Thursday, February 21, 2013

MISITU


Na John Gagarini, Kibaha

WAKALA wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Kanda ya Mashariki wametakiwa kutoa elimu zaidi kwa wananchi juu ya upandaji miti kuliko kuvuna ili kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi ambayo yanapelekea uoto wa asili kutoweka.

Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na Katibu Tawala mkoa wa Pwani Bi Betha Swai wakati akifungua mkutano wa wataalamu wa sekta ya misitu kuweka mikakati mbalimbali juu ya kuboresha misitu kwenye mkoa huo.

Bi Swai alisema kuwa ukatiji wa miti ni mkubwa tofauti na miti inayopandwa jambo ambalo litaipelekea nchi kukumbwa na majanga yanayotokana na uharibifu wa mazingira ikiwemo ukame, mmomonyoko wa ardhi na ukosefu wa vyanzo vya maji.

“Ni vema mkatoa elimu kwa wananchi kwa kiwango kikubwa ili wananchi wakawa na uelewa juu ya uharibifu wa mazingira na umuhimu wa kutunza misitu kwani wengi wao hawaoni umuhimu wake licha ya kuwa wanatumia zao la miti katika kujipatia kipato,” alisema Bi Swai.

Aidha alisema kuwa halmashauri na serikali nazo zijikite kwenye utoaji elimu hiyo na si kutaka tu ushuru huku misitu ikiendelea kuteketea huku mikakati ya kupanda miti ikiwa si mizuri.

“Tuachane na kusema kuwa tumegawa miti sehemu Fulani kwa ajili ya kupanda kwa sasa tuwe na mkakati wa kupanda baadhi ya maeneo mfano kwenye mabonde au sehemu ambako kumefanyika uharibifu mkubwa ili tuonyeshe na si kusema kwa maneno tu,” alisema Bi Swai.

Kwa upande wake Bakari Mohamed alisema kuwa  lengo la kuanzishwa wakala hao amabo ni wapya ni kwa ajili ya kuondoa urasimu na mfumo wa kiutendaji katika utekelezaji wa majukumu ya misitu ili kuleta ufanisi.

Bw Mohamed alisema kuwa moja ya kazi za wakala ni kuihamasisha jamii kuanzisha misitu yao na kuilinda ile iliyopo pia kuwa na vikundi vya uzalishaji nyuki kwa kutumia rasilimali ya misitu.

Mwisho.      




No comments:

Post a Comment