Thursday, May 12, 2016

JESHI LA POLISI LAMSAKA MWANAFUNZI ALIYECHOMA BWENI


Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi Mkoani Pwani bado linaendelea kumtafuta mwanafunzi wa shule ya Sekondari ya Rafsanjani iliyopo Soga Tarafa ya Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani baada ya kuchoma bweni la wasichana la shule hiyo.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Bonaventura Mushongi alisema kuwa mwanafunzi huyo ambaye hakuweza kufahamika alichoma bweni hilo juzi majira ya saa 4 usiku liitwalo Umoja.
Mushongi alisema kuwa hata hivyo tukio hilo halikuwa na madhara kwa wanafunzi zaidi ya kuharibu mali zilizokuwa kwenye bweni hilo ambazo hata hivyo thamani yake haikuweza kufahamika mara moja.
“Tunaendelea kumfuatilia mwanafunzi huyo ili tuweze kumjua na kumchukulia hatua za kisheria lakini hadi sasa bado hatujafanikiwa kumpata kwani aliandika kwenye sanduku la maoni juu ya dhamaira yake hiyo mbaya ya kuchoma bweni,” alisema Mushongi.
Alisema kuwa wanaendelea kuzifanyia kazi taarifa hizo ili waweze kumbaini mwanafunzi huyo ili hatua kali za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yake kwani kitendo alichokifanya ni cha hatari kwa maisha ya wanafunzi wenzake na mali.
“Tunatoa wito kwa wanafunzi wanapokuwa shuleni wazingatie masomo na kuachana na vitendo visivyo kuwa na maadili kwani jeshi halitawavumilia wanafunzi ambao wanabainika kufanya vitendo viovu kwani tutawakamata na kuwapeleka kwenye vyombo vya sheria ikiwa ni pamoja na mahakamani,” alisema Mushongi.
Bweni hilo lilichomwa moto juzi na mwanafunzi huyo lakini hata hivyo kikosi cha zimamoto mkoa wa Pwani polisi pamoja na wananchi walifanikiwa kuzima moto huo na haukuweza kuleta madhara kwa wanafunzi.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment