Thursday, May 19, 2016

MKURANGA YAZUIA MALIPO YA MISHAHARA YA WATUMISHI 15

Na John Gagarini, Mkuranga
WILAYA ya Mkuranga mkoani Pwani imewasimamishia malipo watumishi 15 ambao wameondoka kwenye vituo vyao vya kazi bila ya taarifa kwa mwajiri wake ambaye ni Halmashauri.
Hayo yalisema na mkuu wa Wilaya ya Mkuranga Abdala Kihato alipokuwa akisoma taarifa ya wilaya wakati wa ziara ya mkuu wa mkoa wa Pwani kutembelea shughuli za maendeleo kwenye wilaya hiyo.
Kihato alisema kuwa mishahara hiyo ilizuiliwa kutokana na watumishi hao kutotoa taarifa walipoondoka kwenye vituo vyao vya kazi wakati wa uhakiki watumishi katika zoezi la kutambua watumishi hewa.
“Tulifanya uhakiki wa watumishi 179 na kubaini kuwa watumishi 85 walikuwa ni watoro ambapo 51 wamehamia kwenye vituo vingine vya kazi 10 hawakujitokeza na 15 ndiyo walioondoka kwenye vituo vya kazi bila ya taarifa na watano ni watoro kabisa,” alisema Kihato.
Alisema kuwa zoezi hilo ni endelevu na linaendelea kwani linaoneka lina changamoto nyingi katika kubainisha watumishi hewa na wale ambao wako kisheria.
“Hatua tuliyoichukua kwa wale ambao waliondoka kwenye vituo vyao vya kazi bila ya taarifa ni kusimamisha mishahara yao ili wasije wakwa wanachukua fedha pasipo kufanya kazi,” alisema Kihato.
Kwa upande wake Ndikilo alisema kuwa maofisa utumishi wanapaswa kutoa ushirikiano kwa serikali katika kuhakikisha watumishi hewa wanapatikana na itawachukulia hatua kali wale watakaowaficha watumishi hewa.
Ndikilo alisema kuwa zoezi hilo litakapokamilika mkoa utatoa taarifa juu ya zoezi hilo ambalo lina lengo la kuondoa watumishi hewa ambao wamekuwa wakijipatia fedha pasipo kufanya kazi.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment