Wednesday, May 18, 2016

WAMKATAA MWENYEKITI WAMFUNGIA OFISI

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
WAKAZI wa Mtaa wa Muheza kata ya Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wamefunga ofisi ya mtaa huo kwa madai ya kuukata uongozi ambao wamesema haufanyi kazi kwa utaratibu uliowekwa ikiwa ni pamoja na kutofungua ofisi.
Wakizungumza na waandishi wa habari walisema kuwa uongozi huo tangu umechaguliwa umeshindwa kabisa kuwajibika hivyo kushindwa kuleta maendeleo kwa kipindi chote cha uongozi wao walipochaguliwa mwishoni mwa mwezi Oktoba mwaka jana.
Moja ya wakazi hao ambaye alijitambulisha kwa jina la Modestus Mpelembwa alisema kuwa uongozi huo chini ya mwenyekiti wake Maulid Kipilili umeshindwa kabisa hata kuitisha mikutano ya kisheria ambayo ndiyo sehemu ya wananchi kuweza kuchangia maendeleo na kujua kinachoendelea ndani ya mtaa huo.
“Wananchi wamefikia hatua ya kufunga mlaango wa ofisi kutokana na kuona kuwa hawana msaada wowote na uongozi ambapo hata kama unashida huwezi kusaidiwa kwani hakuna kiongozi hata mmoja anayeonekana zaidi ya kuonekana kwa matukio maalumu,” alisema Melembwa.
Mpelembwa alisema kuwa hata mapato ya mtaa hayaonekani licha ya kuwa mtaa huo ni moja ya mitaa ambayo ina maeneo makubwa ya ardhi ambayo yanauzwa kama viwanja kwa ajili ya makazi kutokana na eneo hilo kuanza kujengeka kwa sasa.
“Ofisi muda mwingi imefungwa kama una shida umpigie simu mwenyekiti na kama ni suala la mauziano ya viwanja ni huko huko na siyo ofisini kama taratibu zinavyosema hali ambayo inaonyesha kuwa hakuna uwazi wa fedha za asilimia zinazotakiwa kubaki kwenye mtaa kwa ajili ya shughuli za maenedeleo,” alisema Mpelembwa.
Naye Angela Mduma alisema kuwa uongozi huo haufai kuwaongoza kwani umeshindwa kukabili changamoto za wananchi ambao waliwachagua kwa ajili ya kutatua kero mbalimbali ikiw ani pamoja na ubovu wa barabara.
“Tuna chanagamoto nyingi ikiwa ni pamoja na ukosefu wa zahanati, shule ya msingi, maji pamoja na huduma nyingine za kijamii lakini endapo uongozi ungekuwa makini kupitia mikutano kama ingekuwa inafanyika tungeweka vipaumbele vya kuanza kuvifanyia kazi lakini uongozi hauna ushirikiano hakuna kilichofanyika hadi sasa,” alisema Mduma.
Mduma alisema kuwa kwa upande wa kinamama wanapata taabu hasa kwenye huduma za kiafya kliniki kwa wajawazito, kuwapeleka watoto wao kliniki na matibabu kwa ujumla kwao ni changamoto kubwa sana.
Naye Modestus Mapunda alisema kuwa mara ya mwisho mwenyekiti aliitisha mkutano wa mtaa lakini cha ajabu muda mfupi baadaye aliahirisha wakati tayari wananchi wameshajiandaa kwa mkutano hali ambayo ilisababisha wananchi kushikwa na hasira na kuifunga ofisi.
“Tunachotaka ni mkuu wa wilaya kuja hapa kwa ajili ya kujua kero zetu kwani uongozi umeshindwa kufanya kazi lakini cha kushangaza wajumbe kutakiwa kutofanya chochote na mwenyekiti na hawaruhusiwi kuingia ofisini hadi watakapoitwa,” alisema Mapunda.
Mwenyekiti wa mtaa huo Maulid Kipilili alisema kuwa hawezi kuongea chochote kwani anaongea na uongozi wa juu na pia suala hilo tayari amelipeleka polisi kulalamika wananchi hao kufunga ofisi ya mtaa.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Maili Moja Ramadhan Lipwai alisema kuwa kufungwa kwa ofisi hiyo ni kinyume cha utaratibu kwani ile ni mali ya umma na wananchi wanapata huduma kupitia ofisi hiyo.
Lipwa alisema kuwa anafanya mawasiliano na viongozi mbalimbali ili kupata suluhu la tatizo hilo ili ofisi hiyo iweze kufunguliwa ili wananchi waweze kupata huduma kupitia ofisi hiyo ambayo imefungwa tangu Mei 15 baada ya mkutano wa mtaa kushindwa kufanyika.
Mwisho.  











   

No comments:

Post a Comment