HALMASHAURI ya Manispaa ya Kibaha imezindua magari mawili yatakayotumika kwenye mradi wa ujenzi wa barabara za lami kwenye kupitia mradi wa uboreshaji miundombinu ya Miji na Vijiji (TACTIC) wenye thamani ya shilingi bilioni 19.8
Akindua magari hayo ambayo yatatumika kwenye mradi huo Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dk Nicas Mawazo alisema magari hayo yatawezesha utekelezaji mradi kuwa rahisi.
Mawazo alisema kuwa magari hayo ni moja ya makubaliano mkataba wa mradi huo na yakimaliza kutumika yanarudi Halmashauri kwa ajili ya shughuli zingine za kutoa huduma kwa wananchi kupitia wataalamu.
"Mradi huu unaenda kuleta mabadiliko chanya na uboreshaji wa miundo mbinu mbalimbali ya Manispaa ya Kibaha na kuwa na mwonekano mzuri na kuleta urahisi wa usafiri na usafirishaji,"alisema Mawazo.
Alisema kuwa katika miradi hiyo ya Tactic wanakwenda kuitekeleza kwa ubora zaidi na Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha inaenda kuwa ya kwanza na mfano kwa Halmashauri zingine katika utekelezaji na usimamizi wa miradi hii nchini.
"Wananchi wa Kibaha wanapaswa kujivunia na kutangaza maendeleo yanayofanywa na serikali hii kwani Manispaa ya Kibaha ina neemeka na dira ya Rais na mmeona maendeleo yanavyokuja kwa kasi na tutakuwa Halmashauri ya mfano kwa kila kitu,"alisema Mawazo.
Akisoma taarifa ya mradi huo Ofisa Utumishi Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mrisho Mlela alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Samia Suluhu Hassan kwa kuleta miradi yenye fedha nyingi na usimamizi mzuri wa viongozi wa Wilaya na Mkoa kwa utekelezaji wa Ilani kwa maslahi ya Manispaa ya Kibaha.
Mlela alimpongeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dk Rogers Shemwelekwa kwa usimamizi mzuri wa masuala mbalimbali ya mapato usimamizi wa miradi pamoja na tija katika utendaji wa Halmashauri.
Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha imepokea magari hayo mawili kutoka kwenye Mkataba wa mradi wa Tactic ambapo yatatumika katika mradi wa ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilometa 4.8 Tughe-Anglikana barabara ya Picha ya Ndege - Lulanzi na soko la Loliondo Mnarani.






