Tuesday, February 12, 2013

WANANE WAFA AJALINI


Na Mwandishi Wetu, Kibaha

WATU nane wamefariki dunia na wengine wawili wamejeruhiwa baada ya magari mawili kugongana uso kwa uso katika Kitongoji cha Kibiki Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.
                   
Akizungumza na waandishi wa habari kamanda wa Polisi mkoani humo Ulrich Matei alisema kuwa kati ya watu waliokufa wanafunzi ni wanne.

Kamanda Matei alisema kuwa tukio hilo lilitokea Februari 11 majira ya jioni na kuyahusisha magari T363 AZG aina ya Toyota Mark II likitokea mkoani Tanga kwenda Morogoro likiendeshwa na Bw Abuu Ahmed na kugonagana na gari namba T 433 AYQ aina ya Mitsubishi Fuso likitoka Morogoro kwenda Dar es Salaam likiendeshwa na Bw Mweta Daniel.
 
“Chanzo cha ajali  hiyo ni mwendo kasi wa dereva wa Toyota Mark II ambaye alipoteza mwelekeo baada ya kujaribu kulipita gari lililokuwa mbele yake kisha kugongana uso kwa uso na Fuso lililokuwa likitokea mbele na kusababisha vifo hivyo,” alisema Kamanda Matei.
 
Kamanda Matei aliwataja waliokufa kuwa ni Esaau Enos (16) aliyekuwa kidato cha tatu, Bahati Mbene  (18) kidato cha nne, Latifa Shabani (17) kidato cha nne na Stella Kazimoto (18) wote  wanafunzi wa shule ya Sekondari Chalinze.
 
“Wengine ni Maria Lelela na mtoto wake Samweli Ismail kati ya miaka mitatu au minne, Hassan Kalunga na Abuu Ahmed dereva wa gari dogo,” alisema Kamanda Matei.
 
Aidha alisema kuwa majeruhi ni William Tobias na  Ahmada Juma aliyekuwa utingo wa fuso ambapo dereva wa Fuso anashikiliwa na Jeshi la polisi kwa uchunguzi zaidi.
 
Alitoa wito kwa madereva kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani ili kuepusha ajali na kudai kuwa Jeshi hilo halitowavumilia madereva wazembe kwa kuwakamata na kuwachukuliwa hatua kali wote watakaoshindwa kutii sheria za usalama barabarani.
           
MWISHO

No comments:

Post a Comment