Thursday, May 26, 2016

MWENYEKITI AKATALIWA KWENYE MKUTANO

Na John Gagarini, Kibaha
SAKATA la Mwenyekiti wa Mtaa wa Muheza wilayani Kibaha mkoani Pwani Maulid Kipilili limechukua sura mpya baada ya wananchi wa mtaa huo kumkataa mwenyekiti huyo kwenye mkutano wa wananchi uliofanyika mtaani hapo.
Wananchi hao walimkataa mwenyekiti wao wakati wa mkutano ulioitishwa na diwani wa kata ya Maili Moja Ramadhan Lutambi ili kujadilia suala la malalamiko ya wananchi wa mtaa huo baada ya kuifunga ofisi ya mtaa hadi pale watakapofikia muafaka juu ya mwenyekiti wao.
Mkutano huo ambao ulifanyika mtaani hapo chini ya diwani huyo wa kata na ofisa Mtendaji wa Kata hiyo Thadeo Mtae wananchi hao walilalamika kuwa mwenyekiti wao tangu achaguliwe kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika mwishoni mwa mwaka 2015 hajaitisha mkutano wa wananchi.
Kabla ya kufikia hatua ya kumkataa mwenyekiti wao wananchi hao walitoa malalamiko yao mbalimbali ikiwa ni pamoja na kulalamika kuwa mwenyekiti wao haitishi vikao vya wananchi, hasomi mapato na matumizi, kutofungua ofisi hivyo kuwapa shida wananchi wanapokwenda kupata huduma za kiofisi.
Akizungumza juu ya mwenyekiti wao kushindwa kuwajibika mwananchi wa mtaa huo Kitai Mganga alisema kuwa ni pamoja na tuhuma nyingine ni kushindwa kusimamia mali za mtaa ikiwa ni pamoja na baadhi ya watu kumega na kuuziana eneo lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa shule ya Msingi lakini hakuna hatua zozote ambazo amezichukuwa.
“Mtaa wetu una changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na ukosefu wa maji, umeme, Shule ya Msingi, bararabara na zahanati lakini kutokana na mwenyekiti wetu kutowajibika tumeshindwa kufanya lolote hata kuweka mikakati ya maenedeleo hakuna,” alisema Mganga.
Naye Paulo Chacha alisema kuwa mwenyekiti lazima awe na wajumbe wa mtaa lakini cha kushangaza wajumbe hawapo hivyo mwenyekiti anafanya kazi peke yake jambo ambalo haliwezi kuleta mafanikio.
Chacha alisema kuwa kamati ya mtaa ni sawa na baraza la mawaziri sasa haiwezekani Rais kuongoza nchi bila ya kuwa na Mawaziri kwani maendeleo hayawezi kupatikana.
Kwa upande wake Maulid Kipilili alisema kuwa kwa upande wa mikutano alishindwa kufanya kutokana na sababu maalumu ikiwa ni pamoja na shughuli za kitaifa.
Kipilili alisema kuwa aliitisha mikutano mitatu ya dharura na miwili ya kikatiba na kuwashangaa wananchi hao kumsingizia kuwa hajafanya kabisa mikutano na mmoja wa Mei 15 ulishindwa kufanyika kutokana na akidi kushindwa kuenea.
“Kuhusu wajumbe wa serikali ya mtaa hawajafika kwa sababu mbalimbali lakini wapo na sina mgogoro na wajumbe wangu na tunafanya kazi vizuri na baadhi ya kamati zipo na zinafanya kazi kama ya maji na shule zipo na aliyeuziwa eneo la shule kama kuna mtu anaushahidi alete ili tuchukue hatua za kisheria,” alisema Kipilili.
Akielezea juu ya changamoto hiyo ya wananchi kumkataa mwenyekiti wao diwani wa kata hiyo Ramadhan Lutambi alisema kuwa kama hawamtaki wanapaswa kufuata taratibu kwani hatua ya kwanza ni hiyo.
Lutambi alisema kuwa kutokana na hali hiyo itabidi uitishwe mkutano wa dharura wa kata kujadili suala hilo na wao ndiyo watakaoamua hatma ya mweneyekiti wao.
Kufuatia kukataliwa na wananchi ofisa mtendaji wa kata ya Maili Moja Thadeo Mtae alisema kuwa hoja zilizotolewa ni 15 ambapo zimejibiwa na mwenyekiti huyo ambapo baadhi wamekataa majibu yake na nyingine wamekubali majibu.
Mtae alisema kuwa atapeleka sehemu husika kwa ajili ya majibu na hatua zaidi kwani yeye hatoweza kutoa majibu hivyo wasubiri majibu ambapo kutaitishwa mkutano mwingine.   

Mwisho.   

No comments:

Post a Comment