Tuesday, July 21, 2026

WANANCHI WAJITOLEA KUFUFUA BARABARA

MTAA wa Machinjioni umefungua barabara ya kuelekea Shule ya Msingi Mamlaka na kurahisisha watumiaji kupita kwa urahisi wakiwemo wanafunzi kwenda Shuleni na magari ya kutoa huduma inapotokea dharura kama vile moto.

Barabara  hiyo ilijifunga wakati wa ujenzi wa barabara ya lami ya kutoka Tamco-Mapinga kuelekea Bagamoyo hivyo kusababisha watumiaji wakiwemo  wanafunzi kuzunguka umbali mrefu ili kwenda shule na kwenye makazi hasa wanaotumia usafiri wa magari na pikipiki.

Akizungumza wakati wa zoezi la kujitolea kufungua barabara hiyo ambayo miaka ya nyuma ilikuwa ikipitika Mwenyekiti wa Mtaa wa Machinjioni Kata ya Tangini Wilaya ya Kibaha Aidan Mchiwa alisema kuwa barabara hiyo ni muhimu kwa wananchi wa eneo hilo.

Mchiwa alisema kuwa barabara hiyo ni muhimu hasa pale endapo ikitokea dharura kama vile moto au wagonjwa ilikuwa ikiwalazimu kuzunguka mbali hasa kwa matumizi ya vyombo vya moto ikiwemo magari na pikipiki.

"Tulikaa na wananchi na kukubaliana kuchanga kiasi cha shilingi 16,000 kila Kaya ili kufanikisha ufunguaji wa barabara hiyo na wananchi waliridhia na zoezi kuanza ambapo pia tuliwasiliana na Dawasa kwani kuna bomba linapita hapo hivyo walitoa wataalamu wao na kutuelekeza namna na kuchimba ili tusiharibu bomba hilo la maji,"alisema Mchiwa.

Emanuel Sabath alisema kuwa wanaushukuru uongozi wa Mtaa kwa kuwafungulia barabara hiyo hivyo kuwarahisishia na kuwaondolea usumbufu kuzungukia mbali na kupita kwenye eneo la mtu.

Sabath alisema kufunguka barabara hiyo kutarahisisha wananchi kupata huduma ikiwa ni pamoja na inapotokea mgonjwa anataka kupelekwa Hospitali wakiwemo wanawake wajawazito na hata gari la zimamoto kupita kwani kulishawahi kutokea moto lakini gari hilo likashindwa kupita.

Alisema kuwa hata wanafunzi wanaosoma Shule ya Msingi Mamlaka hasa wanaotoka maeneo ya Kilimahewa ambapo iliwabidi wazunguke kupita sehemu nyingine ambapo huwabidi kuzunguka hivyo kuchelewa kufika shuleni.

MASAUNI AWATAKA WANANCHI KUTUMIA FURSA YA HEWA UKAA




Na Mwandishi Wetu, Rufiji

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhandisi Hamad Masauni amewataka wananchi kutumia miradi ya utunzaji wa mazingira ili kupata hewa ukaa na kujiongezea kipato.

Masauni aliyasema hayo Wilayani Rufiji alipokuwa akizungumza na wananchi wakati wa ziara yake Mkoani Pwani kutembelea miradi mbalimbali ya maendeleo.

Alisema kuwa hewa ukaaa ni jambo kubwa la kiuchumi hivyo wananchi watumie kila fursa inayogusa hewa ukaa watumie rasilimali vizuri kupitia misitu. 

"Rufiji ina fursa nyingi za uzalishaji hewa ukaa kupitia, misitu migomba mikorosho kwani hii ni biashara nzuri watumieni wataalam ili wawape moingozo ili kuongeza kipato kwa kutumia fursa hii,"alisema Masauni.

Aidha alisema kuwa mabadiliko ya tabia nchi ni chanzo cha biashara kupitia mkataba wa Paris baada ya kukubaliana nchi zenye rasilimali za kupunguza hewa ukaa zilipwe.

"Kupitia kilimo madini na faida ya kuhifadhi miti tutalipwa hiyo ni changamoto muifanyie kazi kwani mna rasilimali za kutosha za kuwa miradi ya hewa ukaa,"alisema Masauni

Aliongeza kuwa Watanzania wanapaswa kutunza amani iliyopo na kuachana na yale yanayoweza kuharibu amani ya nchi kama ilivyokuwa kipindi cha nyuma.

"Kipindi cha nyuma kulitokea changamoto hata wanaccm walikuwa hawavai sare za chama lakini sasa watu wana amani hivyo tunzeni amani kwani  umuhimu wa amani unajulikana na vijana wanasababu ya kuenzi umoja na kurithisha watoto wetu na Muungano ndiyo kiungo cha amani kupitia  waasisi wa taifa letu wametuachia msingi wa amani,"alisema Masauni.

Aliipongeza Wilaya ya Rufiji kwa kutekeleza kikamilifu kupitia ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwenye miradi mbali mbali ya maendeleo ya elimu afya miundombinu kilimo maji.

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Pwani Mwinshehe Mlao alisema kuwa Wilaya hiyo imepiga hatua kubwa ya kimaendeleo ukilinganisha na zamani kupitia uongozi wa Rais Dk Samia Suluhu Hassan.

Mlao alisema kuwa kwa ujumla Mkoa umepiga hatua kubwa ya maendeleo hivyo watu wanapaswa kuona jinsi gani maendeleo yaliyopatikana chini ya CCM.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge 
alisema kuwa mwaka wa fedha Mkoa ulipangiwa kukusanya bilioni 88 lakini hadi Juni 30 mwaka huu tayari zimekusanywa bilioni 135 na kuwa mkoa wa pili baada ya Dar es Salaam. 

Kunenge alisema kuwa Mkoa unajivunia Rais kwa kuwatumikia Watanzania na Rufiji ina miradi mikubwa ya uwekezaji na moja mradi alionyesha Urusi ni kilimo cha ndizi kupitia moja ya kampuni kubwa afrika.

Alisema kuwa kwa sasa kuna mifugo mingi na kuna ranchi ndogo na uchumi usitegemee chanzo kimoja ili kuwa salama kwa kutumia bahari na utalii kwani huwezi kushindana na mabadiliko ya dunia ni kijini na dira 2050 inataka kuwa na ajira milioni nane pato la Taifa trilioni moja pato la mwnanchi milioni 18 kwa mwaka.

Akikaribisha ugeni wa Waziri Mkuu wa Wilaya ya Rufiji Luteni Kanali Fredrick Komba alisema kuwa Wilaya hiyo imefanikiwa kupanda miti ya mikorosho ipatayo milioni 1.5.

POLISI KATA MAILIMOJA AMTEMBELEA MZEE NA KUTOA MSAADA.





Na Mwandishi Wetu, Kibaha

Polisi Kata wa Mailimoja, Mkaguzi wa Polisi, Tupilike Mwabulambo ameambatana na Stesheni Sajenti Lusekelo Mwakalinga wa Wilaya ya Kibaha kumtembelea mzee Hamisi Nampatima wa mtaa wa Uyaoni ikiwa ni sehemu ya mpango wa kuwafikia wahitaji waliopo kwenye kata yake na kutoa msaada.

Akikabidhi baadhi ya mahitaji kwa mzee huyo Julai 20, 2026 INSP Tupilike alieleza kuwa kuna makundi mbalimbali katika jamii ambao wana changamoto ikiwemo za kiusalama na mahitaji muhimu hivyo anatembelea kaya hizo kuwasikiliza na kutoa kile alichojaliwa kwa wakati huo.

Kwa upande wake Mzee Hamis Nampatima, alilishukuru Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani kwa msaada wanaompatia kwani sio mara ya kwanza kufika kwake, Mara kadhaa Sajenti wa Polisi Salum Ally wa Polisi Wilaya ya Kibaha amekua akimsaidia kwa kumpatia pesa na mahitaji mbalimbali ya nyumbani.

Naye, Mwenyekiti wa Mtaa wa Uyaoni, Katani humo, Bw. Fadhili Kindamba alipongeza Jeshi la Polisi kwa namna wanavyoshirikiana na wananchi kuimarisha ulinzi na usalama na kutatua changamoto zao zingine za kijamii.

Sunday, July 19, 2026

WANANCHI MTAA WA MACHINJIONI WAJITOLEA KUFUNGUA BARABARA

MTAA wa Machinjioni umefungua barabara ya kuelekea Shule ya Msingi Mamlaka na kurahisisha watumiaji kupita kwa urahisi wakiwemo wanafunzi kwenda Shuleni na magari ya kutoa huduma inapotokea dharura kama vile moto.

Barabara  hiyo ilijifunga wakati wa ujenzi wa barabara ya lami ya kutoka Tamco-Mapinga kuelekea Bagamoyo hivyo kusababisha watumiaji wakiwemo  wanafunzi kuzunguka umbali mrefu ili kwenda shule na kwenye makazi hasa wanaotumia usafiri wa magari na pikipiki.

Akizungumza wakati wa zoezi la kujitolea kufungua barabara hiyo ambayo miaka ya nyuma ilikuwa ikipitika Mwenyekiti wa Mtaa wa Machinjioni Kata ya Tangini Wilaya ya Kibaha Aidan Mchiwa alisema kuwa barabara hiyo ni muhimu kwa wananchi wa eneo hilo.

Mchiwa alisema kuwa barabara hiyo ni muhimu hasa pale endapo ikitokea dharura kama vile moto au wagonjwa ilikuwa ikiwalazimu kuzunguka mbali hasa kwa matumizi ya vyombo vya moto ikiwemo magari na pikipiki.

"Tulikaa na wananchi na kukubaliana kuchanga kiasi cha shilingi 16,000 kila Kaya ili kufanikisha ufunguaji wa barabara hiyo na wananchi waliridhia na zoezi kuanza ambapo pia tuliwasiliana na Dawasa kwani kuna bomba linapita hapo hivyo walitoa wataalamu wao na kutuelekeza namna na kuchimba ili tusiharibu bomba hilo la maji,"alisema Mchiwa.

Emanuel Sabath alisema kuwa wanaushukuru uongozi wa Mtaa kwa kuwafungulia barabara hiyo hivyo kuwarahisishia na kuwaondolea usumbufu kuzungukia mbali na kupita kwenye eneo la mtu.

Sabath alisema kufunguka barabara hiyo kutarahisisha wananchi kupata huduma ikiwa ni pamoja na inapotokea mgonjwa anataka kupelekwa Hospitali wakiwemo wanawake wajawazito na hata gari la zimamoto kupita kwani kulishawahi kutokea moto lakini gari hilo likashindwa kupita.

Alisema kuwa hata wanafunzi wanaosoma Shule ya Msingi Mamlaka hasa wanaotoka maeneo ya Kilimahewa ambapo iliwabidi wazunguke kupita sehemu nyingine ambapo huwabidi kuzunguka hivyo kuchelewa kufika shuleni.

Friday, July 17, 2026

NSSF YAWATAKA WAAJIRI KUTUMIA MSAMAHA WA TOZO

Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umetangaza nafuu kwa waajiri wenye malimbikizo ya michango kwa kuwapatia fursa ya msamaha wa tozo zitokanazo na ucheleweshaji wa michango, huku ukiwataka kuchangamkia fursa hiyo ili kupunguza mzigo wa madeni, kuimarisha uzingatiaji wa sheria na kulinda haki za wafanyakazi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema kuwa msamaha huo, ulioanza kutekelezwa tarehe 1 Juni 2026, utaendelea hadi 31 Desemba 2026. 

Bw. Mshomba alieleza kuwa tangu kuanza kwa msamaha huo, waajiri wameonyesha mwitikio chanya ambapo hadi sasa zaidi ya waajiri 6,000 wamejitokeza kutumia fursa hiyo na Mfuko umekwishakusanya zaidi ya shilingi bilioni 46 za michango tangu kuanza kwa msamaha huo tarehe 1 Juni 2026.

“Tunawasihi waajiri wote kutumia fursa hii mapema. Fedha ambazo wangezilipa kama tozo wanaweza kuzielekeza katika shughuli za uzalishaji, upanuzi wa biashara, kuongeza tija na kuboresha ustawi wa wafanyakazi,” alisema Bw. Mshomba.

Alisema msamaha huo utaendelea hadi tarehe 31 Desemba 2026, ambapo waajiri watakaolipa malimbikizo yote ya michango ya msingi ifikapo tarehe 31 Agosti 2026 watanufaika na msamaha wa asilimia 100 ya tozo.

Alifafanua kuwa waajiri watakaokamilisha malipo yao kati ya Septemba na Oktoba 2026, watanufaika na msamaha wa asilimia 75, huku wale watakaolipa kati ya Novemba na Desemba 2026 wakipata msamaha wa asilimia 50.

Aidha, alisema waajiri ambao hawakuwa na malimbikizo ya michango hadi tarehe 31 Mei 2026 lakini walikuwa na tozo pekee, watanufaika na msamaha wa asilimia 100 endapo wataendelea kuwasilisha michango yao kwa wakati hadi mwezi Desemba 2026.

Bw. Mshomba alisema fursa hiyo imetolewa ili kuwapa waajiri nafasi ya kurekebisha hali ya ulipaji wa michango na kutumia fedha ambazo zingelipwa kama tozo katika shughuli za uzalishaji, kuongeza tija na kuboresha mazingira ya kazi.

“Fedha ambazo waajiri wamekuwa wakizilipa kwa ajili ya kufidia tozo zinaweza kuelekezwa katika kuboresha maeneo yao ya kazi, kuongeza tija na kuimarisha uzalishaji.

Ndiyo maana fursa hii imetolewa ili waajiri wanufaike,” alisema.
Alisema ulipaji wa michango kwa wakati ni muhimu kwa kuwa unamwezesha mfanyakazi kupata haki zake za hifadhi ya jamii wakati anapopata majanga mbalimbali ikiwemo kustaafu.

NSSF YAENDELEA KUIMARIKA
Katika hatua nyingine, Bw. Mshomba alisema NSSF imeendelea kuimarika katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita, ambapo thamani ya Mfuko imeongezeka kutoka shilingi trilioni 4.8 mwezi Machi 2021 hadi kufikia zaidi ya shilingi trilioni 11.6 Juni 2026.

Alisema ukuaji huo umechangiwa na ongezeko la wanachama na michango, uwekezaji wenye tija, mazingira mazuri ya uwekezaji pamoja na matumizi ya teknolojia katika kuboresha huduma.

Alieleza kuwa kupitia mifumo ya TEHAMA, waajiri na wanachama sasa wanaweza kufuatilia na kuwasilisha michango, kufuatilia madai ya mafao na kupata huduma mbalimbali bila kulazimika kufika katika ofisi za NSSF.

Kuhusu ulipaji wa mafao, Bw. Mshomba alisema Mfuko umeendelea kuboresha mifumo yake ambapo kwa sasa mafao mengi hulipwa ndani ya siku 20, tofauti na siku 60 zinazotakiwa kisheria.

“Lengo letu ni kuhakikisha mwanachama anapata stahiki zake kwa wakati. Endapo kuna ucheleweshaji mara nyingi chanzo huwa ni mwajiri kutowasilisha michango kwa wakati,” alisema.

UWEKEZAJI WENYE TIJA, SKIMU YA HIFADHI KUONGEZA WANUFAIKA
Akizungumzia uwekezaji, alisema NSSF inaendelea kutekeleza miradi ya kimkakati inayochangia ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira, akitolea mfano Kiwanda cha Sukari cha Mkulazi ambacho kimeendelea kuongeza uzalishaji, kutoa ajira na kuwawezesha wakulima wanaokizunguka.

Kuhusu Skimu ya Hifadhi, Bw. Mshomba alisema mpango huo umewezesha wananchi waliojiajiri kujiunga na mfumo wa hifadhi ya jamii na kunufaika na mafao mbalimbali ikiwemo pensheni ya uzee, pensheni ya ulemavu, pensheni ya urithi, mafao ya uzazi, msaada wa mazishi pamoja na huduma za matibabu.

“Tunawahimiza waliojiajiri kujiunga kupitia Skimu ya Hifadhi kwa sababu mpango huu unabadilisha maisha yao na kuwapa uhakika wa kunufaika na mafao mbalimbali. Lengo letu ni kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa Staa wa Mchezo katika kujilinda dhidi ya changamoto za maisha,” alisema Bw. Mshomba.

Alisema NSSF itaendelea kushirikiana na waajiri, wafanyakazi na wadau mbalimbali katika kuimarisha mfumo wa hifadhi ya jamii nchini na kuhakikisha unaleta manufaa kwa Watanzania wengi zaidi.

