Thursday, May 14, 2026

UMOJA WA WANAUME MKOMBOZI WASAIDIA KUPATIKANA DAMU CHUPA 13



UMOJA wa Wanaume Mkombozi (UWWM) umefanikisha kupatikana kwa damu kiasi cha chupa 13 kwa ajili ya Kituo cha Afya Kata ya Pangani Wilayani Kibaha.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa umoja  kilichopo Mtaa wa Mkombozi Wilayani Kibaha Katibu wa UWWM Mwinjilisti William Wami alisema kuwa lengo ni kuisaidia wagonjwa kwenye kituo hicho.

Wami alisema kuwa umoja huo ulianzishwa kwa ajili ya kuisaidia jamii katika masuala mbalimbali ili kuleta maendeleo kwenye Mtaa huo na Wilaya nzima ya Kibaha.

"Mbali ya kuchangia damu pia tumepanda miti kwenye eneo itakapojengwa Zahanati kwenye Kituo cha Afya cha Kata ya Pangani na Shule ya Msingi Mkombozi lengo likiwa ni kutunza mazingira kwenye maeneo hayo,"alisema Wami.

Kwa upande wake mgeni rasmi kwenye uzinduzi huo Diwani wa Kata ya Pangani John Katele ambaye alimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Kibaha alisema kuwa umoja huo umeonyesha moyo wa kibinadamu wa kujitolea ili kunusuru maisha ya wengine.

Katele alisema kuwa damu ni muhimu sana hasa kwa wanawake ambao wanajifungua kwani huhitaji damu nyingi au wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji kwenye kituo hicho. 

Katele alisema kuwa jamii inapaswa kujitolea ili kukabiliana na changamoto ya damu kwenye kituo hicho hivyo kupunguza changamoto hiyo kwani damu huhitajika wakati wote.

Naye Mganga Mfawidhi wa Kituo hicho Alex Ditopile alisema kuwa anawashukuru wananchi waliojitolea damu kwani tayari wameshaanza kuzalisha mama wajawazito na matumizi ya damu ni makubwa kwani kwa mwezi wanatumia chupa 10.

Ditopile alisema kuwa kwa sasa wana chupa tano na inapotokea wameishiwa damu huchukua Kituo cha Afya cha Lulanzi na kwa sasa wanapokea wagonjwa wengi tangu kituo hicho kilipofunguliwa Desemba 2025.

Mwenyekiti wa Mtaa wa Mkombozi Jackson Msaki alisema kuwa kikundi hicho ni kwa ajili ya wanaume wote kwenye Mtaa huo na haubagui mtu yoyote.

Msaki alisema kuwa umoja huo umeweza kuhamasisha kupatika kwa usafiri wa daladala kutokea Mtaa huo hadi Mbezi kujenga choo na kuvuta maji kwenye soko jipya.

Umoja huo ulianzishwa mwaka 2025 kikiwa na wanachama 105 huku kwa sasa kikiwa na wanachama 265 hai wakiwa 205 kikiwa na kauli mbiu ya "Mwanaume Kichwa cha Familia".


Thursday, May 7, 2026

RAIS SAMIA ANAENDELEA KUPELEKA FURAHA NA NEEMA KWA WATUMISHI WA UMMA TANZANIA.-KIKWETE


Nimezungumza na maafisa tawala na RasilimaliWatu , katika mkutano uliofanyika Ukumbi wa AICC, Arusha na kuwakumbusha kutekeleza wajibu wao na kuleta furaha kwa watumishi wa umma ili kwa upande mwengine nao wapeleke furaha na neema kwa Watanzania . 

Nimeyaeleza hayo kufuatia maamuzi mbalimbali yanayofanywa na serikali ya awamu ya sita katika kuhakikisha maslahi ya Watumishi wa umma nchini yanaboreka. 

Uamuzi wa hivi karibuni wa Serikali kupandisha madaraja watumishi 219,042 ni hatua ya kihistoria katika kuimarisha utumishi wa umma nchini Tanzania. 

Hatua hii ambayo imepata ridhaa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na ongezeko la mishahara ya watumishi wa umma (2025): +35.1% , Ongezeko la kima cha chini sekta binafsi (2025/26): +33.4% 

Aidha Sekta mbalimbali zinakwenda athiriwa na maboresho haya ikiwemo afya, elimu, kilimo, mawasiliano, usafirishaji, nishati, viwanda, biashara, hoteli, michezo, uvuvi, baharini, madini ,utamaduni n.k 


Matokeo haya kitakwimu zinaonyesha kasi ya mageuzi ya kiutumishi chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan ambayo inaonyesha uongozi wa kimkakati unaoweka mbele ustawi wa watumishi na ufanisi wa taasisi za umma.

Tuesday, May 5, 2026

VIJANA WATAKA MFUMO UKOPAJI UBORESHWE KUVUTIA VIJANA

UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Wilaya ya Kibaha Mjini umeishauri Wizara ya Maendeleo ya Vijana kuangalia upya mfumo wanamna ya kuwapata vijana kukopa ili wengi waweze kunufaika.

Akizungumza ofisini kwake Katibu wa (UVCCM) Kata ya Tangini Lazaro Benjamin alisema kuwa Wizara inapaswa kuweka mfumo rafiki na kuweka masharti nafuu.

Benjamin alisema kuwa kuweka masharti magumu kunakwamisha vijana wengi kupata fursa ya kufikia mikopo hiyo inayowalenga vijana.

"Vijana ndio nguvu kazi ya Taifa wanapokosa mitaji wanakosa fursa ya kujiajiri na matokeo yake ni kuongezeka kwa ukosefu wa ajira umasikini na hata kukata tamaa,"alisema Benjamin.

Alisema kuwa kuna umuhimu sasa wa kuongeza bajeti ya mikopo ya vijana ili iwafikie wengi zaidi pia kutoa elimu ya ujasiriamali na usimamizi wa fedha ili mikopo itumike kwa ufanisi.

"Lengo liwe ni kuwafikia vijana wengi zaidi iwezekanavyo kwani maendeleo ya Taifa letu yanategemea uwezeshaji wa vijana wake na wafanye maboresho ili kuhakikisha uwiano unazingatiwa,"alisema Benjamin.

Aidha alisema kuwa wanamshukuru Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kutenga kiasi cha shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kuwawezesha vijana kiuchumi kwani hiyo ni hatua kubwa na ya kupongezwa na inaonesha dhamira ya kweli ya serikali katika kuinua vijana wa Taifa la Tanzania.

"Wizara ifanye utafiti kwani takwimu zinaonyesha kuwa jumla ya vijana 30,384 waliomba mikopo hii lakini vijana waliokidhi vigezo vya kukopeshwa ni 1,961tu,"alisema Benjamin.

Aliongeza kuwa idadi kubwa sana ya vijana zaidi ya asilimia 90 hawakupata fursa hiyo utafiti ufanyike ili kujua ni kwa nini idadi hiyo kutokidhi vigezo na kama bajeti ni ndogo basi iongezwe ili asilimia ya vijana wanaoomba mikopo waweze kuongezeka na kupanua wigo wa ajira kwani wakipata watajiajiri.

Sunday, April 26, 2026

Shule

 


INTRNATIONAL

 


SHULE KIMATAIFA

 


ZINGATIENI DIRA YA MAENDELEO

WIZARA ya Elimu Sayansi na Teknolojia imezitaka Shule za Kimataifa nchini kujisajili kwenye mifumo na miongozo ya elimu na kiserikal ili kukidhi matakwa ya kisheria.

Hayo yalisemwa na Dk Maulid Maulid aliyemwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara Caroline Nombo wakati wa kufunga mafunzo ya siku nne kwa wamiliki wa shule hizo juu ya namna ya uendeshaji wa shule hizo mafunzo yaliyofanyika kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere Kibaha.

Maulid alisema kuwa ili elimu inayotolewa na shule hizo za kimataifa lazima zihakikishe zinafanya usajili wao kupitia mifumo iliyowekwa ili kuendana na mfumo wa elimu wa nchi.

"Wamiliki wa shule hizi wanapaswa kufanya usajili kwenye mifumo ya elimu ili elimu inayotolewa itambulike na iwe na ubora unaotambulika na ushindani kimataifa kwa kuzingatia mitaala ya nchi yetu,"alisema Maulid.

Alisema kuwa shule hizo zinapaswa kujisajili kwenye mamlaka mbalimbali za taasisi za elimu ili ziweze kuendana na mifumo iliyopo ikiwemo kwenye Baraza la Mitihani NACTE na mamlaka za serikali.

"Lazima wafuate mifumo yote ya kiithibati na ubora bila kusahau kuzingatia sera ya elimu ambayo ndiyo inayotoa mwongozo wa elimu kwa taasisi za kielimu,"alisema Maulid.

Aidha alisema kuwa pia mitaala yao iendane na Dira ya Taifa ya Maendeleo ili wanafunzi wawe na uelewa wa juu ya Dira hiyo ambapo kwa sasa ni ya 2050.

"Mitaala yao iendane na Dira ya Maendeleo kwani inazingatia utoaji elimu bora ambayo inaangalia viaumbele vya nchi katika kuleta maendeleo kwa wananchi,,'alisema Maulid.

Kwa upande wake moja ya washiriki wa mafunzo hayo ambaye ni mhasibu wa shule ya kimataifa ya Renie Joshua John alisema kuwa mafunzo hayo yatakuwa chachu kwa shule yake kwani amepata elimu ya namna ya kuweka vizuri masuala ya fedha.

John alisema kuwa wamepata uelewa mzuri wa namna ya kuendesha shule zao na kwa kuzingatia taratibu na miongozo ya kisheria ambayo wanapaswa kuifuata.

Mafunzo hayo yaliandaliwa na Tanzania School Leadership Institute (TSLI) na kusimamiwa na Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia waliwahusisha wamiliki, walimu wakuu, wahasibu na viongozi wa shule za kimataifa hapa nchini