UWEKEZAJI kwenye sekta ya elimu ni moja ya njia zinazoonyesha utayari wa kushirikiana kati ya serikali na sekta binafsi katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Elimu Kibaha Robert Shilingi wakati wa kuadhimisha miaka 25 ya Shule ya Msingi Kibaha Independent Pre and Primary School (KIPS).
Shilingi amesema kuwa Dira ya Maendeleo inataka ushirikiano na sekta binafsi kwenye masuala mbalimbali kiwemo kuinua sekta ya elimu ili kuweza kufikia malengo.
"Ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi umetajwa kuwa muhimu katika kuimarisha sekta ya elimu nchini hususani kwa kuongeza fursa za watoto kupata elimu pamoja na kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia,"amesema Shilingi.
Amesema kuwa serikali inaunga mkono wadau wa elimu wakiwemo wa sekta binafsi kwani wanaisaidia serikali katika utoaji elimu ili kufikia mafanikio kwenye sekta hiyo.
"Katika kutimizi miaka 25 kupitia Makampuni ya Njuweni imewekeza katika Shule tatu za Msingi ambazo ni KIPS, KIPS Annex na KIPS Msangani pamoja na Njuweni Institute of Hotel Catering and Tourism Management na Shule tatu za Sekondari ambazo ni Vuchama Ugweno Islamic, Mangio na Pwani Sekondari,"amesema Shilingi.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Makampuni ya Njuweni Alhaj Yusuf Mfinanga amesema kuwa anaishukuru serikali kwa kumpa ushirikiano katika uboreshaji wa elimu kwenye Shule hizo.
Mfinanga amesema kuwa Shule ya Sekondari ya Pwani inatarajiwa kuanza kupokea wanafunzi wa Kidato cha Kwanza mwaka 2027 hatua ambayo itaongeza fursa za elimu ya Sekondari kwa vijana wa Kibaha Pwani na maeneo mengine.
Nae Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi KIPS Salim Nkumbilwa amesema kuwa jumla ya wanafunzi 179 wamehitimu Darasa la Saba kutoka Shule tatu za KIPS, KIPS Annex na KIPS Msangani.





