Thursday, March 9, 2023

KIKWETE AOMBA USHIRIKIANO KUTIMIZA LENGO LA RAIS KUWA NA MUUNDO WA UTUMISHI KWA USTAWI WA TAIFA

MHE. RIDHIWANI KIKWETE AOMBA USHIRIKIANO KUTIMIZA LENGO LA MHE. RAIS LA KUWA NA SERA ZA KIUTUMISHI NA MIUNDO YENYE TIJA KWA USTAWI WA TAIFA

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

NAIBU Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amewataka watumishi wa Idara ya Uendelezaji Sera na Idara ya Uendelezaji Taasisi kumpa ushirikiano wa kutosha kwenye eneo la kusimamia uendelezaji wa sera katika Utumishi wa Umma na miundo ya Taasisi za Umma.

Mhe. Kikwete ametoa rai hiyo Jijini Dodoma wakati wa kikao kazi chake na watumishi wa Idara ya Uendelezaji Sera na Idara ya Usimamizi wa Taasisi kwa nyakati tofauti kilicholenga kufahamu majukumu yanayotekelezwa na Idara hizo pamoja na kuhimiza uwajibikaji.

 Amesema kuwa ili aweze kumsaidia vema Waziri mwenye dhamana kufikia lengo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan la kuwa na sera za utumishi wa umma zenye tija na miundo inayotekelezeka kiutendaji kwa ustawi wa taifa.

Mhe. Kikwete amesema ameteuliwa na Mhe. Rais kumsaidia Waziri mwenye dhamana ya kusimamia utumishi wa umma na utawala bora, hivyo hana budi kufahamu kwa kina majukumu yanayotekelezwa na idara hizo ili aweze kuyazungumzia pale yanapohitaji ufafanuzi na uelewa kwa umma.

“Malengo ya kukutana nanyi leo ni kufahamiana na kujua majukumu yenu kwa kina kwa kuwa mimi nina jukumu la kumsaidia Mhe. Waziri kujibu maswali ya kiutumishi na utawala bora yanayoulizwa Bungeni,” Mhe. Kikwete amesisitiza.

Ameongeza kuwa, anatamani kujua kila kitu kinachofanyika katika idara hizo pamoja na changamoto wanazokabiliana nazo kiutendaji kwani kwa kufanya hivyo atakuwa kwenye nafasi nzuri ya kutekeleza kwa ufanisi lengo la Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan la kutoa huduma bora kwa wananchi.

Aidha Kikwete ameitaka Idara ya Undelezaji Sera kuhuisha sera za kiutumishi ili ziendane na wakati na ziweke mazingira rafiki ya kuzihusisha sekta binafsi kutoa mchango katika kuboresha utumishi wa umma kama Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan alivyoelekeza.

No comments:

Post a Comment