Monday, February 11, 2013

NYUMBA YA MKT YATEKETEA WATOTO WANUSURIA



Na John Gagarini, Kibaha
NYUMBA ya mwenyekiti wa mtaa waPicha ya Ndege wilayani Kibaha mkoani Pwani imeungua moto ambapo watoto wawili wadogo waliokuwa wamelala wamenusurika kufa baada ya kuamka muda mchache kabla ya tukio la moto.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mwenyekiti huyo Bw Godfrey Mwaipopo alisema kuwa moto huo ulitokea majira ya saa 9 alasiri ambapo kulikuwa hakuna mtu na nyumba ikiwa imefungwa kabla ya majirani kujitokeza na kuzima moto huo.
Bw Mwaipopo alisema kuwa watoto hao Ibrahim Hausi (2) mjukuu wake na Olebu Lugano mwaka mmoja na nusu ambaye ni mtoto wa shemeji yake walikuwa wamelala kama kawaida kwani mara baada ya kula ni kawaida kutakiwa kulala walilala ambapo kwa bahati nzuri waliamka na kwenda kucheza.
“Tunamshukuru Mungu kwani wakati moto huo unatokea watoto wale walisha amka na kwenda kucheza kwani kulikuwa hakuna mtu mzima mimi nilikuwa kwenye kikao Halmashauri ya Mji na mke wangu alikwenda kwenye masuala ya mikopo lakini ghafla nilipigiwa simu na jirani na kuambiwa kuwa nyumba yangu inawaka moto,” alisema Bw Mwaipopo.
Alisema alipofika alikuta majirani wakiwa wamejaa na kufanya jitihada baada ya kuvunja milango na kuanza kuzima moto huo ambao ulianzia kwenye swichi ya umeme, na kuzima moto huo ambao ulianza kusambaa kwa kasi.
“Kwa kweli hakuna mtu aliyejeruhiwa na moto huo licha ya vitu kadhaa kuungua ikiwemo vyeti, nguo makochi na kitanda na cha kushangaza ni kwamba eneo hili lina tatizo la maji lakini maji yalipatikana kwani kila mtu alichukua akiba na kuja kuuzima moto pia walitumia mchanga,” alisema Bw Mwaipopo.  
Aidha alisema kuwa gari la zima moto lilifika lakini walikuta moto umeshazimwa na lilichelewa kutokana na miundombinu kutoruhusu kupita hivyo walitumia muda mwingi kutafuta njia ya kupita.
Aliwashukuru sana wananchi wa mtaa huo kwa kujitokeza kwa wingi kwa kutoa msaada wa kuzima moto huo vinginevyo nyumba hiyo ingeteketea yote na kusingeweza kuokolewa kitu.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
ASKARI wa usalama barabarani mkoani Pwani wametakiwa kuongeza juhudi katika kuzuia ajali za magari barabarani ambapo kwa mwaka jana mkoa huo uliongoza kwa kupunguza ajali hapa nchini.
Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki mjini Kibaha na aliyewahi kuwa kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani Ernest Mangu wakati wa sherehe ya kumwaga ambapo amehamishiwa mkoa wa Mwanza na kumkaribisha kamanda mpya Ulrich Matei.
Kamanda Mangu alisema kuwa kwa kipindi cha mwaka mmoja na miezi mitano aliyokaa kwenye mkoa huo kwa kushirikiana na askari wengine walifanikiwa kupunguza ajali ambapo mkoa uliongoza na kuwa wakwanza.
“Mkoa wa Pwani ulikuwa ni moja ya mikoa iliyokuwa ikiongoza kwa kuwa na ajali nyingi za magari hasa ikizingatiwa kuwa mkoa huo ndiyo lango kuu la kuingilia Jiji la Dar es Salaam kutoka mikoani na nje ya nchi,” alisema Kamanda Mangu.
Alisema kuwa kikubwa kilichosababisha mkoa kufanikiwa kupunguza ajali za magari ni kutokana na ushirikiano baina ya askari wa usalama barabarani na wadau wengine ikiwemo kamati ya usalama barabarani ya mkoa.
“Nawaomba mumpe ushirikiano kamanda mpya ili muendeleze rekodi ambayo mliiweka mwaka jana kwa kufanya kazi nzuri ya kuzuia ajali barabarani ambazo zimekatisha maisha ya watu na wengine kuwa na ulemavu,” alisema Kamanda Mangu.
Kwa upande wake kamanda Matei alisema kuwa kwa kushirikiana na wenzake watafuata nyayo za mwenzake ili kuhakikisha mkoa unakuwa mbele kupambana na ajali.
“Mbali ya kuongoza kwa kupunguza ajali pia mkoa ulifanikiwa kuongoza kwa kukusanya fedha kutokana na makosa mbalimbali ya barabarani na kuushinda hata mkoa kama Mwanza amabo ni Jiji,” alisema Kamanda Matei.
Kamanda Matei alisema kuwa anaomba ushirikiano toka kwa wananchi wa mkoa huo ili waweze kukabiliana na maovu mbalimbali kwenye mkoa huo, sherehe hiyo ilihudhuriwa na viongozi waandamizi wa jeshi hilo.
Mwisho.

  

No comments:

Post a Comment