Thursday, February 25, 2016

WAZIRI SIMBACHAWENE AIKATALIA KEC COTC KUWA CHUO KIKUU

Na John Gagarini, Kibaha
WAZIRI wa Ofisi ya Rais Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Simbachawene amelitaka Shirika la Elimu Kibaha (KEC) kutokibadili Chuo cha Waganga Wasaidizi (COTC) kuwa Chuo Kikuu ili lisiharibu malengo ya chuo kusomesha watu wenye elimu ya kawaida.
Simbachawene aliyasema hayo alipotembelea Shirika hilo hivi karibuni na kusema kuwa ndiyo sababu chuo hicho hakikuingizwa kwenye Taasisi ya elimu ya juu kwani malengo yake ni kusomesha watu ambao ni wa ngazi ya kati.
Alisema kuwa kwa sasa kumekuwa na hali ya kila chuo kutaka kuwa chuo kikuu hali ambayo itasababisha kusiwe na wataalamu wa ngazi ya kati ambao wameonekana kuwa ndiyo wawajibikaji wakubwa.
“Kama kila chuo au taasisi itakuwa na malengo ya kuwa chuo kikuu kuna hatari ya kuwapoteza wasomi wa ngazi ya kati kwani endapo kila mtu atakuwa amesoma chuo kikuu hakutakuwa na watu wa kufanyakazi kwani kila mtu atatakuwa mtawala,” alisema Simbachawene.
Alisema kuwa chuo hicho kilianzishwa kwa malengo ya kuwapatia elimu watu wa vijijini lakini kikishafanywa chuo kikuu wananchi wenye elimu ya kati hawatapata nafasi ya kusoma hivyo malengo ya kuisaidia jamii hayataweza kufikiwa.
“Tunashindwa kupata wagunduzi kwani wanakuwa ni watu wenye elimu ya kawaida sana kama ilivyo kwa nchi zilizoendelea hawa ni watu waliosoma elimu ya kawaida na wengine wanatoka vijijini hivyo na hapa ni sehemu ya kuanzia lakini tukikibadilisha na kuwa chuo kikuu ni sawa na kuvunja daraja ambalo watu wamekuwa wakitumia kuvukia kwenda mbele,” alisema Simbachawene.
Aidha alisema kuwa kuna tatizo la wataalamu wa kati kutokana na watu wengi kuiacha elimu ya kati na kutaka kupata elimu ya juu hivyo kumekuw ana pengo hapo katikakati pia wazingatie malengo ya kuanzishwa chuo hicho ambacho zamani kilijukana kama chuo cha maendeleo ya waganga vijijini.
Mwisho.

ACHOMWA MOTO KWA WIZI WA MCHELE DUKANI

Na John Gagarini, Kibaha
MTU mmoja aliyetambuliwa kwa jina moja la Ngozi mkazi wa Mlandizi wilayani Kibaha mkoani Pwani ameuwawa kwa kuchomwa moto na wananchi wenye hasira kali kwa madai ya kuiba mchele na mafuta ya kupikia dukani.
Tukio hilo lilitokea Fabruari 25 majira ya saa 9 alfajiri katika mtaa wa Tangini baada ya marehemu akiwa na mwenzake ambaye alikimbia kuvunja na kutoa mchele huo kilogramu 100 na mafuta ya lita tatu galoni mbili.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa huo Leons Karoli alisema kuwa watu hao waligunduliwa na baadhi ya madereva wa Bodaboda waliokuwa wakipita kwenye eneo la tukio na kuwakuta watuhumiwa hao wakiwa na vitu hivyo wakiwa wamevipakia kwenye pikipiki ya marehemu aina ya Boxer.
“Mashuhuda walisema kuwa marehemu alikuwa ndani ya hilo duka na kujifanya kama ndiye mwenye duka akijifanya ndiyo analifungua lakini watu walikuwa na wasiwasi kwani ilikuwa ni asubuhi sana jambo ambalo si la kawaida kwa mmiliki huyo kulifungua muda huo huku ambaye mmiliki wake ni Mmbando,” alisema Karoli.
Karoli alisema kuwa baada ya watu kuwa na wasiwasi waliwasiliana na watu kujaa kisha kuanza kumpiga marehemu hadi alipopoteza fahamu na mwenzake alifanikiwa kutoroka kwa kukimbia na kumwacha mwenzake ambaye alibainika kuwa ni muuza matunda pia ni dereva bodaboda.
“Tulifanya mawasiliano na polisi na kuwajulisha kuwa kuna mwizi kakamatwa lakini kabla hawajafika watu hao wenye hasira walimpiga kisha kumchoma moto kwa kutumia mafuta ya petroli na kusababisha kifo chake,” alisema Karoli.
Alisema kuwa marehemu alikuwa na begi ambalo lilikuwa na vifaa mbalimbali ikiwa ni pamoja na mkasi mkubwa unaotumika kukatia makufuli, nondo, vocha za simu pamoja na fedha taslimu kiasi cha shilingi 150,000.
Jeshi la polisi mkoani Pwani lilithibitisha kutokea tukio hilo na kuwataka wananchi kutojichukulia sheria mkononi kwa kutoa taarifa polisi kwa hatua zaidi za kisheria na si kuwauwa watuhumiwa wa matukio ya kihalifu.
Mwisho.
  



MSHINDI UVAAJI SARE ZA CCM ALONGA

Na John Gagarini, Kibaha
MSHINDI wa Uvaaji wa sare za Chama Cha Mapinduzi (CCM)Kibaha Mjini mkoani Pwani Said Ngombe amempongeza mwenyekiti wa chama hicho Dk Jakaya Kikwete kwa kutaka kuenziwa watu wanaokifanya chama kishinde kwenye chaguzi mbalimbali.
Mshindi huyo akizungumza na wandishi wa habari mjini Kibaha baada ya kupewa tuzo na Dk Kikwete wakati wa sherehe za kuzindua jengo la CCM Kibaha Mjini lililojengwa na Mbunge wa Jimbo hilo Silvestry Koka  alisema kuwa kuthamini mchango wa wanachama au makada wake ni moja ya njia za kuwapa motisha ili waendelee kukitetea chama chao.
Ngombe alisema kuwa anamshukuru mwenyekiti kuliona hilo na kutaka viongozi wa maeneo mengine kuiga utaratibu huo wa kuthamini mchango wa wanaccm waliosababisha chama kushinda au kukipigania.
“Tunamshukuru mwenyekiti kwa kutupa tuzo na kuwataka viongozi wa maneo mbalimbali kuwaenzi wanaccm waliojitolea kukipigania chama bila ya kuchoka na mimi nimekuwa nikivaa sare ya chama kila siku ambapo kwa sasa nina miaka tisa mfululizo bila ya kuacha,” alisema Ngombe.
Alisema kuwa anajisikia fahari kupewa tuzo hiyo ya uvaaji wa sare kwani imempa moyo wa kuendelea kukipigania chama licha ya kukumbwa na changamoto nyingi kutoka kwa wapinzani wao vyama vingine.
“Kuvaa kwangu sare za chama kwenye eneo lango la kufanyia kazi imekuwa chachu ya chama chake kufanya vizuri kwani watu wamekuwa wakinifahamu kwa uvaaji wangu huu na nimekuwa nikiwakabili wapinzani wetu kwa hoja kwani wakishaniona wamekuwa wakinitania na mimi ndo ninapopata muda wa kuwapa sera za chama huku wengine wakijiunga na chama kupitia kwangu kwani naonyesha msimamo wangu wa chama,” alisema Ngombe.
Aidha alisema kuwa anashangazwa na baadhi ya wanaccm kuogopa kuvaa sare za chama kwani hata kwenye vikao wengine wamekuwa hawavai licha ya kutakiwa kuvaa wanapokuwa kwenye mikutano na vikao vya chama.
Alishauri tuzo hizo ziambatane na fedha kidogo kwa ajili ya kuongeza motisha kwa wanaofanya vizuri kwneye nyanja mbalimbali za kukipigania chama bila ya kuwa na woga wa aina yoyote tofauti na ilivyo wanachama au wapenzi wa chama.
Mwisho.   

BIBI AINGIA MATATANI KIFO CHA MWANAE

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
BIBI Nuru Mchenga mwenye umri wa zaidi ya miaka (80) mkazi wa Maili Moja B wilayani Kibaha mkoani Pwani amejikuta kwenye wakati mgumu baada ya wananchi kumlalamikia kukaa na maiti ya mwanae kwa masaa kadhaa bila ya kuwataarifu watu.
Mbali ya kumshangaa kukaa na maiti muda mrefu pia walimshangaa bibi huyo kumsafisha mwanae kwa taratibu za dini ya Kiislamu jambo ambalo ni kinyume kwani huwa linafanywa na wanaume.
Tukio hilo lilitokea Fabruari 24 majira ya mchana ambapo Mwanae Kassimu alifariki majira ya saa nane hapo nyumbani kwake baada ya kudaiwa kuwa alikuwa anaumwa.
Wakizungumza na waandishi wa habari majirani wa Bibi huyo ambao hawakutaka kutajwa majina yao magazetini walisema kuwa wameshangazwa na kitendo hicho cha kukaa na maiti kwa muda wote huo bila kuomboleza kama ilivyo kwa watu wanaofiwa ambao hulio kuashiria kuwa kuna msiba.
Walisema kuwa kilichowashangaza ni jinsi gani bibi huyo alipomfanyia usafi mwanae wa kiume jambo ambalo ni kinyume na taratibu za dini ya Kiislamu hali ambayo ndiyo imezua maswali mengi.
Alisema marehemu alipaswa kufanyiwa taratibu za kidini na mwanaume na si mwanamke kama alivyofanya bibi huyo ambaye watu wengi wamemshangaa kwa ujasiri huo.
“Inasikitisha sana kuona bibi huyu anafanya vitu kama hivyo ndiyo maana kumekuwa na maneno mengi kutokana na kifo cha mwanae kutokana na alivyofanya na pia haonyeshi kusikitika kifo cha mwanae tofauti na misiba mingine,”  walisema majirani hao.
Kwa upande wake Bibi huyo akizungumza na waandishi wa habari nyumbani kwake alisema kuwa mwanae alilogwa kwa kutupiwa jini na watu ambao hawaipendi familia yake na kusababisha kifo hicho.
Mchenga alisema kuwa siku ya tukio hilo mwanae alikuwa tu nyumbani nay eye alikuwa akiendelea na shughuli zake na kushangaa kuona mwanae hana uchangamfu.
“Ilipofika mchana mwanangu alifariki na kabla hajafariki tulikubaliana nikifa mimi yeye ataniosha na akifa yeye mimi nitamwosha ndiyo sababu ya mimi kufanya hivyo,” alisema Mchenga.
Alisema kuwa anashangaa kuona watu wanataka kumfanyia fujo nyumbani kwake na kusema kuwa watu wanasema maneno mengi juu ya kifo cha mwanae huyo.
Kutokana na watu kujazana nyumbani kwa bibi huyo ilibidi jeshi la polisi kuuchukua mwili wa marehemu majira ya saa 3 usiku na baadaye walirudi tena majira ya saa tano kasoro na kumchukua bibi huyo kutokana na kuhofia usalama wake kwani watu walikuwa wakimzonga na kumzomea, Jeshi la polisi limethibitisha kutokea tukio hilo.
Mwisho.
  



Sunday, February 21, 2016

WAZIRI SIMBACHAWENE ALIPA NENO SHIRIKA LA ELIMU KIBAHA

Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI imesema kuwa itaangalia upaya uendeshaji wa Shirika la Elimu Kibaha (KEC) ili lizalishe liweze kujiendesha kwa ufanisi badala ya kuitegemea serikali ili kuboresha maslahi ya wafanyakazi wake na kutoa huduma bora kwa wananchi.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Simbachawene alipotembelea Shirika hilo kujionea utendaji kazi wake na na kuongea na wafanyakazi kujua changamoto zinazowakabili na kusema kuwa linapaswa kujiendesha kwa faida na si kuwa tegemezi.
Simbachawene alisema kuwa Shirika hilo la Umma lilianzishwa kwa lengo la kusaidia wananchi hasa wale wa vijijini kwa wakati ule lakini linapasw akubadilika kutokana na wakati na kuacha mifumo ya uendeshaji wa kizamani ambayo haiendani na hali halisi ya wakati uliopo hivyo kushindwa kunufaisha watumishi na wananchi.
“Haiwezekani Shirika kama hili lenye rasilimali na vyanzo vingi vya mapato ikiwa ni pamoja na ardhi kubwa linakuwa na watumishi ambao ni maskini huku wakikosa stahiki zao za kimsingi na kufanya liyumbe ni jambo la kusikitisha sana hivyo serikali itakaa na kuangalia njia za kuweza klirudisha kwenye uhalisia wake,” alisema Simbachawene.
Alisema kuwa Shirika linayumba kw asababu hakuna mipango mikakati ya kujiendesha kisasa kwani maono yake yanaonekana bado ni ya kizamani kwa kuendelea kudeka kwa serikali licha ya kuwa na fursa nyingi zianazolizunguka.
“Mbali ya mfumo wa uendeshaji kuwa na matataizo mengi pia wafanyakazi wamelalamika sana juu ya maslahi yao ikiwa ni pamoja na malipo ya kazi z aziada, kupandishwa madaraja na maslahi mengine nitakuja na majibu ya maswali yenu pia tume itaundwa kila sekta ili kubaini matatizo yaliyopo na kuyafanyia kazi,” alisema Simbachawene.
Kwa upanade wake mwenyekiti wa bodi ya Shirika Patrick Makungu alisema kuwa watazifanyia kazi changamoto mbalimbali ambazo zinawakabili wafanyakazi ambazo zinawafanya watumishi washindwe kutoa huduma bora.
Naye mkurugenzi wa Shirika la Elimu Kibaha Dk Cyprian Mpemba alisema kuwa wanakabiliwa na changamoto nyingi ambazo zinawafanya washindwe kutoa huduma bora ikiwa ni pamoja na kuwa na mahitaji ya fedha kiasi cha shilingi bilioni 6.5 kwa ajili ya uendesheaji.
Dk Mpemba alisema kuwa mbali ya changamoto hizo wamepata mafaniko kupitia mfumo wa kieletroniki wa ukusanyaji wa mapato ya Hospitali ya Rufaa ya mkoa ya Tumbi ambayo iko chini ya Shirika hilo kufanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi milioni 3,000,000 toka 300,000 kwa siku.
Waziri alitembelea Hospitali hiyo, aliangalia mfumo wa ukusanyaji mapato wa kieletroniki uliobuniwa na shirika hilo, kampuni ya ufugaji kuku ya Organia, Shirika hilo lilianzishwa miaka zaidi ya 40 iliyopita na nchi za NORDIC likiwa na lengo la kupambana na adui watatu ambao ni ujinga, umaskini na maradhi na lina wafanyakazi zaidi ya 900 na lina miliki Hospitali ya Tumbi, Chuo cha Waganga wasaidizi, Chuo cha Ufundi Stadi VETA, Shule z a sekondari Kibaha wavulana na Wasichana, Tumbi, shule ya msingi Tumbi na awali     

 MWISHO

MBUNGE AKABIDHI VITABU VYA SAYANSI

MBUNGE wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete kushoto akimkabidhi kitabu ofisa elimu wa mji wa Halmashauri ya Chalinze Zainab Makwinya kulia na katikati ni mwanfunzi wa shule ya sekondari ya Mdaula Budi Tanganyika  

Na John Gagarini, Chalinze

KATIKA kuhamasisha wanafunzi kupenda masomo ya Sayansi shirika lisilo la Kiserikali la Kulea Childcare Villages la Chalinze  kwa kushirikiana na Mbunge wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete wamekabidhi vitabu 3,438 vyenye thamani ya shilingi milioni 70.
Vitabu hivyo vya Sayansi ni kwa ajili ya wanafunzi wote wa shule za Sekondari na vichache kwa wanafunzi wa Msingi kwa wanafunzi wa Jimbo la Chalinze ili kuwahamsisha kujifunza mambo mbali mbalimbali ya Sayansi.
Akikabidhi vitabu hivyo kwa mwalimu mkuu wa shuke ya Sekondari ya Mdaula Melkisedek Komba, Mbunge wa Jimbo hilo alisema kuwa lengo la kutolewa vitabu hivyo ni kuhamasisha wanafunzi kusoma masomo hayo ili kupata wataalamu wengi wa Sayansi .
Ridhiwani alisema kuwa masomo ya Sayansi ndiyo yanaotoa wataalamu mbalimbali hivyo wadau wa elimu wanapaswa kutoa hamasa ya kwa wanafunzi kujifunza Sayansi ili waongeze idadi ya wanaosoma kwa lengo la kuwa na wanasayansi wengi.
“Sisi tukiwa ni wadau wa maendeleo tutaendelea kusaidiana na wadau wengine ili kuhakikisha kuwa tunawahamsisha wanafunzi kuyapenda masomo haya ambayo baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakiyaogopa kwa madai kuwa ni magumu hivyo ni vema tukawawekea mazingira ya kuona kuwa ni sawa na masomo mengine,” alisema Ridhiwani.
Alisema kuwa serikali imekuwa ikishirikiana na wadau mbalimbali kama ilivyo kwa shirika la Kulea Childcare ambalo limepata vitabu hivyo toka kwa marafiki zao wa nchini Marekani kwa ajili ya kusaidia sekta ya elimu.
Kwa upande wake mwasisi wa shirika hilo la Kulea Romie Mtenda alisema kuwa shirika lake limekuwa likisaidia sekta ya elimu ambapo hiyo ni mara ya pili kutoa msaada wa vitabu katika Jimbo hilo pia wamekuwa wakitoa misaada ya kielimu.
Mtenda alisema kuwa shirika lao limekuwa likitoa misaada kwa watoto yatima, wajane na watu wasishio kwenye mazingira magumu ikiwa ni pamoja na kuwasaidiaada, malazi, makazi na huduma nyingine za kijamii.   
Naye mwalimu mkuu wa Mdaula Komba alisema kuwa vitabu hivyo vitasaidia wanafunzi kwa ajili ya kujifunza Sayansi ambayo imekuwa ndiyo somo kuu kwa ajili ya wataalamu ambao wanabuni vitu mbalimbali ambavyo hutumiwa na watu.
Komba alisema kuwa msaada huo umekuja wakati mwafaka kwani wanafunzi wamekuwa na mahitaji ya vitabu vya Sayansi kwa ajili ya kujisomea hivyo vitawasaidia sana kupenda masomo hayo ambayo ni Bioloji, Sayansi na Hesabu. Vitabu hivyo vimetolewa kwa mgawanyo wa tarafa tano ambazo ni Chalinze vitabu 998, Msoga 910, Miono 610, mSata 610 na Kwaruhombo 610.

Mwisho.

Tuesday, February 16, 2016

KATA KUKUTANA NA WAKULIMA NA WAFUGAJI

Na John Gagarini, Pwani
KATA ya Kiwangwa wilayani Bagamoyo mkoani Pwani imeweka mpango wa kukutana na wakulima na wafugaji ili kukabiliana na changamoto za jamii hizo ambazo zimekuwa zikigombana kutokana na wafugaji kudaiwa kulisha mazao mifugo kwenye mashamba ya wakulima.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu diwani wa kata hiyo Hussein Malota alisema kuwa lengo la kukutana na pande hizo ni kujadili jinsi gani ya kukabili changamoto hizo ambazo zimekuwa zikisababisha mapigano.
Malota alisema kuwa wiki tatu zilizopita kulitokea ugomvi baina ya pande hizo mbali baada ya wafugaji kudaiwa kuachia ngombe na kula mazao ya wakulima hali ambayo ili sababisha vurugu za hapa na pale.
“Tayari tumeunda kamati za maridhiano za wakulima watano na wafugaji watano ili kutunga sheria ndogondogo ambazo endapo mmoja atakiuka ataadhibiwa kulingana na makubaliano ya kamati hiyo ili kudhibiti wale watakaokiuka makubaliano hayo,” alisema Malota.
Alisema kuwa tatizo kubwa ni baadhi ya wafugaji wapya wanaoingia kwenye vijiji mbalimbali kwani hawajui taratibu mara waingiapo kwenye maeneo ya wenyeji hali ambayo inasababisha migogoro baina ya pande hizo.
“Tumeunda kamati hizi ili zitunge sheria ambazo zitawaabana wale watakaokiuka kwani wajumbe wa hizo kamati watawajulisha wenzao makubaliano yaliyoafikiwa lengo likiwa ni kupunguza migogoro ya wakulima na wafugaji waishi kwa amani kama jamii moja,” alisema Malota.
Aidha alisema kuwa changamoto nyingine walioiona ni baadhi ya wafugaji kuwaachia watoto wachunge mifugo hiyo ambayo ni makundi makubwa na kushindwa kuyamudu wakati wakichunga na kusababisha matatizo.
Mwisho.