na kuna kituo cha kupooza umeme kilichopo Chalinze ambapo kuna kv 400 zinazopelekwa Mkoani Dodoma,"alisema Kunenge.

Alisema kuwa vituo vingine vya vitakavyojengwa ni Kwala, Zegereni na Zinga na mradi huo mbali ya kuhudumia wananchi pia ziada itauzwa nje ya nchi ambapo kwa sasa umeme ni wa uhakika.

"Uwekezaji wa viwanda vikubwa na vya kati umeongezeka kwa viwanda 307 ambapo imetokana na kuwa na uhakika wa nishati ya umeme na sasa kuna mpango wa kuleta gesi kutoka Kinyerezi kwenda Chalinze,"alisema Kunenge.

Aidha alisema kuwa kwa sasa vijiji vyote vya Mkoa wa Pwani vina umeme ukiondoa vijiji nane vilivyopo Visiwani ambavyo vinatumia umeme wa jua.

"Pia kwa sasa upembuzi yakinifu unafanyika eneo la Mloka ambapo kutajengwa bwawa la maji safi ambapo mbali ya Mkoa wa Pwani pia mikoa ya Morogoro na Lindi itanufaika na mradi huo utakaokuwa na uwezo wa kuzalisha lita milioni 1.5 lakini kwa kuanzia utazalisha lita 750,000 kwa siku,"alisema Kunenge.

Aliongeza kuwa upembuzi unaendelea kwa ajili ya kuwa na mabwawa kwa ajili ya skimu ya umwagiliaji eneo la Mkongo na Kibiti kwa maji yatakayokuwa yanatoka kwenye mradi huo na kuondoa mafuriko ambayo hutokea kipindi cha mvua.

"Hatimaye Tanzania imetimiza ndoto ya Nyerere ya kujitosheleza kwa umeme ambapo bwawa linazalisha umeme megawati 2,115 na uzinduzi ni historia na tunatarajia wananchi kujitokeza kwa wingi na wageni kutoka nje ya nchi,"alisema Kunenge.

Mradi huo una thamani ya shilingi trilioni saba na ulianza awamu ya tano ya Hayati Dk John Pombe Magufuli na Rais Dk Samia Suluhu Hassan aliukuta ukiwa asilimia 35 na kuukamilisha na kutimiza ndoto za Watanzania.