Sunday, May 29, 2016

KITUO CH AFYA MKOANI CHAHITAJI JENERETA

Na John Gagarini, Kibaha
KITUO cha Afya cha Mkoani kinakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa Jenereta ili kukabiliana na tatizo la ukatikaji umeme kwenye chumba cha akinamama wanapojifungulia hivyo kuwaomba wadau mbalimbali.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mganga mkuu wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Happiness Ndosi wakati akipokea msaada wa vifaa mbalimbali kwa watoto waliozaliwa na watakaozaliwa kutoka shirika lisilokuwa la kiserikali la Abubaker Darwesh International Charitable Foundation (ADICF) la Jijini Dar es Salaam.
Dk Ndosi alisema kuwa kukatika kwa umeme kwenye kituo hicho ni changamoto kubwa hasa nyakati za usiku na wakati mama wajawazito wanapokuwa wanajifungua hali ambayo inahatarisha maisha ya akinamama hao.
“Kutokana na hali hiyo tunawaomba wadau mbalimbali wajitokeze kutusaidia kupata jenereta kwa ajili ya kusaidia mara umeme unapokatika katika chumba cha uzalishaji mama wajawazito ili kunusuru maisha yao,” alisema Dk Ndosi.
Aidha alisema mbali ya changamoto hiyo pia wanakabiliwa na changamoto nyingine ikiwa ni pamoja na ukosefu wa chumba cha upasuaji, Ultra Sound na X-Ray, gari la wagonjwa kwani lililopo ni chakavu, magodoro na vitanda hasa ikizingatiwa kuwa kituo hicho kiko mbioni kuwa Hospitali ya Wilaya.
Kwa upande wake mwanzilishi na meneja mradi wa shirika hilo Bilal Abubekar alisema kuwa shirika lake limeamua kutoa misaada hiyo kwa lengo la kuisaidia jamii hasa kwa watoto wadogo wenye umri chini ya miaka mitano ili kuisaidia serikali kuhakikisha watoto chini ya miaka mitano wanapata huduma bora.
Abubaker alisema kuwa shirika lao limekuwa likisaidia makundi mbalimbali ikiwa ni pamoja na wajane yatima na watu wenye mahitaji, pia kusaidia elimu watu wenye ulemavu.
Naye moja ya wagonjwa waliopata msaada huo Mariamu Ally alishukuru shirika hilo na kusema kuwa wameonyesha moyo wa upendo na kuwataka waendelee kusaidia hospitali hiyo ili iweze kukabiliana na changamoto zilizopo kwa wagonjwa.
Alisema kuwa moja ya changamoto iliyopo kwenye wodi hiyo ni kuchanganywa kati ya akinamama waliojifungua na wale wanaosubiri kujifungua na kutaka watu hao kutenganishwa ili kila moja wawe na sehemu yao.
Mwisho.   


No comments:

Post a Comment