Monday, June 29, 2026

POLISI MKOANI PWANI LINACHUNGUZA VIFO VYA MWANAMKE NA MTOTO

JESHI la Polisi Mkoani Pwani linafanya uchunguzi wa tukio la mauaji ya mwanamke mmoja na mtoto ambao hawakufahamika yaliyotokea Mbwewe Wilaya ya Kipolisi Chalinze Mkoa wa Pwani.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani Salim Morcase kwa vyombo vya habari zilisema kuwa tukio hilo la mauaji ya watu wawili lililotokea Juni 2 mwaka huu  majira ya saa 9:00 alasiri huko Kitongoji cha Nung'uli Kijiji cha Kwang'andu Kata ya Mbwewe Halmashauri ya Chalinze Wilaya ya Bagamoyo.

Taarifa hiyo ilibainika kuwa watu hao ni mwanamke
mmoja anayekadiriwa kuwa na umri kati ya miaka (20-25) na mtoto ambaye hakufahamika jinsia yake kutokana na kuungua sana na moto mwenye
umri unaokadiriwa kuwa miaka (3-6) ambao mpaka sasa bado hawajafahamika wala watu waliosababisha mauaji hayo.

"Ikumbukwe katika eneo la tukio hilo zilikutwa tiketi mbili za basi la Passion Video Coach linalofanya safari zake kati ya Dar es Salaam kwenda Miono kupitia Chalinze zilizokatwa tarehe Mei 31 mwaka huu,"alisema taarifa hiyo.

Taarifa zilisema kuwa tiketi hizo zilikiwa na majina ya Adela na Modest ambapo Jeshi bado linachunguza chanzo cha mauaji hayo wakati miili ya wahanga imehifadhiwa katika Hospitali ya Msoga Halmashauri ya Chalinze.

Kutokana na mauaji hayo Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani linaendelea kutoa wito kwa mtu yeyote anayewafahamu watu hao au mwenye taarifa zozote zinazoweza kusaidia kuwatambua wafike Ofisi ya kamanda wa Polisi Mkoa
wa Pwani.

 "Au wapige simu namba 073900995, 065837601 0 na 0753855570 ili kuendelea kusaidia uchunguzi na kuwapata ndugu wa marehemu kwa wakati,"iliongeza taarifa hiyo.

AKINAMAMA WATAKIWA KUWAKUMBUKA VIJANA WAKIUME

MWANASIASA mkongwe na aliyewahi kuwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto Sophia Simba ameitaka jamii kuwawezesha kiuchumi vijana wa kiume ambao wamesahaulika.

Simba ameyasema hayo Mjini Kibaha wakati wa kuadhimisha miaka 10 ya Kikundi cha Super Women 2017 na kuwa baada ya wanawake kufanikiwa vijana wakiume nao waangaliwe.

Amesema kuwa kwa muda mrefu jamii iliwekeza kudai haki za wanawake ambapo kwa sasa wamepiga hatua ya kimaendekeo baada ya nguvu kubwa kutumika huku wale wa kiume wakiwa wamesahaulika.

Simba ambaye pia aliwahi kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora alisema kuwa kwa sasa vijana wa kiume wana hali mbaya kiuchumi.

"Tumshukuru Mungu kwani kwa sasa wanawake angalau wamepiga hatua kiuchumi tuwaangalie na vijana wakiume ili nao kwa kuwajengea uwezo wa kiuchumi,"amesema Simba.

Aidha alikipongeza kikundi hicho kwa mafanikio waliyoyapata kwa muda huo tangu kuanzishwa kwake kwani baadhi ya vikundi vinaanzishwa na havichukui muda mrefu vinakufa.

Naye mwanzilishi wa kikundi hicho Beth Msimbe amesema kuwa wamepata mafanikio makubwa ikiwa ni pamoja na kukopeshana fedha kwa riba nafuu kupitia mfuko wa kikundi kwa fedha wanazoweka ambapo mkopo ni mara tatu ya fedha waliojiwekea.

Msimbe amesema kuwa wameweza kukuza biashara zao na kuwa wafanyabiashara wakubwa pia wamekuwa wakifanya matendo ya huruma kwa watu wenye uhitaji na kuwataka wanawake wawe na wavumilivu kwa kufuata sheria na taratibu.

Kwa upande wake mwenyekiti kikundi hicho Betha Kimambo amesema kuwa wanatarajia kuanzisha mradi wa kukodisha vyombo ili kuongeza kipato ndani ya kikundi.

Kimambo amesema kuwa mbali ya kupata mafanikio kuna baadhi ya changamoto ikiwa ni pamoja na baadhi ya wanachama kujitoa.





Sunday, June 28, 2026

VIJANA WENYE VIPAJI VYA MICHEZO WATAKIWA KUWA NA NIDHAMU

VIJANA wenye vipaji vya michezo nchini wametakiwa kusoma kwabidii na kuwa na nidhamu ili waweze kufikia viwango vya juu na kuwa tegemeo kwa Taifa.

Hayo yamesemwa na Gilbert Maregesi ambaye alimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Kibaha wakati wa kufunga tamasha la michezo lililoandaliwa na Compassion Kanda ya Mashariki lililofanyika kwenye Viwanja vya Shirika la Elimu Kibaha Tumbi.

Maregesi amesema kuwa serikali imekuwa ikiwekeza kwenye sekta ya michezo kwa vijana ili kuendeleza vipaji vyao na kuwa tegemeo kwa Taifa kwenye sekta hiyo ambayo pia ni ajira kwa vijana.

"Ili kulinda vipaji vyenu mnapaswa kuwa na nidhamu ili muweze kufika mbali kwani mbali ya kunufaika binafsi pia mtaliwezesha Taifa kuwa na wachezaji wazuri watakaoliwakilisha Taifa kwenye michezo mbalimbali,"amesema Maregesi. 

Naye mwakilishi wa meneja wa Compassion Kanda ya Mashariki Daudi Lawi inayoundwa na mikoa ya Pwani Morogoro na Dar es Salaam amesema tamasha hilo la awamu ya nne limeshirikisha wanamichezo 430 kutoka mikoa hiyo.

Lawi amesema kuwa baada ya kukamilisha tamasha hilo lilobeba ujumbe wa Kipaji changu Mtaji wangu watachaguliwa wachezaji bora ambao watawakilisha Kanda hiyo kwenye mashindano ya Taifa.

Kwa upande wake James Mhina Kanda ya Mlandizi ambao walikuwa wenyeji wa mashindano hayo amesema kuwa michezo hiyo inajenga mahusiano na kipaji ni msaada katika maisha.

Mwenyekiti wa Mashindano hayo Lucas Kiluwasha amesema kuwa vipaji vyao ndiyo mtaji wao hivyo wavitumie vizuri na kuwataka wadau wa michezo kushuhudia michezo ili wachukue vipaji na kuviendeleza.

Rais wa Vijana Kanda ya Mashariki amesema kuwa michezo hiyo imewasaidia kuwaongezea ujuzi na kukuza vipaji vyao na kujumuika na kufahamiana kwani hiyo ndiyo njia ya mafanikio.

Mgeni rasmi ametoa fursa ya vijana Milovan Kilingo kutoka Gairo na Joshua Joakim wa Mkuza Kibaha kujiunga na bendi ya Jkt Ruvu ili waendeleze vipaji vyao.

Baadhi ya michezo iliyochezwa ni pamoja na mpira wa miguu, pete, riadha na michezo ya ndani ikiwemo sanaa ya uimbaji, upigaji wa vyombo vya muziki, maonyesho ya mavazi na sarakasi na yalishirikisha vijana wenye umri chini ya mi 17 na 22.

MWANADIPLOMASIA OMARY PUNZI ATEULIWA KUSHIRIKI MKUTANO WA CREATIVE

Mwanadiplomasia na Mchambuzi wa Masuala ya Kidiplomasia Siasa , Itifaki na Maadili Omary Punzi ateuliwa kushiriki katika mkutano wa Creative Convergence 2026 . 

Mkutano huu unaojumuisha Africa Creative Market (ACM), Creative Industry Business Summit (CIBS), na Kwimbo National Arts Festival, unafanyika kuanzia Juni 29 hadi Julai 4, 2026 jijini Lusaka, Zambia.

Mkutano huo unaisimamiwa na Wizara ya Vijana, Michezo na Sanaa nchini Zambia 

Utafanyika katika  kumbi za mikutano zilizopo Mulungushi International Conference Centre kuanzia Juni 29 hadi Julai 2, 2026 na kuanzia tarehe 3 hadi 4 Julai 

Tamasha la Sanaa,  tamasha la Kwimbo  huko Polo B, Lusaka Showgrounds. 

Mkutano huo utakutanisha Vijana zaidi 10000  kutoka Bara la Afrika.

kushiriki  Programu na Warsha (Sessions & Masterclasses)

Mijadala ya Biashara, Mijadala inayohusu biashara ya sanaa, filamu, muziki, teknolojia (kama AI), na mitindo.

Mafunzo ya Kitaalamu, Ufikiaji wa masterclasses zinazoendeshwa na washirika wa sekta, mfano mafunzo ya upigaji picha au uigizaji.

Kuunganisha Mtandao wa Biashara (Networking & Deal Rooms)

Ushirikiano wa Kibiashara, mikutano ya kibiashara (kama vile Deal Rooms au Creative Pitch Zone) ambapo wabunifu wanakutana na wawekezaji, wafadhili, na watengeneza sera ili kugeuza mawazo kuwa mikataba ya kazi.

MAWAZO YA VIJANA




SERIKALI imesema kuwa itatumia mawazo ya vijana walioshiriki shindano la Vijana Uchumi Challenge kuwa mpango ambao utaleta suluhisho la namna ya kutatua baadhi ya changamoto ndani ya jamii.

Hayo yalisemwa Kibaha na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Jenifa Omollo wakati wa kufunfa mafunzo ya siku nne kwa vijana 100 walioandika mawazo juu ya masuala ya uchumi kupitia jukwaa la Vijana Uchumi Challenge.

Omollo alisema kuwa mawazo yaliyoandikwa na vijana yameonyesha kuwa yakiboreshwa yanaweza kuwa mpango mzuri ambao unaweza kukabili changamoto mbalimbali ndani ya jamii na Taifa kwa ujumla.

"Mawazo yote yaliyowasilishwa hayataachwa badala yake yataboreshwa na kupatiwa fursa ili yawe mpango ambao utakuwa suluhu kwa baadhi ya changamoto ili kuleta tija na kusaidia Taifa mojawapo likatoa ajira kwa vijana,"alisema Omollo.

Alisema kuwa mawqzo hayo ni bunifu ambazo zimeonyesha jinsi gani vijana walivyokuwa na vipaji ambavyo vitatoa ajira na kuwa na manufaa kwa watu wengi hivyo kulisaidia Taifa.

"Vijana wana fursa nyingi kiuchumi lakini wanakosa taarifa sahihi kwani mawazo kama haya wanaweza kuyapatia fedha za Halmashauri nchini kupitia manunuzi ya umma kwenye mfumo wa Nest au mpango wa yendelezaji vipaji,"alisema Omollo.

Aidha alisema moja ya sekta yenye fursa nyingi ni kilimo ambayo imeajiri asilimia 75 ya Watanzania vijana wanaweza kunufaika kiuchumi kupitia mnyororo wa thamani na fursa kupitia dijitali.

Naye mwenyekiti wa kamati ya Vijana Uchumi Challenge Joseph Malecela alisema kuwa jumla ya mawazo zaidi ya 7,000 ya vijana kote nchini wenye umri kati ya miaka 15 hadi 35 yaliwasilishwa na kuchujwa na kubaki 100 ambayo yatashindanishwa kupata mshindi.

 

Malecela alisema kuwa washiriki hao 100 ambao waliiingia kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere wamechujwa na majaji wabobezi wa masuala ya uchumi na fedha na kubaki 10 watashindana ili kumpata mshindi wa shindano hilo.


Rais Dk Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye kilele cha kumpata kijana mwenye wazo zuri Julai 6 mwaka huu Jjiini Dar es Salaam  kwenye Ukumbi wa Julius Nyerere Internation Convention Centre (JNICC) Jijuni Dar es Salaam.



mwisho

WALIPA KODI WATAKIWA KUONYESHA UZALENDO KWA KULIPA KWA WAKATI

WALIPA kodi wa Mkoa wa Pwani wametakiwa kulipa kwa wakati ili kuonesha uzalendo kwa nchi na mapato yanayokusanywa yaweze kutumika kwenye miradi mikubwa ya kimkakati ya maendeleo.

Hayo yalisemwa na Lilian Shirima aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Kibaha wakati wa mazoezi ya wadau na walipakodi ikiwa ni kuelekea miaka 30 ya mamlaka hiyo.

Shirima alisema kuwa utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati ya maendeleo inatokana na kodi zinazolipwa hivyo wanapaswa kulipa kodi kwa wakati ili zifanikishe malengo ya utekelezaji wa miradi hiyo.

"Wafanyabiashara wanapaswa kutoa risiti pale wanapofanya mauzo na wananchi nao wanapaswa kudai risiti pale wanaponunua bidhaa kwani huo ndiyo uzalendo wa nchi,"alisema Shirima.

Kwa upande wake Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani Peter Eliona    alisema kuwa wafanyabiashara wanapaswa kuwa na utamaduni wa kulipa kodi kwani kukwepa kulipa kodi ni kurudisha nyuma maendeleo ya nchi ambapo mapato hayo yanaleta maendeleo.

Eliona alisema kuwa kulipaji kodi ni uzalendo hivyo wanapaswa kulipa kodi kwani fedha zinazokusanywa kazi yake kubwa ni kuleta maendeleo kupitia miradi mbalimbali hasa ile mikubwa kama vile miradi ya elimu afya miundombinu ya barabara na reli.

Alisema kuwa fedha hizo matumizi yake ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo ya wananchi hivyo kutolipa kodi na kurudisha nyuma jitihada za serikali za kuleta maendeleo kwa wananchi.

Aidha alisema kuwa katika kuelekea miaka 30 ya TRA wamefanya shughuli mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuimarisha afya kwa kufanya mazoezi kufanya usafi kwenye eneo la wafanyabiashara Chalinze.

"Ulipaji wa kodi unasaidia serikali katika utoaji wa huduma mbalimbali kwa wananchi zikiwemo za kiafya na huduma zote ambazo wananchi wanapaswa kuzipata kwenye maeneo yao,"alisema Eliona.

Naye Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara (JWT) Mkoa wa Pwani Abdala Ndauka alisema kuwa ulipaji kodi umekuwa rahisi kwa sasa kutokana na mahusiano mazuri yaliyopo baiba ya wafanyabiashara na mamlaka.

Ndauka alisema mtaji mkubwa wa mfanyabiashara ni afya njema hivyo mazoezi hayo yanasaidia kuimarisha afya na kukabiliana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

MAWAZO VIJANA CHALLENGE KUTUMIKA KIMAENDELEO



SERIKALI imesema kuwa itatumia mawazo ya vijana walioshiriki shindano la Vijana Uchumi Challenge kuwa mpango ambao utaleta suluhisho la namna ya kutatua baadhi ya changamoto ndani ya jamii.

Hayo yalisemwa Kibaha na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Jenifa Omollo wakati wa kufunfa mafunzo ya siku nne kwa vijana 100 walioandika mawazo juu ya masuala ya uchumi kupitia jukwaa la Vijana Uchumi Challenge.

Omollo alisema kuwa mawazo yaliyoandikwa na vijana yameonyesha kuwa yakiboreshwa yanaweza kuwa mpango mzuri ambao unaweza kukabili changamoto mbalimbali ndani ya jamii na Taifa kwa ujumla.

"Mawazo yote yaliyowasilishwa hayataachwa badala yake yataboreshwa na kupatiwa fursa ili yawe mpango ambao utakuwa suluhu kwa baadhi ya changamoto ili kuleta tija na kusaidia Taifa mojawapo likatoa ajira kwa vijana,"alisema Omollo.

Alisema kuwa mawqzo hayo ni bunifu ambazo zimeonyesha jinsi gani vijana walivyokuwa na vipaji ambavyo vitatoa ajira na kuwa na manufaa kwa watu wengi hivyo kulisaidia Taifa.

Naye mwenyekiti wa kamati ya Vijana Uchumi Challenge Joseph Malecela alisema kuwa jumla ya mawazo zaidi ya 7,000 ya vijana kote nchini wenye umri kati ya miaka 15 hadi 35 yaliwasilishwa na kuchujwa na kubaki 100 ambayo yatashindanishwa kupata mshindi.

Malecela alisema kuwa washiriki hao 100 ambao waliiingia kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere wamechujwa na majaji wabobezi wa masuala ya uchumi na fedha na kubaki 10 watashindana ili kumpata mshindi wa shindano hilo.

Rais Dk Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye kilele cha kumpata kijana mwenye wazo zuri Julai 6 mwaka huu Jjiini Dar es Salaam kwenye Ukumbi wa Julius Nyerere Internation Convention Centre (JNICC) Jijuni Dar es Salaam.







mwisho


Thursday, June 25, 2026

MAWAKALA WAITWA KUCHANGAMKIA VIPAJI TUMBI KIBAHA

MAWAKALA wa michezo ikiwemo soka wametakiwa kujitokeza kushuhudia vipaji vya wacehzaji chini ya miaka 17 na 22 kwenye mashindano ya Compassion ili kuwa na timu bora zitakazozalisha wachezaji wakulitumikia Taifa ambapo moja zao la wachezaji hao ni Dickson Job anayechezea timu ya Yanga.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Lucas Kiluwasha ambaye ni mwenyekiti wa Mashindano ya Compassion Kanda ya Mashariki kwenye Viwanja vya Shirika la Elimu Kibaha Tumbi.

Mashindano hayo ambayo ni ya nne kufanyika yameweza kuwatoa wachezaji wengi akiwemo Dickson Job wa Yanga, Paschal Msindo wa timu ya Azam na Haji Abdala kipa wa timu ya Serengeti Boys chini ya miaka 17 iliyoshika nafasi ya pili kwenye michuano ya Afcon ya vijana iliyofanyika Morocco hivi karibuni.

Mbali ya kuzalisha wachezaji hao ambao wanatambulika pia imezalisha wachezaji wengine ambao wako timu za Yanga B, Azam na Fountain Gate pamoja na msanii wa muziki wa kisasa Dogo Janja na wasanii mbalimbali hapa nchini.

Kiluwasha amesema kuwa mashindano hayo ambayo hufanyika kila mwaka yanashirikisha jumla ya mikoa mitatu ya Pwani, Dar es Salaam na Morogoro ambapo kuna wachezaji zaidi ya 430 kauli mbiu ya mwaka huu inasema “Kipaji Changu Mtaji Wangu”.

“Michezo inayoshindaniwa ni pamoja na soka, mpira wa pete, riadha na michezo ya ndani ikiwa ni pamoja na kupiga vyombo vya muziki, ubunifu wa mavi na sanaa mbalimbali lengo ni kuinua na kuibua vipaji kwa vijana,”alisema Kiluwasha.

Alisema kuwa kwa sasa mara wanapopatikana vijana wa michezo husika huwapeleka ili wakaendeleze vipaji vyao ambapo wa soka huwapeleka kwenye timu zenye Academy ili waweze kukuza vipaji vyao na kujipatia ajira kupitia michezo.

“Changamoto kubwa ni ushiriki mdogo wa wadau kujitokeza kuhudhuria mashindano yao pia baadhi ya wachezaji kwenda kushiriki michezo ya Umisseta na Umitashumta kwani nao hufanya kipindi cha likizo hivyo kuwa na mwingiliano,”alisema Kiluwasha.

Aidha alisem akuwa malengo yao ya baadaye ni kuanzisha timu ya mipra wa miguu ili ishiriki ligi mbalimbali na hatimaye kufika ligi kuu pia wanazikaribisha timu mbalimbali kama zinahitaji wachezaji kuona nao ili kukubalina na kuwachukua ili wakaendeleze vipaji vyao.

Wachezaji hao wanatoka kwenye vituo vya huduma ya mtoto na kijana kwenye makanisa ya Kiinjili na Kipentekoste kwenye mikoa hiyo na wachezaji watakaofanya vizuri watachaguliwa kwenda kushiriki mashindano hayo kitaifa.

Tuesday, June 23, 2026

WAZO BORA LA KIJANA KUNYAKUA MILIONI 50

KIJANA mwenye wazo bora kati ya vijana 100 watakaowania kinyanganyiro cha Vijana Uchumi Challenge anatarajiwa kujinyakulia kitita cha shilingi milioni 50.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Dk Kedmon Mapana wakati akizungumza na vijana hao 100 watakaokuwa kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere iliyopo Kibaha Mkoani Pwani.

Mapana amesema kuwa wapili akijinyakulia shilingi milioni 20 na watatu milioni 10 ambapo vijana wanaoshiriki ni wenye umri chini ya miaka 35 kutoka nchi nzima.

"Wizara ilitoa shindano la vijana kutoa wazo la kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia mawazo ya vijana kukuza ubunifu na Ujasiriamali na kuwapa vijana fursa ya kuonyesha mawazo yao ya kibiashara na miradi ya kibunifu inayoweza kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi,"amesema Mapana.

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya Vijana Uchumi Challenge Joseph Malecela amesema kuwa jumla ya mawazo zaidi ya 7,000 ya vijana kote nchini yaliwasilishwa na kuchujwa na kubaki 100 ambayo yatashindanishwa kupata mshindi.

Malecela amesema kuwa washiriki hao 100 ambao wameingia kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere watachujwa na majaji wabobezi wa masuala ya uchumi na fedha na kubaki 30 na baadaye 10.

Kilele kinatarajiwa kufanyika Jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi atakuwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan.

VIJANA 100 KUWANIA MILIONI 50 VIJANA UCHUMI CHALLANGE

NAIBU Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Dk Kedmon Mapana amesema vijana kuwa na ujuzi na mtaji ni suluhisho la kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050.

Ameyasema hayo Mjini Kibaha kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere wakati akifungua Jukwaa la Vijana Uchumi Challenge.

Mapana amesema kuwa Waziri wa Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Joel Nanauka alizindua shindano la vijana kwa ajili ya kuwawezesha vijana nchini Tanzania kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na ubunifu. 

"Lengo kuu la mpango huu ni kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia mawazo ya vijana kukuza ubunifu na Ujasiriamali na kuwapa vijana fursa ya kuonyesha mawazo yao ya kibiashara na miradi ya kibunifu inayoweza kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi,"amesema Mapana.

Amesema kuwa pia ni kuongeza ajira kwa kusaidia miradi ya vijana kuanzishwa au kukua ambapo shindano linakusudia kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa kuwezesha vijana kujiajiri na kuajiri wengine.

"Kwa wale ambao hawatafanikiwa kushinda mawazo yao yatachukuliwa na kufanyiwa kazi kwa kupewa mafunzo kutokana na mawazo yao ya bunifu zao kupitia sekta mbalimbali zikiwemo za kilimo uvuvi mifugo tehama na ujasiamali,"amesema Mapana.

Aidha amesema vijana wasilalamike bali watoe mawazo na suluhisho nini kifanyike hata ikitokea changamoto kama za kupanda bei ya mafuta ili uchumi wa nchi uwe stahimilivu

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya Vijana Uchumi Challenge Joseph Malecela amesema kuwa jumla ya mawazo zaidi ya 7,000 ya vijana kote nchini yaliwasilishwa na kuchujwa na kubaki 100 ambayo yatashindanishwa kupata mshindi.

Malecela amesema kuwa washiriki hao 100 ambao wameingia kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere watachujwa na majaji wabobezi wa masuala ya uchumi na fedha na kubaki 30 na baadaye 10.

Amesema kuwa washindi 10 watakwenda kwenye kilele kitakachofanyika Jijini Dar es Salam Julai 6 ambapo mshindi atapata kiasi cha shilingi milioni 50 huku wapili akijinyakulia shilingi milioni 20 na watatu milioni 10 ambapo vijana wanaoshiriki ni wenye umri chini ya miaka 35.

Kilele kinatarajiwa kufanyika Jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi atakuwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan.

PWANI YAKUSANYA BILIONI 266

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani imefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 266 katika kipindi cha miaka 10 iliyopita na kuvuka malengo yaliyowekwa ya kukusanya shilingi bilioni 235 katika kipindi hicho.

 

Akizungumza kwenye Kongamano la Mamlaka hiyo ya kutimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake Meneja wa TRA Mkoa wa Pwani Peter Jackson alisema kuwa mafanikio hayo ni ongezeko la asilimia 113 ya makusanyo kwa kipindi hicho.

 

Jackson alisema kuwa mafanikio hayo yametokana na ushirikiano ulioonyeshwa na wafanyabiashara na wadau wote wa kodi ambapo katika kipindi hicho malaengo ya makusanyo yalikuwa ni bilioni 23 lakini zilikusanywa kiasi cha shilingi bilioni 27.

 

“Kwa wastani makusanyo kwa kipindi cha miaka 10 ni ongezeko la asilimia 10 ambapo yamekuwa yakiongezeka hadi kufikia kiasi hicho na kuonyesha jinsi gani mamlaka hiyo inavyopiga hatua katika kuleta maendeleo ya nchi,”alisema Jackson.

 

Alisema kuwa makusanyo yana faida kubwa kwani yanatumika kwa ajili ya kufanya shughuli za kimaendeleo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ikiwemo ya barabara ujenzi wa reli ya kisasa SGR huduma za afya, huduma za elimu na masuala mbalimbali.

 

Aidha alisema kuwa ukusanyaji wa mapato makubwa ndiyo njia ya kukuza uchumi wa nchi ambapo walipa kodi wanapaswa kulipa kwa hiyari na kwa wakati ili kuondoa changamoto za kupewa adhabu ambayo inawarudisha nyuma.

 

“Kwa sasa tumeweka mifumo madhubuti ya ukusanyaji na namna ya kuwafikia kwa urahisi walipa kodi na kuwaondolea usumbufu wa kufika ofisini badala yake wanauwezo wa kulipa au kufanya shughuli zote wakiwa maeneo yao jambo ambalo limerahisisha utendaji kazi,”alisema Jackson.

 

Akizungumzia kuhusu changamoto alisema kuwa ukuaji wa uchumi usio rasmi umekuwa ni tatizo kwani unakuwa nje ya mfumo rasmi hivyo kusababisha kukosekana kwa mapato kutokana na kukwepa au kupunguza kodi kuongezeka kwa biashara mtandaoni biashara haramu na za magendo ambazo huathiri ushindani wa kibiashara..

 

Kwa upande wake mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT) Mkoa wa Pwani Abdala Ndauka alisema kuwa baadhi ya wafanyabiashara hawana uelewa juu ya masuala ya ulipaji kodi hivyo kuna haja ya kutolewa elimu ya kutosha.

 

Ndauka alisema kuwa ulipaji kodi unapaswa kuwa rafiki na si kama adhabu bali uwe rafiki hata hivyo malalamiko kwa sasa yamepungua kwani kwa sasa kumekuwa na majadiliano juu ya changamoto zinazowakumba walipa kodi na watengeneze walipa kodi wapya.

 

Mwenyekiti wa Chemba ya wafanyabiashara Mkoa wa Pwani Said Mfinanga alisema kuwa matumizi ya teknolojia yamesaidia kuwapunguzia muda walipa kodi kwenda ofisini ili kufanya kufanya taratibu mbalimbali juu ya masuala ya ya biashara zao.

 

Mfinanga alisema kuwa mfumo wa teknolojia pia utumike kutoa elimu juu ya masuala ya ulipaji kodi na taratibu zote zihusikanazo na masula ya kodi ili kujenga uelewa wa pamoja kwa walipa kodi na mamlaka hiyo ambayo inajuhusisha na ukusanyaji wa mapato ya serikali.   

 

Naye mwenyekiti wa Shirikisho la Umoja wa Machinga (SHIUMA) Mkoa wa Pwani Philemon Maliga alisema kuwa ili kuboresha ukusanyaji wa mapato Mamlaka inapaswa kuwa na mahusiano bora na mazuri na walipakodi kwnai kundi lao ni kubwa na lina uwezo wa kuchangia pato la serikali.

 

Maliga alisema kuwa TRA iatoe limu kuanzia mashuleni na sehemu mbalimbali ili kuwajengea walipa kodi utamaduni wa kulipa mapato ili kuonyesha uzalendo wa nchi yao kwani kodi ndiyo msingi mkubwa wa maendeleo.

 

Monday, June 15, 2026

TAARIFA KWA UMMA


Ofisi ya Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, inapinga na kukanusha vikali taarifa ya uongo na upotoshaji inayosambaa mitandaoni, ikidai kuwa Dkt. Kikwete anahusishwa na mradi unaodaiwa kuwa wa uwekezaji unaowaahidi Watanzania kipato cha uhakika kupitia jukwaa la kifedha linalotumia teknolojia ya akili mnemba

Taarifa hiyo inadai kuwa maelfu ya Watanzania tayari wamenufaika na mradi huo baada ya kuwekeza kiasi cha shilingi 653,000, huku wakiahidiwa kupata zaidi ya shilingi 9,200,000 kwa mwezi. Madai hayo si ya kweli hata kidogo.

Ofisi ya Rais Mstaafu inapenda kuweka wazi kwamba Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete hajawahi kushiriki, kuidhinisha, kutangaza, kuunga mkono, wala kuhusika kwa namna yoyote ile na mpango huo wa kifedha. 

Ofisi yake haijawahi kuruhusu matumizi ya jina, picha, au heshima yake kuhusishwa na mradi huo unaodaiwa, na haitajihusisha na shughuli za aina hiyo.

Wananchi wanashauriwa kupuuza taarifa hiyo ya uongo na kuwa makini dhidi ya miradi ya kitapeli na vitendo haramu vya aina hiyo. 

Mtu yeyote atakayekutana na taarifa kama hizo za upotoshaji anapaswa kuzichukulia kama habari za uongo, kuepuka kuzisambaza, kujisajili, au kutuma fedha kwa mtu au jukwaa lolote linalohusishwa nazo.

Sunday, June 14, 2026

PWANI YAENDELEA KUHAMASISHA UCHANGIAJI DAMU KUOKOA MAISHA YA WATU

MKOA wa Pwani umekusanya jumla ya chupa za damu 1,129 kwa ajili ya Hospitali na Vituo vya Afya.

Hayo yamesemwa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani Kusirye Ukio wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mchangiaji Damu wa Dunia kimkoa ambapo maadhimisho hayo yamefanyika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani Tumbi.

Kwa upande wake Msimamizi wa Huduma kwa Mteja na Wachangiaji Damu Salama Makao Makuu Kaito Tamba amesema kuwa kwa sasa mpango ni kukusanya chupa 600,000 kwa mwaka 

Akisoma risala ya siku hiyo Mkuu wa Idara ya Maabara Hospitali ya Tumbi Simon Lupatu amesema kuwa kauli mbiu ya mwaka huu inasema "Changia Damu Okoa Maisha" ambapo wanahitaji mashine kwa ajili ya uzalishaji mazao ya damu.

Naye Mkuu wa Idara ya Kinamama na Uzazi wa Hospitali ya Tumbi Dk Alfonce Moyo amesema kuwa takwimu zinaonyesha vifo vilivyotokea kwa mwezi Januari hadi Juni mwaka huu asilimia 80 vilitokana na kupoteza damu nyingi.

Saturday, June 13, 2026

*SERIKALI YADHAMIRIA KUWAENDELEZA WACHIMBAJI WADOGO NCHINI*

▪️Taarifa ya mapendekezo ya kuwaendeleza Wachimbaji wadogo yawasilishwa

▪️Prof Mkumbo aeleza umuhimu wa sekta ya madini kufikia Dira 2050

Lengo ni Kuongeza Ajira, Kupunguza Umaskini na Kukuza Uchumi

▪️Mfuko wa Dhamana  kutatua changamoto ya mitaji kwa wachimbaji

▪️Serikali yaanzisha mfuko wa Madini kwa ajili ya Utafiti wa Madini

📍 Dar Es Salaam

Serikali imesisitiza kufanyia kazi kwa haraka Mapendekezo yaliyotolewa na Timu ya Wataalamu iliyoundwa Kuishauri Wizara ya Madini kuhusu namna ya Kuwaendeleza Wachimbaji Wadogo Kiuchumi na kueleza kuwa, utatuzi wa changamoto za Mitaji, Teknolojia na upatikanaji wa taarifa sahihi za Kijiolojia kwa Wachimbaji Wadogo wa Madini ni hatua muhimu ya kuongeza ajira kwa watanzania, kupunguza umaskini na kukuza uchumi wa Taifa kuelekea Dira 2050.

Hayo yamebainishwa Juni 13, 2026 jijini Dar Es Salaam  na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, wakati wa hafla ya Kupokea Mapendekezo ya Kuwaendeleza Wachimbaji Wadogo Nchini na kusisitiza kwamba, maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha mipango ya maendeleo inajibu changamoto tatu kuu za taifa ambazo ni kuongeza mitaji kwa wananchi, kuzalisha ajira na kupunguza umaskini.

Amesema kuwawezesha wachimbaji wadogo kupata mitaji na teknolojia, kunafungua fursa za kuongeza uzalishaji, ajira na kipato cha wananchi na kuongeza kuwa hiyo ndiyo njia mojawapo ya kupambana na umaskini.

‘’Kazi kubwa ya Waziri ni kutoa mwelekeo wa kisera wa taasisi au wizara anayoiongoza. Kwa muda niliokaa kwenye Wizara yangu, Mhe. Mavunde amekua akijua kipaumbele anachokitaka na jinsi ya kukipata,’’amesisitiza Prof. Mkumbo.

Ameongeza kwamba, hali ya umaskini nchini  bado ipo kwa kiwango cha juu na kutolea mfano wa Mkoa wa Geita ambao unaoongoza kwa shughuli za uchimbaji madini ya dhahabu nchini ambapo  hali ya umaskini inafikia asilimia 38 na kusisitiza kwamba, wachimbaji wadogo wanapowezeshwa wanasaida kutatua changamoto kama hizo na kuongeza kuwa, Sekta ya Madini imewekwa kama moja ya sekta muhimu za kimageuzi  inayotarajiwa kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi na ajira ambapo awali haikuwa ikibeba watu wengi.

Naye, Waziri wa Madini Anthony Mavunde akizungumza katika halfa hiyo, amesema Serikali iliamua kuunda kamati hiyo kutokana na mchango mkubwa unaotolewa na wachimbaji wadogo katika Sekta ya Madini, licha ya kukabiliwa na changamoto za mitaji, teknolojia na upatikanaji wa huduma za kifedha , hivi sasa wanachangia asilimia 40 ya makusnyo ya maduhuli ya Serikali.

Ameongeza kwamba, kuwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika Sekta ya Madini ndani ya miaka ya hivi karibuni yanaonyesha umuhimu wa kuwawezesha zaidi wachimbaji wadogo ili waongeze mchango wao katika uchumi wa taifa.

Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, Mwaka wa Fedha  2015/16 Sekta ya Madini katika mwaka mmoja iliingiza shilingi bilioni 161 pekee katika Mfuko Mkuu wa Serikali. 

Hata hivyo, kufuatia mageuzi mbalimbali yaliyofanyika ikiwemo mabadiliko ya sheria, kuanzishwa kwa masoko ya madini na udhibiti wa biashara haramu ya madini, makusanyo yameongezeka kwa kiwango kikubwa kufikia Shilingi trilioni 1.107 mwaka 204/25 na mpaka kufikia  tarehe 13, Juni, tayari Serikali imekusanya shilingi trilioni 1.3.