Wednesday, July 8, 2026

DKT. NICAS MAWAZO AKUTANA NA BALOZI KAIRUKI NCHINI UINGEREZA, WAJADILI FURSA ZA UWEKEZAJI KIBAHA

London, Uingereza | Julai 8, 2026
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kibaha, Dkt. Nicas Mawazo ambaye yupo nchini Uingereza katika ziara nchini humo, leo Julai 8, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Uingereza, Mheshimiwa Balozi Kairuki.

Katika mazungumzo hayo, Balozi Kairuki amepongeza juhudi zinazofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuimarisha diplomasia ya uchumi, kuvutia uwekezaji na kusukuma mbele agenda ya maendeleo ya taifa.

Aidha, Balozi Kairuki ameipongeza Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha kwa mafanikio yake katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo na ukusanyaji wa mapato ya ndani, akieleza kuwa halmashauri hiyo imeendelea kuwa miongoni mwa halmashauri zinazofanya vizuri nchini.

Mazungumzo kati ya viongozi hao yamejikita katika kutafuta fursa za ushirikiano wa kiuchumi kwa Manispaa ya Kibaha, ikiwemo namna ya kuvutia wahisani, wawekezaji na wadau wa maendeleo kutoka Uingereza ili kuwekeza katika sekta mbalimbali zenye mchango mkubwa kwa maendeleo ya manispaa hiyo.

Dkt. Mawazo amesema kuwa mazungumzo hayo ni sehemu ya jitihada za kuitangaza Manispaa ya Kibaha kimataifa na kufungua milango ya ushirikiano itakayochochea uwekezaji, ukuaji wa uchumi na uboreshaji wa huduma kwa wananchi.

Friday, July 3, 2026

KUNENGE AMSHUKURU RAIS DK SAMIA KUKUZA VIPAJI VYA MICHEZO KWA VIJANA

MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge amemshukuru Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kuinua vipaji vya wanamichezo vijana ili kuwa tegemeo kwa Taifa.

Kunenge ameyasema hayo wakati akizindua michezo ya riadha Kitaifa kwenye uwanja wa Filbert Bayi Mkuza Wilayani Kibaha.

Amesema kuwa Rais ameweka mazingira mazuri kwa wanamichezo nchini ambapo kwa sasa nchi inafanya vizuri kwenye michezo mbalimbali ikiwemo riadha.

"Nawapongeza Shirikisho la Riadha Tanzania kwa kuweka misingi mizuri kwa vijana wadogo ambao wameonyesha umahiri wa kukimbia licha ya kuwa na umri mdogo huu ndiyo uwekezaji mzuri kwenye vipaji,"amesema Kunenge.

Aidha amesema kuwa riadha ni mchezo ambao hupambani na mpinzani wako bali unapambana na rekodi hata ukishinda kama hujafikia rekodi nzuri bado hujapata mafanikio.

"Nimefurahi nimewaona manguli wa riadha nchi kama vile Steven Akwari, Juma Ikangaa, Filbert Bayi, Seleman Nyambui hawa waliiletea nchi sifa kubwa huko duniani vijana wanapaswa kuwaiga ili nao wafanye vyema,"alisema Kunenge.

Amebainisha kuwa Mkoa wa Pwani uko kwenye mipango mbalimbali ya kujenga viwanja ambavyo vitakuwa na ubora ili kupata wanamichezo wazuri wa baadaye.

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya ufundi wa Shirikisho la Riadha Tanzania Alfredo Shahanga amesema kuwa wanajivunia kwa wanariadha wake kufanya vizuri akiwemo Alfonce Simbu kwa kushinda medali ya dhahabu kwenye mbio za marathoni za Dunia za Tokyo.

Shahanga amesema kuwa changamoto kubwa ni upungufu wa fedha viwanja vizuri vyenye vifaa vya kisasa na uwekezaji kwa vijana hata hivyo wanashirikiana na wadau mbalimbali ili kuhakikisha changamoto hizo zinapungua na mchezo unachezwa.

Naye katibu wa Chama cha Riadha Mkoa wa Pwani Elisha Daniel amesema kuwa mashindano hayo yameanza vyema kwani walifanya maandalizi vizuri na matarajio mwaka huu mafanikio yatakuwa makubwa.

Daniel akizungumzia juu ya timu ya mkoa huo amesema kuwa maandalizi ya timu yako vizuri na wanategemea kufanya vizuri kwani vijana wameandaliwa vizuri na walimu wao lengo ni kuupambania mkoa.