Saturday, February 13, 2016

RC AWAPA MWEZI MAWAKALA MWEZI MMOJA KUWASILISHA MAPATO WANAYODAIWA NA HALMASHAURI

Na John Gagarini, Kibaha
MAWAKALA wote wanaokusanya mapato ya Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani wametakiwa walipe makusanyo yao yote wanayodaiwa na Halmashauri ndani ya mwezi mmoja.
Agizo hilo lilitolewa jana na mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo wakati akifungua baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo nakusema kuwa ucheleweshaji wa fedha hizo unasababisha Halmashauri kushindwa kufanya mipango yake ya maendeleo.
Alisema kuwa baadhi ya mawakala wamekuwa wakichelewesha makusanyo na tozo mbalimbali wanazozitoza toka kwa wananchi kwa niaba ya Halamashauri hivyo wanapaswa kupeleka malipo hayo kwa wakati.
“Moja ya hoja ambazo zimekuwa zikiwasilishwa na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) ni kushindwa kukusanya mapato ya ndani ya mawakala kwa wakati na kukosa mikakati ya kuongeza mapato ya Halmashauri,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa suala lingine ni mikataba inayoingiwa inakuwa si mizuri na inatoa mwanya kwa wakala kuacha kuwasilisha mapato bila ya kuchukuliwa sheria kutokana na kuchelesha mapato hayo.
“Pia nashauri madiwani wajiepushe na kuomba zabuni mbalimbali katika Halamashauri ili kuepuka migongano ya kimaslahi na muweze kuisimamia vizuri kwani endapo mtakuwa na maslahi hamtaweza kuisimamia hivyo kushindwa kuleta maendeleo,” alisema Ndikilo.
Aliwataka Madiwani kusimamia fedha za makusanyo ya ndani zianarudi kwa wananchi kwa kugaramia huduma mbalimbali na miradi ya maendeleo kwa ustawi wa wananchi.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Halmashauri Leonard Mlowe alisema kuwa watendaji wa halmashauri wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa kuwa waadilifu ili kufanikisha maendeleo kwa wananchi yanapatikana.
Mlowe amewataka watendaji hao kuwasimamia mawakala ili wahakikishe wanawasilisha fedha za makusanyo mbalimbali zinafika kwa wakati ili kuwaletea maendeleo wananchi.

Mwisho.    

No comments:

Post a Comment