Friday, February 3, 2023

WAKAMATWA NA SILAHA MMOJA ATUHUMIWA MAUAJI

JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani linamshikilia mtu mmoja mwanaume (53) ambaye jina limehifadhiwa mkulima mkazi wa Kijiji cha Ruvu Stesheni Wilaya ya Kibaha akiwa na silaha aina ya Shortgun Greener yenye namba za usajli 729 na maganda sita ya Risasi za Shortgun na unga wa baruti.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani ACP Pius Lutumo alisema kuwa mtuhumiwa huyo anashikiliwa kwa kukutwa na silaha hiyo.

Lutumo alisema kuwa mtuhumiwa huyo alishafanya tukio la mauaji huko Kisarawe na kutorokea katika kijiji cha Ruvu Stesheni Wilaya ya Kibaha.

"Mtuhumiwa huyo atafikishwa mahakamani mara upelelezi utakapokamilika na kuwataka watu waache kutumia silaha hizo kinyume cha sheria,"alisema Lutumo.

Katika tukio lingine ambalo lilitokea mnamo Januari 8 mwaka huu majira ya saa 06:45 mchana huko maeneo ya Msanga Sokoni Kata ya Msanga, Tarafa ya Maneromango Wilaya ya Kisarawe mtu mmoja mwanaume (47) ambaye jina lake limehifadhiwa mfanyabiashara mkazi wa Msanga Sokoni alikamatwa kwa kukutwa na Bunduki aina ya Riffle yenye namba za usajili zilizofutika.

Lutumo alisema kuwa mtuhumiwa huyo hakuwa na vibali vya umiliki wa silaha hiyo ambapo ilikamatwa wakati Polisi wakiwa kwenye misako ambayo imefanyika ndani ya kipindi cha mwezi mmoja.

Aidha alisema kuwa pia risasi sita zilikamatwa baada ya kufanya misako katika wilaya za mkoa huo kwa lengo la kudhibiti makosa ya uvunjaji, unyang’anyi wa kutumia nguvu, wizi, wizi wa mifugo, utumiaji wa dawa za kulevya pamoja na matumizi ya pombe harammu ya moshi (gongo).

"Jeshi la Polisi mkoa wa Pwani limefanya misako na operesheni mbalimbali kuanzia tarehe 1 Januari hadi tarehe  31 Januari mwaka huu ambapo Jumla ya watuhumiwa 19 wanaume wamekamatwa,"alisema Lutumo.

Aliongeza kuwa katika misako hiyo walifanikiwa kukamata pikipiki mbili za aina tofauti, Televisheni Spika, deki, feni na meza ya Tv vyote kimoja kimoja
Viti 13 waya ya Fensi rola tatu, Gongo (Pombe ya Moshi) lita 140 na Bhangi gunia 12, Puli 57 na kete 157.

"Upelelzi wa matukio haya bado unaendelea na utakapokamilika watuhumiwa hawa wote watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowahusu,"alisema Lutumo.

Alibainisha kuwa Jeshi la Polisi linaomba wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa kutoa taarifa zozote zinazo husiana na uhalifu na wahalifu kwa wakati kwa kuwatumia wakaguzi kata waliopo kwenye maeneo yao yote ndani ya Mkoa wa Pwani nao watazifanyia kazi kwa wakati na haraka.


Thursday, February 2, 2023

WATAKIWA KUPIMA VIWANJA VIWANJA


MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakari Kunenge ametoa mwezi mmoja kwa wananchi wa mitaa ya Lumumba na Mkombozi Kata ya Pangani Wilayani Kibaha kupima viwanja vyao ambavyo serikali ilitoa baada ya kuvamia eneo lililokuwa la Kituo cha Mitamba Kibaha.

Aidha amewataka wananchi waliovamia sehemu ya Shamba hilo kuondoka kwani wako hapo kinyume cha sheria kwani eneo hilo lilikabidhiwa kwa Halmashauri ya Mji Kibaha kwa ajili ya kuliendeleza.

Kunenge aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na wananchi wa mitaa hiyo kutatua migogoro ya ardhi baada ya wananchi wa mitaa hiyo kugomea zoezi upimaji ardhi wakitaka warasimishiwe eneo ambalo walipewa baada ya kulivamia.

Alisema mtu anayerasimishiwa ni yule ambaye anamiliki ardhi kihalali lakini wao walipewa tu hivyo wanapaswa kupimiwa kwa gharama ya mita za mraba shilingi kwa shilingi 1,5000.

"Natoa mwezi mmoja kwa wananchi wote kwenye mitaa hiyo kupima ardhi yao ili wamiliki kihalali na malipo yalipunguzwa kutoka 2,500 hadi 1,500 kwa mita za mraba baada ya wengi kulalamika kuwa hawana uwezo,"alisema Kunenge.

Alibainisha kuwa eneo hilo lilikuwa likimilikiwa na iliyokuwa Wizara ya Kilimo na Mifugo wakati huo ambapo watu walilivamia na Wizara ilibidi ilimege na kuwaachia wananchi sehemu mwaka 2012.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Mhandisi Mshamu Munde alisema kuwa walitoa matangazo ya wananchi kupima viwanja lakini mwitikio ukawa ni mdogo.

Munde alisema kuwa kutokana na hali ya ugumu wa kupima maeneo hayo wakitaka wayarasimishe hivyo kwa mwezi huo mmoja wanaamini watu watajitokeza kupima maeneo yao 

Shamba hilo la Mitamba lilianzishwa mwaka 1982 na 1983 na Wizara ya Kilimo na Mifugo wakati huo kwa lengo la kutoa mafunzo na uzalishaji wa ngombe bora Mitamba lilikuwa na ukubwa wa hekari 4,000 ambapo ilitoa fidia milioni 20 kwa wananchi waliokuwa wakikaa kwenye eneo hilo wapatao 1,557.




Tuesday, January 31, 2023

HESHIMUNI VIAPO VYENU

VIONGOZI WATAKIWA KUHESHIMU VIAPO VYAO.



Na Elizabeth Paulo,Dodoma

WAKUU wa wilaya wapya walioteuliwa wametakiwa kuheshimu na kuviishi viapo vyao walivyoviapa kwa uadilifu na uaminifu mkubwa katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. 

Katibu  Msaidizi  wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kanda ya kati Dodoma Bibi Jasmini Awadhi alitoa kauli hiyo alipokuwa akimwapisha Mkuu wa wilaya ya Chemba Gelard Mongela  katika hafla fupi iliyofanyika  katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Dodoma.

Awadhi aliisema kuwa wakuu hao wa Wilaya wahakikishe wanajitoa kutumikia viapo walivyoapa mbele na kuviweka katika kumbukumbu zao za kila siku ili viwasidie kuyakumbuka yale yote yaliyoelezwa katika viapo hivyo wanapotekeleza majukumu yao ya kila siku.

Katika hatua nyingine  alimpongeza Mkuu wa wilaya ya Chemba  kwa kuteuliwa kwake na kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amempatia heshima kubwa ya kuiongoza wilaya ya Chemba.

Adha aliwapongeza wakuu wengine wapya wa wilaya za Bahi Godwini Gondwe na Mpwapwa Sophia Kizigo waliohamishiwa mkoani Dodoma katika mabadiliko ya vituo vya wakuu wa wilaya yaliyofanyika hivi karibuni.

Hafla ya kumuapisha Mkuu wa wilaya ya Chemba na kuwakaribisha wakuu wa wilaya wapya ilifunguliwa na mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe Rosemary Senyemule ambayo pia ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa mkoa wa Dodoma, Viongozi  wa dini, Viongozi wa vyama vya siasa, kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa pamoja na Menejimenti ya Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Dodoma.

Sunday, January 29, 2023

SHULE BORA KUINUA KIWANGO CHA UBORA WA ELIMU AWALI NA MSINGI

 


Na Wellu Mtaki, Dodoma

SERIKALI kupitia mradi wa Shule Bora wenye lengo la kuinua ubora wa Elimu ya awali na Msingi  utahakikisha unaongeza ufaulu wa masomo kwa wanafunzi kwa kuboresha ujifunzaji, Ufundishaji, kuimalisha Ujumuishi.

Hayo yamesemwa na Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma Dk.Fatuma Mganga wakati akifungua mafunzo ya mpango wa Serikali wa SHULE BORA kwa waandishi wa habari Jijini Dodoma.

Dk Mganga amesema kuwa moja ya malengo yaliyopo kwa sasa mkoani humo kwa mwaka 2023 ni kuongeza ufaulu kwa asili 95 ya matokeo ya mtihani wa darasa la saba na asilimia 75 ya wanafunzi wanaohitimu kidato cha nne wawe na ufaulu wa daraja la kwanza hadi la tatu.

"Suala la Elimu katika Mkoa wa Dodoma bado halijatangazwa vizuri na kuwataka waandishi wa habari wakatumie kalamu zao wakawe chachu katika kuielimisha jamii kuwa wanajukumu la kushiriki kikamilifu katika kuboresha elimu,"alisema Dk Mganga.

Amesema kuwa Mwaka huu peke yake zaidi ya wanafunzi 90,000 wanatarajiwa kuanza masomo ambapo hadi kufikia Januari 26  asilimia 89.7 ya wanafunzi wa darasa la awali wameripoti shule huku asilimia 94.2 kwa darasa la kwanza na asilimia 66.95 kidato cha kwanza wakiwa wameripoti shuleni.

Naye Mratibu wa mpango wa SHULE BORA Mkoa wa Dodoma Mtemi Zombwe amesema kuwa ili kufanikisha mchakato wa kuinua na kuboresha elimu ni vyema kila mmoja akatambua kuwa anajukumu la kushiriki katika mchakato huo.

Zombwe amesema kuwa katika ngazi ya kitaifa SHULE BORA itatoa pia msaada wa kiufundi kwa serikali ya Tanzania, pamoja na utekelezaji wa mradi wa pili wa LIPWA KWA MATOKEO yaani Education Program for Results Two.

Mradi wa Shule Bora ni Mpango wa Serikali ya  Tanzania, ikifadhiliwa na Serikali ya Uingereza kwa lengo la kuinua ubora wa elimu ya Awali na Msingi katika mikoa tisa hapa nchini kwa ushauri elekezi kutoka Cambridge Education ikishirikiana na mashirika ya ADD International, International Rescue Committee na Plan International.

WANAOFANYA VITENDO VYA UKATILI WATAKIWA KUACHA MARA MOJA



Na Elizaberth Paulo,Dodoma

MKUU wa mkoa wa Dodoma Mheshimiwa Rosemary Senyamule ametoa wito kwa wanaume pamoja na wale wote wanaotenda vitendo vya kikatili kuacha mara moja kwani kundi kubwa linaloathirika na vitendo hivyo ni watoto na wanawake.

Aidha amesema mkoa wa Dodoma ni miongoni mwa mikoa ambayo kuna vitendo vya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto.

Senyamule ametoa wito huo katika hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Dodoma (General Hospital) alipokua akizindua kituo jumuishi cha utoaji wa huduma kwa manusura wa vitendo vya Ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto.

"Mradi huu wa USAID AFYA YANGU umekuja wakati muafaka hapa Jijini na tunashukuru kwa sababu mkoa huu pia una changamoto ya vitendo vya kikatili,"amesema Senyamule.

Amesema kuwa manusura wa vitendo vya kikatili wamekuwa wakipata changamoto katika kupata huduma kwa haraka na kwa taratibu kutokana na mtawanyiko wa maeneo ya huduma muhimu wanayohitaji ikiwemo huduma za afya, ustawi wa jamii na huduma za kisheria.

"Jengo hili la kutoa huduma jumuishi kwa manusura wa vitendo vya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto ni moja ya malengo ya mpango jumuishi wa utoaji huduma kwa walengwa iliyozinduliwa mwaka 2013 kwa lengo la kuhakikisha huduma inatolewa kwa manusura wa ukatili kwa haraka, uratibu mzuri, na kurahisisha mfumo wa rufaa kwa manusura kwa kupata huduma maalum kama msaada wa Kisheria,"amesema Senyamule.

Ameongeza kuwa hali hiyo imesababisha baadhi ya manusura kukosa huduma kwa wakati na kupata madhara yakiwemo maambukizi ya virusi vya Ukimwi, Ulemavu wa kudumu, mimba zisizotarajiwa na mimba za utotoni kutokana na vitendo vya ukatili alivyofanyiwa.

"Baadhi ya manusura kurubuniwa na kupoteza ushahidi ambao ungesaidia manusura kupata haki yake pindi shauri linapofikishwa katika vyombo vya Sheria, kutumia gharama kubwa katika kufikia maeneo ya kupatia huduma hivyo kusababisha matukio mengi ya ukatili kutokutolewa taarifa katika vyombo vya Sheria hali Iliyosababisha manusura kukosa huduma mbalimbali pamoja na haki za kisheria,"amesema Senyamule

Ameagiza wahudumu wa jengo ambalo wanatoa huduma kwa manusura kufanya kazi saa 24 kwani vitendo vya kikatili vinatokea muda wowote hivyo kuanzisha utaratibu wa kuwa katika hospitali hiyo muda wote na kuwaasa kutumia vifaa kwa umakini mkubwa na kwa weledi kwa manufaa ya kuchakata takwimu za manusura wanaopatiwa huduma katika jengo hilo lililozinduliwa ndani ya hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Dodoma.

Kwa upande wake Chip Lyons Rais wa shirika la EGPAF ambao ni wadau waliofadhili ukarabati wa jengo hilo la utoaji wa huduma kwa manusura wa vitendo vya ukatili amesema mradi huo unatakribani miaka 13 tangu kuanzishwa kwake kutokana na ushirikiano mzuri na Viongozi wa Tanzania hata uongozi wa mkoa wa Dodoma.

Naye Anna Hoffman Naibu Mkurugenzi wa Shirika la afya la USAID amesema mradi huo Unatekelezwa katika mikoa Sita nchini ikiwemo mkoa wa Arusha, Manyara, Kilimanjaro, Tabora na Dodoma huku Ukilenga kufikia maeneo mengi hapa Tanzania.


Thursday, January 26, 2023

MNEC WAZAZI TAIFA ATAKA CCM WATANGAZE MAFANIKIO YA RAIS DK SAMIA SULUHU HASSAN

MJUMBE wa Halmashauri Kuu Chama Cha Mapinduzi Taifa (MNEC) Wazazi Hamoud Jumaa amewataka viongozi wa CCM kutumia mikutano ya hadhara iliyoruhusiwa na Rais Dk Samia Suluhu Hassan kueleza miradi ya maendeleo inayofanywa na kutekelezwa na Serikali ya awamu ya sita.

Akizungumza na wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Kibaha Vijijini pamoja na baadhi ya viongozi na wanaCCM kusiwe na kigugumizi kukisemea Chama na kusimamia miradi mbalimbali inayotekelezwa.

Jumaa alisema kuwa Rais ametoa fursa nzuri kuruhusu mikutano ya hadhara kwa vyama vya siasa hivyo ni wakati sasa kwa viongozi na wanaccm kuelezea yale yaliyofanywa katika kuleta maendeleo ya wananchi.

"Viongozi wenzangu, madiwani,wabunge na wanaCCM tutoke kusemea Chama na kupanda majukwaani kuitendea haki ilani ambayo utekelezaji wake unafanya vizuri,"alisema Jumaa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM Kibaha Vijijini Mkali Kanusu alisema kuwa watahakikisha wanasimamia utekelezaji wa miradi na watashirikiana na watendaji wa serikali ili kufanikisha miradi ya maendeleo kwa wananchi.

Naye Katibu wa CCM Safina Nchimbi alisema kuwa anamshukuru MNEC Taifa kuahidi kujenga ofisi ili ziendane na umri wa Chama na kinaendelea na mipango yake mbalimbali ya kimaendeleo na kuhakikisha chama kinakubalika kwa wananchi.


Tuesday, January 17, 2023

UJENZI TAASISI ZA SERIKALI UZINGATIE BAJETI

Na Wellu Mtaki Dodoma

SERIKALI kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) imetoka wito kwa taasisi zote zinazoendelea na ujenzi Dodoma zihakikishe ujenzi huo unakamilika kwa kizingatia taratibu zote za ujenzi ikiwemo ubora, muda , bajeti iliyotengwa na thamani ya fedha Ili kuleta tija.

Wito huo umetolewa Jijini Dodoma na Mhe. George Simbachawene Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera , Bunge na Uratibu wakati wa hafla ya kukabidhi vibali vya ujenzi wa ofisi za taasisi Dodoma huku akiagiza taasisi nyingine ambazo bado hazijaaza maandalizi ya ujenzi Dodoma ziwasilishwe Ofisi ya Waziri Mkuu mahitaji ya viwanja vya ujenzi wa ofisi za taasisi Dodoma kwa ajili ya uratibu wa pamoja.

Simbachawene amesema kuwa serikali ya awamu ya sita imeendelea kutekeleza kikamilifu Mpango wa kuhamia Dodoma ambapo wananchi wanapata huduma zote katika makao makuu ya nchi na kwamba watumishi wote wa serikali ikiwemo wizara zote, vyombo vya ulizi na usalama, muhimili wa bunge na baadhi ya taasisi zimeamia Dodoma na wanaendelea kutekeleza majukumu yao.

Aidha amesema kuwa ifikapo march 2023 muhimili wa mahakama unatarajiwa kuhamia Jijini Dodoma kwani ujenzi wa jengo hilo umefika zaidi ya asilimia 90.

Pia ametoa rai kwa viongozi wa mkoa wa Dodoma, Wizara, Halmashauri, taasisi za serikali, sekta binafsi, wananchi na wadau wengine kuendelea kutoa ushirikiano katika utekelezaji wa Mpango wa serikali wa kuahamia Dodoma pamoja na ujenzi wa makao makuu Ili kufikia malengo ya kuwa na Jiji Bora la kuvutia litakalokidhi mahitaji ya kijamii na kiuchumi kwa miaka mingi ijayo.

Lengo la hafla hiyo ni kukabidhi vibali vya ujenzi kwa taasisi zilizopewa idhini ya ujenzi wa ofisi Jijini Dodoma kama sehemu ya kutambua mchango wa taasisi hizo katika kuunga mkono utekelezaji wa Mpango wa serikali kuhamisha shughuli zake Jijini Dodoma.