Wednesday, August 5, 2026

AHUKUMIWA MAISHA JELA KWA ULAWITI MWINGINE MIAKA 20 NA FAINI M 1 KWA KUDHALILISHA MTOTO

SAMWEL Mang'ombe (29) mkazi wa Wilaya ya Bagamoyo amehukumiwa kifungo cha maisha jela kwa kosa la kulawiti mtoto mwenye umri wa miaka (10) ambaye alikuwa ni jirani yake.

Hayo yamesemwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani Salim Morcase alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwezi Julai.

Kwenye tukio lingine Salim Masanja (33) Mkazi wa Wilayani Kibaha amehukumiwa kifungo cha miaka 20 jela na kulipa fidia ya shilingi milioni moja kwa tuhuma za kumdhalilisha mtoto wa kike (6).

Morcase amesema kuwa mshtakiwa huyo ni baba mdogo wa mhanga ambaye alikuwa akiishi naye nyumbani kwake na kesi hizo ni za ukatili wa kijinsia.

Amesema kuwa kesi zilizofikishwa mahakamani kwa kipindi hicho zilikuwa 117 huku kesi 63 zilisikilizwa na kumalizika ambapo kesi 48 zimepata mafanikio.

Amesema kuwa jamii kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wanapaswa kushirikiana ili kukabiliana na vitendo vya ukatili kwa watoto.

POLISI YAWAREJESHA SHULENI WANAFUNZI 114

JESHI la Polisi Mkoani Pwani limefanikisha kuwarejesha Shuleni wanafunzi 114 ambao walishindwa kuripoti shule kutokana na sababu mbalimbali.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mjini Kibaha Kamanda wa Polisi Mkoani Pwani Salim Morcase amesema kuwa jumla ya wanafunzi 573 walikuwa hawajaripoti shuleni.

Morcase amesema kuwa kati ya wanafunzi hao ambao hawakuripoti Shule za Msingi walikuwa 251 na wa Sekondari walikuwa ni 322 ambao walibainika katika kipindi hicho licha ya kuwa wanafunzi hao kuwa na wa miaka tofauti tofauti.

Amesema kuwa changamoto nyingine ni mimba za utotoni ukosefu wa mahitaji ya msingi kama vile sare za Shule na madaftari  na changamoto za kiafya na kiuchumi.

Amewataka wazazi na walezi kushirikina na viongozi wa dini na wa kiserikali katika kupambana na viashiria vya vitendo vya ukatili wanavyofanyiwa watoto ndani ya jamii.


Saturday, August 1, 2026

HALMASHAURI YA MANISPAA KIBAHA YAZINDUA MAGARI MRADI WA (TACTIC)

HALMASHAURI ya Manispaa ya Kibaha imezindua magari mawili yatakayotumika kwenye mradi wa ujenzi wa barabara za lami kwenye kupitia mradi wa uboreshaji miundombinu ya Miji na Vijiji (TACTIC) wenye thamani ya shilingi bilioni 19.8

Akindua magari hayo ambayo yatatumika kwenye mradi huo Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dk Nicas Mawazo alisema magari hayo yatawezesha utekelezaji mradi kuwa rahisi.

Mawazo alisema kuwa magari hayo ni moja ya makubaliano mkataba wa mradi huo na yakimaliza kutumika yanarudi Halmashauri kwa ajili ya shughuli zingine za kutoa huduma kwa wananchi kupitia wataalamu.

"Mradi huu unaenda kuleta mabadiliko chanya na uboreshaji wa miundo mbinu mbalimbali ya Manispaa ya Kibaha na kuwa na mwonekano mzuri na kuleta urahisi wa usafiri na usafirishaji,"alisema Mawazo.

Alisema kuwa katika miradi hiyo ya Tactic wanakwenda kuitekeleza kwa ubora zaidi na Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha inaenda kuwa ya kwanza na mfano kwa Halmashauri zingine katika utekelezaji na usimamizi wa miradi hii nchini.

