Sunday, June 28, 2026

MAWAZO VIJANA CHALLENGE KUTUMIKA KIMAENDELEO



SERIKALI imesema kuwa itatumia mawazo ya vijana walioshiriki shindano la Vijana Uchumi Challenge kuwa mpango ambao utaleta suluhisho la namna ya kutatua baadhi ya changamoto ndani ya jamii.

Hayo yalisemwa Kibaha na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Jenifa Omollo wakati wa kufunfa mafunzo ya siku nne kwa vijana 100 walioandika mawazo juu ya masuala ya uchumi kupitia jukwaa la Vijana Uchumi Challenge.

Omollo alisema kuwa mawazo yaliyoandikwa na vijana yameonyesha kuwa yakiboreshwa yanaweza kuwa mpango mzuri ambao unaweza kukabili changamoto mbalimbali ndani ya jamii na Taifa kwa ujumla.

"Mawazo yote yaliyowasilishwa hayataachwa badala yake yataboreshwa na kupatiwa fursa ili yawe mpango ambao utakuwa suluhu kwa baadhi ya changamoto ili kuleta tija na kusaidia Taifa mojawapo likatoa ajira kwa vijana,"alisema Omollo.

Alisema kuwa mawqzo hayo ni bunifu ambazo zimeonyesha jinsi gani vijana walivyokuwa na vipaji ambavyo vitatoa ajira na kuwa na manufaa kwa watu wengi hivyo kulisaidia Taifa.

Naye mwenyekiti wa kamati ya Vijana Uchumi Challenge Joseph Malecela alisema kuwa jumla ya mawazo zaidi ya 7,000 ya vijana kote nchini wenye umri kati ya miaka 15 hadi 35 yaliwasilishwa na kuchujwa na kubaki 100 ambayo yatashindanishwa kupata mshindi.

Malecela alisema kuwa washiriki hao 100 ambao waliiingia kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere wamechujwa na majaji wabobezi wa masuala ya uchumi na fedha na kubaki 10 watashindana ili kumpata mshindi wa shindano hilo.

Rais Dk Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye kilele cha kumpata kijana mwenye wazo zuri Julai 6 mwaka huu Jjiini Dar es Salaam kwenye Ukumbi wa Julius Nyerere Internation Convention Centre (JNICC) Jijuni Dar es Salaam.







mwisho


Thursday, June 25, 2026

MAWAKALA WAITWA KUCHANGAMKIA VIPAJI TUMBI KIBAHA

MAWAKALA wa michezo ikiwemo soka wametakiwa kujitokeza kushuhudia vipaji vya wacehzaji chini ya miaka 17 na 22 kwenye mashindano ya Compassion ili kuwa na timu bora zitakazozalisha wachezaji wakulitumikia Taifa ambapo moja zao la wachezaji hao ni Dickson Job anayechezea timu ya Yanga.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Lucas Kiluwasha ambaye ni mwenyekiti wa Mashindano ya Compassion Kanda ya Mashariki kwenye Viwanja vya Shirika la Elimu Kibaha Tumbi.

Mashindano hayo ambayo ni ya nne kufanyika yameweza kuwatoa wachezaji wengi akiwemo Dickson Job wa Yanga, Paschal Msindo wa timu ya Azam na Haji Abdala kipa wa timu ya Serengeti Boys chini ya miaka 17 iliyoshika nafasi ya pili kwenye michuano ya Afcon ya vijana iliyofanyika Morocco hivi karibuni.

Mbali ya kuzalisha wachezaji hao ambao wanatambulika pia imezalisha wachezaji wengine ambao wako timu za Yanga B, Azam na Fountain Gate pamoja na msanii wa muziki wa kisasa Dogo Janja na wasanii mbalimbali hapa nchini.

Kiluwasha amesema kuwa mashindano hayo ambayo hufanyika kila mwaka yanashirikisha jumla ya mikoa mitatu ya Pwani, Dar es Salaam na Morogoro ambapo kuna wachezaji zaidi ya 430 kauli mbiu ya mwaka huu inasema “Kipaji Changu Mtaji Wangu”.

“Michezo inayoshindaniwa ni pamoja na soka, mpira wa pete, riadha na michezo ya ndani ikiwa ni pamoja na kupiga vyombo vya muziki, ubunifu wa mavi na sanaa mbalimbali lengo ni kuinua na kuibua vipaji kwa vijana,”alisema Kiluwasha.

Alisema kuwa kwa sasa mara wanapopatikana vijana wa michezo husika huwapeleka ili wakaendeleze vipaji vyao ambapo wa soka huwapeleka kwenye timu zenye Academy ili waweze kukuza vipaji vyao na kujipatia ajira kupitia michezo.

“Changamoto kubwa ni ushiriki mdogo wa wadau kujitokeza kuhudhuria mashindano yao pia baadhi ya wachezaji kwenda kushiriki michezo ya Umisseta na Umitashumta kwani nao hufanya kipindi cha likizo hivyo kuwa na mwingiliano,”alisema Kiluwasha.

Aidha alisem akuwa malengo yao ya baadaye ni kuanzisha timu ya mipra wa miguu ili ishiriki ligi mbalimbali na hatimaye kufika ligi kuu pia wanazikaribisha timu mbalimbali kama zinahitaji wachezaji kuona nao ili kukubalina na kuwachukua ili wakaendeleze vipaji vyao.

Wachezaji hao wanatoka kwenye vituo vya huduma ya mtoto na kijana kwenye makanisa ya Kiinjili na Kipentekoste kwenye mikoa hiyo na wachezaji watakaofanya vizuri watachaguliwa kwenda kushiriki mashindano hayo kitaifa.

Tuesday, June 23, 2026

WAZO BORA LA KIJANA KUNYAKUA MILIONI 50

KIJANA mwenye wazo bora kati ya vijana 100 watakaowania kinyanganyiro cha Vijana Uchumi Challenge anatarajiwa kujinyakulia kitita cha shilingi milioni 50.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Dk Kedmon Mapana wakati akizungumza na vijana hao 100 watakaokuwa kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere iliyopo Kibaha Mkoani Pwani.

Mapana amesema kuwa wapili akijinyakulia shilingi milioni 20 na watatu milioni 10 ambapo vijana wanaoshiriki ni wenye umri chini ya miaka 35 kutoka nchi nzima.

"Wizara ilitoa shindano la vijana kutoa wazo la kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia mawazo ya vijana kukuza ubunifu na Ujasiriamali na kuwapa vijana fursa ya kuonyesha mawazo yao ya kibiashara na miradi ya kibunifu inayoweza kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi,"amesema Mapana.

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya Vijana Uchumi Challenge Joseph Malecela amesema kuwa jumla ya mawazo zaidi ya 7,000 ya vijana kote nchini yaliwasilishwa na kuchujwa na kubaki 100 ambayo yatashindanishwa kupata mshindi.

Malecela amesema kuwa washiriki hao 100 ambao wameingia kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere watachujwa na majaji wabobezi wa masuala ya uchumi na fedha na kubaki 30 na baadaye 10.

Kilele kinatarajiwa kufanyika Jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi atakuwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan.

VIJANA 100 KUWANIA MILIONI 50 VIJANA UCHUMI CHALLANGE

NAIBU Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Dk Kedmon Mapana amesema vijana kuwa na ujuzi na mtaji ni suluhisho la kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050.

Ameyasema hayo Mjini Kibaha kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere wakati akifungua Jukwaa la Vijana Uchumi Challenge.

Mapana amesema kuwa Waziri wa Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Joel Nanauka alizindua shindano la vijana kwa ajili ya kuwawezesha vijana nchini Tanzania kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na ubunifu. 

"Lengo kuu la mpango huu ni kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia mawazo ya vijana kukuza ubunifu na Ujasiriamali na kuwapa vijana fursa ya kuonyesha mawazo yao ya kibiashara na miradi ya kibunifu inayoweza kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi,"amesema Mapana.

Amesema kuwa pia ni kuongeza ajira kwa kusaidia miradi ya vijana kuanzishwa au kukua ambapo shindano linakusudia kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa kuwezesha vijana kujiajiri na kuajiri wengine.

"Kwa wale ambao hawatafanikiwa kushinda mawazo yao yatachukuliwa na kufanyiwa kazi kwa kupewa mafunzo kutokana na mawazo yao ya bunifu zao kupitia sekta mbalimbali zikiwemo za kilimo uvuvi mifugo tehama na ujasiamali,"amesema Mapana.

Aidha amesema vijana wasilalamike bali watoe mawazo na suluhisho nini kifanyike hata ikitokea changamoto kama za kupanda bei ya mafuta ili uchumi wa nchi uwe stahimilivu

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya Vijana Uchumi Challenge Joseph Malecela amesema kuwa jumla ya mawazo zaidi ya 7,000 ya vijana kote nchini yaliwasilishwa na kuchujwa na kubaki 100 ambayo yatashindanishwa kupata mshindi.

Malecela amesema kuwa washiriki hao 100 ambao wameingia kambini kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere watachujwa na majaji wabobezi wa masuala ya uchumi na fedha na kubaki 30 na baadaye 10.

Amesema kuwa washindi 10 watakwenda kwenye kilele kitakachofanyika Jijini Dar es Salam Julai 6 ambapo mshindi atapata kiasi cha shilingi milioni 50 huku wapili akijinyakulia shilingi milioni 20 na watatu milioni 10 ambapo vijana wanaoshiriki ni wenye umri chini ya miaka 35.

Kilele kinatarajiwa kufanyika Jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi atakuwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan.

PWANI YAKUSANYA BILIONI 266

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani imefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 266 katika kipindi cha miaka 10 iliyopita na kuvuka malengo yaliyowekwa ya kukusanya shilingi bilioni 235 katika kipindi hicho.

 

Akizungumza kwenye Kongamano la Mamlaka hiyo ya kutimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake Meneja wa TRA Mkoa wa Pwani Peter Jackson alisema kuwa mafanikio hayo ni ongezeko la asilimia 113 ya makusanyo kwa kipindi hicho.

 

Jackson alisema kuwa mafanikio hayo yametokana na ushirikiano ulioonyeshwa na wafanyabiashara na wadau wote wa kodi ambapo katika kipindi hicho malaengo ya makusanyo yalikuwa ni bilioni 23 lakini zilikusanywa kiasi cha shilingi bilioni 27.

 

“Kwa wastani makusanyo kwa kipindi cha miaka 10 ni ongezeko la asilimia 10 ambapo yamekuwa yakiongezeka hadi kufikia kiasi hicho na kuonyesha jinsi gani mamlaka hiyo inavyopiga hatua katika kuleta maendeleo ya nchi,”alisema Jackson.

 

Alisema kuwa makusanyo yana faida kubwa kwani yanatumika kwa ajili ya kufanya shughuli za kimaendeleo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ikiwemo ya barabara ujenzi wa reli ya kisasa SGR huduma za afya, huduma za elimu na masuala mbalimbali.

 

Aidha alisema kuwa ukusanyaji wa mapato makubwa ndiyo njia ya kukuza uchumi wa nchi ambapo walipa kodi wanapaswa kulipa kwa hiyari na kwa wakati ili kuondoa changamoto za kupewa adhabu ambayo inawarudisha nyuma.

 

“Kwa sasa tumeweka mifumo madhubuti ya ukusanyaji na namna ya kuwafikia kwa urahisi walipa kodi na kuwaondolea usumbufu wa kufika ofisini badala yake wanauwezo wa kulipa au kufanya shughuli zote wakiwa maeneo yao jambo ambalo limerahisisha utendaji kazi,”alisema Jackson.

 

Akizungumzia kuhusu changamoto alisema kuwa ukuaji wa uchumi usio rasmi umekuwa ni tatizo kwani unakuwa nje ya mfumo rasmi hivyo kusababisha kukosekana kwa mapato kutokana na kukwepa au kupunguza kodi kuongezeka kwa biashara mtandaoni biashara haramu na za magendo ambazo huathiri ushindani wa kibiashara..

 

Kwa upande wake mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT) Mkoa wa Pwani Abdala Ndauka alisema kuwa baadhi ya wafanyabiashara hawana uelewa juu ya masuala ya ulipaji kodi hivyo kuna haja ya kutolewa elimu ya kutosha.

 

Ndauka alisema kuwa ulipaji kodi unapaswa kuwa rafiki na si kama adhabu bali uwe rafiki hata hivyo malalamiko kwa sasa yamepungua kwani kwa sasa kumekuwa na majadiliano juu ya changamoto zinazowakumba walipa kodi na watengeneze walipa kodi wapya.

 

Mwenyekiti wa Chemba ya wafanyabiashara Mkoa wa Pwani Said Mfinanga alisema kuwa matumizi ya teknolojia yamesaidia kuwapunguzia muda walipa kodi kwenda ofisini ili kufanya kufanya taratibu mbalimbali juu ya masuala ya ya biashara zao.

 

Mfinanga alisema kuwa mfumo wa teknolojia pia utumike kutoa elimu juu ya masuala ya ulipaji kodi na taratibu zote zihusikanazo na masula ya kodi ili kujenga uelewa wa pamoja kwa walipa kodi na mamlaka hiyo ambayo inajuhusisha na ukusanyaji wa mapato ya serikali.   

 

Naye mwenyekiti wa Shirikisho la Umoja wa Machinga (SHIUMA) Mkoa wa Pwani Philemon Maliga alisema kuwa ili kuboresha ukusanyaji wa mapato Mamlaka inapaswa kuwa na mahusiano bora na mazuri na walipakodi kwnai kundi lao ni kubwa na lina uwezo wa kuchangia pato la serikali.

 

Maliga alisema kuwa TRA iatoe limu kuanzia mashuleni na sehemu mbalimbali ili kuwajengea walipa kodi utamaduni wa kulipa mapato ili kuonyesha uzalendo wa nchi yao kwani kodi ndiyo msingi mkubwa wa maendeleo.

 

Monday, June 15, 2026

TAARIFA KWA UMMA


Ofisi ya Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, inapinga na kukanusha vikali taarifa ya uongo na upotoshaji inayosambaa mitandaoni, ikidai kuwa Dkt. Kikwete anahusishwa na mradi unaodaiwa kuwa wa uwekezaji unaowaahidi Watanzania kipato cha uhakika kupitia jukwaa la kifedha linalotumia teknolojia ya akili mnemba

Taarifa hiyo inadai kuwa maelfu ya Watanzania tayari wamenufaika na mradi huo baada ya kuwekeza kiasi cha shilingi 653,000, huku wakiahidiwa kupata zaidi ya shilingi 9,200,000 kwa mwezi. Madai hayo si ya kweli hata kidogo.

Ofisi ya Rais Mstaafu inapenda kuweka wazi kwamba Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete hajawahi kushiriki, kuidhinisha, kutangaza, kuunga mkono, wala kuhusika kwa namna yoyote ile na mpango huo wa kifedha. 

Ofisi yake haijawahi kuruhusu matumizi ya jina, picha, au heshima yake kuhusishwa na mradi huo unaodaiwa, na haitajihusisha na shughuli za aina hiyo.

Wananchi wanashauriwa kupuuza taarifa hiyo ya uongo na kuwa makini dhidi ya miradi ya kitapeli na vitendo haramu vya aina hiyo. 

Mtu yeyote atakayekutana na taarifa kama hizo za upotoshaji anapaswa kuzichukulia kama habari za uongo, kuepuka kuzisambaza, kujisajili, au kutuma fedha kwa mtu au jukwaa lolote linalohusishwa nazo.

Sunday, June 14, 2026

PWANI YAENDELEA KUHAMASISHA UCHANGIAJI DAMU KUOKOA MAISHA YA WATU

MKOA wa Pwani umekusanya jumla ya chupa za damu 1,129 kwa ajili ya Hospitali na Vituo vya Afya.

Hayo yamesemwa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani Kusirye Ukio wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mchangiaji Damu wa Dunia kimkoa ambapo maadhimisho hayo yamefanyika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani Tumbi.

Kwa upande wake Msimamizi wa Huduma kwa Mteja na Wachangiaji Damu Salama Makao Makuu Kaito Tamba amesema kuwa kwa sasa mpango ni kukusanya chupa 600,000 kwa mwaka 

Akisoma risala ya siku hiyo Mkuu wa Idara ya Maabara Hospitali ya Tumbi Simon Lupatu amesema kuwa kauli mbiu ya mwaka huu inasema "Changia Damu Okoa Maisha" ambapo wanahitaji mashine kwa ajili ya uzalishaji mazao ya damu.

Naye Mkuu wa Idara ya Kinamama na Uzazi wa Hospitali ya Tumbi Dk Alfonce Moyo amesema kuwa takwimu zinaonyesha vifo vilivyotokea kwa mwezi Januari hadi Juni mwaka huu asilimia 80 vilitokana na kupoteza damu nyingi.