Monday, March 11, 2024

KATA YA MAILI MOJA WAELEZEA MAFANIKIO NA CHANGAMOTO

KATA ya Maili Moja Wilayani Kibaha Mkoani Pwani imeelezea mafanikio na changamoto huku wakiitaka Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) kukarabati miundombinu ya barabara ambayo imeharibika vibaya.

Diwani wa Kata hiyo Ramadhan Lutambi ameelezea baadhi ya mafanikio na changamoto mbele ya Katibu Tawala wa Wilaya ya Kibaha Moses Magogwa ambaye alimwakilisha mkuu wa Wilaya ya Kibaha wakati wa mkutano wa hadhara kwenye mtaa wa Uyaoni.

Lutambi amesema baadhi ya mafanikio ni kwenye sekta ya elimu ambapo kwenye sekondari ya Bundikani kwenye matokeo ya kidato cha nne mwaka jana wamefanikiwa kuondoa daraja sifuri na ujenzi wa madarasa mapya.

Amesema kwa upande wa shule za msingi wamefanikiwa kuanzisha shule mpya ya Muheza, shule za Maendeleo na Maili Moja zimejengewa madarasa mapya, kwa upande wa serikali za mitaa kujenga ofisi zake badala ya kupanga.

"Kuna baadhi ya changamoto lakini kubwa ni miundombinu ya barabara hii ni tatizo kwa mitaa yote suala la urasimishaji, umeme kukatika mara kwa mara, baadhi ya maeneo kukosa maji na umeme na mikopo ya kausha damu,"amesema Lutambi.

Kwa upande wake katibu tawala wa Wilaya ya Kibaha Moses Magogwa amesema kuhusu changamoto ya barabara atawaelekeza Tarura ili wakae na wananchi ili kuangalia vipaumbele vya barabara ili zianze kufanyiwa marekebisho.

Magogwa amesema kuhusu urasimishaji wote waliopewa hiyo kazi wakutane naye ofisini ili kuangalia namna ya kutatua changamoto hiyo ili kuondoa malalamiko ya wananchi.

Amesema kuhusu mikopo ya kausha damu viongozi wa mitaa wakae na wamiliki wa taasisi hizo za mikopo ili kuangalia namna ya kudai marejesho badala ya kuwadhalilisha watu.

Ameongeza kuwa serikali inasikiliza kero za wananchi ili kuzitatua kwani Rais Dk Samia Suluhu Hassan anapambana kuhakikisha wananchi wanaishi kwenye mazingira mazuri.

Saturday, March 9, 2024

BAWACHA YAWATAKA WANAWAKE WANAOLEA WATOTO PEKE YAO KUOMBA MSAADA


Na, Wellu Mtaki, Dodoma 

Mwenyekiti wa Baraza la wanawake wa chama cha demokrasia na maendeleo CHADEMA (BAWACHA) Sharifa Suleiman amewakumbusha wazazi wanaoleo watoto peke yao kuomba msaada wa malezi  kwani kumekuwa na wimbi kubwa la watoto kukosa malezi ya wazazi wote wawili

Bi. Sharifa ameyasema hayo Jijini Dodoma wakati wa maadhimisho ya  siku ya Wanawake Duniani ambapo kitaifa yamefanyika Jijini Dodoma huku akiongeza kuwa suala la malezi na makuzi linahitajika kwa pande zote mbili kwani wanategemeana kwenye malezi.

Aidha ameongeza kuwa changamoto ya afya ya akili imefanya wazazi wengi kukimbia familia zao jambo linalofanya hali ya familia kwasasa kuwa katika hali mbaya.

Naye Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe amewasisitiza wanawake kuwa na udhubutu wa kugombea nafasi mbalimbali za uongozi serikalini.

Nao baadhi ya wahudhuriaji katika maadhimisho hayo wamezungumzia kuhusiana na kitu kinachosababisha wanaume wengi kukimbia familia zao na kushindwa kutimiza jukumu lao la malezi.

Friday, March 8, 2024

WANAWAKE WATAKIWA KUWA NA MATUMIZI SAHIHI YA FEDHA

 

Na Wellu Mtaki, Dodoma

WANAWAKE nchini wametakiwa kutambua suala la matumizi sahihi ya fedha ili kuweza kujiongezea kipato zaidi na kujikwamua kiuchumi.

Hayo yameelezwa na  Mkurugezi Msaidizi sehemu ya usimamizi Rasilimali watu Wizara ya fedha Bi, Faudhia Nombo wakati akimwakilisha katibu mkuu wizara ya fedha katika  maonesho ya banda la wizara hiyo  leo Machi 7  siku ya ufunguzi  wa maonyesho ya wanawake  kuelekea maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani.

Nombo amesema wizara inaendelea kutoa Elimu kwa wanawake kujiandaa wakati wa kustafu kazi katika kipindi cha uzee pamoja na suala la kutunza fedha 

"Wizara haitokaa kimya ila itahakikisha inaendelea kutoa Elimu kwa wanawake ili pindi wanapostafu kazi wapate fedha za kujikimu kipindi chote cha uzee , wapo wanawake wanatumia fedha katika majukumu ambayo si sahihi na mwisho wa siku fedha hupotea na kuelekea mwisho mbaya uzeeni," amesema Nombo.

Aidha amesema kuwa wanawake wengi wanatamani kuingia katika vikoba ili kuweza kujikimu kiuchumi ila wanashidwa kutambua namna ya utunzaji wa fedha hivyo wizara imeona watoe mafunzo ya namna ya kutunza fedha katika maonesho ya siku ya wanawake Dunia.

Pia ametoa wito kwa wanawake wa Dodoma kutambua fursa zilizopo katika wizara hiyo na kutumia kiusahihi ili kufanikisha shughuli zao za kiuchumi.

KUNDO ATAKA VYOMBO VYA HABARI NCHINI KUANZISHA VIPINDI VYA KUHAMASISHA MILA NA DESTURI ZA WATANZANIA.

NAIBU Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Mathew Kundo amevitaka vyombo vya habari kuanzisha vipindi vinavyohamasisha mila na Destiri ya mtanzania ili kuwaelimisha vijana kuhusu tamaduni zao.

Mhandisi Kundo ametoa kauli hiyo Leo Februari 13,2024 Jijini Dodoma , alipomwakilisha Waziri wa Habari,Mawasiliano na Teknolojia ya habari Mhe. Nape Nnauye, katika ufunguzi wa Mkutano wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji Nchini ulioenda sambamba na kilele cha maadhimisho ya siku ya Utangazaji Duniani

“Ni muhimu sana kwenu TCRA kuliangalia suala hili kwa umakini mkubwa kwani Mkifanya hivi itawasaidia sana kufanya kazi kwa ufanisi,na Sisi kama Serikali tunawaahidi kuendeleza ushirikiano uliopo ili kuleta maendeleo kwa jamii, "amesema Mhandisi Kundo

Pia Mhandisi Kundo ameiagiza Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA),kuhakikisha inajitathmini Mara kwa Mara ili kujua ni wapi kuna mapungufu na kuweza kuyafanyia kazi mapungufu hayo.

Katika hatua nyingine Mhandisi Kundo amebainisha kuwa katika kuelekea uchaguzi wa Serikali za Mitaa Vyombo vya Habari vinatakiwa kuwa mstari wa mbele katika kuzingatia Maadili na kanuni za utoaji Habari kwa jamii kwa maslahi ya Taifa.

“Vyombo vya habari vina wajibu mkubwa katika Taifa letu hivyo Ni muhimu kila mmoja kuzingatia taaluma na kutimiza majukumu yake kwa weledi mkubwa,amesisitiza Naibu Waziri

Aidha amewaasa Waandishi wa habari kuhakikisha wanazingatia usawa katika kuripoti matukio ya kampeni za Uchaguzi na matokeo Yake bila upendeleo

Kwa upande Wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania( TCRA )Jones Kilimbe amewataka watangazaji na waandishi wa habari kuzingatia Madili na kanuni ya kazi zao.

Amegusia pia uchaguzi  wa Serikali za mitaa kuwa,vyombo vya habari vina jukumu la kutoa elimu kwa wapiga kura ikiwa ni pamoja na kuhabarisha umma kuhusu mwenendo mzima wa kampeni bila upendeleo na kutoa ripoti sahihi za siku ya kupiga kura.

Amesema TCRA kama wadau wa Utangazaji watahakikisha wanakuwa bega kwa bega na vyombo vya Utangazaji kwa kuhakikisha wanatoa mwelekeo wa maudhui yenye ubora bila upotoshaji.

Thursday, February 29, 2024

BMH YAENDELEA KUPANDIKIZA BETRI KWENYE MOYO



Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) ya jijini Dodoma imefanya upandikiza betri kwenye moyo kwa watu watatu.

Upandikizaji wa betri kwenye moyo ambao kitaalamu unaitwa _pacemakers_  _implantation_ unafanyika kwa watu wenye matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo na kusababisha mapigo ya moyo kuwa chini ya kiwango kinachotakiwa kwa mtu wa kawaida ambayo ni 60-100 kwa dakika.Wengi wao huwa ni chini ya 40.

Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya Moyo wa BMH, Daktari Bingwa wa Moyo, Happiness Kusima, amesema leo kuwa BMH imefikisha upandikizaji kwa watu 18 toka huduma ianzishwe mwaka 2021.

"Jana tumepandikiza watu watatu (3), leo tumepandikiza watu wawili," amesema Daktari huyo Bingwa wa Moyo.

Dkt Happiness amesema upandikizaji huu umefanyika kwenye kambi ya Madaktari Bingwa wa Moyo wa BMH kwa kujengewa uwezo na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) ya jijini Dar es Salaam.

ZEGERENI FC MABINGWA LIKUNJA CUP


TIMU ya soka ya Zegereni Fc imetwaa ubingwa wa Likunja Cup baada ya kuifunga Visiga Veterans kwa mabao 2-0

Mchezo huo ulifanyika kwenye uwanja wa Shule ya Msingi Zegereni ulihudhuriwa na mashabiki wengi licha ya mvua kubwa kunyesha.

Washindi walipata seti ya jezi na mpira mmoja huku mshindi wa pili akijinyakulia jezi seti moja ambapo zawadi hizo zilitolewa na Mwenyekiti wa CCM Kibaha Mjini Mwajuma Nyamka.

Nyamka amesema kuwa michezo ni ajira hivyo mashindano hayo ni moja ya utekelezaji wa ilani ya CCM hivyo kuwataka wadau wa michezo kuandaa michezo mingi.

Amesema kuwa mbali ya michezo kuwa ajira pia ni afya hivyo wananchi washiriki michezo na wahakikishe wanadumisha ulinzi na kuwaondoa vijana kwenye matumizi ya dawa za kulevya.

Naye mwandaaji wa mashindano hayo Rashid Likunja ambaye ni mwenyekiti wa serikali ua mtaa wa Zegereni amesema kuwa jumla ya timu 12 zilishiriki mashindano hayo.

Likunja amesema mashindano hayo kwa mwaka huu ni mwaka wa 10 kuyaandaa ambapo mwakani zawadi zitaongezwa ili kuleta msisimko.

Wednesday, February 28, 2024

Taasis ya Digital Agenda for Tanzania Initiatives yasisitiza haki ya faragha na ulinzi wa taarifa binafsi Nchini.*


Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Wataalamu kutoka Taasisi ya Digital Agenda for Tanzania Initiative imekutanaa pamoja na wadau kutoka Wizara ya habari, mawasiliano na teknolojia ya habari  wamekutana Jijini Dodoma kujadiliana kuhusu utetezi wa haki kidigitali.

