Monday, February 18, 2013



Na Mwandishi Wetu, Kibaha
MWANAFUNZI wa darasa la kwanza wa  shule ya Msingi Mbaya, Geuza Patrick (12) amekufa kwa kujinyonga kwa kamba ya katani.
Kwa mujibu wa kaimu kamanda wa Polisi mkoani Pwani Gregory Mushi alisema kuwa tukio hilo lilitokea Februari 13 mwaka huu majira ya saa 12 jioni huko kitongoji cha Msufini tarafa ya Chalinze wilayani Bagamoyo.
Kamanda Mushi alisema kuwa mwanafunzi huyo alijinyonga kwenye Mti wa Mwembe nyumbani kwao.
Alisema kuwa chanzo cha kujinyonga bado hakijafahamika na polisi wanaendelea na uchunguzi kuhusiana na tukio hilo.
Aidha alisema mwili wa marehemu ulikabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya mazishi.
Mwisho.
Na Mwandishi Wetu, Kibaha
SHULE ya Sekondari ya Bundikani ya Kata ya Maili Moja wilayani Kibaha imeanza kuchukua hatua kali kwa wanafunzi wanaovaa suruali za kubana maarufu kama modo kwa kuzichana.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwalimu mkuu wa shule hiyo Flora Chibululu alisema kuwa juzi walichana suruali za wanafunzi watatu kutokana na kwenda shuleni na suruali hizo kinyume cha sheria.
Alisema kuwa baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo wamekuwa na tabia ya kuzirekebisha  kwa kuzibana suruali hizo licha ya kuwa zinashonwa kawaida na kukiuka taratibu za shule.
“Suruali hizo za shule hushonwa vizuri lakini wao huzipeleka kwa fundi na kuzibana sawa na miili yao maarufu kama modo, tulishawapiga marufuku kuzibadili nguo hizo lakini wanakaidi hali iliyotufanya tuchukue hatua hiyo ili kuleta nidhamu shuleni,” alisema Chibululu.
Chibululu alisema kuwa baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakikiuka taratibu za shuleni na kuiga tabia ambazo zinashusha taaluma hivyo shule itakabiliana na vitendo kinyume cha taratibu za shule.
Aidha alisema wataendelea kuzichana suruali hizo kwa mwanafunzi atakaye vaa kinyume cha sheria za shule kwani huo ni utovu wa nidhamu na lazima wanafunzi wafuate taratibu za shule.
Mwisho.  
Na Mwanidshi Wetu, Kibaha
WAFANYABIASHARA kwenye kata ya Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wametakiwa kupima afya zao kwa mujibu wa sheria ili waweze kuhudumia wateja wao wakiwa na afya njema vinginevyo watapelekwa mahakamani kwa kukiuka kanuni za afya.
Hayo yalisemwa na ofisa afya wa kata hiyo Ally Shah, wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha na kusema kuwa watakaokataa kupima afya zao watapelekwa mahakamani.
Shah alisema kuwa hivi karibuni baadhi ya wafanyabiashara waligoma kwenda kupima afya zao wakidai kuwa kiwango cha kupima ni shilingi 5,000 ambayo ilipangwa na halmashauri wakidai kuwa ni kubwa.
“Wafanyabiashara wanatakiwa kupima afya ili kutoa huduma wakiwa na afya njema ili kuepuka maambukizi ya magonjwa mbalimbali kama vile kifua kikuu na magonjwa ambayo yanaambukiza kwa haraka,” alisema Shah.
Alisema kuwa baadhi ya wafanyabiashara hao wamekuwa na hofu ya kupima afya kuwa wataonekana na maambukizi ya ugonjwa wa UKIMWI jambo ambalo alisema kuwa upimaji huo hauhusiani na kupima vipimo vya ugonjwa huo.
“Wasihofie kupima afya kwani magonjwa yanayopimwa hayahusiani na ugonjwa wa UKIMWI na kama mtu anataka kupima ugonjwa huo ni hiyari yake mwenyewe na si kwa lazima kama sheria inavyoelekeza,” alisema Shah.
Aidha alisema kuwa magonjwa yanayopimwa ni pamoja na magonjwa ya zinaa, kifua kikuu na haja kubwa hivyo wafanyabiashara wapime afya zao kwani ni kwa faida yao na wateja wanaowahudumia.
Katika hatua nyingine alisema kwa sasa wanaendelea na kuboresha usafi wa mazingira ambapo vimeundwa vikundi mbalimbali vya usafi kwa ajili ya kuhakikisha mazingira ya Mji wa Kibaha ambapo sheria ndogondogo ya halmashauri inawatoza kiasi cha shilingi 50,000 kwa mtu atakayechafua mazingira.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment