Sunday, July 20, 2014

MGOMO WA WACHINJAJI NGOMBE WAISHA



Na John Gagarini, Kibaha
HATIMAYE ule mgomo wa wachinjaji ngombe na wamiliki wa mabucha wilayani Kibaha mkoani Pwani umekwisha baada ya pande mbili zilizokuwa zikitofautia Halmashauri ya Mji wa Kibaha na wamiliki wa mabucha hayo chini ya mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba kukaa meza moja na kumaliza mgomo huo uliodumu kwa muda wa siku mbili kuanzia Julai 18 hadi 19.
Mgomo huo ambao uliendeshwa na wamiliki hao wa mabucha ambao ndiyo wachinjaji wa ng’ombe kupitia Umoja wa wafanyabiashara wa nyama na mazao yake wilayani Kibaha  (UWABINK) walifanya mgomo wa kuuza nyama kwa mji wa Kibaha na vitongoji vyake kwa madai kuwa machinjio mpya ya Mtakuja waliohamishiwa haina huduma muhimu ikiwemo maji huku wakitaka kutumia ile ya zamani ya Maili Moja.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jana mjini Kibaha kwa njia ya simu mkuu wa wilaya ya Kibaha Kihemba alisema kuwa kulitokea tofauti baina ya pande hizo mbili hali iliyosababisha mgomo huo ambao uliathiri walaji wa nyama wa mji huo na maeneo ya wilaya ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam.
Kihemba alisema kuwa suala la maji pande hizo zimekubaliana Halmashauri watanunua maji kwa kipindi cha wiki moja na UWABINK nao watanunua wiki moja hivyo watapeana zamu ya kununua maji hadi suala hilo litakapopatiwa ufumbuzi ambapo halmashauri imetenga kiasi cha shilingi milioni 19 kwa ajili ya kuchimba kisima kirefu cha maji Septemba mwaka huu.
“Muafaka ni kwamba waendelee kuchinja kwenye machinjio ya zamani kwa muda wa siku tatu kuanzia Julai 20 hadi Julai 22 kisha wahamie kule, kwani kwa kipindi hicho taayari marekebisho yatakuwa yamefanywa na maji watashirikiana kununua,” alisema Kihemba.
Aidha alisema kuwa baada ya siku tatu watatakiwa hamie huko machinjio mpya na ile ya zamani itabomolewa ili kupisha shughuli nyingine kwenye eneo hilo hivyo anaamini muafaka huo utaondoa msuguano uliojitokeza.
“Kuhusu zizi walikuwa hawajajenga hivyo wajenge zizi hilo katika kipindi hicho walichokubaliana ambapo waliingia mkataba wa uendeshaji ambapo wao wanachinja halmashauri wao ni wa miliki wa miuondombinu na wao hulipa ushuru kwa kila mwezi ni zaidi ya shilingi milioni moja,” alisema Kihemba.
Kwa upande wake msemaji wa umoja huo Athumani Mkanga alisema waliamua kufanya mgomo huo kupinga kuhamishiwa kwenye machinji hayo ya Mtakuja kutoka yale ya Maili Moja kwani yalikuwa hayajakamilika na hayakuwa na huduma muhimu ikiwemo maji na umeme ambapo ule wa jua hautakidhi mahitaji yao.
Mkanga alisema kuwa walikaa meza moja na halmashauri chini ya mkuu wa wilaya ambaye alikuwa mwenyekiti na kukubaliana kuwa watashirikiana katika masuala mbalimbali kwenye machinjio hayo mapya.
“Tumekubaliana baadhi ya mambo ikiwemo sula la maji ambapo tutayanunua kwa zamu wakati wao wanaendelea na utaratibu wa kuchimba kisima kirefu ili kukabiliana na tatizo la maji na masuala mengine,” alisema Mkanga.
Alibainisha kuwa wamekubaliana na marekebisho hayo lakini wanachokitaka ni kuboreshwa kwa huduma ili waweze kufanya shughuli zao bila ya kikwazo chochote lengo likiwa ni kutoa huduma bora kwa walaji.
Mwisho.

Picha zikionyesha machinjio mpya ya Mtakuja iliyopo kata ya Pangani wilayani Kibaha mkoani Pwani ambayo wachinjaji na wamiliki wa mabucha mjini Kibaha waliigomea wakidai kuwa baadhi ya miundombinu yake haijakamilika ikiwemo maji.

No comments:

Post a Comment