Lengo la kikao hicho ni kutoa matokeo ya ripoti mbili zilizofanywa na Taasisi ya Digital Agenda Tanzania Initiative kuhusu utambuzi Kwa kutumia taarifa za kibayometriki,usajili wa laini za simu unaofanywa na Makampuni ya simu nchini.

Tafiti  imebainisha kuwa makampuni  ya simu nchini licha ya kufanya vizuri katika kutoa huduma lakini bado kuna mapungufu  katika kulinda haki ya faragha na ulinzi wa taarifa binafsi zonazowahusu wateja wao.

Akibainisha mapungufu hayo mkurugenzi mtendaji wa taasisi hiyo Peter Mmbando amesema kuwa ulinzi wa data, uhuru wa kujieleza pamoja na uendeshaji wake vilibainika kuwa ni moja kati ya mapungufu ya mitandao hiyo.

Mmbando amesema kuwa, elimu zaidi Kwa wananchi inapaswa ku ndelea kutolewa ili kuhakikisha taarifa zao zinakuwa salama pamoja na kuhakikisha wanaepukana na makosa ya kimtandao ambayo yamekuwa yakifanyika.

Kwa upande wake  Mtaalamu wa ulinzi wa taarifa binafsi Nchini Tanzania,Mrisho Swetu ameitaka jamii kuamka na kuwa mstari wa mbele katika kulinda taarifa zao. Amesisitiza kuwa taarifa binafsi nyeti za kibayometriki mfano alama za vidole zina athari kubwa endapo zitatumika vibaya.

Pia ameendelea kuhimiza wadhibiti na wachakataji wa taarifa binafsi Nchini kuboresha viwango vya ulinzi wa taarifa binafsi pamoja  na kuendelea kutoa elimu ya ulinzi wa taarifa binafsi kwa mujibu wa sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi,2022. Wadhibiti na wachakataji wanapaswa kuheshimu haki ya faragha na hyo itasaidia kuongeza uaminifu na wateja wao.

Kwa upande wa Jamii amesema,wadau wa serikali na sekta binafsi waendelee kutoa elimu kwa umma kuhusu haki ya faragha na ulinzi wa taarifa binafsi.Jamii inapaswa kupewa elimu ya kutosha kuhusu ulinzi wa taarifa binafsi pamoja na haki zao kama haki ya kuomba kufutwa kwa taarifa zako,haki ya kurekebisha,haki ya kupata fidia pale itakapotokea misingi ya sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi imekiukwa.

Aidha,ameendelea kusema, mafunzo hayo wamelenga kuyafikia makundi yote katika jamii, mikoa yote ambapo kwa upande wa watu wenye ulemavu wa kuona na kusikia wapo kwenye mpango wa kukutana na wataalamu wa lugha ya alama ili  kujua elimu hiyo itawafikiaje jamii hiyo ya watu wenye ulemavu. 

"Lengo ni kuikumbusha jamii matumizi sahihi  ya taarifa  binafsi,kujua haki zao ,lakini ni muhimu wafahamu kuwa taarifa zao binafsi zikitumika vibaya zinaweza kuleta madhara,lakini wafahamu kuwa endapo kutatokea  uvunjifu wa sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi basi ni wapi wanaweza kupeleka malalamiko yao" amesema Mrisho Swetu 

Naye, Afisa Mwandamizi Tume ya Haki za binadamu za Utawara Saidi Zuberi amesema mafunzo hayo yatakwenda  kumasaidia mwananchi kuweza kulinda  taarifa zake na kutambua haki za faragha. 

Pia ametoa wito kwa watoa elimu wa tume ya ulinzi wa data kuwa na miongozo itayoweza kutoa elimu ya haki ya faragha katika jamii .