"Wananchi wa Kibaha wanapaswa kujivunia na kutangaza maendeleo yanayofanywa na serikali hii kwani Manispaa ya Kibaha ina neemeka na dira ya Rais na mmeona maendeleo yanavyokuja kwa kasi na tutakuwa Halmashauri ya mfano kwa kila kitu,"alisema Mawazo.

Akisoma taarifa ya mradi huo Ofisa Utumishi  Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mrisho Mlela alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Samia Suluhu Hassan kwa kuleta miradi yenye fedha nyingi na usimamizi mzuri wa viongozi wa Wilaya na Mkoa kwa utekelezaji wa Ilani kwa maslahi ya Manispaa ya Kibaha.

Mlela alimpongeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dk Rogers Shemwelekwa kwa usimamizi mzuri wa masuala mbalimbali ya mapato usimamizi wa miradi pamoja na tija katika utendaji wa Halmashauri.

Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha imepokea magari hayo mawili kutoka kwenye Mkataba wa mradi wa Tactic ambapo yatatumika katika mradi wa ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilometa 4.8 Tughe-Anglikana barabara ya Picha ya Ndege - Lulanzi na soko la Loliondo Mnarani.

MADARASA JANJA KUPUNGUZA CHANGAMOTO UPUNGUFU WA WALIMU NCHINI

MEYA wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dk Nicas Mawazo amezindua Darasa Janja (Live Teaching) Shule ya Sekondari Bundikani na kuiomba Serikali kuanzisha madarasa hayo kote nchini ili kukabiliana na upungufu wa walimu

Mawazo alitoa ombi hilo wakati akizindua darasa hilo shuleni hapo ambapo shule hiyo ni Sekondari ya Kata ya Maili Moja Wilayani Kibaha na kuwa darasa janja yatasaidia kuwafanya wanafunzi kuwa na ari ya kusoma.

Amesema kuwa mwalimu mmoja anayefundisha kupitia darasa janja moja anaweza kufundisha shule zote ambazo zitakuwa zimeunganishwa kwenye mfumo huo wa darasa la aina hiyo kote nchini kwa wakati mmoja.

"Mfumo huu wa darasa janja ni mzuri kwa kukabiliana na changamoto ya upungufu wa walimu kwani mwalimu mmoja anauwezo kufundisha shule zote ambazo zimeunganishwa kwenye mfumo huo,"amesema Nicas.

Aidha amesema kuwa pia mbali ya kufundisha wakati mmoja pia yale aliyofundisha mwalimu huyo yanaweza kurekodiwa na kuwafundisha wanafunzi wengine kwa ubora ule ule.

"Jambo zuri ni kuwa walimu wote wanaofundisha kupitia madarasa janja wote ni wale wenye umahiri wa kufundisha hivyo watawajengea wanafunzi uwezo mkubwa wa kujifunza na kupata ujuzi,"amesema Mawazo.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mrisho Mlela amesema kuwa wataendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa madarasa janja kwenye shule za sekondari.

Mlela amesema kuwa wameendelea kuboresha sekta ya elimu kwa kujenga shule tatu za mfumo wa Kiingereza na shule hizo zote zimejengwa kutokana na fedha za mapato ya ndani na kutengeneza madawati viti na meza 4,000 kwa shule za msingi na sekondari.

Naye Mkuu wa Shule ya Bundikani Bernard Muyenjwa amesema kuwa wanaishukuru Serikali kwa kuwapatia darasa hilo janja kwani litarahisisha katika ufundishaji na kupunguza changamoto ya upungufu wa walimu.

Muyenjwa amesema kuwa kuanzishwa kwa darasa janja hilo shuleni kwao kutasaidia walimu kufundisha bila ya kuchoka wala kutumia nguvu kubwa na kuwapa wanafunzi umahiri na kujua namna ya kutumia teknolojia.

mwisho

Thursday, July 30, 2026

BINTI ATUHUMIWA KUMUUA MAMA YAKE MZAZI KWA KUMKATAZA KWENDA KWENYE SHEREHE YA KUMBUKIZI YA KUZALIWA RAFIKI YAKE.

