Monday, May 23, 2016

SERIKALI KUWAWEKEA MAZINGIRA MAZURI WAWEKEZAJI

Na John Gagarini, Kisarawe
SERIKALI itaendelea kuweka mazingira mazuri kwa wawekezaji wa ndani na nje ambao watafuata taratibu za nchi ili kuongeza pato la taifa kupitia sekta ya uwekezaji ambayo kwa sasa inakuwa kwa kasi kwenye mikoa mbalimbali.
Hayo yalisemwa na kiongozi wa Mbio za Mwenge Kitaifa George Mbijima alipokuwa akiweka jiwe la msingi kwenye Bandari ya Nchi Kavu inayojengwa kwenye Kijiji cha Kazimzumbwi wilayani Kisarawe mkoani Pwani.
Mbijima alisema kuwa nchi kwa sasa iko kwenye kipindi cha utekelezaji  kwa vitendo sera ya uwekezaji ili iweze kuleta manufaa kwa wananchi pamoja na serikali ili iweze kuwaletea maendeleo wananchi kupitia uwekezaji.
“Serikali inathamini mchango wa wawekezaji kwani wana nafasi kubwa ya kuleta maendeleo kwa wananchi pamoja na nchi lakini kikubwa ni kuwa wazi wakati wa kufanya taratibu za uwekezaji ili kuondoa malumbano yanayojitokeza baina ya wananchi na wawekezaji,” alisema Mbijima.
Alisema kuwa baadhi ya wawekezaji wamekuwa wakikiuka taratibu za uwekezaji kwa kutokuwa wazi wakati wakufanya michakato ya uwekezaji kwani wanapaswa kuwa wazi kwa pande zinazohusika ili kuondoa mikanganyiko.
“”Wawekezaji wanapaswa kufuata sheria za nchi zilizowekwa ili faida inayopatikana iweze kuleta manufaa kwa wananchi wanaozunguka maeneo ya uwekezaji hivyo wanapaswa kushirikiana na wananchi ili kuondoa migogoro isiyo na tija kwa uwekezaji”,  alisema Mbijima.
Aidha alisema kuwa serikali inatoa ushirikiano na wawekezaji kwnai mbali ya kutoa ajira kwa wananchi pia serikali inapata mapato yake kupitia sekta hiyo ili iweze kuendesha shughuli zake kupitia kodi na ushuru mbalimbali.
Kwa upande wake mkurugenzi wa Kampuni ya DSM Corridor Group  Sada Shaban alisema kuwa ujenzi huo wa Bandari kavu ulianza 2013 na kukamilika mwaka huu kwa baadhi ya vitengo ukiwa umegharimu kiasi cha shilingi bilioni 7.5 ambapo gharama iliyobakia ni kiasi cha shilingi bilioni 38 hadi kukamilika kwake.
Shaban alisema kuwa eneo hilo litakuwa ni hifadhi ya bidhaa mbalimbali ikiwa ni pamoja na maghala ya mazao mbalimbali, madini na mizigo ya kila aina na itasaidia kupunguza msongamano barabarani kwani ikitoka hapo inapakizwa kwenye treni ambayo iko jirani na bandari hiyo. Mwenge huo ukiwa wilayani Kisarawe ulizindua na kuweka mawe ya msingi kwenye miradi yenye thamani ya shilingi bilioni 6.5 leo mwenge unakimbizwa wilayani Rufiji.
Mwisho.





No comments:

Post a Comment