Monday, February 8, 2016

WATU 53,000 WAKUMBWA NA MAFURIKO PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
WATU 53,446 wilayani Rufiji mkoani Pwani wamekumbwa  na mafuriko hali iliyowafanya wazungukwe na maji na kuhitaji msaada kufuatia mvua za Vuli zinazoendelea hapa nchini.
Aidha tayari boti mbili za uokozi tayari zimepelekwa kwenye maeneo hayo kwa ajili ya kuwaondoa watu hao waliozungukwa na maji na kuwapeleka sehemu salama.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu toka kwenye eneo la tukio, Mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kuwa maji hayo ambayo yametoka maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na mkoa wa Morogoro.
“Vijiji vingi wilayani humo vimezingirwa na maji na watu wengi waliokumbwa na kadhia hiyo ni wale waliohamia mashambani kwa ajili ya kilimo na kukutwa na maji hayo pamoja na nyumba ambazo ziko mabondeni,” alisema Ndikilo.  
Alisema kuwa mvua hizo ambazo zilizoanza kidogo kidogo tangu Januari 31 mwaka huu zimeathiri zaidi kwenye maeneo ya kata za Mwaseni, Tarafa ya Mkongo, Tarafa ya Ikwiriri na kata ya Muhoro.
“Kutokana na athari za mvua hizo hekta zaidi ya 7,000 za Mahindi na hekta zaidi ya 8,000 za Mpunga  zimesombwa na maji na tayari mkoa umewasiliana na Waziri Mkuu kwenye kitengo cha Wakala wa mazao kuomba msaada wa chakula tani 1,280 za mahindi,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa wameteua wafanyabiashara sita kwa ajili ya kununua mahindi na kuyasaga kwa ajili ya chakula ikiwa ni njia ya kuwasaidia wananchi pia kukabili mfumuko wa bei ambao unaweza kujitokeza kutokana na hali hiyo.
Katika hatua nyingine mkoa umeomba tani 10 za mbegu za mahindi na tani tano za mbegu za Mtama kwa ajili ya kupanda kukabiliana na athari ya mazao ambayo yamesombwa na maji ya mvua za Vuli ambazo wiki ijayo zitaanza mvua za Masika.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI imeombwa kuipatia Idara ya Ziamamoto mkoani Pwani vifaa kwa ajili ya kukabiliana na majanga ya moto na kuokoa watu wanaokumbwa na majanga mbalimbali.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini Kibaha Kamanda wa Kikosi cha Zimamoto mkoani Pwani Goodluck Zelote alisema kuwa kutokana na uhaba wa vifaa baadhi ya wilaya hazina vituo vya zimamoto.
Zelote alisema kuwa kwenye mkoa wa Pwani kati ya wilaya sita ni wilaya tatu tu za Kibaha, Bagamoyo na Mafia ndiyo zenye vikosi hivyo huku wilaya za Kisarawe, Rufiji na Mkuranga zikiwa hazina huduma hiyo.
“Ingependeza angalau kila wilaya kuwa japo na kikosi cha Zimamoto na uokoaji japo hakitaweza kutoa huduma kwenye eneo lote lakini angalau zingesaidia ambapo kwa sasa utendaji kazi unakuwa mgumu,” alisema Zelote.
Alisema kuwa vifaa hivyo ni magari pamoja na vifaa vya uokoaji ambapo alitoa mfano wa ajali ya moto ambayo ilitokea hivi karibuni Chalinze walifika na kunusuru nyumba yote kuteketea kwa moto lakini kutokana na umbali uliopo walinusuru vyumba kadhaa.
“Kwa sasa tunachokifanya ni kutoa elimu zaidi ya kujikinga na kuzuia moto kwa kutumia vifaa vya kuzimia moto ambavyo kila mtu anapaswa kuwa navyo kuanzia kwenye maeneo ya huduma hadi majumbani,” alisema Zelote.
Aidha alisema kuwa moja ya changamoto wanayoipata ni ujenzi holela ambao hauzingatii mipango miji hali ambayo inasababisha magari ya kuzimia moto kushindwa kufika kwenye nyumba ambazo zinawaka moto na kuwataka watu wazingatie kanuni za ujenzi.
Mwisho.  



No comments:

Post a Comment