Thursday, May 19, 2016

MKURANGA MBIONI KUMALIZA TATIZO LA MADAWATI

Na John Gagarini, Kibaha
WILAYA ya Mkuranga mkoani Pwani limechonga madawati 5,043 ili kukabiliana na tatizo la upungufu wa madawati kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.
Mkuu wa wilaya ya Mkuranga Abdala Kihato akisoma taarifa ya wilaya hiyo kwa mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo wakati wa ziara yake kutembelea wilaya hiyo kukagua shughuli za maendeleo.
Kihato alisema kuwa wilaya hiyo ilikuwa na upungufu wa madawati 5,131 hivyo kubakiwa na upungufu wa madawati 500 ambayo wanatarajia kukamilisha utengenezaji muda mfupi ujao.
“Tatizo la upungufu wa madawati kwa wanafunzi wa shule za Sekondari tatizo hilo hakuna ila tatizo kubwa liko kwa wanafunzi wa shule za Msingi kutokana na uwingi wao na hata wale wa darasa la kwanza ambapo kwa mwaka huu walioandikishwa ni wengi sana,” alisema Kihato.
Alisema kuwa hawana wasiwasi kwani hadi ule muda uliowekwa wa Juni 30 kwa wilaya zote kuondoa tatizo la wanafunzi kukaa chini litakuwa limekwisha kabisa kwani wanashirikiana na wadau mbalimbali kutengeneza madawati.
“Tunawahimiza watendaji wa vijiji na kata kuhakikisha wanakamilisha zoezi hilo ili kuwaondolea adha wanafunzi kukaa chini na kuwafanya washindwe kujifunza vizuri masomo yao,” alisema Kihato.
Aidha aliwaomba wadau wa maendeleo ndani ya wilaya hiyo kuwaunga mkono katika kufanikisha zoezi hilo la uchongaji wa madawati kwa wanafunzi kwenye wilaya hiyo.
Naye mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa anaipongeza wilaya hiyo kwa kuweza kufanikisha kuchonga madawati hayo ambayo sasa yanaenda kuondoa tatizo hilo la upungiufu wa madawati.
Ndikilo alisema kuwa mkoa huo ulikuwa una upungufu wa madawati 43,047 kwa shule za msingi lakini kwa jitihada hizo zitakuwa zimepunguza kwa kiasi kikubwa upungufu huo.

Mwisho.

MKURANGA YAZUIA MALIPO YA MISHAHARA YA WATUMISHI 15

Na John Gagarini, Mkuranga
WILAYA ya Mkuranga mkoani Pwani imewasimamishia malipo watumishi 15 ambao wameondoka kwenye vituo vyao vya kazi bila ya taarifa kwa mwajiri wake ambaye ni Halmashauri.
Hayo yalisema na mkuu wa Wilaya ya Mkuranga Abdala Kihato alipokuwa akisoma taarifa ya wilaya wakati wa ziara ya mkuu wa mkoa wa Pwani kutembelea shughuli za maendeleo kwenye wilaya hiyo.
Kihato alisema kuwa mishahara hiyo ilizuiliwa kutokana na watumishi hao kutotoa taarifa walipoondoka kwenye vituo vyao vya kazi wakati wa uhakiki watumishi katika zoezi la kutambua watumishi hewa.
“Tulifanya uhakiki wa watumishi 179 na kubaini kuwa watumishi 85 walikuwa ni watoro ambapo 51 wamehamia kwenye vituo vingine vya kazi 10 hawakujitokeza na 15 ndiyo walioondoka kwenye vituo vya kazi bila ya taarifa na watano ni watoro kabisa,” alisema Kihato.
Alisema kuwa zoezi hilo ni endelevu na linaendelea kwani linaoneka lina changamoto nyingi katika kubainisha watumishi hewa na wale ambao wako kisheria.
“Hatua tuliyoichukua kwa wale ambao waliondoka kwenye vituo vyao vya kazi bila ya taarifa ni kusimamisha mishahara yao ili wasije wakwa wanachukua fedha pasipo kufanya kazi,” alisema Kihato.
Kwa upande wake Ndikilo alisema kuwa maofisa utumishi wanapaswa kutoa ushirikiano kwa serikali katika kuhakikisha watumishi hewa wanapatikana na itawachukulia hatua kali wale watakaowaficha watumishi hewa.
Ndikilo alisema kuwa zoezi hilo litakapokamilika mkoa utatoa taarifa juu ya zoezi hilo ambalo lina lengo la kuondoa watumishi hewa ambao wamekuwa wakijipatia fedha pasipo kufanya kazi.

Mwisho.

MWENGE KUPITIA MIRADI YENYE THAMANI YA BILIONI 66.3

Na John Gagarini, Bagamoyo
MWENGE wa Uhuru jana ulianza mbio zake mkoani Pwani baada ya kumaliza kuzunguka mkoa wa Dar es Salaam ambapo utakimbizwa kwenye Wilaya Sita za mkoa huo na kupitia miradi 47 yenye thamani ya shilingi bilioni 66.3.

Akizungumza mara  baada ya kukabidhiwa mwenge  wa uhuru kutoka wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam  mkuu wa mkoa wa Pwani, mhandisi Evarist Ndikilo, alisema miradi hiyo imetekelezwa kwa ushirikiano wa serikali kuu na wananchi.

Ndikilo alisema kuwa kati ya miradi hiyo 47, miradi 14 itawekwa mawe ya msingi, 11 itazinduliwa,11 itafunguliwa na miradi mingine 11 itakaguliwa na mwenge huo utakapokuwa mkoani hapa.

 “Miradi mingine  imetekelezwa na Halmashauri, wahisani wa kitaifa na kimataifa pamoja na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi ambapo ujumbe wa mwenge  mwaka huu unasema vijana ni nguvu kazi ya taifa na shirikisho la kuwezeshwa hivyo tupige vita matumizi ya madawa ya kulevya,” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa kwa kutambua changamoto za vijana mkoa umejipanga katika kutatu  changamoto za vijana kwa ushirikiano na vijana wenyewe ambao katika mkoa huu wapo vijana 379,646 kati ya watu milioni 1.9.

“Mkoa umejipanga kutekeleza ujumbe huo kwa vitendo kwani  msingi mkubwa wa ujumbe ni vijana ndio nguzo na ni chachu kubwa ya maendeleo katika taifa hivyo lazima tuwape nafasi,” alisema Ndikilo.

Aidha aliwataka vijana kuchangamkia fursa za kiuchumi na kijamii zilizopo ili kujibu changamoto hususan za ajira walizonazo na ni wakati wa vijana kujitokeza kutumia fursa mbalimbali zikiwemo kujiajiri na kuwajibika ili kukabiliana na changamoto walizonazo kwa kuzigeuza kuwa fursa za ajira kwenye maeneo yao.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Paulo Makonda akimkabidhi Ndikilo mwenge huo wa Uhuru alishukuru kukabidhi mwenge  huo kwa mkoa wa Pwani huku ukiwa umetembea mkoani kwake bila ya tatizo lolote na Mwenge leo  utakimbizwa katika wilaya ya Kibaha.

Mwisho


WANANCHI WALILIA DARAJA

Na John Gagarini, Kibaha
WANANCHI wa mtaa wa Mkombozi wilayani Kibaha mkoani Pwani umeiomba Halmashauri ya Mji wa Kibaha kuwajengea kivuko au daraja kwenye mto Mpiji kwa ajili ya kuvuka kwenda Majohe wilaya ya Kinondoni kupata huduma za kijamii ambako ni jirani na ikilinganishwa na Maili Moja wilaya ya Kibaha umbali wa kilometa zaidi ya 10.
Akizungumza na waandishi wa habari mkazi wa mtaa huo Malaki Lakibuka alisema kuwa  huduma hizo wanazipata Majohe kutokana na ukaribu uliopo wa kilometa mbili ukilinganisha na Kibaha ambako ni mbali kwa zaidi ya kilometa 10, lakini tatizo lililopo ni kukosa kivuko au daraja.
Lakibuka alisema kuwa wako kwenye wakati mgumu kuvuka mto huo kutokana na kuwa na mamba wengi jambo ambalo ni hatari kwa usalama wao ambapo kwa miaka ya nyuma watu walikuwa wakiliwa na mamba.
“Tunapata taabu sana kuvuka hapo mtoni kwani mamba ni wengi na pia endapo utapita vibaya unaweza kuchukuliwa na maji hasa wakati wa mvua hivyo kuhatarisha maisha yetu na ikizingatiwa kuwa watumishi wanaofanya kazi Majohe,” alisema Lakibuka.
Naye mweneykiti wa mtaa huo ambao ni mpya Moshi Mhagama alisema kuwa kutokuwa na kivuko ni changamoto kubwa kwa wananchi ambao wanategemea  hali inakuwa mbaya kipindi cha mvua ambapo mto huo unakuwa umejaa maji.
Moshi alisema kuwa wanategemea Majohe kama ni sehemu ya kupata mahitaji yao ya kawaida ambako ni jirani ikilinganishwa na Kibaha ambako ni mbali sana hivyo tungeomba Halmashauri iwasaidie ujenzi huo ambapo nao tayari walishaanza kuchangishana fedha kwa ajili ya ujenzi wa kivuko.
“Kwa wagonjwa au mama wajawazito ni taabu kwani wanajifungulia wakiwa njiani lakini pangekuwa na daraja wangepita kwa urahisi na kuwawahisha wagonjwa kupata matibabu pia kuna wafanyakazi wanafanya kazi ngambo ya pili ni shida sana kuvuka mvua zinapokuwa nyingi,” alisema Moshi.
Naye diwani wa kata hiyo Agustino Mdachi alisema kuwa jambo hilo alilipeleka Halmashauri lakini alijibiwa kuwa uwezo wa kujenga daraja hilo haupo kutokana na gharama za ujenzi kuwa kubwa sana kiasi cha zaidi ya bilioni mbili.
Mdachi alisema kuwa changamoto kwenye eneo hilo ni kubwa sana kwani mbali pia kuna mamba ambao ni hatari kwa watu wanaovuka hapo hivyo kuhatarisha maisha yao.
“Mbali ya Halmashauri kusema kuwa hawana uwezo wa kujenga daraja kwa sasa pia walisema hawawezi kujenga kivuko cha muda kwani gharama itakuwa mara mbili wao wanataka wajenge kitu cha kudumu ambapo ni ujenzi wa daraja,”alisema Mdachi.
Mwisho. 

Wednesday, May 18, 2016

WAMKATAA MWENYEKITI WAMFUNGIA OFISI

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
WAKAZI wa Mtaa wa Muheza kata ya Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wamefunga ofisi ya mtaa huo kwa madai ya kuukata uongozi ambao wamesema haufanyi kazi kwa utaratibu uliowekwa ikiwa ni pamoja na kutofungua ofisi.
Wakizungumza na waandishi wa habari walisema kuwa uongozi huo tangu umechaguliwa umeshindwa kabisa kuwajibika hivyo kushindwa kuleta maendeleo kwa kipindi chote cha uongozi wao walipochaguliwa mwishoni mwa mwezi Oktoba mwaka jana.
Moja ya wakazi hao ambaye alijitambulisha kwa jina la Modestus Mpelembwa alisema kuwa uongozi huo chini ya mwenyekiti wake Maulid Kipilili umeshindwa kabisa hata kuitisha mikutano ya kisheria ambayo ndiyo sehemu ya wananchi kuweza kuchangia maendeleo na kujua kinachoendelea ndani ya mtaa huo.
“Wananchi wamefikia hatua ya kufunga mlaango wa ofisi kutokana na kuona kuwa hawana msaada wowote na uongozi ambapo hata kama unashida huwezi kusaidiwa kwani hakuna kiongozi hata mmoja anayeonekana zaidi ya kuonekana kwa matukio maalumu,” alisema Melembwa.
Mpelembwa alisema kuwa hata mapato ya mtaa hayaonekani licha ya kuwa mtaa huo ni moja ya mitaa ambayo ina maeneo makubwa ya ardhi ambayo yanauzwa kama viwanja kwa ajili ya makazi kutokana na eneo hilo kuanza kujengeka kwa sasa.
“Ofisi muda mwingi imefungwa kama una shida umpigie simu mwenyekiti na kama ni suala la mauziano ya viwanja ni huko huko na siyo ofisini kama taratibu zinavyosema hali ambayo inaonyesha kuwa hakuna uwazi wa fedha za asilimia zinazotakiwa kubaki kwenye mtaa kwa ajili ya shughuli za maenedeleo,” alisema Mpelembwa.
Naye Angela Mduma alisema kuwa uongozi huo haufai kuwaongoza kwani umeshindwa kukabili changamoto za wananchi ambao waliwachagua kwa ajili ya kutatua kero mbalimbali ikiw ani pamoja na ubovu wa barabara.
“Tuna chanagamoto nyingi ikiwa ni pamoja na ukosefu wa zahanati, shule ya msingi, maji pamoja na huduma nyingine za kijamii lakini endapo uongozi ungekuwa makini kupitia mikutano kama ingekuwa inafanyika tungeweka vipaumbele vya kuanza kuvifanyia kazi lakini uongozi hauna ushirikiano hakuna kilichofanyika hadi sasa,” alisema Mduma.
Mduma alisema kuwa kwa upande wa kinamama wanapata taabu hasa kwenye huduma za kiafya kliniki kwa wajawazito, kuwapeleka watoto wao kliniki na matibabu kwa ujumla kwao ni changamoto kubwa sana.
Naye Modestus Mapunda alisema kuwa mara ya mwisho mwenyekiti aliitisha mkutano wa mtaa lakini cha ajabu muda mfupi baadaye aliahirisha wakati tayari wananchi wameshajiandaa kwa mkutano hali ambayo ilisababisha wananchi kushikwa na hasira na kuifunga ofisi.
“Tunachotaka ni mkuu wa wilaya kuja hapa kwa ajili ya kujua kero zetu kwani uongozi umeshindwa kufanya kazi lakini cha kushangaza wajumbe kutakiwa kutofanya chochote na mwenyekiti na hawaruhusiwi kuingia ofisini hadi watakapoitwa,” alisema Mapunda.
Mwenyekiti wa mtaa huo Maulid Kipilili alisema kuwa hawezi kuongea chochote kwani anaongea na uongozi wa juu na pia suala hilo tayari amelipeleka polisi kulalamika wananchi hao kufunga ofisi ya mtaa.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Maili Moja Ramadhan Lipwai alisema kuwa kufungwa kwa ofisi hiyo ni kinyume cha utaratibu kwani ile ni mali ya umma na wananchi wanapata huduma kupitia ofisi hiyo.
Lipwa alisema kuwa anafanya mawasiliano na viongozi mbalimbali ili kupata suluhu la tatizo hilo ili ofisi hiyo iweze kufunguliwa ili wananchi waweze kupata huduma kupitia ofisi hiyo ambayo imefungwa tangu Mei 15 baada ya mkutano wa mtaa kushindwa kufanyika.
Mwisho.  











   

Thursday, May 12, 2016

NOAH KUTOSAJILIWA KUBEBA ABIRIA BARABARA KUU

Na John Gagarini, Kibaha
MAGARI ya kusafirisha abiria aina ya Noah Hiace pamoja na pikipiki yamesababisha vifo vya watu 102 huku 246 wakijeruhiwa katika kipindi cha kuanzia 2015 hadi Machi 2016.
Kutokana na kukithiri kwa ajali za vyombo hivyo Mamlaka ya Udhibiti  wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA) mkoa wa Pwani imesitisha utoaji wa lesseni mpya kwa magari aina ya Noah maarufu kwa jina la ‘Mchomoko’, na Hiace  kwenye barabara zote kuu ikiwamo barabara ya Morogoro.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha ofisa mfawidhi wa SUMATRA mkoa wa Pwani Nashon Iroga alisema kuwa kwa mujibu wa waraka walioupata kutoka makao makuu magari  hayo yote madogo  ya abiria yanayokwenda masafa  marefu kupitia barabara kuu hayatapewa leseni ya kubeba abiria.
“Barabara kuu kuna vyombo vikubwa vya  usafiri hivyo hayataruhusiwa kupata leseni mpya badala yake yaliyokwisha pata leseni yataendelea hadi hapo muongozo mwingine utakapo toka tena,” alisema Iroga.
Alisema kuwa agizo hilo limetolewa baada ya ongezeko kubwa la magari madogo ya kubeba abiria hasa magari  aina ya noah, kufanya safari ndefu huku baadhi  yakiwa yamebeba abiria na mizigo  bila kuangalia usalama wa abiria  na matokeo yake ni kusababisha ajali za mara kwa mara na msongamano katika barabara kuu.
“Ukiangalia kwa hali ya kawaida magari aina ya Noah yanabeba abiria wachache lakini ili wapate faida inabidi watoze viwango vikubwa vya nauli, kubeba abiria kuliko uwezo wake na kwenda mwendo kasi  ili wafanye safari nyingi na kupata faida, matokeo yake wanahatarisha usalama wa maisha ya abiria,” alisema Iroga.
Aidha alisema kuwa  magari hayo madogo yakiwamo Noah na Hiace yanayobeba abiria yatapewa lesseni mpya za kufanya biashara kutumia ruti za barabara  za ndani na sio barabara kuu.

Mwisho.

JESHI LA POLISI LAMSAKA MWANAFUNZI ALIYECHOMA BWENI


Na John Gagarini, Kibaha
JESHI la Polisi Mkoani Pwani bado linaendelea kumtafuta mwanafunzi wa shule ya Sekondari ya Rafsanjani iliyopo Soga Tarafa ya Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani baada ya kuchoma bweni la wasichana la shule hiyo.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Bonaventura Mushongi alisema kuwa mwanafunzi huyo ambaye hakuweza kufahamika alichoma bweni hilo juzi majira ya saa 4 usiku liitwalo Umoja.
Mushongi alisema kuwa hata hivyo tukio hilo halikuwa na madhara kwa wanafunzi zaidi ya kuharibu mali zilizokuwa kwenye bweni hilo ambazo hata hivyo thamani yake haikuweza kufahamika mara moja.
“Tunaendelea kumfuatilia mwanafunzi huyo ili tuweze kumjua na kumchukulia hatua za kisheria lakini hadi sasa bado hatujafanikiwa kumpata kwani aliandika kwenye sanduku la maoni juu ya dhamaira yake hiyo mbaya ya kuchoma bweni,” alisema Mushongi.
Alisema kuwa wanaendelea kuzifanyia kazi taarifa hizo ili waweze kumbaini mwanafunzi huyo ili hatua kali za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yake kwani kitendo alichokifanya ni cha hatari kwa maisha ya wanafunzi wenzake na mali.
“Tunatoa wito kwa wanafunzi wanapokuwa shuleni wazingatie masomo na kuachana na vitendo visivyo kuwa na maadili kwani jeshi halitawavumilia wanafunzi ambao wanabainika kufanya vitendo viovu kwani tutawakamata na kuwapeleka kwenye vyombo vya sheria ikiwa ni pamoja na mahakamani,” alisema Mushongi.
Bweni hilo lilichomwa moto juzi na mwanafunzi huyo lakini hata hivyo kikosi cha zimamoto mkoa wa Pwani polisi pamoja na wananchi walifanikiwa kuzima moto huo na haukuweza kuleta madhara kwa wanafunzi.

Mwisho.