Thursday, February 25, 2016

ZIMAMOTO PWANI WAZUIA UUZAJI PETROLI MAJUMBANI

Na John Gagarini, Kibaha
KIKOSI cha zimamoto na uokoaji mkoni pwani kimewata wananchikuacha kuuza mafuta aina ya Petroli majumbani mwao ili kuepukana na milipuko ya moto inayotokana na mafuta hayo ambayo ni hatari.
Hayo yalisema mjini Kibaha na kamanda wa kikosi hicho Goodluck Zelote alipoongea na mwandishi wa habari hizi na kusema kuwa uuzaji huo wa kiholela ni hatari kwani umesababisha madhara makubwa ya uharibifu wa mali na watu kupoteza maisha.
Zelote alisema kuwa uuzaji huu si salama kwani kuhifadhi mafuta ya petrol ndani ni hatari kutokana na mafuta hayo kuwa ni rahisi kuwaka hivyo kuyauza kwenye nyumba za kuishi ni hatari sana kwa maisha ya watu.
“Utaratibu wa kuuza mafuta unafahamika lakini kwa sasa kumeibuka watu kuweka mafuta kwenye madumu pamoja na kwenye chupa za maji kisha kuyauza kwa madereva pikipiki na mafuta haya huhifadhiwa ndani jambo ambalo ni la hatari sana kwani watu wamepoteza maisha,” alisema Zelote.
Alisema kuwa mafuta hayo yanatakiwa yawekwe kwenye matenki na kuchimbiwa chini ndiyo utaratibu unaotakiwa lakini baadhi wanakiuka taratibu hizo kwa kuyahifadhi kwenye madumu ya maji.
“Tayari tumeshatoa elimu kuhusiana na kuepuka vitu ambavyo vinachangia moto kuwa majumbani ikiwa ni pamoja na kuepukana na utaratibu huo pamoja na kutohifhadhi pikipiki ndani ya nyumba kwani ni hatari bali wamiliki wangeangalia namna ya kuzihifadhi pikipiki zao,” alisema Zelote.
Aidha alisema kuwa bado wanendelea na utaratibu wa kutoa elimu kwenye maeneo mbalimbali ambayo yana mikusanyiko ya watu kama vile mashuleni, vituo vya mabasi, mikutano na kwenye masoko kwa lengo la kuwapatia elimu juu ya kujikinga na majanga.
“Vifaa vya kuzimia moto vinapaswa kuwa kwenye sehemu mbalimbali za huduma pamoja na majumbani ambapo sheria iko wazi na kuna adhabu kutegemeana na kosa na ukubwa wa huduma na kuna faini ambayo inaanzia 100,000 au kifungo cha miezi sita,” alisema Zelote.
Mwisho.

WAJERUMANI WAFAGILIA ELIMU BURE TANZANIA

Na John Gagarini, Kibaha
BAADHI ya Raia wa nchi ya Ujerumani waliokuja nchini kwa ajili ya kufanya shughuli za kujitolea kwa jamii wilayani Kibaha mkoani Pwani wameipongeza serikali ya awamu ya tano kwa kuanzisha utaratibu wa elimu bure kwa wanafunzi kuanzia elimu ya msingi hadi sekondari.
Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha wakati wa zoezi la kusafisha eneo la kujenga shule ya sekondari ya mtaa wa Mbwate raia hao walisema kuwa utaratibu huo unatoa fursa kwa watoto wengi waliofikia umri wa kwenda shule kupata nafasi hiyo.
Laura Pommerenke alisema kuwa utoaji wa elimu kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari utalifanya Taifa la Tanzania kuwa na watoto wengi watakaokuwa wemekwenda shule tofauti na ilivyokuwa zamani.
“Utaratibu wa elimu bure ni mzuri kwani hata kule kwetu ambako watu wanauwezo wanafunzi wanapata elimu bure hali ambayo inawafanya watoto kupata elimu inayostahili kwa wakati na kuondokana na watu kutokuwa na elimu,” alisema Pommerenke.
Alisema kuwa msingi wa elimu ya awali ukiwekwa utasaidia nchi kukabiliana na tatizo la watoto wa Tanzania kukosa elimu hali ambayo itazidi kuongeza umaskini lakini wakipata elimu watakuwa na uwezo wa kujitegemea.
Naye Marie Vogel alisema kuwa alisikia kuwa elimu ya Msingi na Sekondari ili kuwa na gharama jambo ambalo liliwafanya watoto wengi washindwe kwenda shule hivyo kuwafanya watoto wengi kuwa mitaani au kuanza maisha kabla ya wakati wao.
Vogel alisema kuwa serikali ya Tanzania inapongezwa kutokana na kuchukua maamuzi hayo ya kutoa elimu bure kwa wanafunzi wa elimu ya msingi na sekondari kwani mpango huo utakuwa na manufaa makubwa kwa nchi.
Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa huo Abdala Mtandio alisema kuwa mpango wao wa kujenga shule ya sekondari kwenye mtaa wao umezingatia tatizo la watoto wengi kusoma mbali na kujikuta wakitumia mwingi njiani.
Mtandio alisema kuwa malengo yao ni kujenga madarasa manne ya kuanzia ili wanafunzi waanze kusoma hapo na wanahitaji kiasi cha shilingi milioni 50 za kuanzia pia wamewaomba wadau mbalimbali kujitokeza kuwasaidia.
Mwisho.

WAZIRI SIMBACHAWENE AIKATALIA KEC COTC KUWA CHUO KIKUU

Na John Gagarini, Kibaha
WAZIRI wa Ofisi ya Rais Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Simbachawene amelitaka Shirika la Elimu Kibaha (KEC) kutokibadili Chuo cha Waganga Wasaidizi (COTC) kuwa Chuo Kikuu ili lisiharibu malengo ya chuo kusomesha watu wenye elimu ya kawaida.
Simbachawene aliyasema hayo alipotembelea Shirika hilo hivi karibuni na kusema kuwa ndiyo sababu chuo hicho hakikuingizwa kwenye Taasisi ya elimu ya juu kwani malengo yake ni kusomesha watu ambao ni wa ngazi ya kati.
Alisema kuwa kwa sasa kumekuwa na hali ya kila chuo kutaka kuwa chuo kikuu hali ambayo itasababisha kusiwe na wataalamu wa ngazi ya kati ambao wameonekana kuwa ndiyo wawajibikaji wakubwa.
“Kama kila chuo au taasisi itakuwa na malengo ya kuwa chuo kikuu kuna hatari ya kuwapoteza wasomi wa ngazi ya kati kwani endapo kila mtu atakuwa amesoma chuo kikuu hakutakuwa na watu wa kufanyakazi kwani kila mtu atatakuwa mtawala,” alisema Simbachawene.
Alisema kuwa chuo hicho kilianzishwa kwa malengo ya kuwapatia elimu watu wa vijijini lakini kikishafanywa chuo kikuu wananchi wenye elimu ya kati hawatapata nafasi ya kusoma hivyo malengo ya kuisaidia jamii hayataweza kufikiwa.
“Tunashindwa kupata wagunduzi kwani wanakuwa ni watu wenye elimu ya kawaida sana kama ilivyo kwa nchi zilizoendelea hawa ni watu waliosoma elimu ya kawaida na wengine wanatoka vijijini hivyo na hapa ni sehemu ya kuanzia lakini tukikibadilisha na kuwa chuo kikuu ni sawa na kuvunja daraja ambalo watu wamekuwa wakitumia kuvukia kwenda mbele,” alisema Simbachawene.
Aidha alisema kuwa kuna tatizo la wataalamu wa kati kutokana na watu wengi kuiacha elimu ya kati na kutaka kupata elimu ya juu hivyo kumekuw ana pengo hapo katikakati pia wazingatie malengo ya kuanzishwa chuo hicho ambacho zamani kilijukana kama chuo cha maendeleo ya waganga vijijini.
Mwisho.

ACHOMWA MOTO KWA WIZI WA MCHELE DUKANI

Na John Gagarini, Kibaha
MTU mmoja aliyetambuliwa kwa jina moja la Ngozi mkazi wa Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani ameuwawa kwa kuchomwa moto na wananchi wenye hasira kali kwa madai ya kuiba mchele na mafuta ya kupikia dukani.
Tukio hilo lilitokea Fabruari 25 majira ya saa 9 alfajiri katika mtaa wa Tangini baada ya marehemu akiwa na mwenzake ambaye alikimbia kuvunja na kutoa mchele huo kilogramu 100 na mafuta ya lita tatu galoni mbili.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa huo Leons Karoli alisema kuwa watu hao waligunduliwa na baadhi ya madereva wa Bodaboda waliokuwa wakipita kwenye eneo la tukio na kuwakuta watuhumiwa hao wakiwa na vitu hivyo wakiwa wamevipakia kwenye pikipiki ya marehemu aina ya Boxer.
“Mashuhuda walisema kuwa marehemu alikuwa ndani ya hilo duka na kujifanya kama ndiye mwenye duka akijifanya ndiyo analifungua lakini watu walikuwa na wasiwasi kwani ilikuwa ni asubuhi sana jambo ambalo si la kawaida kwa mmiliki huyo kulifungua muda huo huku ambaye mmiliki wake ni Mmbando,” alisema Karoli.
Karoli alisema kuwa baada ya watu kuwa na wasiwasi waliwasiliana na watu kujaa kisha kuanza kumpiga marehemu hadi alipopoteza fahamu na mwenzake alifanikiwa kutoroka kwa kukimbia na kumwacha mwenzake ambaye alibainika kuwa ni muuza matunda pia ni dereva bodaboda.
“Tulifanya mawasiliano na polisi na kuwajulisha kuwa kuna mwizi kakamatwa lakini kabla hawajafika watu hao wenye hasira walimpiga kisha kumchoma moto kwa kutumia mafuta ya petroli na kusababisha kifo chake,” alisema Karoli.
Alisema kuwa marehemu alikuwa na begi ambalo lilikuwa na vifaa mbalimbali ikiwa ni pamoja na mkasi mkubwa unaotumika kukatia makufuli, nondo, vocha za simu pamoja na fedha taslimu kiasi cha shilingi 150,000.
Jeshi la polisi mkoani Pwani lilithibitisha kutokea tukio hilo na kuwataka wananchi kutojichukulia sheria mkononi kwa kutoa taarifa polisi kwa hatua zaidi za kisheria na si kuwauwa watuhumiwa wa matukio ya kihalifu.
Mwisho.
  



MSHINDI UVAAJI SARE ZA CCM ALONGA

Na John Gagarini, Kibaha
MSHINDI wa Uvaaji wa sare za Chama Cha Mapinduzi (CCM)Kibaha Mjini mkoani Pwani Said Ngombe amempongeza mwenyekiti wa chama hicho Dk Jakaya Kikwete kwa kutaka kuenziwa watu wanaokifanya chama kishinde kwenye chaguzi mbalimbali.
Mshindi huyo akizungumza na wandishi wa habari mjini Kibaha baada ya kupewa tuzo na Dk Kikwete wakati wa sherehe za kuzindua jengo la CCM Kibaha Mjini lililojengwa na Mbunge wa Jimbo hilo Silvestry Koka  alisema kuwa kuthamini mchango wa wanachama au makada wake ni moja ya njia za kuwapa motisha ili waendelee kukitetea chama chao.
Ngombe alisema kuwa anamshukuru mwenyekiti kuliona hilo na kutaka viongozi wa maeneo mengine kuiga utaratibu huo wa kuthamini mchango wa wanaccm waliosababisha chama kushinda au kukipigania.
“Tunamshukuru mwenyekiti kwa kutupa tuzo na kuwataka viongozi wa maneo mbalimbali kuwaenzi wanaccm waliojitolea kukipigania chama bila ya kuchoka na mimi nimekuwa nikivaa sare ya chama kila siku ambapo kwa sasa nina miaka tisa mfululizo bila ya kuacha,” alisema Ngombe.
Alisema kuwa anajisikia fahari kupewa tuzo hiyo ya uvaaji wa sare kwani imempa moyo wa kuendelea kukipigania chama licha ya kukumbwa na changamoto nyingi kutoka kwa wapinzani wao vyama vingine.
“Kuvaa kwangu sare za chama kwenye eneo lango la kufanyia kazi imekuwa chachu ya chama chake kufanya vizuri kwani watu wamekuwa wakinifahamu kwa uvaaji wangu huu na nimekuwa nikiwakabili wapinzani wetu kwa hoja kwani wakishaniona wamekuwa wakinitania na mimi ndo ninapopata muda wa kuwapa sera za chama huku wengine wakijiunga na chama kupitia kwangu kwani naonyesha msimamo wangu wa chama,” alisema Ngombe.
Aidha alisema kuwa anashangazwa na baadhi ya wanaccm kuogopa kuvaa sare za chama kwani hata kwenye vikao wengine wamekuwa hawavai licha ya kutakiwa kuvaa wanapokuwa kwenye mikutano na vikao vya chama.
Alishauri tuzo hizo ziambatane na fedha kidogo kwa ajili ya kuongeza motisha kwa wanaofanya vizuri kwneye nyanja mbalimbali za kukipigania chama bila ya kuwa na woga wa aina yoyote tofauti na ilivyo wanachama au wapenzi wa chama.
Mwisho.   

BIBI AINGIA MATATANI KIFO CHA MWANAE

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
BIBI Nuru Mchenga mwenye umri wa zaidi ya miaka (80) mkazi wa Maili Moja B wilayani Kibaha mkoani Pwani amejikuta kwenye wakati mgumu baada ya wananchi kumlalamikia kukaa na maiti ya mwanae kwa masaa kadhaa bila ya kuwataarifu watu.
Mbali ya kumshangaa kukaa na maiti muda mrefu pia walimshangaa bibi huyo kumsafisha mwanae kwa taratibu za dini ya Kiislamu jambo ambalo ni kinyume kwani huwa linafanywa na wanaume.
Tukio hilo lilitokea Fabruari 24 majira ya mchana ambapo Mwanae Kassimu alifariki majira ya saa nane hapo nyumbani kwake baada ya kudaiwa kuwa alikuwa anaumwa.
Wakizungumza na waandishi wa habari majirani wa Bibi huyo ambao hawakutaka kutajwa majina yao magazetini walisema kuwa wameshangazwa na kitendo hicho cha kukaa na maiti kwa muda wote huo bila kuomboleza kama ilivyo kwa watu wanaofiwa ambao hulio kuashiria kuwa kuna msiba.
Walisema kuwa kilichowashangaza ni jinsi gani bibi huyo alipomfanyia usafi mwanae wa kiume jambo ambalo ni kinyume na taratibu za dini ya Kiislamu hali ambayo ndiyo imezua maswali mengi.
Alisema marehemu alipaswa kufanyiwa taratibu za kidini na mwanaume na si mwanamke kama alivyofanya bibi huyo ambaye watu wengi wamemshangaa kwa ujasiri huo.
“Inasikitisha sana kuona bibi huyu anafanya vitu kama hivyo ndiyo maana kumekuwa na maneno mengi kutokana na kifo cha mwanae kutokana na alivyofanya na pia haonyeshi kusikitika kifo cha mwanae tofauti na misiba mingine,”  walisema majirani hao.
Kwa upande wake Bibi huyo akizungumza na waandishi wa habari nyumbani kwake alisema kuwa mwanae alilogwa kwa kutupiwa jini na watu ambao hawaipendi familia yake na kusababisha kifo hicho.
Mchenga alisema kuwa siku ya tukio hilo mwanae alikuwa tu nyumbani nay eye alikuwa akiendelea na shughuli zake na kushangaa kuona mwanae hana uchangamfu.
“Ilipofika mchana mwanangu alifariki na kabla hajafariki tulikubaliana nikifa mimi yeye ataniosha na akifa yeye mimi nitamwosha ndiyo sababu ya mimi kufanya hivyo,” alisema Mchenga.
Alisema kuwa anashangaa kuona watu wanataka kumfanyia fujo nyumbani kwake na kusema kuwa watu wanasema maneno mengi juu ya kifo cha mwanae huyo.
Kutokana na watu kujazana nyumbani kwa bibi huyo ilibidi jeshi la polisi kuuchukua mwili wa marehemu majira ya saa 3 usiku na baadaye walirudi tena majira ya saa tano kasoro na kumchukua bibi huyo kutokana na kuhofia usalama wake kwani watu walikuwa wakimzonga na kumzomea, Jeshi la polisi limethibitisha kutokea tukio hilo.
Mwisho.
  



Sunday, February 21, 2016

WAZIRI SIMBACHAWENE ALIPA NENO SHIRIKA LA ELIMU KIBAHA

Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI imesema kuwa itaangalia upaya uendeshaji wa Shirika la Elimu Kibaha (KEC) ili lizalishe liweze kujiendesha kwa ufanisi badala ya kuitegemea serikali ili kuboresha maslahi ya wafanyakazi wake na kutoa huduma bora kwa wananchi.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Simbachawene alipotembelea Shirika hilo kujionea utendaji kazi wake na na kuongea na wafanyakazi kujua changamoto zinazowakabili na kusema kuwa linapaswa kujiendesha kwa faida na si kuwa tegemezi.
Simbachawene alisema kuwa Shirika hilo la Umma lilianzishwa kwa lengo la kusaidia wananchi hasa wale wa vijijini kwa wakati ule lakini linapasw akubadilika kutokana na wakati na kuacha mifumo ya uendeshaji wa kizamani ambayo haiendani na hali halisi ya wakati uliopo hivyo kushindwa kunufaisha watumishi na wananchi.
“Haiwezekani Shirika kama hili lenye rasilimali na vyanzo vingi vya mapato ikiwa ni pamoja na ardhi kubwa linakuwa na watumishi ambao ni maskini huku wakikosa stahiki zao za kimsingi na kufanya liyumbe ni jambo la kusikitisha sana hivyo serikali itakaa na kuangalia njia za kuweza klirudisha kwenye uhalisia wake,” alisema Simbachawene.
Alisema kuwa Shirika linayumba kw asababu hakuna mipango mikakati ya kujiendesha kisasa kwani maono yake yanaonekana bado ni ya kizamani kwa kuendelea kudeka kwa serikali licha ya kuwa na fursa nyingi zianazolizunguka.
“Mbali ya mfumo wa uendeshaji kuwa na matataizo mengi pia wafanyakazi wamelalamika sana juu ya maslahi yao ikiwa ni pamoja na malipo ya kazi z aziada, kupandishwa madaraja na maslahi mengine nitakuja na majibu ya maswali yenu pia tume itaundwa kila sekta ili kubaini matatizo yaliyopo na kuyafanyia kazi,” alisema Simbachawene.
Kwa upanade wake mwenyekiti wa bodi ya Shirika Patrick Makungu alisema kuwa watazifanyia kazi changamoto mbalimbali ambazo zinawakabili wafanyakazi ambazo zinawafanya watumishi washindwe kutoa huduma bora.
Naye mkurugenzi wa Shirika la Elimu Kibaha Dk Cyprian Mpemba alisema kuwa wanakabiliwa na changamoto nyingi ambazo zinawafanya washindwe kutoa huduma bora ikiwa ni pamoja na kuwa na mahitaji ya fedha kiasi cha shilingi bilioni 6.5 kwa ajili ya uendesheaji.
Dk Mpemba alisema kuwa mbali ya changamoto hizo wamepata mafaniko kupitia mfumo wa kieletroniki wa ukusanyaji wa mapato ya Hospitali ya Rufaa ya mkoa ya Tumbi ambayo iko chini ya Shirika hilo kufanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi milioni 3,000,000 toka 300,000 kwa siku.
Waziri alitembelea Hospitali hiyo, aliangalia mfumo wa ukusanyaji mapato wa kieletroniki uliobuniwa na shirika hilo, kampuni ya ufugaji kuku ya Organia, Shirika hilo lilianzishwa miaka zaidi ya 40 iliyopita na nchi za NORDIC likiwa na lengo la kupambana na adui watatu ambao ni ujinga, umaskini na maradhi na lina wafanyakazi zaidi ya 900 na lina miliki Hospitali ya Tumbi, Chuo cha Waganga wasaidizi, Chuo cha Ufundi Stadi VETA, Shule z a sekondari Kibaha wavulana na Wasichana, Tumbi, shule ya msingi Tumbi na awali     

 MWISHO

MBUNGE AKABIDHI VITABU VYA SAYANSI

MBUNGE wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete kushoto akimkabidhi kitabu ofisa elimu wa mji wa Halmashauri ya Chalinze Zainab Makwinya kulia na katikati ni mwanfunzi wa shule ya sekondari ya Mdaula Budi Tanganyika  

Na John Gagarini, Chalinze

KATIKA kuhamasisha wanafunzi kupenda masomo ya Sayansi shirika lisilo la Kiserikali la Kulea Childcare Villages la Chalinze  kwa kushirikiana na Mbunge wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete wamekabidhi vitabu 3,438 vyenye thamani ya shilingi milioni 70.
Vitabu hivyo vya Sayansi ni kwa ajili ya wanafunzi wote wa shule za Sekondari na vichache kwa wanafunzi wa Msingi kwa wanafunzi wa Jimbo la Chalinze ili kuwahamsisha kujifunza mambo mbali mbalimbali ya Sayansi.
Akikabidhi vitabu hivyo kwa mwalimu mkuu wa shuke ya Sekondari ya Mdaula Melkisedek Komba, Mbunge wa Jimbo hilo alisema kuwa lengo la kutolewa vitabu hivyo ni kuhamasisha wanafunzi kusoma masomo hayo ili kupata wataalamu wengi wa Sayansi .
Ridhiwani alisema kuwa masomo ya Sayansi ndiyo yanaotoa wataalamu mbalimbali hivyo wadau wa elimu wanapaswa kutoa hamasa ya kwa wanafunzi kujifunza Sayansi ili waongeze idadi ya wanaosoma kwa lengo la kuwa na wanasayansi wengi.
“Sisi tukiwa ni wadau wa maendeleo tutaendelea kusaidiana na wadau wengine ili kuhakikisha kuwa tunawahamsisha wanafunzi kuyapenda masomo haya ambayo baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakiyaogopa kwa madai kuwa ni magumu hivyo ni vema tukawawekea mazingira ya kuona kuwa ni sawa na masomo mengine,” alisema Ridhiwani.
Alisema kuwa serikali imekuwa ikishirikiana na wadau mbalimbali kama ilivyo kwa shirika la Kulea Childcare ambalo limepata vitabu hivyo toka kwa marafiki zao wa nchini Marekani kwa ajili ya kusaidia sekta ya elimu.
Kwa upande wake mwasisi wa shirika hilo la Kulea Romie Mtenda alisema kuwa shirika lake limekuwa likisaidia sekta ya elimu ambapo hiyo ni mara ya pili kutoa msaada wa vitabu katika Jimbo hilo pia wamekuwa wakitoa misaada ya kielimu.
Mtenda alisema kuwa shirika lao limekuwa likitoa misaada kwa watoto yatima, wajane na watu wasishio kwenye mazingira magumu ikiwa ni pamoja na kuwasaidiaada, malazi, makazi na huduma nyingine za kijamii.   
Naye mwalimu mkuu wa Mdaula Komba alisema kuwa vitabu hivyo vitasaidia wanafunzi kwa ajili ya kujifunza Sayansi ambayo imekuwa ndiyo somo kuu kwa ajili ya wataalamu ambao wanabuni vitu mbalimbali ambavyo hutumiwa na watu.
Komba alisema kuwa msaada huo umekuja wakati mwafaka kwani wanafunzi wamekuwa na mahitaji ya vitabu vya Sayansi kwa ajili ya kujisomea hivyo vitawasaidia sana kupenda masomo hayo ambayo ni Bioloji, Sayansi na Hesabu. Vitabu hivyo vimetolewa kwa mgawanyo wa tarafa tano ambazo ni Chalinze vitabu 998, Msoga 910, Miono 610, mSata 610 na Kwaruhombo 610.

Mwisho.

Tuesday, February 16, 2016

KATA KUKUTANA NA WAKULIMA NA WAFUGAJI

Na John Gagarini, Pwani
KATA ya Kiwangwa wilayani Bagamoyo mkoani Pwani imeweka mpango wa kukutana na wakulima na wafugaji ili kukabiliana na changamoto za jamii hizo ambazo zimekuwa zikigombana kutokana na wafugaji kudaiwa kulisha mazao mifugo kwenye mashamba ya wakulima.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu diwani wa kata hiyo Hussein Malota alisema kuwa lengo la kukutana na pande hizo ni kujadili jinsi gani ya kukabili changamoto hizo ambazo zimekuwa zikisababisha mapigano.
Malota alisema kuwa wiki tatu zilizopita kulitokea ugomvi baina ya pande hizo mbali baada ya wafugaji kudaiwa kuachia ngombe na kula mazao ya wakulima hali ambayo ili sababisha vurugu za hapa na pale.
“Tayari tumeunda kamati za maridhiano za wakulima watano na wafugaji watano ili kutunga sheria ndogondogo ambazo endapo mmoja atakiuka ataadhibiwa kulingana na makubaliano ya kamati hiyo ili kudhibiti wale watakaokiuka makubaliano hayo,” alisema Malota.
Alisema kuwa tatizo kubwa ni baadhi ya wafugaji wapya wanaoingia kwenye vijiji mbalimbali kwani hawajui taratibu mara waingiapo kwenye maeneo ya wenyeji hali ambayo inasababisha migogoro baina ya pande hizo.
“Tumeunda kamati hizi ili zitunge sheria ambazo zitawaabana wale watakaokiuka kwani wajumbe wa hizo kamati watawajulisha wenzao makubaliano yaliyoafikiwa lengo likiwa ni kupunguza migogoro ya wakulima na wafugaji waishi kwa amani kama jamii moja,” alisema Malota.
Aidha alisema kuwa changamoto nyingine walioiona ni baadhi ya wafugaji kuwaachia watoto wachunge mifugo hiyo ambayo ni makundi makubwa na kushindwa kuyamudu wakati wakichunga na kusababisha matatizo.
Mwisho.

          

MADEREVA BODABODA KUWA NA UTAMBULISHO

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA Cha Madereva na Wamiliki wa Pikipiki wilayani Kibaha mkoani Pwani (CHAWAMAPIKI) kimeandaa utaratibu wa kuwa na makoti maalumu ambayo yanayongaa ambayo yatakuwa na namba mgongoni ili kukabiliana na madereva wanaokiuka taratibu za uendeshaji pikipiki.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwenyekiti wa chama hicho Hussein Kijazi alisema kuwa kumekuwa na lawama nyingi kwa madereva wa Bodaboda kukiuka taratibu za uendeshaji hali ambayo inaweza kuchangia kuongezeka kwa ajali.
Kijazi alisema kuwa ili kuwadhibiti madereva wanaokiuka taratibu wameona bora waanzishe utaratibu huo ili iwe rahisi kuwabaini wale wanokwenda kinyume cha sheria na kuwachukulia hatua za kisheria.
“Utaratibu huu tunatarajia utaanza wakati wowote kuanzia sasa kwani kumekuwa na malalamiko mengi toka kwa watu mbalimbali wakilalamika kuwa madereva hao wanavunja sheria na kuwa moja ya chanzo cha ajali,” alisema Kijazi.
Alisema kuwa mtu akiona kuna tataizo kwa dereva fulani anataja tu namba na wao watafuatilia ni dereva gani mwenye hiyo namba kisha chama kitamwita na kumpa adhabu inayostahili kutokana na kosa lake.
“Makoti hayo yanayongaa hata nyakati za usiku yatatusaidia kuwabaini madereva wanaokiuka utartibu wetu ambao tumejiwekea kwani baadhi ya watu wanalalamika kuwa madereva wengine wanajihusisha na vitendo vya uhalifu lakini wakiwa na makoti hayo itakuwa ni vigumu kuvunja taratibu kwani lazima watajulikana na wataadhibiwa,” alisema Kijazi.
Aidha wameipongeza serikali kwa kufuta baadhi ya kodi zikiwemo zile za TRA 90,000, Motor Vehicle 50,000 na kodi ambazo zilikuwa ni kero kwao. Chama hicho kinawanachama 400 na wamiliki zaidi ya 100 na wana vituo 13 na kina lengo la kusaidia wakati wa matatizo ikiwa ni pamoja na kufiwa.
Mwisho.

WAUZA MAJI WANAWAKE KWENYE MAGARI WAILILIA HALMASHAURI KUVUNJA VIBANDA VYAO

Na John Gagarini, Kibaha
WAFANYABIASHARA wanawake  wanaouza Maji ya kunywa kwenye magari  ilipokuwa mizani ya zamani ya Maili Moja wilayani Kibaha wameilalamikia Halmashauri ya Mji wa Kibaha kwa kuwavunjia vibanda vyao kwa madai kuwa ni uchafu licha ya kuwa wanakusanya ushuru kwao.
Moja ya wafanyabiashara hao ambao ni Veronica Damiani akizungumza na waandishi wa habari alisema kuwa wanashangaa Halmashauri hiyo kuwavunjia vibanda vyao bila ya kuwaandikia barua ya kuwataka wasifanye biashara zao.
Damiani alisema kuwa wao wanajua serikali kabla ya kufanya kitu lazima itoe taarifa ya maandishi kabla ya kufanya jambo lolote lakini wao wanashangaa kuondolewa bila ya kupewa barua ya kuwahamisha katika eneo hilo.
“Sisi hatukatai kuondoka ila wangetupa taarifa juu ya kututaka tuondoke katika eneo hili na siku chache zilizopita walikuja wakatuambia kuwa tuendelee na biashara wakati majadiliano yanaendelea lakini tunashangaa jana wamekuja na migambo na kutubomolea vibanda vyetu huku wakitupa masaa matatu kwa ajili ya kuhama,” alisema Damiani.
Alisema kuwa sasa wao watenda wapi kufanya biashara kwani maji wanayouza wengine wamekopa mikopo kwenye taasisi za kifedha kwa lengo la kujipatia kipato chao na familia zao ambapo wengine ni wajane.
“Tunakopa fedha kwa ajili ya kufanyabiashara hizi sasa tutarejeshaje fedha tulizokopa tunaomba viongozi wa ngazi za juu watuangalie kwa jicho la huruma hatuna kipato kingine zaidi ya biashara hizi ambazo zinatusaidia kuwasomesha watoto wetu kuanzia shule za msingi, sekondari na vyuo,” alisema Damiani.
Kwa upande wake Mhandisi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Dismas Marango akijibu kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Gladys Dyamvunye alisema kuwa wafanyabiashara hao walikuwa wakifanyabiashara zao kimakosa kwani hawakuwa na kibali chakufanyia biashara kwenye eneo hilo.
Marango alisema kuwa hawakuwapa barua kwani sehemu hiyo si kwa ajili ya kufanyabiashara na kwamba mabanda hayo yanaonekana kama uchafu na waliwapa taarifa kwa maneno wiki tatu zilizopita za kuwataka waondoke kwenye eneo hilo.
Mwisho.

NGO ZATAKIWA ZISIJIINGIZE KWENYE SIASA

Na John Gagarini, Kibaha
MASHIRIKA yasiyo ya Kiserikali wilayani Kibaha mkoani Pwani yametakiwa kutojiingiza kwenye masuala ya kisiasa badala yake wajikite katika kuwaletea wananchi maendeleo kama yalivyoandikishwa kwenye maeneo yao husika.
Akizungumza mjini Kiabaha kwwenye Jukwaa la Uwajibikaji kwa asasi isiyo ya kiserikali ya kitaifa ya ushirikiano wa Maendeleo kwa Vijana (YPC) mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba alisema kuwa mashirika kama hayo endapo yatajihusisha na siasa yatafutwa.
Kihemba alisema kuwa mashirika hayo yalianzishwa kwa lengo la kuwasaidia wananchi katika masuala ya kimaendeleo na si kujihusisha na siasa kama baadhi yanavyofanya kwa kujiingiza kwenye siasa.
“Msijiingize kwenye siasa bali mnapaswa mshirikiane na serikali katika kukabiliana na changamoto lakini endapo mtaingia kwenye siasa mnaweza kuathiri utendaji kazi wenu na tutayafuta yale ambayo yanajiingiza kwenye siasa kwani vyama vya siasa ndiyo vinapaswa kushiriki siyo nyie kwani kazi yenu ni maendeleo,” alisema Kihemba.
Alisema kuwa shirika hilo limefanya kazi kubwa kuwahamasisha vijana kushiriki kwenye kuwania nafasi za uongozi pamoja na kuwajengea uwezo wa uwajibikaji ni vema wakaendelea na shughuli za kimaendeleo kwa kuwaonyesha wananchi fursa za maendeleo kwani wao ni wabia.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi mwenyekiti wa bodi ya YPC Mkuku Mlongecha alisema kuwa asasi yao haijihusishi na masuala ya kisiasa bali ni kuwajengea uwezo vijana kushiriki kwenye shughuli za maendeleo pamoja na uongozi.
Mlongecha alisema kuwa malengo mengine ni kuwajengea uwezo wa kisiasa, kijamii, uchumi, kujitolea pamoja na mafunzo kwa vijana ambapo asilimia zaidi ya 70 ya madiwani na wenyeviti wa serikali za mitaa na vijiji ni vijana.
Mwisho.

MASHAMBAPORI YARUDI SERIKALINI


Na John Gagarini, Kibaha
KATIKA kutekeleza agizo la Rais Dk John Magufuli la kuwanyanganya watu wasioendeleza mashamba kwenye wilaya ya Kibaha mkoani Pwani imerudisha mashamba 17 serikalini ambayo yatatumika kwa ajili ya ujenzi wa viwanda.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba wakati wa kuzindua Jukwaa la Uwajibikaji kwa Asasi ya Kitaifa ya Ushirikiano wa Maendeleo  ya Vijana (YPC) ya mkoa wa Pwani na kusema kuwa mashamba hayo pia yatatumika kwa ajili ya makazi.
Kihemba alisema kuwa mashamba hayo yalikuwa kero kwa wananchi kutokana na kutoendelezwa kwa muda mrefu na wamiliki licha ya kutakiwa kuyaendeleza kisheria lakini wameshindwa na kuyafanya mapori makubwa.
“Baadhi ya mashamba yamerudishwa serikalini kama tulivyoagizwa na tutahakikisha tunayapima kwa ajili ya viwanda ili kuweza kuimarisha uchumi wa wakazi wa wilaya ya Kibaha pia sehemu yatapimwa kwa ajili ya makazi,” alisema Kihemba.
Alisema kuwa maeneo hayo yaliyorejeshwa hayapaswi kuvamiwa kwani kuna taarifa baadhi ya watu wameanza kuyavamia mashamba hayo jambo ambalo ni kinyume cha sheria kwani yatatumiwa kwa mipango itakayokuwa imepangwa na si kwa watu kuyavamia.
“Ni marufuku watu kuyavamia maeneo hayo ambayo yalirejeshwa serikalini na kwa wale watakaojenga nyumba zao zitabomolewa wanachotakiwa ni kusubiri utaratibu utakaowekwa na serikali na si kujichukulia kinyume cha sheria,” alisema Kihemba.
Aidha alisema kuwa kwa kuwa serikali ya awamu ya tano imepania kuinua uchumi wa Watanzania kupitia viwanda ili wawe na uchumi wa kati ni vema na wao wakaunga mkono mpango huo kwa kuanzisha viwanda kwa kushirikiana na sekta binafsi.
Mwisho.

MADIWANI KUHAKIKI MAPATO YA STENDI

Na John Gagarini, Kibaha
MADIWANI wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha wanatarajiwa kusimamia utaratibu wa mapato kwenye stendi kuu ya mabasi ya Maili Moja ili kuhakiki ni magari mangapi ya abiria yanayolipa ushuru kwenye stendi hiyo.
Utaratibu huo ulipitishwa kwenye baraza la madiwani wa Halmashauri hiyo ukiwa na lengo la kuhakikisha kuwa fedha zinazopatikana kwenye chanzo hicho kikubwa cha mapato cha Halmashauri hiyo.
Akizungumza kwenye kikao hicho mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Leonard Mloe alisema kuwa madiwani hao watakaa kituoni hapo ili kupata ukweli wa magari mangapi yanayolipa ushuru yanapopita hapo stendi.
“Tumeamua kufanya hivyo kwani mapato yanayopatikana kwa sasa hayana usahihi kwani idadi ya magari yanayolipa ushuru ni machache huku magari yanayopita hapo ni kubwa hivyo kukaa hapo kutatusaidia kujua ukweli wa mapato halisi ya stendi,” alisema Mlowe.
Mlowe alisema kuwa wanataka wakadirie mapto kwa uhakika na si kubahatisha kwani kwa sasa hawaridhiki na mapato yanayopatikana kwa sasa hivyo wameamua madiwani wake hapo ili kupata majibu sahihi.
“Hichi ni moja ya chanzo chetu cha mapato cha uhakika hivyo lazima tujue tunapata nini na kujua ni magari ya abiria ni mangapi yanayolipa ushuru wa stendi kwani iatatusadia kuwa na uhakika wa mapato ya chanzo hicho,” alisema Mloe.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Tumbi Hemed Chanyika alisema kuwa mapato ya stendi hayafahamiki undani wake kwani inaonekana baadhi ya watu wanatumia risiti feki za ushuru wa stendi kujinufaisha.
Chanyika alisema kuwa kwa madiwani hao kukaa hapo itasaidia sana kwani idadi ya magari ya abiria yanayoingia na kutoka kwenye stendi hiyo ambapo mabasi madogo yanalipia kiasi cha shilingi 500 na makubwa 1,000 kila yanapoingia na kutoka.
Mwisho.

Sunday, February 14, 2016

MAMA AMFANYIA UKATILI MWANAE WA KAMBO AMVUTA SEHEMU ZA SIRI


Na John Gagarini, Kibaha
SHEILA Husein mkazi wa Janga Kata ya Janga Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani amejikuta matatani baada ya kumpiga mtoto wake wa kambo wa kiume mwenye umri wa miaka (2) na kumjeruhi sehemu mbalimbali za mwili ikiwa ni pamoja na kumvuta sehemu zake za siri.
Akizungumza na waandishi wa habari mwenyekiti wa Mtaa wa Janga na Diwani wa kata hiyo Chande Mwalika alisema kuwa mtoto huyo amekuwa akipigwa kila siku kwa fimbo hali ambayo imemfanya awe na makovu mengi mwilini.
Mwalika alisema kuwa moja ya majirani ambaye alishindwa kuvumilia vitendo hivyo Adinani Mkupa nakutoa taarifa hiyo alisema kuwa vitendo vilivyokuwa vikifanywa na mtuhumiwa huyo ni vya kikatili na haviwezi kuvumilika.
“Amekuwa akimchapa mwanae kwa fimbo bila ya kumuonea huruma hali ambayo imemfanya mtoto huyo aharibike mwili mzima kutokana na vipigo hivyo na kibaya zaidi ni pale alipofikia hatua ya kumvuta sehemu zake za siri na hakuna sababu maalumu inayomfanya amwazibu mtoto huyo kwani bado ni mdogo sana na hana uwezo wa kuongea,” alisema Mwalika.
Alisema kuwa kutokana na hali hiyo ilibidi watoe ripoti kwa kwenye uongozi wa kata kwa ajili ya hatua zaidi kwa mtuhumiwa ambaye ni mama wa nyumbani huku mumewe aliyetajwa kwa jina moja la Abdul akiwa ni mfanyabiashara kwenye magulio.
Kwa upande wake ofisa mtendaji wa kata ya Janga Michael Mwakamo alisema kuwa baada ya kupata taarifa hiyo ilibidi mgambo wapelekwe nyumbani kwa mtuhumiwa kwa ajili ya kumchukua kwa ajili ya kutoa maelezo ni kwanini anamtesa mtoto huyo.
Mwakamo alisema kuwa mtuhumiwa huyo alichukuliwa na kwenda ofisini hapo na baada ya mahojiano ilibidi apelekwe polisi kwa hatua zaidi na baada ya mahojiano kukamilika alipelekwa Mahakama ya Mwanzo ya Mlandizi.
“Tulimuuliza ni kwani ni anamfanyia vitendo vya ukatili mtoto wake huyo wa kambo alijibu kuwa hata mumewe humpiga mtoto huyo hivyo nay eye akaona afanye hivyo lakini hakuna sababu nyingine ya yeye kumchapa kupita kiwango mtoto huyo;” alisema Mwakamo.
Hakimu wa mahakama ya Mwanzo ya Mlandizi Sharifa Mtumuya alimsomea mashitaka ya shambulio ambapo mtuhumiwa alikana shitaka hilo na kupelekwa mahabusu baada ya taratibu za dhamana kushindikana na kesi hiyo itasikilizwa tena Februari 16 mwaka huu.
Mahakama iliamuru mtoto huyo akae kwa ofisa kilimo wa kata ya Janga Neema Sonje hadi itakapoamuliwa vingine wakati kesi hiyo ikiwa inaendelea kwani haitawezekana kuendelea kukaa kwenye nyumba aliyokuwa akiishi.
Mwisho.      
Na Mwandishi Wetu, Kibaha

MKUU wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amewaonya baadhi ya  madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha kuacha mara moja tabia ya kumtishia kumfukuza kazi  Mkurugenzi  Mtendaji wa Mji huo pamoja na Mweka Hazina wake kwa madai kwamba amekataa kulipa deni la shilingi milioni 231 la mkandarasi mmoja  anayayetoa huduma mbalimbali ndani ya Halmashauri hiyo.

Akizungumza katika kikao cha baraza la madiwani wa mji huo mkuu huyo wa mkoa aalisema kuwa anasikitishwa na kitendo cha baadhi ya madiwani hao wa kusimamia halmashauri ili iweze kufanya kazi kwa makini na kutekeleza miradi ya maendeleo kwa ufanisi na  badala  yake wanafanya kazi ya kuihujumu halmashauri kwa maslahi yao binafsi.

Ndikilo alisema kuwa madiwani hao badala ya kushinikiza Halmashauri kutekeleza miradi ya maendeleo lakini wamekuwa wakiwapigia debe watoa huduma na kuwatisha watendaji.

“Shutuma ya baadhi ya madiwani kuhujumu halmashauri hiyo kwa kuwatishia kuwaazimia watendahi  wakuu wa mji huo kuwafukuza kazi kwa madai kwamba wamekataa  kulipa deni la shilingi milioni 231 ambazo halmashauri hiyo inadaiwa na mkandarasi mmoja anayetoa huduma ndani ya mji wa Kibaha haipendezi na wanapaswa kuangalia wajibu wao wa kuwatumikia wananchi;” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa si vema kuegemea kwa mtoa huduma wanapaswa kuacha mara moja tabia ya kuwatishia watendaji ambao wamekataa kulipa deni la mzabuni huyo
na kuacha kuingiza maslahi binafisi katika utendeji wa kazi na badala yake watimize wajibu wao wa kuisimamia halmashauri.
Kwa upande wake mwenyekiti wa halmashauri ya mji huo Leonard Mloe alikiri kuwepo kwa taarifa za baadhi ya madiwani kutaka waungwe mkono kuweka maazimio ya kumfukuza kazi mweka hazina wa mji wa kibaha kwa kukataa kuizinisha malipo hayo.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM mkoa wa Pwani kimempongeza Rais wa awamu ya Tano Dk John Pombe Magufuli kwa kuweza kuzuia mianya ya upotevu wa mapato kwa kuwabana wakwepa kodi na kuliingizia Taifa mapato yanayozidi kiasi cha trilioni tatu kwa kipindi chake cha siku 100 madarakani.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha wakati wa kikao cha Halmashauri Kuu cha mkoa huo katibu mwenezi wa CCM mkoa Dk Zainab Gama akisoma tamko la mkoa kuhusu utendaji kazi wa Rais Magufuli alisema kuwa ni wa kutukuka.

Dk Gama alisema kuwa Rais ameweza kubana matumizi ya serikali na kufanikisha nchi kupata fedha nyingi ikiwa ni pamoja na kupunguza safari za nje kwa viongozi hivyo kuiwezesha serikali kubana matumizi yasiyo ya lazima ya shilingi bilioni 7 ambazo zitatumika kwenye miradi ya maendeleo.

“Jambo linguine ni kubadilisha mfumo wa sherehe za Kitaifa uliyokuwa unatumia gharama kubwa na badala yake siku za sherehe hizo ni kufanya usafi wa mazingira kote nchini;” alisema Dk Gama.

Alisema kuwa katika kuonyesha dhamira yake ya dhati ya kuwatumikia wananchi aliteua baraza dogo la mawaziri ambao ni makini na hata baada ya kuteuliwa tayari wameanza kazi kwa kasi kubwa inayoendana na kauli Mbiu yake ya Hapa Kazi Tu.

“Tunaunga mkono dhamira yake ya dhati ya kuinua uchumi kuwa wa kati kwa kusisitiza kujenga viwanda na pia kuboresha mtandao wa barabara za juu katika Jiji la Dar es Salaam Fly Overs pamoja na barabara za njia sita kutoka Dar es Salaam hadi Chalinze,” alisema Dk Gama.

Aidha alisema kuwa katika kipindi hicho aliweza kuwachukulia hatua kali za kinidhamu watendaji wabovu katika taasisi mbalimbali za serikali ambazo walisababisha wananchi kuichukia serikali yao/
Awali akifungua kikao hicho mwenyekiti wa CCM mkoa wa Pwani Mwinshehe Mlao alisema kuwa katika uchaguzi ujao wa Chama utakaofanyika mwakani viongozi wanaoteua wagombea wanapaaswa kuwa makini ili kupata viongozi bora.

Mlao alisema kuwa viongozi wanaoteuliwa kukisimamia chama wanapaswa kuwa na uwezo na si mradi tu ambao baadaye wanakuja kufanya chama kinapata wakati mgumu wakati wa uchaguzi mkuu.

Mwisho.

WATAFUTA MILIONI 50 UJENZI WA MADARASA YA SEKONDARI

NA John Gagarini, Kibaha
WAKAZI wa Mtaa wa Mbwate kata ya Msangani wilayani Kibaha mkoani Pwani wanahitaji kiasi cha Shilingi milioni 50 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa manne ya shule ya sekondari kwenye mtaa huo.
Mtaa huo una wanafunzi zaidi ya 500 wanaotoka kwenye mtaa huo kwenda kusoma kwenye shule ya sekondari ya Nyumbu ambayo iko umbali wa kilometa zaidi ya 10 hali ambayo inawapa wakati mgumu wanafunzi hao kutokana na umbali.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwenye eneo ambalo wanalifanyia usafi kwa ajili ya ujenzi wa shule hiyo mwenyekiti wa mtaa huo Abdala Mtandio alisema kuwa walikuwa wamelenga kuanza ujenzi mwakani lakini kutokana na wanafunzi wengi wanaotoka kwenye mtaa huo kusoma mbali wameona afadhali waanze na madarasa machache ili kuwasaidia watoto wao ili wasome karibu na wanakoishi.
“Tunaomba wadau watusaidie kupata fedha hizo ili tuanze ujenzi kwani kwa sasa shule ya sekondari ya Kata ya Nyumbu  imeelemewa na wanafunzi hivyo tunaiomba Halmashauri iwapunguzie wanafunzi hao kwenye shule tutakayojenga kwani kwenye mtaa wetu kuna eneo kubwa kwa ajili ya ujenzi wa shule ya sekondari wakati kule hawana eneo la kuongeza madarasa,” alisema Mtandio.
Mtandio alisema kuwa kutokana na serikali kutaka shule kuongeza madarasa kwa zile ambazo zina wanafunzi wengi ni vema Hlamashauri ikaongeza nguvu kwenye ujenzi wa shule ambayo wanataka kujenga ili kupunguza mlundikano wa wanafunzi kwenye shule hiyo ya Nyumbu.
“Tunaomba wadau watusaidie kwani kwa sasa eneo limepatikana kwa ajili ya ujenzi ambalo lina ukubwa wa hekari 10 tumeanza kwa kujitolea kufyeka vichaka na sasa tunajitolea kungoa visiki ambapo pia tunaomba Halmashauri itusaidie greda kwa ajili ya kungoa visiki tuliomba muda mrefu ambapo tathmini ilifanyika na kuonekana kuwa zinahitajika kiasi cha shilingi milioni nane kwa ajili ya greda,” alisema Mtandio.
Kwa upande wake mmoja wa wakazi wa mtaa huo Steven Mwita alisema kuwa malengo ya mtaa wetu ni kuanza ujenzi kuanzia mwezi wanne hivyo wanawaomba serikali na wadau wengine wa maendeleo wawasaidie kwa kuwachangia kwa hali na mali ili wafikie lengo la kujenga shule ya sekondari.
Mwita alisema kuwa matarajio yao ni kufanya ujenzi wa kisasa wa ghorofa ili baadaye wawe na elimu ya juu yaani kidato cha tano na cha sita kwa lengo la kuinua sekta ya elimu kwenye mtaa pamoja na wilaya nzima ya Kibaha

Mwisho.

Saturday, February 13, 2016

WAATHIRIKA WA MAFURIKO WAPATIWA MAHINDI YA MSAADA

Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI kupitia Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula Nchini (NFRA)  imeupatia mkoa wa pwani tani 1,283 za mahindi kwa ajili ya wahanga wa mafuriko wilayani Rufiji.
Mahindi hayo yatasagwa kwa ajili ya kuwapatia unga bure  wananchi 53,446 kwenye tarafa za Mkongo,Ikwiriri na muhoro wilayani humo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini kibaha mkuu wa mkoa wa pwani injinia evarist ndikilo alisema kuwa mahindi hayo yaliwasili juzi wilayani humo.
"Tunatarajia mahindi hayo yatawawasaidia waathirika hao, kisha yatasagwa na wananchi walioathirika watapewa bure," alisema ndikilo.
Ndikilo alisema kuwa tayari magari ya kubeba mahindi hayo kutoka halmashauri yameshachukua mahindi hayo ya msaada kwa kipindi cha mwezi Februari na Machi
" Pia tumeteua wafanyabiashara sita ambao watanunua mahindi kwa wakala hao kisha kuyauza kwa bei ndogo ili kila mwananchi amudu kununua," alisema ndikilo.
Aidha alisema mkakati uliopo kwa sasa wa kiwasaidia wananchi hao ni kuhamasisha wafanyabiashara kupeleka bidhaa kama Michele,unga na maharage, kufanya tathmini ya mafuriko, kuhamasisha kulima mazao ya muda mfupi Mtama, viazi, kunde na muhogo.
"Hadi sasa hakuna taarifa yoyote ya kifo kilichotokana na mafuriko hayo ambayo yameathiri watu ambao wanalima kandokando ya Mto rufiji ambapo Daraja la mto muhoro limefunikwa na maji," alisema ndikilo.
Aliwaomba wadau mbalimbali kujitokeza kutoa misaada ya kiutu kwa waathirika wa mafuriko hayo yaliyoathiri hekta 8,133 za mpunga na hekta 7,171 za Mahindi.
Chanzo cha mafuriko hayo yalianza kuingia kijiji cha mloka tarehe 31 januari hadi februari 6 ambapo maji hayo yametokea mto rufiji unaopokea maji ya mvua kutoka mikoa Iringa, Mbeya na Morogoro.
Mwisho.

RC AWAPA MWEZI MAWAKALA MWEZI MMOJA KUWASILISHA MAPATO WANAYODAIWA NA HALMASHAURI

Na John Gagarini, Kibaha
MAWAKALA wote wanaokusanya mapato ya Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani wametakiwa walipe makusanyo yao yote wanayodaiwa na Halmashauri ndani ya mwezi mmoja.
Agizo hilo lilitolewa jana na mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo wakati akifungua baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo nakusema kuwa ucheleweshaji wa fedha hizo unasababisha Halmashauri kushindwa kufanya mipango yake ya maendeleo.
Alisema kuwa baadhi ya mawakala wamekuwa wakichelewesha makusanyo na tozo mbalimbali wanazozitoza toka kwa wananchi kwa niaba ya Halamashauri hivyo wanapaswa kupeleka malipo hayo kwa wakati.
“Moja ya hoja ambazo zimekuwa zikiwasilishwa na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) ni kushindwa kukusanya mapato ya ndani ya mawakala kwa wakati na kukosa mikakati ya kuongeza mapato ya Halmashauri,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa suala lingine ni mikataba inayoingiwa inakuwa si mizuri na inatoa mwanya kwa wakala kuacha kuwasilisha mapato bila ya kuchukuliwa sheria kutokana na kuchelesha mapato hayo.
“Pia nashauri madiwani wajiepushe na kuomba zabuni mbalimbali katika Halamashauri ili kuepuka migongano ya kimaslahi na muweze kuisimamia vizuri kwani endapo mtakuwa na maslahi hamtaweza kuisimamia hivyo kushindwa kuleta maendeleo,” alisema Ndikilo.
Aliwataka Madiwani kusimamia fedha za makusanyo ya ndani zianarudi kwa wananchi kwa kugaramia huduma mbalimbali na miradi ya maendeleo kwa ustawi wa wananchi.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Halmashauri Leonard Mlowe alisema kuwa watendaji wa halmashauri wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa kuwa waadilifu ili kufanikisha maendeleo kwa wananchi yanapatikana.
Mlowe amewataka watendaji hao kuwasimamia mawakala ili wahakikishe wanawasilisha fedha za makusanyo mbalimbali zinafika kwa wakati ili kuwaletea maendeleo wananchi.

Mwisho.    

Monday, February 8, 2016

WATU 53,000 WAKUMBWA NA MAFURIKO PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
WATU 53,446 wilayani Rufiji mkoani Pwani wamekumbwa  na mafuriko hali iliyowafanya wazungukwe na maji na kuhitaji msaada kufuatia mvua za Vuli zinazoendelea hapa nchini.
Aidha tayari boti mbili za uokozi tayari zimepelekwa kwenye maeneo hayo kwa ajili ya kuwaondoa watu hao waliozungukwa na maji na kuwapeleka sehemu salama.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu toka kwenye eneo la tukio, Mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kuwa maji hayo ambayo yametoka maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na mkoa wa Morogoro.
“Vijiji vingi wilayani humo vimezingirwa na maji na watu wengi waliokumbwa na kadhia hiyo ni wale waliohamia mashambani kwa ajili ya kilimo na kukutwa na maji hayo pamoja na nyumba ambazo ziko mabondeni,” alisema Ndikilo.  
Alisema kuwa mvua hizo ambazo zilizoanza kidogo kidogo tangu Januari 31 mwaka huu zimeathiri zaidi kwenye maeneo ya kata za Mwaseni, Tarafa ya Mkongo, Tarafa ya Ikwiriri na kata ya Muhoro.
“Kutokana na athari za mvua hizo hekta zaidi ya 7,000 za Mahindi na hekta zaidi ya 8,000 za Mpunga  zimesombwa na maji na tayari mkoa umewasiliana na Waziri Mkuu kwenye kitengo cha Wakala wa mazao kuomba msaada wa chakula tani 1,280 za mahindi,” alisema Ndikilo.
Aidha alisema kuwa wameteua wafanyabiashara sita kwa ajili ya kununua mahindi na kuyasaga kwa ajili ya chakula ikiwa ni njia ya kuwasaidia wananchi pia kukabili mfumuko wa bei ambao unaweza kujitokeza kutokana na hali hiyo.
Katika hatua nyingine mkoa umeomba tani 10 za mbegu za mahindi na tani tano za mbegu za Mtama kwa ajili ya kupanda kukabiliana na athari ya mazao ambayo yamesombwa na maji ya mvua za Vuli ambazo wiki ijayo zitaanza mvua za Masika.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI imeombwa kuipatia Idara ya Ziamamoto mkoani Pwani vifaa kwa ajili ya kukabiliana na majanga ya moto na kuokoa watu wanaokumbwa na majanga mbalimbali.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mjini Kibaha Kamanda wa Kikosi cha Zimamoto mkoani Pwani Goodluck Zelote alisema kuwa kutokana na uhaba wa vifaa baadhi ya wilaya hazina vituo vya zimamoto.
Zelote alisema kuwa kwenye mkoa wa Pwani kati ya wilaya sita ni wilaya tatu tu za Kibaha, Bagamoyo na Mafia ndiyo zenye vikosi hivyo huku wilaya za Kisarawe, Rufiji na Mkuranga zikiwa hazina huduma hiyo.
“Ingependeza angalau kila wilaya kuwa japo na kikosi cha Zimamoto na uokoaji japo hakitaweza kutoa huduma kwenye eneo lote lakini angalau zingesaidia ambapo kwa sasa utendaji kazi unakuwa mgumu,” alisema Zelote.
Alisema kuwa vifaa hivyo ni magari pamoja na vifaa vya uokoaji ambapo alitoa mfano wa ajali ya moto ambayo ilitokea hivi karibuni Chalinze walifika na kunusuru nyumba yote kuteketea kwa moto lakini kutokana na umbali uliopo walinusuru vyumba kadhaa.
“Kwa sasa tunachokifanya ni kutoa elimu zaidi ya kujikinga na kuzuia moto kwa kutumia vifaa vya kuzimia moto ambavyo kila mtu anapaswa kuwa navyo kuanzia kwenye maeneo ya huduma hadi majumbani,” alisema Zelote.
Aidha alisema kuwa moja ya changamoto wanayoipata ni ujenzi holela ambao hauzingatii mipango miji hali ambayo inasababisha magari ya kuzimia moto kushindwa kufika kwenye nyumba ambazo zinawaka moto na kuwataka watu wazingatie kanuni za ujenzi.
Mwisho.  



Sunday, February 7, 2016

WANANCHI WATAKIWA KUTOWAHIFADHI WAGENI

Na John Gagarini, Kibaha
IDARA ya Uhamiaji Mkoani Pwani imewataka  wananchi kutokubali kukaa na wageni ambao si raia Watanzania kwani ni kinyume cha taratibu na endapo watabainika watachukulia hatua za kisheria kwa kuwatunza wageni.
Hayo yalisemwa na Naibu Kamishna wa Idara hiyo Grace Hokororo alipozungumza na mwandishi wa habari hizi ofisni kwake mjini Kibaha na kusema kuwa kuna watu wanaishi na wageni jambo ambalo ni kosa kisheria.
Hokororo alisema kuwa kuna baadhi ya watu wamekuwa wakiishi na wageni majumbani mwao wengine wakiwa wamewapangisha, wamewaajiri au kuwapangisha kwenye nyumba zao kama Raia wa Tanzania bila ya kufuata taratibu.
“Mgeni yoyote anapoingia nchini anapaswa kufuata taratibu na lazima serikali au idara hivyo watu wanaokaa nao au kufanya nao shughuli yoyote bila ya kufuata taratuibu za nchi ni kosa na endapo wanagundua kuwa siyo raia wanapaswa kutoa taarifa ili hatua zichukuliwe kwa mhamiaji haramu,” alisema Hokororo.
Alisema kuwa changamoto inayowakabili ni uchache wa watumishi hali ambayo inawafanya washindwe kuwadhibiti wahamiaji haramu hao ambao wamekuwa wakileta athari nyingi kwa raia  endapo atakaa kinyemela bila ya kufuata taratibu.
“Kuna athari mbalimbali zinazotokana na Raia wa nje kuishi bila ya kibali ikiwa ni pamoja na kunyakua rasilimali kama vile mashamba na vitu vingine lakini akiishi kwa kufuata taratibu kuna namna ya kupewa rasilimali bila ya kumwathiri mwenyeji,” alisema Hokororo.
Aidha alisema kuwa changamoto nyingine ni mkoa kutawanyika na njia za kuingilia ni nyingi kwa kupitia kwenye Bahari ambako hakuna vyombo vya kufanya doria kwenye bandari ambazo nyingine ni bubu ambazo zinatumika kama milango ya kuingilia.

Mwisho.

Monday, February 1, 2016

UWAMAMI WATAKA SULUHU NA HALMASHAURI KISARAWE

Na John Gagarini, Kisarawe

UMOJA wa Wafanyabiashara wa Mazao ya Misitu Wilayani Kisarawe mkoani Pwani (UWAMAMI) wameomba suluhu na Halmashauri ya Wilaya ili waache mgomo wa kufanya biashara hiyo kwa kurejeshewa fedha zao za faini ambazo walitozwa kimakosa.

Wafanyabiashara hao walisema kuwa wataachana na mgomo huo endapo Halmashauri hiyo hiyo itawarudishia fedha zao kiasi cha zaidi ya shilingi milioni nne ambazo wafanyabiashara hao walipigwa kinyume cha taratibu.

Akizungumza na waandishi wa habari Makamu Mwenyekiti wa umoja huo Mohamed Dikata alisema kuwa mgomo huo utaendelea hadi pale Halmashauri itakapowarejeshea fedha zao kwani hali hiyo imeathiri biashara zao hasa ikizingatiwa walikiri kuwa walifanya makosa katika upigaji fani huo kwa wafanyabiashara ambao walizidisha mzigo wa mazao ya misitu walipokuwa wakiitoa mashambani.

“Sisi tunatoa huduma kwa wananchi hivyo tunaomba Halmashauri warudishe fedha hizo ambazo ni sehemu ya mitaji yetu na tumejaribu kukaa mara kadhaa bila ya kufikia muafaka kwani wao wanataka kutulipa kidogo kidogo fedha zetu jambo ambalo hatujaliafiki tulipigwa faini ambapo wengine walipigwa faini na kufikia zaidi ya milioni moja na kutoa fedha taslimu kwani nini  wao warejeshe kwa mafungu kwani sehemu ya fedha tulizotoa ni za biashara hivyo kuyumbishwa katika shughuli zetu za kibiashara," alisema Dikata.

Aidha alisema kuwa wanataka watumishi wa Halmashauri waliohusika waondolewe kwani wamekiuka taratibu za kazi zao kwa kuwalipisha faini zisizostahili kwani si mara yao ya kwanza hivyo wanapaswa kuchukuliwa hatua za kisheria.

“Walitupiga faini ya shilingi 16,000 kwa kila gunia badala ya shilingi 1,600 kwa gunia ambalo linakuwa limezidi na sisi hatukatai kulipa faini ambayo ni halali tunachopinga ni kuzidishiwa mara 10 zaidi ya faini halali,” alisema Dikata.

Jitihada za kumpata mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe hazikufanikiwa kwani alikuwa nje ya ofisi kikazi ambapo kaimu wake naye hakupatikana hata hivyo ofisa Mipango wa Patrick Alute alikiri kuwa na tatizo hilo na kusema kuwa mazungumzo yanaendelea baina ya wafanyabiashara hao.

Alute alisema kuwa Halmashauri inaendelea na mazungumzo ili kufikia muafaka, umoja huo hujihusisha na biashara ya uuzaji wa mkaa pamoja na kuni ambapo gunia moja hulipiwa kiasi cha shilingi 20,000 kama ushuru wa Halmashauri.

Mwisho.