Monday, May 23, 2016

VIJANA WAILILIA SERIKALI KUWAINUA KIUCHUMI

Na John Gagarini, Kisarawe

SERIKALI imeombwa kusaidia vikundi vya vijana vinavyopata mafunzo mbalimbali ya kuwainua kiuchumi ili waweze kujiajiri wakiwa Vijijini badala ya kukimbilia Mijini.

Akisoma risala ya wahitimu mbele ya mgeni rasmi ambaye ni kiongozi wa Mbio za Mwenge Kitaifa George Mbijima kwenye Kijiji cha Kibuta wilayani Kisarawe, Mariam Christopher alisema kuwa mafunzo hayo yatawawezesha kuweza kukabili mazingira wanayoishi huko huko waliko kuliko kukimbilia mjini kutafuta ajira.

Christopher alisema kuwa masomo waliyojifunza ni ya ufundi kwa vijana wa kata ya Kurui kupitia mradi wa kuwajengea uwezo vijana (YEE) unaosimamiwa na shirika lisilokuwa la kiserikali Plan International wilaya ya Kisarawe.

“Tunashukuru wafadhili wetu kwani tumeweza kujifunza mambo mengi ya ufundi tunaamini yatatusaidia tukiwa huku huku bali kikubwa ni Halmashauri kutuwekea mazingira mazuri ya kufanya kazi ili tuisaidie jamii ya Kijijini hasa ikizingatiwa nako kuna hitaji maendeleo,” alisema Christopher.

Alisema kuwa mafunzo hayo wameyapata kwa kina katika fani mbalimbali za upambaji, mapishi, udereva, ushonaji na utengenezaji wa mapambo na wanatarajia kuboresha shughuli hizo Vijijini ili kuleta maendeleo kwa familia zao na wao binafsi.

Aidha alisema kuwa mafunzo hayo yanafadhiliwa na Eu, Vso, Uhiki, Veta na Plan International wilayani humo na yanatekelezwa kwenye kata Sita za Kibuta, Kisarawe, Manerumango, Msimbu, Kurui na Marumbo na yanatarajiwa kuwafikia vijana 1,000 kwa kipindi cha miaka mitatu.

Kwa upande wa kiongozi wa mbio za mwenge Kitaifa George Mbijima alisema kuwa Halmashauri inapaswa kuwatengenea vijana asilimia tano ya mapato yao kwa ajili ya kuwakopesha vijana kwani suala hilo liko kisheria na wanapaswa kutekeleza ili kuwajenga vijana kiuchumi, Mwenge huo leo unatarajiwa kukimbizwa wilaya ya Rufiji.

Mwisho. 





No comments:

Post a Comment