Thursday, May 19, 2016

MKURANGA MBIONI KUMALIZA TATIZO LA MADAWATI

Na John Gagarini, Kibaha
WILAYA ya Mkuranga mkoani Pwani limechonga madawati 5,043 ili kukabiliana na tatizo la upungufu wa madawati kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.
Mkuu wa wilaya ya Mkuranga Abdala Kihato akisoma taarifa ya wilaya hiyo kwa mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo wakati wa ziara yake kutembelea wilaya hiyo kukagua shughuli za maendeleo.
Kihato alisema kuwa wilaya hiyo ilikuwa na upungufu wa madawati 5,131 hivyo kubakiwa na upungufu wa madawati 500 ambayo wanatarajia kukamilisha utengenezaji muda mfupi ujao.
“Tatizo la upungufu wa madawati kwa wanafunzi wa shule za Sekondari tatizo hilo hakuna ila tatizo kubwa liko kwa wanafunzi wa shule za Msingi kutokana na uwingi wao na hata wale wa darasa la kwanza ambapo kwa mwaka huu walioandikishwa ni wengi sana,” alisema Kihato.
Alisema kuwa hawana wasiwasi kwani hadi ule muda uliowekwa wa Juni 30 kwa wilaya zote kuondoa tatizo la wanafunzi kukaa chini litakuwa limekwisha kabisa kwani wanashirikiana na wadau mbalimbali kutengeneza madawati.
“Tunawahimiza watendaji wa vijiji na kata kuhakikisha wanakamilisha zoezi hilo ili kuwaondolea adha wanafunzi kukaa chini na kuwafanya washindwe kujifunza vizuri masomo yao,” alisema Kihato.
Aidha aliwaomba wadau wa maendeleo ndani ya wilaya hiyo kuwaunga mkono katika kufanikisha zoezi hilo la uchongaji wa madawati kwa wanafunzi kwenye wilaya hiyo.
Naye mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa anaipongeza wilaya hiyo kwa kuweza kufanikisha kuchonga madawati hayo ambayo sasa yanaenda kuondoa tatizo hilo la upungiufu wa madawati.
Ndikilo alisema kuwa mkoa huo ulikuwa una upungufu wa madawati 43,047 kwa shule za msingi lakini kwa jitihada hizo zitakuwa zimepunguza kwa kiasi kikubwa upungufu huo.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment