Sunday, May 29, 2016

WAIOMBA HALMASHAURI IWALIPE FIDIA BAADA YA KUPEWA SIKU 14 KUVUNJA NYUMBA ZAO

Na John Gagarini, Kibaha
BAADHI ya wakazi kwneye eneo la Sagulasagula maarufu kama Loliondo Mtaa wa Machinjioni kata ya Tangini wilayani Kibaha mkoani Pwani wanaodaiwa kuvamia eneo lililotengwa kwa ajili ya soko wameiomba Halmashauri ya Mji kuwalipa fidia na maeneo ya kuishi baada ya kupewa siku 14 kuhama kwenye eneo hilo.
Wakizungumza mara baada ya kamati ya ulinzi na usalama ya Wilaya kupitia na kuangalia eneo hilo na kutoa maagizo kwa wakazi hao kubomoa nyumba zipatazo 55 zilizojengwa kwenye eneo hilo walisema kuwa kwa kuwa ni mpango wa maendeleo basi nao waangaliwe kwani wamekaa hapo kwa muda mrefu.
Said Tekelo alisema kuwa baadhi ya watu wako hapo tangu mwaka 1970 na mwaka 2003 Rais Benjamin Mkapa wakati ule alifuta hati ya eneo hilo toka eneo la Viwanda na kutaka lirejeshwe kwenye mtaa kwa ajili ya matumizi mengine.
“Baada ya kurejeshwa kwenye mtaa baadhi ya watu walipimiwa maeneo yao baada ya kupigwa picha na kamahaitoshi hata alipokuja waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi alitoa miezi mitatu sasa sita Halmashauri ikae na wakazi hao ili kujadili namna nzuri ya kufanya,” alisema Tekelo.
Alisema kuwa licha ya maagizo hayo walikwenda Mahakamani kwenda kulalamika walipotakiwa kuondoka na kesi iliendeshwa na wao kushindwa na Mahakama ili amuru Halmashauri ikae nao lakini hakuna kilichofanyika hadi mwishoni mwa wiki walipotakiwa kuvunja wenyewe na endapo hawatafanya hivyo Halmashauri itabomoa nyumba hizo.
“Tumeambiwa tubomoe wenywe na kuanzia leo Tanesco na Dawasco wameshapewa maagizo ya kuondoa miundombinu yao ilkiwa ni maandalizi ya kubomoa sisi tunaomba Halmashauri itufikirie kwa kutulipa fidia pamoja na maeneo kwa ajili ya kuishi kwani wenzetu jirani ambao tuko kwenye mgogoro mmoja wamelipwa na kupewa viwanja,” alisema Tekelo.
Kwa upande wake Diwani wa kata ya Tangini Theodori Joseph alisema kuwa suala hilo ni la muda mrefu ambapo baraza la Madiwani miaka ya nyuma waliwatambua wakazi hao kutaka walipwe fidia na walikuwa wakishirikiana nao katika mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuchukua kodi za majengo.
Joseph alisema kuwa kuna haja ya Halmashauri kuwafikiria wakazi hao kwani wengine wako hapo miaka 40 iliyopita na wameendeleza ardhi kwa kipindi chote hicho lakini jirani zao ambao wametengwa na barabara wao  wamepewa fidia na watapewa viwanja.
Ofisa Habari wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Inocent Byarugaba alisema kuwa eneo hilo lilitengwa kwa ajili ya soko na liko kwenye Ramani ya Mji na  wakazi hao walilivamia eneo hilo na wanapaswa kuliachia.
Byarugaba alisema kuwa tayari eneo hilo liko kwenye maandalizi ya ujenzi wa soko unatarajiwa kuanza wakati wowote kuanzia sasa kwani tayari ramani imeshatoka ambapo soko linalotumika kwa sasa liko kwenye hifadhi ya barabara na litabomolewa muda wowote na Tanroads.
Naye kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri Lucy Kimoi alisema kuwa wakazi hao wanapaswa kuondoka na kwa sasa wanaandaa notisi kwa ajili ya kuwataka waliachie eneo hilo kwani wako hapo kinyume cha Sheria.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment