Friday, February 8, 2013

WANAOCHUKUA SHERIA MKONONI WAONYWA



Na  John Gagarini, Kibaha
SERIKALI imewaonya wananchi wanaojichukulia sheria mkononi kwa kuwaua watuhumiwa badala yake wawapeleke kwenye vyombo husika ili wachukuliwe hatua za kisheria.
Hayo yalisemwa na kamanda wa polisi mkoani Pwani Ulrich Matei ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho ya siku ya sheria (Law Day) na kusema kuwa watu wengi wamepoteza maisha katika mkoa huo kutokana na watu kujichukulia sheria mkononi.
Kamanda Matei alisema kuwa vyombo vya kutoa haki vipo hivyo wananchi wa mkoa huo hawapaswi kuwaua watuhumiwa kwani wengine wanakuwa hawana hatia.
“Watu wengi wameuawa na watu wanaoojiita kuwa wana hasira kali na kuwafanyia vitendo vya kinyama watuhumiwa wa wizi wa pikipiki, kuku na vitu vidogovidogo,serikali haitakuwa tayari kuona vitendo hivyo vinaendelea,” alisema Kamanda Matei.
Alisema kuwa watu hao wanaojiita wenye hasira kali mbali ya kuua watuhumiwa wameharibu miundombinu mbalimbali ya watu na serikali jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
“Tabia hii kwa sasa imeshamiri na kushika mizizi kwa sasa kwenye mkoa wa Pwani jambo hili ni kinyume cha sheria na haki za binaadamu kwani hata katiba inalinda haki ya mtu kuishi,” alisema Kamanda Matei.
Aidha alivitaka vyombo vya kutoa haki kutochelewesha kutoa maamuzi ili kuondoa dhana kuwa haki haitendeki na kufikia watu kujichukulia sheria mkononi.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment