Monday, February 18, 2013

Na John Gagarini, Kibaha
DIWANI wa kata ya Maili Moja Bw Andrew Lugano amesikitishwa na mamalaka ya maji safi na majitaka (DAWASCO) kushindwa kuwahudumia wananchi hali inayosababisha kukosa maji kwa zaidi ya mwezi sasa.
Akizungumza mara baad aya kufanya ziara kwenye kata hiyo kuangalia maeneo ambayo yamekuwa yakikosa maji kwa muda mrefu, huku akiwa ameambatana na meneja wa DAWASCO Bw Robert Mugabe alisema kuwa hakuna sababu ya wananchi kukosa maji kwa muda wote huo na uongozi upo.
Bw Lugano alisema kuwa amekuwa akipata kero hiyo ya maji toka kwa wananchi na jitihada zake za kufuatilia zimekuwa zikigonga mwamba hali iliyomlazimu kumtoa meneja huyo ofisini kwake Jumamosi na kumwonyesha jinsi gani wananchi wanavyotaabika kwa kukosa maji.
“Siwezi kukubali kuona wananchi wakihangaika kutafuta maji huku chanzo cha maji kikiwa jirani hivyo lazima kampuni hiyo ijali wananchi ili waondokane na kero hiyo,” alisema Bw Lugano.
Moja ya wakazi wa kata hiyo ambaye anakaa mtaa wa Mzimuni Bw Mohamed Atiki alisema kuwa wamekuwa wakipata tabu kubwa ya kupata maji hali inayowasababisha kununua maji kwa bei ya shilingi 500 kwa dumu la lita 20.
“Tumekuwa tukihangaika kwa kipindi kirefu licha ya kutoa taarifa ya ukosefu wa maji kwenye kampuni hii ya maji hivyo lazima wabadili utendaji kazi wao,” alisema Bw Atiki.
Kwa upande wake meneja wa DAWASCO Kibaha Bw Robert Mugabe alisema kuwa tatizo kubwa lililosababisha wananchi kukosa maji ni kutokana na ujenzi wa barabara katika kata hiyo.
“Mabomba mengi yamekatwa kutokana na ujenzi wa barabara lakini hata hivyo tayari tumewasiliana na mkandarasi ili kuangalia namana ya kuweza kurekebisha hali hiyo,” alisema Bw Mugabe.
Bw Mugabe alisema kuwa tayari wameshafanya tathmini ya uharibifu uliofanyika na wakati wowote wataanza kufunga mabomba yaliyokatwa ili wananchi hao waendelee kupata maji kama kawaida.
Mwisho.
Diwani wa kata ya Maili Moja Kibaha kushoto Andrew Lugano akizungumza na meneja wa DAWASCO Kibaha kulia Robert Mugabe, kuhusiana na kata hiyo kuwa na tatizo kubwa la ukosefu wa maji (Picha na John Gagarini)

No comments:

Post a Comment