WAKAZI wa Mtaa wa Muheza Kata ya Maili Moja Wilayani Kibaha Mkoani Pwani wameomba kupatiwa ruti ya Daladala kutoka Maili Moja kwenda kwenye Mtaa huo na kupunguza gharama za pikipiki ambazo ni 4,000.
Aidha wamesema usafiri wao mkubwa ni pikipiki na hutumia kiasi cha shilingi 8,000 kwenda na kurudi kufuata mahitaji au kupata huduma za msingi za kila siku.
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara ulioandaliwa na Diwani wa Kata ya Maili Moja mwananchi Veronica Christopher alisema kuwa maombi yao ni kupatiwa ruti ili wawe na usafiri wa uhakika.
Christopher alisema kuwa suala la usafiri ni changamoto kubwa kwani hakuna usafiri wa uhakika zaidi ya pikipiki ambapo gharama zake ni kubwa sana na kipindi cha mvua gharama inaongezeka kwani barabara inaharibika sana kutokana na utelezi na tope jingi.
"Kwa sasa maisha ni magumu sana hebu fikiria ili uende kufuata mahitaji au huduma uwe na 8,000 au zaidi kwa kwenda na kurudi na kwenda huko ni lazima kwani ndiko huduma na mahitaji muhimu hupatikana hivyo tukipata ruti ya Daladala itatupunguzia gharama,"alisema Christopher.
Alisema kuwa Maili Moja ndiyo Mjini na kwa wale wanaofanya safari kwenda maeneo mbalimbali lazima wafike Maili Moja ambako ndiko wanakopata mahitaji lakini usafiri gharama ni kubwa sana za kwenda na kurudi.
Akijibu hoja hiyo Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kibaha Dk Nicas Mawazo alisema kuwa mpango huo ni mzuri na leo atakutana na wenye viti wa Mitaa iliyoko kwenye Kata ya Maili Moja na LATRA ofisini kwake ili kupanga ruti hiyo.
Mawazo alisema kuwa hoja hiyo ni ya msingi kwani Serikali ina lengo la kuwapunguzia mzigo wananchi kwa kuwatatulia changamoto kama hizo ambazo ziko ndani ya uwezo wa serikali.
Naye Diwani wa Kata ya Maili Moja Ramadhan Lutambi alisema mpango wa kuboresha barabara kupitia Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini TARURA imetenga shilingi milioni 50 kwa kila Kata ambapo Mtaa huo wenye wakazi 12,000 na Mtaa wa Maili Moja wenye wakazi 4,000 watanufaika.
Lutambi alisema kuwa fedha hizo zimetengwa kwenye bajeti ya mwaka 2026/2027 kwa ajili ya uboreshaji wa miundombinu ya barabara ikiwemo madaraja na makalavati.
Alisema kuwa baadhi ya maeneo mvua ikinyesha kwenye vivuko hakupitiki kutokana na maji kujaa ambapo kipaumbele kitawekwa kwenye maeneo ya Mkwanda Machokodo Makanyaga na Kwakamese kutawekwa Makalavati.