Monday, February 25, 2013

MWANAFUNZI AFANYIWA UNYAMA



Na John Gagarini, Kibaha
MWANAFUNZI wa shule ya sekondari ya Pangani Kata ya Pangani ambaye alikuwa aingie kidato cha pili mwaka huu mwenye umri wa miaka (16) ameshindwa kwenda shule baada ya kutekwa na vijana watatu kwa kipindi cha miezi mitatu ambapo alipata mimba na vijana hao waliitoa.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha huku akibubujikwa na machozi alisema kuwa vijana hao ambao ni wakulima kati yao wawili ni ndugu walimteka kwa kutumia visu walivyokuwanavyo.
Aliwataja vijana hao ambao anawatuhumu kumfanyia kitendo hicho kuwa ni Jonas Edward, Isaka Joseph na Faida Joseph ambao ni ndugu walimteka Novemba 3 mwaka jana baada ya kumdanganya kuwa anatakiwa kwenda kuchukua mzigo wa ndugu yake.
“Baada ya kwenda kufuata mzigo huo niliwakuta wakiwa na visu vitatu ambapo kila mmoja alikuwa na kisu na kunipeleka kwenye nyumba waliyokuwa wakiishi kusema kuwa hapo ndipo nitakapokuwa naishi na endapo nitajaribu kutoka basi wataniua,” alisema mwanafunzi huyo.
Alisema kuwa kwa kipindi chote hicho walikuwa wakifunga mlango kwa nje kwa kutumia kufuli kwa nje hali ambayo ilimfanya ashindwe kutoka pia ikizingatiwa kuwa nyumba hiyo iko mbali na nyumba zingine na kuwa katika kichaka.
“Faida ambaye ndiye aliyenifanya kama mke wake alinipa mimba lakini baada ya kuona hivyo walinilazimisha kuitoa kwa kutumia majani ya chai ambayo yalichemshwa na maji na kuniamuru ninywe na kusababisha mimba kutoka ambapo nilitokwa na damu nyingi na kupata maumivu makali,” alisema mwanafunzi huyo.
Aidha alisema kuwa walimtengenezea kajumba kadogo kwa kupanga matofali na miti kisha yeye kuingia humo mfano wa kaburi ambapo alikuwa akijisaidia kwenye mifuko ya plastiki na chupa kwa ajili ya haja ndogo na kuoga ni humo ndani.
“Kwa upande wa chakula walikuwa wakipika usiku tu kwani walikuwa wakifika majira ya saa sita au saba usiku wanapika tunakula ila asubuhi na mchana nilikuwa sili chakula hata mavazi yangu waliyachoama moto nikawa navaa nguo ya moja ya vijana hao,” aliongeza.
Aliongeza kuwa siku moja vijana hao walisahau kufunga mlango na ndipo alipotoka na kuomba msaada kwa mtu ambaye alimpeleka hadi nyumbani kwa walezi wake ambao ni babu na bibi yake ambao ndiyo waliokuwa wakiishi naye kwa muda wote.
Kwa upande wake babu wa mwanafunzi huyo Daud Zakayo alisema kuwa mwanafunzi huyo alitoweka katika mazingira ya kutatanisha na walifanya jitihada kumtafuta ambapo walitoa taarifa polisi na kwa ndugu lakini bila ya mafanikio.
Zakayo alisema kuwa baada ya mjukuu wao kupatikana walitoa taarifa polisi ambapo vijana hao walikamatwa kwa ajili ya mahojiano kuhusiana na tukio hilo. Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alipoulizwa kuhusiana na tukio hilo alisema kuwa bado hajapata taarifa.
Mwisho.  

No comments:

Post a Comment