Tuesday, February 16, 2016

NGO ZATAKIWA ZISIJIINGIZE KWENYE SIASA

Na John Gagarini, Kibaha
MASHIRIKA yasiyo ya Kiserikali wilayani Kibaha mkoani Pwani yametakiwa kutojiingiza kwenye masuala ya kisiasa badala yake wajikite katika kuwaletea wananchi maendeleo kama yalivyoandikishwa kwenye maeneo yao husika.
Akizungumza mjini Kiabaha kwwenye Jukwaa la Uwajibikaji kwa asasi isiyo ya kiserikali ya kitaifa ya ushirikiano wa Maendeleo kwa Vijana (YPC) mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba alisema kuwa mashirika kama hayo endapo yatajihusisha na siasa yatafutwa.
Kihemba alisema kuwa mashirika hayo yalianzishwa kwa lengo la kuwasaidia wananchi katika masuala ya kimaendeleo na si kujihusisha na siasa kama baadhi yanavyofanya kwa kujiingiza kwenye siasa.
“Msijiingize kwenye siasa bali mnapaswa mshirikiane na serikali katika kukabiliana na changamoto lakini endapo mtaingia kwenye siasa mnaweza kuathiri utendaji kazi wenu na tutayafuta yale ambayo yanajiingiza kwenye siasa kwani vyama vya siasa ndiyo vinapaswa kushiriki siyo nyie kwani kazi yenu ni maendeleo,” alisema Kihemba.
Alisema kuwa shirika hilo limefanya kazi kubwa kuwahamasisha vijana kushiriki kwenye kuwania nafasi za uongozi pamoja na kuwajengea uwezo wa uwajibikaji ni vema wakaendelea na shughuli za kimaendeleo kwa kuwaonyesha wananchi fursa za maendeleo kwani wao ni wabia.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi mwenyekiti wa bodi ya YPC Mkuku Mlongecha alisema kuwa asasi yao haijihusishi na masuala ya kisiasa bali ni kuwajengea uwezo vijana kushiriki kwenye shughuli za maendeleo pamoja na uongozi.
Mlongecha alisema kuwa malengo mengine ni kuwajengea uwezo wa kisiasa, kijamii, uchumi, kujitolea pamoja na mafunzo kwa vijana ambapo asilimia zaidi ya 70 ya madiwani na wenyeviti wa serikali za mitaa na vijiji ni vijana.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment