Sunday, July 27, 2014

ATUHUMIWA KUMWUA MKEWE KWA KUMCHOMA KISU KUTOKANA NA WIVU WA KIMAPENZI



Na John Gagarini, Kibaha
KIJANA aliyetambuliwa kwa jina la Omary Iddi mkazi wa Kijiji cha Mwanabwito kata ya Ruvu wilayani Kibaha mkoani Pwani anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka (25) anatuhumiwa kumwua mkewe kwa kumchoma kisu kutokana na wivu wa mapenzi.
Mtuhumiwa huyo ambaye alikuwa akifanya ya kusimamia shamba la mtu pamoja na kufanya kazi ya bodaboda anatuhumiwa kufanya mauaji hayo nyumbani kwa wakwe zake baada ya kuona kuwa mkewe amegoma kwenda kwake kutokana na ugomvi uliokuwepo baina yao.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu mwenyekiti wa Kijiji cha Boko Mnemela Hassan Mohamed alisema kuwa tukio hilo limetokea Julai 27 majira ya saa mbili asubuhi.
Mohamed alisema kuwa siku moja kabla ya tukio hilo Julai 26 mtuhumiwa huyo akiwa na amesindikizwa na mtu mmoja ambaye jina lake bado halijapatikana walikuwa na kikao cha kusuluhishwa baada ya kuhitilafiana  na kikoa hicho kilifanyika nyumbani kwa wazazi wa marehemu.
“Kwa mujibu wa watu waliohudhuria kikao hicho walisema kuwa kikao hicho kilifanyika kuanzia majira ya saa 2 usiku hadi saa 5 usiku ambapo hata hivyo mwafaka haukuweza kufikiwa kwani marehemu alikataa kwenda kwa mume wake,” alisema Mohamed.
Alisema kuwa siku iliyofuata watu waliokuwa wakihusika kusuluhisha waliondoka na yeye pamoja na mtu aliyeambatana naye waliondoka lakini ghafla alirudi akidai kuwa anafuata betri ya simu aliyoisahau nyumbani kwao na marehemu.
“Alimkuta mkewe akipepeta mchele jikoni na kuanza kumbembeleza lakini inaonekana aligoma kabisa kurudi kwa mumewe hali ambayo ili mkasirisha mumewe na kuanza kumchoma kwa kutumia kisu huko jikoni kisha wakatoana nje huku marehemu akipiga kelele,” alisema Mohamed.
“Mtuhumiwa alimchoma marehemu kwenye ziwa la upande wa kulia na kwenye uti wa mgongo karibu na bega la upande wa kushoto na alimchoma kisu mbele ya bibi yake mama yake wa kufikia na mdogo wake ambao walipiga kelele na kushindwa kumsaidia ambapo mtuhumiwa huyo alikimbia maporini,” alisema Mohamed.
Mwenyekiti huyo alipoulizwa juu ya chanzo cha mauaji hayo alisema kuwa kwa mujibu wa watu waliokuwa wakijua ugomvi wao walisema kuwa mtuhumiwa alikerwa na tabia ya mkewe kurudishiwa zaidi chenchi anapokwenda kwenye duka lililopo kijijini hapo.
“Marehemu alikuwa akimjulisha mumewe juu ya hali hiyo ambapo inasemekana aligoma kurudi kutokana na kuambulia vipigo na kutishiwa kuuwawa na mwanaume huyo na kupelekea kufanyika kikao cha usuluhishi na muuza duka kifanyike ili kupata mwafaka lakini ikashindikana na kutokea mauaji hayo ya kusikitisha,” alisema Mohamed.
Jitihada za kumpata kamanda wa Polisi mkoani Pwani Kamishna Msaidizi Mwanadamizi wa Polisi Ulrch Matei hazikuweza kuzaa matunda ili aweze kuzungumzia tukio hilo.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment