Wednesday, July 16, 2014

SHERIA KANDAMIZI KWA WANAWAKE KIKWAZO KUPATA HAKI



Na John Gagarini, Kibaha
IMEELEZWA kuwa ucheleweshaji wa ubadilishaji wa sheria kandamizi kwa wanawake na watoto hapa nchini kumechangia kiasi kikubwa kuendelea vitendo vya unyanyasaji wa makundi hayo ndani ya jamii.
Sheria hizo ambazo zilitungwa miaka ya nyuma zinaonekana kuyakandamiza makundi hayo ambayo yanaonekana ni manyonge ndani ya jamii kwani watu wameendeleza kuyakandamiza hasa katika mgawanyo wa mali.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na Jane Mgaigita mwezeshaji wa mafunzo ya siku mbili yaliyoandaliwa na kituo cha msaada wa Kisheria kwa wanawake (WLAC) kwa wadau wa kituo hicho wakiwemo maakimu, watendaji wa mitaa na kata pamoja na polisi, wilaya ya Kibaha mkoani Pwani juu ya haki za wanawake.
Magigita alisema kuwa baadhi ya sheria ni kandamizi ambazo inapaswa zibadilishwe ili makundi hayo yaweze kupata haki zao hasa pale inapofikia wakati wa mgawanyo wa mali.
“Wanawake wengi na watoto wamekuwa wakikandamizwa na sheria hizo zikiwemo zile za ndoa na masula ya mirathi ambazo bado zinatumiwa na Mahakama zikiwemo zile za mwanzo hivyo ni vema zikarekebishwa ili kuondoa unyanyasaji ndani ya jamii,” alisema Magigita.
Alisema kuwa wao kama wanaharakati wamekuwa wakipeleka mapendekezo ya mabadiliko ya sheria hizo kandamizi ili zibadilishwe lakini zimekuwa hazifanyiwe marekebisho na kuwafanya wanajamii hao kuzidi kukandamizwa kutokana na hali hiyo.
“Baadhi ya sheria za masuala mengine zimekuwa zikirekebishwa harakaharaka  lakini hizi za wanawake hazipewi nafasi kabisa na kufumbiwa macho hivyo kuendeleza unyanyasaji, ” alisema Magigita.
Kwa upande wake hakimu mkazi mfawidhi wa mkoa wa Pwani Salome Mshasha alisema kuwa mbali ya changamoto hiyo ya sheria pia baadhi ya wanawake wamekuwa wakikata tamaa na kuacha kutoa taarifa juu ya haki zao.
“Baadhi ya wanawake wamekuwa wakijirudisha nyuma kwenye suala la kudai haki zao jambo ambalo linawafanya wasipate haki na kuwaacha wanaume wakijinufaisha,” alisema Mshasha.
Naye mwenyekiti wa baraza la Ardhi la wilaya ya Kibaha Maketa Bigambo alisema kuwa wao kama wadau wa utoaji haki watahakikisha kila kundi linapata haki yake ili kuondoa malalamiko hayo.
Bigambo alisema jambo ambalo linatakiwa ni pamoja na wanake kutokata tamaa kufuatilia haki zao kwenye vyombo vinavyohusika ili kukabiliana na ukandamizaji unaofanywa na baadhi ya wanafamilia.
Mwisho.     


No comments:

Post a Comment