BINTI mwenye umri wa miaka (16) Mkulima na Mkazi wa Kijiji cha Msoga Chalinze Wilayani Bagamoyo anashikiliwa kwa tuhuma za mauaji ya mama yake mzazi baada ya kumzuia kuhudhuria sherehe ya kumbukumbu ya kuzaliwa rafiki yake.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani Salim Morcase kuwa Mama yake Hadija Shaha ambaye ni mlemavu wa miguu.

Morcase amesema kuwa tukio hilo lilitokea Julai 28 mwaka huu majira ya saa 5:00 usiku huko katika Kijiji cha Msoga Chalinze ambapo mtuhumiwa alimuua mama yake kwa kumchoma kwa kitu chenye ncha kali.

"Chanzo cha tukio hilo ni kuwa marehemu alimkataza binti yake Rahma Tito kwenda kuhudhuria sherehe ya kuzaliwa ya rafiki yake (birthday party) iliyokuwa inafanyika maeneo ya jirani na Hospitali ya Msoga,"amesema Morcase. 

Amesema kuwa baada ya binti huyo kuzuiwa kwenda kwenye sherehe alianza kumshambulia mama yake kisha kumchoma na kitu chenye ncha kali kichwani.

"Julai 29 mwaka huu  majira ya saa 1:00 asubuhi fundi ujenzi alifika nyumbani kwa Shaha kufuata mfuko wa saruji na fedha yake ya ujenzi ndipo alipogonga mlango na kufunguliwa na binti  wa marehemu jirani huyo aligundua kuna mwili wa marehemu ukiwa umelala sakafuni ukiwa na majeraha kichwani yanayotiririsha damu,"amesema Morcase.

Amesema kuwa mwili wa marehemu ulipelekwa Hospitali ya Msoga ambapo ulifanyiwa uchunguzi wa daktari kisha ulikabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya taratibu za mazishi. 

"Mara baada ya upelelezi kukamilika mtuhumiwa atafikishwa mahakamani kujibu tuhuma hizo na Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani linatoa rai kwa wazazi walezi viongozi wa dini na jamii kwa ujumla kushirikiana katika malezi ya watoto,"amesema Morcase.

Aidha amesema kuwa ushirikiano huo utasaidia kubaini tabia na changamoto za watoto wao kwenye makuzi ili hatua zichukuliwe mapema kabla hayajatokea madhara yoyote.

Tuesday, July 28, 2026

MAGANYA ATAKA WANACHAMA WASICHAFUANE.

MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa Fadhili Maganya amewataka wanachama waache kuchafuana kuelekea uchaguzi wa ndani mwakani.

Maganya aliyasema hayo Mjini Kibaha alipokuwa  akizungumza na viongozi wa Jumuiya hiyo pamoja na wanachama wa CCM Kibaha Mjini wakati wa ziara yake kutembelea Mkoa wa Pwani kukagua uhai wa chama na miradi ya maendeleo.

Alisema kuwa chama hakina shida nao bali wafuate miongozo na utaratibu wa chama kama unavyoelekeza.

"Mwakani tunaingia kwenye uchaguzi wa ndani baadhi wameanza kuchafuana tusikubali hali hiyo asitokee mtu wa kutoa maelekezo bali chama ndiyo kinatoa maelekezo,"alisema Maganya.

Aidha alisema kuwa watu wanaanza kukinzana na uchaguzi wa mwakani na unabeba taswira ya uchaguzi wa 2030 hivyo chama kitangulizwe mbele na siyo mtu.

"Tuwaacheni walioko madarakani wafanye kazi kwani muda wa uchaguzi bado watu wasubiri hadi muda utakapofika,"alisema Maganya.

Alibainisha kuwa kuna baadhi ya watu wanasiasa wa upinzani na wanaharakati wamekuwa wakibeza na kutoa lugha za maudhi na kudhalilisha wasipewe nafasi kwani wakidai eti serilali iliyopo ni haramu.

"Tusiruhusu tabia hiyo kwani Rais Dk Samia Suluhu anafanya kazi kubwa kwa kushirikiana na chama chake kwani Tume ya Uchaguzi iliita vyama vyote na kutaka visaini sheria za uchaguzi lakini baadhi vilikataa,"alisema Maganya.

