Thursday, May 19, 2016

WANANCHI WALILIA DARAJA

Na John Gagarini, Kibaha
WANANCHI wa mtaa wa Mkombozi wilayani Kibaha mkoani Pwani umeiomba Halmashauri ya Mji wa Kibaha kuwajengea kivuko au daraja kwenye mto Mpiji kwa ajili ya kuvuka kwenda Majohe wilaya ya Kinondoni kupata huduma za kijamii ambako ni jirani na ikilinganishwa na Maili Moja wilaya ya Kibaha umbali wa kilometa zaidi ya 10.
Akizungumza na waandishi wa habari mkazi wa mtaa huo Malaki Lakibuka alisema kuwa  huduma hizo wanazipata Majohe kutokana na ukaribu uliopo wa kilometa mbili ukilinganisha na Kibaha ambako ni mbali kwa zaidi ya kilometa 10, lakini tatizo lililopo ni kukosa kivuko au daraja.
Lakibuka alisema kuwa wako kwenye wakati mgumu kuvuka mto huo kutokana na kuwa na mamba wengi jambo ambalo ni hatari kwa usalama wao ambapo kwa miaka ya nyuma watu walikuwa wakiliwa na mamba.
“Tunapata taabu sana kuvuka hapo mtoni kwani mamba ni wengi na pia endapo utapita vibaya unaweza kuchukuliwa na maji hasa wakati wa mvua hivyo kuhatarisha maisha yetu na ikizingatiwa kuwa watumishi wanaofanya kazi Majohe,” alisema Lakibuka.
Naye mweneykiti wa mtaa huo ambao ni mpya Moshi Mhagama alisema kuwa kutokuwa na kivuko ni changamoto kubwa kwa wananchi ambao wanategemea  hali inakuwa mbaya kipindi cha mvua ambapo mto huo unakuwa umejaa maji.
Moshi alisema kuwa wanategemea Majohe kama ni sehemu ya kupata mahitaji yao ya kawaida ambako ni jirani ikilinganishwa na Kibaha ambako ni mbali sana hivyo tungeomba Halmashauri iwasaidie ujenzi huo ambapo nao tayari walishaanza kuchangishana fedha kwa ajili ya ujenzi wa kivuko.
“Kwa wagonjwa au mama wajawazito ni taabu kwani wanajifungulia wakiwa njiani lakini pangekuwa na daraja wangepita kwa urahisi na kuwawahisha wagonjwa kupata matibabu pia kuna wafanyakazi wanafanya kazi ngambo ya pili ni shida sana kuvuka mvua zinapokuwa nyingi,” alisema Moshi.
Naye diwani wa kata hiyo Agustino Mdachi alisema kuwa jambo hilo alilipeleka Halmashauri lakini alijibiwa kuwa uwezo wa kujenga daraja hilo haupo kutokana na gharama za ujenzi kuwa kubwa sana kiasi cha zaidi ya bilioni mbili.
Mdachi alisema kuwa changamoto kwenye eneo hilo ni kubwa sana kwani mbali pia kuna mamba ambao ni hatari kwa watu wanaovuka hapo hivyo kuhatarisha maisha yao.
“Mbali ya Halmashauri kusema kuwa hawana uwezo wa kujenga daraja kwa sasa pia walisema hawawezi kujenga kivuko cha muda kwani gharama itakuwa mara mbili wao wanataka wajenge kitu cha kudumu ambapo ni ujenzi wa daraja,”alisema Mdachi.
Mwisho. 

No comments:

Post a Comment