Friday, February 8, 2013

SAKATA KUGOMBEA MPAKA LACHUKUA SURA MPYA


Na Mwandishi Wetu, Kibaha
SAKATA la kugombea mipaka kwa wakazi wawili wa Mtaa wa Visiga Kati wilayani Kibaha mkoani Pwani limechukua sura mpya baada ya mlalamikiwa kuwasweka walalamikaji rumande licha ya licha ya baraza la ardhi la mtaa huo kutoa maamuzi.
Maamuzi ya baraza hilo yalitoa maamuzi kuwa mlalamikiwa Bw Salum Mnjovu asogeze mpaka huo ambao ulileta mzozo baina yake na jirani yake Bw Henrik Simbanyamba.
Hata  hivyo baada ya maamuzi hayo Bw Simbanyamba alilalamika kuwa yeye na Bw Ally Mnola na Bi Ashura Mohamed walikamatwa na polisi baada ya Bw Mnjovu kwenda polisi kulalamika kuwa wameharibu mali zake.
Alisema kuwa anashangaa kukamatwa kwani shauri lilisha amuliwa na baraza na hata kama ana malalamiko ilipaswa aende mahakama ya juu kwenda kutoa mamalamiko yake.
Alisema walikamatwa na askari wa kituo cha polisi Visiga na kushikiliwa kwa muda kabla ya kuachiwa nakuwa nje kwa dhamana hadi Jumanne ambapo suala hilo litaendelea.
“Tunachotaka sheria zifuatwe kwani sisi majirani zake tuna kosa gani hadi tunakamatwa kwani kama ni maamuzi yalitolewa na baraza likaweka mipaka halali,” alisema Bw Simbanyamba.
Bw Mnjovu alitakiwa arekebishe mpaka lakini alipingana na maamuzi hayo kwa kusema kuwa yeye alipouziwa na Bw Seko Mbaruku alionyeshwa tofauti na anashangaa kwanini asogeze mpaka ambapo alilalamika kuwa ameweka kisima cha chini hivyo itabidi kibomolewe.
“Mimi sikubaliani na maamuzi yaliyotolewa kwani wakati nanunua eneo hili kwa thamani ya shilingi milioni 5 toka kwa Bw Mbaruku nilionyeshwa mipaka mbele ya uongozi wa mtaa akiwemo mwenyekiti Bw Hemed Mpaki na ofisa Mtendaji wa mtaa Bw Benedict Maganga nashangaa leo kuambiwa kuwa mpaka umekosewa,” alisema Bw Mnjovu.
Alisema kuwa anashangaa kuona maamuzi yanatolewa huku viongozi wa mtaa hawapo ambao ndiyo walikuwepo wakati wa mauziano na mipaka ilipokuwa inaonyeshwa walikuwepo.
“Sijaridhika na maamuzi nitakwenda mbele ili niweze kupata haki yangu kwani naona haki haijatendeka kwa upande wangu niko hapa miaka miwili iliyopita hakukuwa na maneno, pia mawe niliyoweka niliweka kwenye mpaka wangu na sikuingia kwenye eneo la mtu,” alisema Bw Mnjovu.
Naye mlalamikaji Bw Simbanyamba alisema kuwa alishangaa kuona jirani yake akingoa michungwa ambayo ndiyo iliyokuwa mipaka kasha kuweka mawe ndani ya eneo lake jambo ambalo lilimfanya aende kwenye baraza kutafuta haki yake.
“Miezi miwili iliyopita tuliona anaweka mawe na tulivyojaribu kumwambia kuwa mipaka hiyo ni ya asili hivyo asiitoe lakini alingoa michungwa na mnazi kisha kusogeza mpaka,” alisema Bw Simbanyamba.
Kaimu mwenyekiti wa baraza hilo Bi Mwanahawa Husein alisema kuwa baraza hilo limefuata sheria na halijamuonea mtu kwani lenyewe linatenda haki na kama mlalamikiwa anaona kaonewa anaruhusiwa kukata rufaa ndani ya siku 45.
Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa huo Bw Hemed Mpaki alisema kuwa mipaka ilikuwa ni michungwa ambapo wakati wa mauziano mlalamikaji Bw Simbanyamba hakuwepo.
“Muuzaji Bw Mbaruku alimwelekeza vibaya mipaka na suala la kupanda mawe ilibidi majirani wote wawepo ili kuondoa migogoro jambo ambalo majirani hawakushierikishwa,” alisema Bw Mpaki.
 Mwisho.
  

No comments:

Post a Comment