Amesisitiza kuwa jukumu la Serikali yoyote duniani ni kuwawezesha wananchi wake kufanya shughuli za uzalishaji kwa tija zaidi sababu ambayo ilipelekea  Serikali kuweka mkakati maalum wa kuwawezesha wachimbaji wadogo ili waweze kukua na kuwa wachimbaji wa kati na baadaye wakubwa.

Kuhusu changamoto ya mitaji, Waziri Mavunde  amesema Serikali imeanza utekelezaji wa Kampuni ya dhamana ya mikopo (Credit Guarantee Corporation) itakayosaidia  wachimbaji kupata mikopo kutoka taasisi za fedha mbalimbali.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo  Dkt. Victor Tesha  amesema suluhu ya changamoto hizo ni kujenga mfumo jumuishi wa kuwawezesha wachimbaji wadogo kupitia upatikanaji wa mitaji, teknolojia za kisasa, taarifa za kijiolojia na uratibu wa taasisi zinazohusika na sekta hiyo huku akipendekeza kuanzishwa kwa Mfuko wa Madini Tanzania utakaowezesha miradi yenye sifa kupata fedha za kuendeleza uzalishaji, kununua mitambo na kuboresha shughuli za uchimbaji, na kuongeza kwamba, mfuko huo utasaidia kugharamia tafiti na taarifa za kijiolojia kwa wachimbaji.

Ameongeza kuwa, baada ya mfuko huo kukua na kuimarika, hatua itakayofuata itakuwa ni kuanzisha Benki ya Wachimbaji itakayotoa huduma maalumu za kifedha kwa sekta ya madini kwa masharti yanayoendana na mazingira ya wachimbaji.

‘’Kamati pia imependekeza mikopo ielekezwe zaidi katika ununuzi wa mitambo na teknolojia badala ya fedha taslimu pekee, ili kuongeza tija, uzalishaji na usalama katika shughuli za uchimbaji,’’ amesema Tesha.


 Naye, rais wa Shirikisho la Vyama Vya Wachimbaji Wadogo John Bina, ameipongeza Serikali kwa ripoti hiyo na kueleza imetokana  na Serikali kusikiliza na kuyafanyia kazi maoni na changamoto za wachimbaji wadogo, pamoja na kuipongeza kwa kutenga asilimia 10 ya mapato yanayotokana na shughuli za madini kwa ajili ya utafiti.

Wednesday, June 10, 2026

HALMASHAURI YA MANISPAA YA KIBAHA YATOA MIKOPO YA SHILINGI MILIONI 991.5 KWA VIKUNDI

HALMASHAURI ya Manispaa ya Kibaha Mkoani Pwani imetoa mikopo ya jumla ya shilingi milioni 991.5 kwa vikundi 51 vya ujasiriamali.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dk Rogers Shemwelekwa wakati wa hafla ya utoaji mikopo ya robo ya tatu.

Shemwelekwa amesema kuwa fedha hizo kiasi cha shilingi milioni 359 ni kwa vikundi 17 vya wanawake shilingi milioni 557 kwa vikundi 25 vya Vijana.

"Kiasi cha shilingi milioni 75.5 kilitolewa kwa watu wenye ulemavu 17 ambapo fedha hizo zimetokana na asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha,"amesema Shemwelekwa.

Amesema kuwa miradi iliyokopeshwa kwa vikundi hivyo ni pamoja na mradi wa usafirishaji ambapo pikipiki 25 zimetolewa na TOYO moja, Bajaji nne, pia miradi ya ufugaji kuku, uchomeleaji ,ushonaji na hardware.

"Viwanda vidogo vya utengenezaji batiki, sabuni, kilimo cha umwagiliaji, kiwanda na stationery miradi hiyo yote inatokana na vikundi hivyo ambavyo ni vya wajasiriamali,"amesema Shemwelekwa.

Aidha amesema kuwa kwa mwaka wa fedha wa 2024/25 ambapo mikopo ilianza kutolewa mwezi Disemba 2024 kwa kanuni mpya hali ya urejeshaji kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu imefikia asilimia 52. 

"Pia mikopo ya mwaka huu wa 2025/26 ambayo imetolewa kuanzia mwezi Novemba 2025 marejesho yamefikia asilimia 26 ambapo inaashiria marejesho yapo vizuri,"amesema Shemwelekwa.

Kwa upande wake Mgeni rasmi Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka amesema kuwa kutolewa mikopo hiyo ni jitihada kubwa zinazofanywa katika ukusanyaji wa mapato.

Koka amesema kuwa Halmashauri imeendelea kuimarika kwenye upande wa mapato hali ambayo inaongeza utoaji wa mikopo kutokana na asilimia 10 ya mapato.

Naye Mwenyekiti wa Kikundi cha Lulu ya Wajane Kanyenda Mweri alisema kuwa fedha hizo zitawasaidia wao kama wajane kukuza mtaji wao wa ufugaji wa kuku.

Mweri alisema wanaishukuru Halmashauri na Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kurejesha mikopo hiyo ya asilimia 10 baada ya kusitishwa  kwa muda na kuwekwa utaratibu mpya.

Tuesday, June 9, 2026

LULU YA WAJANE KUANZISHA MRADI WA MINOFU YA KUKU

KIKUNDI cha Lulu ya Wajane kilichopo Kongowe Wilayani Kibaha Mkoani Pwani kinatarajia kuanzisha mradi wa uuzaji wa minofu ya kuku.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa kikundi hicho Kanyenda Mweri wakati akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea kikundi hicho ambacho kinajihusisha na ufugaji wa kuku.

Mweri amesema kuwa kikundi chao kinaundwa na wanachama watano kiliwezeshwa na Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha mkopo wa asilimia 10 kiasi cha shilingi milioni 46 ambapo tayari wameshazirejesha.

"Tumeomba mkopo mwingine wa fedha nyingi kidogo ambapo tutanunua mashine ya kuchakata minofu, mashine ya kunyonyolea kuku, mashine ya kutotolesha na kuuza vifaranga, mashine ya kusaga vyakula vya kuku na kufufua mashine ya kusaga unga,"amesema Mweri.

Amesema kuwa tayari wameshafanya utafiti juu ya soko la minofu ambapo mbali ya minofu watauza kuku na viungo vyake ikiwemo miguu, vichwa na vyote vitokanavyo na kuku.

"Uwezo wa kurejesha mkopo tutakaokopeshwa tunao kwani mkopo uliopita tulikopeshwa milioni 46 tukazirejesha mapema kabla ya muda kwani tulipewa miaka mitatu kurejesha lakini tulirejesha kwa miezi 11 tu na kupewa cheti cha wajasiriamali bora,"amesema Mweri.

Aidha amesema kuwa kutokana na mradi wa ufugaji kuku unaoendelea kila mwezi wanajilipa kiasi cha shilingi  100,000 pia wameweza kuwaajiri mabinti wa wawili ambao ni wahitimu wa vyuo wakiwa na diploma ya mifugo ambao ndiyo wanafanya shughuli za kitaalamu na kijana mmoja wa kiume.

"Tunamshukuru Mungu kwani ameweza kutuunganisha na kutupa mshikamano ambao ndiyo siri ya mafanikio yetu na ushirikiano tunaoupata kutoka kwa wataalamu wa Halmashauri na Mkurugenzi,"amesema Mweri..

Amesema kuwa walianzisha kikundi hicho kwa malengo ya kusaidiana kutatua changamoto na kutafuta fursa mbalimbali za ujasiriamali na kûwa na miradi ya kiuchumi endelevu kwani wanawake wanapofiwa na waume zao ndugu huwanyanyasa naa kuwanyanganya mali. 

"Matarajio yetu ni kuwa kikundi imara na hodari ambapo kwa sasa tayari wameanzisha kikundi cha vijana wanawake wanaojulikana kama Lulu Nazi wanaozalisha bidhaa zitokanazo na nazi,"amesema Mweri.

Ameongeza kuwa wanaiomba Halmashauri wawapatie mikopo kutokana na maombi kwani malengo wanakuwa wameshayaweka hivyo kuwakopesha chini ya walichoomba husababisha kufanya malengo yasifikiwe ya kile walichokiombea.

"Pia watoe mikopo kwa muda uliopangwa ambapo wao wanasubiri awamu ya pili tangu Desemba mwaka jana hadi leo bado hawajapata mkopo waliouomba ambapo gharama zinaongezeka za mahitaji mfano chakula cha kuku bei imeongezeka na mkopo hesabu zilizopigwa tayari zinakuwa chini,"amesema Mweri.

Amewataka wanawake wajane kutokata tamaa katika kupambania maisha yafamilia zao kwani wao ndiyo walezi wa familia na kulinda maadili ya watoto wao na kikundi hicho kilianzishwa mwaka 2022 na kimesajiliwa.

mwisho.







 



 

POLISI PWANI KUFANYA UCHUNGUZI KISAYANSI KUCHUNGUZA MADAI MZAZI KUBADILISHIWA MTOTO

JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani linafanya uchunguzi wa kitaalamu na kisayansi ili kubaini ukweli juu ya lalamiko la mwanamke aitwaye Filomena Mataris (36) Mkazi wa Gongo la Mboto Dar es Salaam kudai kubadilishiwa mtoto baada ya kujifungua katika Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo.

Uchunguzi huo unafanyika baada ya mlalamikaji kudai kuambiwa mtoto wake aliyejifungua amefariki na kuzikwa pasipo yeye na mume wake kushiriki mazishi ya mtoto wake ambapo alizikwa na ndugu zake.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani Salim Morcase alisema kuwa Juni 5 mwaka huu Filomena Mataris akiwa na mume wake Caros Kapata walifika kituo cha Polisi Bagamoyo wakilalamika kubadilishiwa mtoto kwenye Hospitali ya Bagamoyo. 

Morcase alisema kuwa walipofika polisi walieleza kuwa Aprili 14 mwaka huu Filomena Mataris alihamia Kerege Wilayani Bagamoyo kwa mtoto wa dada yake aitwaye Avetha Mabadiliko kwa ajili ya uangalizi wa karibu akitokea Gongo la Mboto Dar es Salaam.

"Mnamo Mei 17 mwaka huu majira ya saa 3:000 asubuhi Mataris alipata uchungu wa kujifungua hivyo aliongozana na ndugu yake huyo Mabadiliko kwenda Hospitali ya Kerege kwa ajili ya kujifungua,"alisema Morcase.

Alisema kuwa baada ya kufika hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo daktari alibaini Mataris ana dalili ya uzazi pingamizi hivyo alielekeza apelekwe Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji.

"Iipofika Mei 18 mwaka huu majira ya saa 8:00 usiku Mataris alihamishiwa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo ambapo saa 8:30 usiku alijifungua mtoto wa kiume kwa njia ya upasuaji na alieleza kuwa alimuona mtoto wake na kumbeba akiwa mzima wa afya,"alisema Morcase.

Aidha alisema Mataris alisema kuwa baada ya kupewa huduma na kwenda wodini alioneshwa picha za mtoto kwenye simu ya daktari na kuambiwa ndiye mtoto wake na ameshafariki. 

"Mtoto aliyeonyeshwa kwenye picha alikuwa na changamoto kama vile kichwa kubonyea na kuwa na uvimbe kifuani tofauti na mtoto wake aliyembeba baada ya kujifungua,"alisema Morcase.

Aliongeza kuwa baada ya kuonyeshwa picha hizo aliambiwa na daktari kuwa mwili umekabidhiwa kwa ndugu zake ambao ni Mabadiliko na shangazi
yake aitwaye Adora Mathias kwa ajili ya mazishi. 

"Mtoto huyo alizikwa bila uwepo wa Mataris ambaye ni mama wa mtoto wala baba wa
mtoto hakufahamishwa kuhusu mazishi hayo na mara baada ya kupata taarifa hiyo kutoka kwa familia hiyo Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani lilifungua jalada la uchunguzi lenye
namba BAG/PE/33/2026,"alisema Morcase.

Aliongeza kuwa Polisi walianza ufuatiliaji ulianza ambapo walimhoji Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo Dk. Mariam Ngwele aliyeeleza kuwa baada ya kumpokea Mataris.

Alisema kuwa Dk Ngwele alieleza kuwa Mataris  alijifungua kwa njia ya upasuaji lakini mtoto hakuwa wa kawaida kwani alikuwa na kichwa kilichobonyea na uvimbe sehemu ya kifuani na changamoto ya upumuaji hivyo alifariki muda mfupi baada ya kuzaliwa.

Kamanda Morcase alisema kuwa kutokana na changamoto hiyo Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani linaendelea na uchunguzi zaidi wa kitaalamu
na kisayansi ili kubaini ukweli wa taarifa hiyo.

Sunday, June 7, 2026

MAFANIKIO YA GLOBAL PARTNERSHIP FOR EDUCATION CHINI YA UENYEKITI WA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE

Na Albert Kawogo 

TANGU Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete ateuliwe kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Global Partnership for Education mwezi Septemba 2021, taasisi hiyo imeendelea kuimarisha juhudi za kuboresha elimu katika nchi zinazoendelea duniani. 

Dkt. Kikwete akiwa kiongozi wa kwanza kutoka Afrika kushika nafasi hiyo muhimu katika historia ya shirika hilo,chini ya uongozi wake, GPE imeongeza juhudi za kuhakikisha watoto wengi zaidi wanapata elimu bora, hususan wale wanaotoka katika mazingira magumu, maeneo yenye migogoro, wakimbizi na watoto wenye ulemavu.

Taasisi hiyo imeendelea kushirikiana na serikali mbalimbali duniani kuboresha mifumo ya elimu na kuongeza uwekezaji katika sekta hiyo ambapo ufanisi mkubwa umeonekana.

Moja ya mafanikio makubwa yaliyoshuhudiwa ni kuongezeka kwa ufadhili wa miradi ya elimu katika nchi wanachama. Katika kipindi cha mkakati wa GPE 2025, mamia ya mamilioni ya watoto wamefikiwa kupitia programu za kuboresha upatikanaji wa elimu, mafunzo kwa walimu, usambazaji wa vitabu na ujenzi wa miundombinu ya shule.

Kufikia mwaka 2024, GPE iliripoti kuwafikia watoto milioni 253, kutoa mafunzo kwa walimu milioni 1.9, kusambaza vitabu milioni 169 na kujenga au kukarabati zaidi ya madarasa 36,000.

Aidha, chini ya uenyekiti wa Dkt. Kikwete, GPE imepanua ushirikiano wake kwa kuongeza nchi wanachama na wadau wapya wa maendeleo.

Mwaka 2024, nchi za Jordan na Lebanon zilijiunga rasmi na ushirikiano huo, huku Saudi Arabia ikitangaza mchango mkubwa wa kifedha kwa ajili ya kuboresha elimu katika nchi zenye kipato cha chini.

Katika eneo la usawa wa kijinsia, GPE imeongeza juhudi za kuhakikisha wasichana wanapata fursa sawa za elimu ambapo pia shirika hilo limeimarisha programu za kuwajumuisha watoto wenye ulemavu, wakimbizi na makundi mengine yaliyokuwa yakibaki nyuma katika upatikanaji wa elimu.

Dkt. Kikwete ambaye ni Rais mstaafu wa Tanzania ameongoza juhudi za kuhamasisha ufadhili zaidi wa elimu duniani, akisisitiza kuwa elimu ni msingi wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii

 Kupitia  mikutano yake mbalimbali ya kimataifa, Dkt Kikwete amekuwa mstari wa mbele kwenye kutetea uwekezaji mkubwa katika elimu ili kukabiliana na changamoto zilizotokana na athari za COVID-19, migogoro ya kimataifa na mabadiliko ya tabianchi.

Kwa ujumla, kipindi cha uenyekiti wa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete  GPE 

imeonyesha mafanikio makubwa hasa katika kupanua fursa za elimu, kuimarisha ubora wa kujifunza, kuongeza ushirikiano wa kimataifa na kuhakikisha watoto walio katika mazingira magumu wanapata haki yao ya msingi ya elimu bora.

Wednesday, June 3, 2026

RAIS DK SAMIA SULUHU HASSAN AWEKA SHADA LA MAUA KABURI ASKARI ASIYEFAHAMIKA

Na Mwandishi Wetu, TBN, Moscow

KENGELE kubwa iliyogongwa mara tisa, bendi ya jeshi ikiongoza nyimbo za maombolezo Rais Dk Samia Suluhu Hasan majira ya saa tano na dakika 23 aliweka shada la maua kwa kaburi la askari asiyefahamika, mjini hapa.

Aidha Baada ya shughuli la uwekaji wa taji hilo katika eneo ambalo moto huwaka daima ikiwa ni kumbukumbu ya wapiganaji wa Urusi waliopoteza maisha katika vita kuu ya pili, gadi tatu zilipita kwa mwendo wa haraka na kutoa heshima kwa Rais Samia baada ya kupigwa kwa wimbo wa taifa la Tanzania.

Hali ya  askari katika uwanja huo walioonesha nidhamu ya hali ya juu ya kusimama tisti katika maeneo yao bila kutikisika , ubadilishanaji wa gadi za ulinzi na pia mwendo wa pole ambao ulimsindikiza Rais Samia kwenda kwenye tukio la uwekeaji wa shahada. Vilikuwa vitu vinavyovutia kuangalia.

Rais Samia ambaye yupo katika ziara ya kiserikali nchini hapa  baadaye alienda kukutana na mwenyeji wake Rais Vladmir Putin 

Zaidi ya maofisa 300 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania JWTZ wamepata nafasi ya masomo katika nchi ya Urusi kwa ajili ya shahada ya kwanza na ya pili.

Askari hao wameenda kujifunza masuala ya kupambana na ugaidi, sayansi na teknolojia,mafunzo ya kijeshi, ulinzi wa amani, ununuzi na uhifadhi wa silaha,namna ya kukabiliana na majanga.

Tanzania na Urusi zina ushirikiano wa kijeshi kwa kuzingatia makubaliano ya ushirikiano wa kijeshi yaliyosainiwa mwaka 2016  na makubaliano ya mwaka 2018 ya ushirikiano wa kifundi wa kijeshi.

Tanzania yenye ukuaji wa uchumi wa asilimia 5.5 kwa mwaka 2024 na ikikadiriwa kufikia asilimia 6 mwaka huu na ikiwa na mkakati wa kuhakikisha kwamba Dira ya maendeleo ya mwaka2050 inatekelezwa ziara ya Rais Samia nchini Urusi inatarajiwa kuzaa matunda yanayotarajiwa  ya kuinua sekta ya ajira kukuza biashara na kuimarisha uwekezaji.

DK SAMIA SULUHU HASSAN KUTUNUKIWA SHAHADA YA UZAMIVU YA CHUO KIKUU CHA RUDIN URUSI

Na Mwandishi Wetu ,TBN, Moscow

Rais Dkt  Samia Suluhu Hassan ambaye yupo hapa shirikisho la Urusi kwa ziara ya kitaifa anatarajiwa kutunukiwa shahada ya uzamivu na Chuo Kikuu cha Rudin nchini hapa.

Tuzo hiyo inatokana na kutambua kazi yake na mchango wake katika jami ya Tanzania na dunia katika masuala ya msingi yanayohusu Maisha ya binadamu.

Chuo cha RUDIN chenye wanafunzi wa kitanzania 570 kufikia mwaka 2025 katika miaka zaidi ya 65 ya RUDIN, watanzania 1,132 wamepitia chuo hicho.

RUDIN kimesomesha zaidi ya wataalamu 200,000 duniani na sasa ina watu 44,000 kutoka nchi 160 duniani.

Chuo hiki ni cha 367 kwa ubora duniani kwa mujibu wa QS World University Ranking ya mwaka 2025.

Rais Dkt Samia ambaye amepokelewa jana na Waziri wa maendeleo ya Uchumi wa Russia Maxim Reshetnikov anatarajiwa kukutana na mwenyeji wake Rais Vladimir Putin na kufanya mazungumzo ya ana kwa ana kwa ajili ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi.

Aidha akiwa nchini hapa, akiwa kiongozi wa pili wa Tanzania kutembelea Urusi, ziara ya kwanza ikiwa imefanywa na baba wa taifa Mwalimu Julius Nyerere, atashiriki Jukwaa la uchumi la St Petersburg ambapo tanzania itanadi fursa za uwekezaji, na diplomasia ya Uchumi  kwa viongozi, wawekezaji na watunga sera wa kimataifa.

Katika kufanikisha dira ya Maendeleo 2050 ziara hii ni kikolezo cha utekelezaji kwa mafanikio ya dira hiyo ambayo inahitaji raslimali watu wenye utaalamu na upeo mkubwa kusimamia na kuendesha miradi ya kimkakati itakayopelekea ajira, viwanda na biashara zitakazoingiza dola trilioni moja na kuwa katika uchumi wa kati wa juu.

Katika WhatsApp yake Rais Samia amesema Ziara hiyo ni muhimu hasa taifa linapoelekea kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 ambayo inataka ushiriki mkubwa wa sekta binafsi.

 "Tutafanya mazungumzo na wenyeji wetu yanayolenga kuimarisha ushirikiano katika sekta za kimkakati zinazogusa maisha ya wananchi." 

"Aidha, tutashiriki majukwaa ya biashara na uwekezaji na kutatangaza fursa zilizopo nchini, pamoja na kufungua zaidi fursa za masoko kwa bidhaa za Tanzania nchini Urusi."