Aliongeza kuwa uchaguzi ulikuwa wazi kwa kila chama na viongozi walichaguliwa kwa utaratibu uliowekwa na Tume ya Uchaguzi hivyo havina haja ya kulalamika.

"Kamati za siasa za chama zinapaswa kutatua migogoro ya ardhi kwa kushirikiana na serikali ambayo inafanya kazi kubwa kutatua migogoro hiyo,"alisema Maganya.

Naye Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya (CCM-NEC) kupitia Jumuiya ya Wazazi na Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Hamoud Jumaa alisema kuwa Jumuiya imekuwa mstari wa mbele kuimarisha chama.

Jumaa alisema kuwa kwa sasa Jumuiya hiyo imeimarika sana na kuwa mhimili mkubwa wa chama katika utekelezaji wa ilani.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka alisema kuwa Jumuiya ya Wazazi imefanya kazi kubwa katika utekelezaji wa ilani.

Koka alisema kuwa kwenye uchaguzi Mkuu Jumuiya hiyo iliongoza kwa kupiga kura na kuufanya Mkoa wa Pwani kuongoza kwenye suala la kura.

Awali akitoa taarifa ya Wilaya Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Moses Magogwa alisema kuwa uptikanaji wa huduma kwa sasa kwa wananchi ni asilimia 98.

Magogwa alisema kuwa Hslmashauri ya Manispaa imekuwa ikifanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato ambapo asilimia 60 yanatokana kodi na ushuru mbalimbali wa huduma.

Alisema kuwa ujenzi wa barabara ya njia sita kutoka Maili Moja hadi Picha ya Ndege unatarajia kuanza na barabara kwa ajili ya magari ya mizigo nao utaanzia Picha ya Ndege.

ZAHANATI YA KILIMAHEWA YAWAPUNGUZIA UMBALI WANANCHI KUPATA HUDUMA

MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi CCM Fadhili Maganya amepongeza ujenzi wa Zahanati ya Kilimahewa Kata ya Tangini Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha na kuitaka kuweka dirisha la Wazee ili waweze kupata huduma kwa urahisi wakati wa kupata matibabu.

Maganya ameysema hayo Mjini Kibaha alipotembelea Zahanati hiyo wakati wa ziara yake ya kutembelea Mkoa wa Pwani kuimarisha uhai wa chama na kutembelea miradi ya maendeleo na kusema kuwa ujenzi huo ni wa mapato ya ndani.

Amesema kuwa wazee waliambiwa kuwa watatengewa dirisha kwa ajili ya kuwapatia huduma hivyo ni vema dirisha hilo likawepo kwa ajili ya kuwahudumia na siyo kusema kuwa wapishwe ili wahudumiwa bali wawe na dirisha lao maalum.

"Tuliahidi kuwa tutawawekea dirisha lao maalum kwa ajili ya kupata huduma hivyo Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha lazima ihakikishe inawawekea dirisha lao ili wapate huduma za afya kwani wao lazima wahudumiwe vizuri pasipokuwa na changamoto,"amesema Maganya. 

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Catherine Saguti alisema kuwa lengo ni kurahisha upatikanaji wa huduma za afya kwenye Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha na ulianzishwa kutokana ongezeko la mahitaji ya huduma za afya kwenye eneo hilo.

Saguti amesema kuwa ujenzi ulianza Juni 2024 Halamshauri ilipokea kiasi cha shilingi milioni 233.5 na wananchi walichangia kiasi cha shilingi milioni 1 na shilingi milioni 50 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba hivyo kufanya gharama za mradi kuwa shilingi milioni 284.6.

Amesema kuwa serikali imeajiri wauguzi 32 ambapo Zahanati hiyo ina watumishi saba wanaotoa huduma na Zahanati hiyo imepatiwa watumishi wawili hivyo hakuna upungufu wa watumishi.

Zahanati ilianza kutoa huduma Aprili 2026 na hadi sasa imeshatoa huduma kwa watu 1,103 na inatoa huduma mbalimbali.