Thursday, August 20, 2015

HABARI MBALIMBALI ZA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
UMOJA wa Wafanyakazi wa Viwanda na Biashara Tanzania (TUICO) kimewataka wanachama wake kukitumia chama chao ili kujileta maendeleo.
Hayo yalisemwa hivi karibuni mjini Kibaha na mwenyekiti wa chama hicho Betty Msimbe mara baada ya uchaguzi wa chama hicho ambapo alifanikiwa kuwa mwenyekiti wa chama hicho
Msimbe alisema kuwa baada ya kupata nafasi hiyo ya kukiongoza chama hicho atahakikisha kuwa wanachama wanapata maendeleo kwa kutumia chama chao ambacho kina lengo la kuwaletea umoja na kutetea haki zao.
“Malengo yangu ni kuongeza wingi wa wanachama, kutetea haki za wafanyakazi kuhakikisha mkoa unavuka malengo yake ya kazi, haki na maslahi ya wafanyakazi sehemu za kazi,” alisema Msimbe.
Alisema kuwa atafanya mafunzo maeneo ya kazi ili wafanyakazi wapate elimu juu ya haki zao na elimu kwa viongozi wa matawi kuhusu kutetea maslahi ya wafanyakazi ili waweze kuboresha utendaji kazi wao.
“Kikubwa ninachokiomba toka kwa wanachama na viongozi wenzangu ni ushirikiano ambao utasaidia kukipeleka mbele chama na kufikia malengo ya kuhakikisha haki za wafanyakazi zinapatikana,” alisema Msimbe.
Naye Naibu Katibu Mkuu Msaidizi sekta ya biashara TUICO Taifa Peles Jonathan alisema kuwa atahakikisha anasimamia haki na maslahi ya wafanyakazi kwa nchi nzima na kufanya umoja huo kuwa na demokrasia ya uwakilishi wa kulinda na kutetea haki za wanachama.
Jonatahan alitoa wito  kwa sekretarieti kufanya kazi kwa pamoja ili chama kiweze kufikia malengo waliyojiwekea ili kuwaunganisha kwa pmoja wafanyakazi ili waweze kuwajibika vizuri.
Katika uchaguzi huo ambao ulisimamiwa na katibu wa chama hicho Kassim Matewele ambaye alimtangaza Msimbe kuwa mshindi kwa kura (41) ambaye alimshinda Abimelick Magoma aliyepata kura (18).
Kwenye nafasi ya wajumbe wa kamati ya utendaji mkoa nafasi mbili nafasi ya  Viwanda ni Hasan Kindagule aliyepata kura (35) na Msaidizi wake Athuman Makonga kura (22), upande wa Biashara Shukuru Goso aliyepata kura (32) na msaidizi wake Joyce Kalumuna kura (29).
Kwa upande wa Fedha Furaha Mbwambo  alishinda kwa kupata kura (45) na msaidizi wake ni Zaituni Mtoro aliyepata kura (41), Huduma na ushauri mshindi alikuwa ni Tumaini Kivuyo na msaidizi wake Kandrid Ngowi ambaye alipata kura (35).
Waliochaguliwa Mkutano Mkuu Kanda, Viwanda ni Masiku Serungwi aliyepata kura (35), biashara ni Kamatanda Kamatanda aliyepata kura (57), Fedha Furaha Mbwambo aliyepata kura (60), kwa upande wa huduma na ushauri mshindi alikuwa ni Kandrid Ngowi aliyepata kura (40).
Wajumbe wa mkutano mkuu Taifa upande wa Viwanda  mshindi ni Athuman Makonga kura (59), Biashara ni Shukuru Ngoso kura (58), Fedha Zaituni Mtoro kura (57) na huduma na Ushauri Margareth Chaleo kura ( 45).
Mwisho.

Na John Gagarini, Mkuranga

KIJIJI cha Mwanambaya Kata Mipeko wilaya ya Mkuranga kimewaomba wadau mbalimbali wa maendeleo kuwasaidia kupata kiasi cha  milioni 150 kwa ajili ya mradi wa kuvuta maji kutoka kijiji jirani cha Kisemvule.

Akizungumza na waandishi wa habari msemaji wa kijiji hicho Abubakar Sisaga alisema kuwa wanakabiliwa na changamoto kubwa ya maji hivyo wameanza mchakato wa kuvuta maji kutoka kijiji cha Kisemvule.

Sisaga alisema kuwa awali walikuwana wazo la kuchimba visima lakini kutokana na uwezo kutokana na gharama za uchimbaji kisima kuwa ni kubwa.

“Tunawaomba wadau mbalimbali wa maendeleo wajitokeze kutusaidia tufanikishe zoezi hilo la uvutaji maji ili kukabiliana na changamoto hiyo ya ukosefu wa maji kwani kwa sasa wanatumia maji ya visima vifupi ambavyo kipindi cha kiangazi hukauka,” alisema Sisaga.

Alisema kuwa endapo watafanikiwa kupata maji yatawasaidia kuweza kutumia muda wao kwa ajili ya kufanya shughuli za maendeleo tofauti na sasa wanatumia muda mwingi kuhangaika na maji jambo ambalo ni changamoto kubwa.

“Mbali ya changamoto ya maji kijiji kinakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo ni za kawaida lakini wanakijiji wanajitahidi kuzitatua kadiri ya uwezo wao hivyo tunaomba wadau mbalimbali wajitokeze kutuunga mkono kwenye jitihada zetu za kuleta maendeleo,” alisema Sisaga.

Aidha alisema kuwa wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo ili kwa pamoja waweze kufanikiwa na kujikwamua na hali duni na kujiletea maendeleo.

Naye Mwenyekiti wa kijiji hicho Leyla Chabruma alisema kuwa wana ushirikiano mkubwa na wadau wa maendeleo ambao wanashirikiana na wananchi kwa ujumla hali inayoleta maendeleo ndani ya kijiji hicho ambacho kinategemea mapato yake kwa mauzo ya bidhaa mbalimbali ikiwemo mashamba, viwanja na vitu mbalimbali.

MWISHO.

Na John Gagarini, Kibaha

BAADHI ya wafanyabiashara na wasafiri wanaotumia kituo cha mabasi cha Maili Moja wameiomba Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani kuhakikisha wanatatua tatizo la taa kutowaka kwa zaidi ya mwezi mmoja sasa na kuwasababishia usumbufu mkubwa wataumiaji wa stendi hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari moja ya wafanyabiashara wanaofanya biashara kwenye stendi hiyo nyakati za usiku Said Pengo alisema kuwa wamekuwa wakifanya biashara kwenye mazingira magumu kwenye eneo hilo.

Pengo alisema kuwa ukosefu wa taa hapo stendi ni changamoto kubwa sana inayowafanya kushindwa kufanya biashara kwa vizuri kutokana na kuzingirwa na giza.

“Tunaiomba Halmashauri yetu itusaidie tuweze kupatiwa huduma ya taa kwani taizo la ukosefu wa taa linatusababishia usumbufu mkubwa na tunashindwa kufanya biashara zetu kwa uhuru kutokana na giza linalokuwa linatanda,” alisema Pengo.

Alisema kuwa ni hatari kwa hali ya usalama wao pamoja na wateja wanaotumia eneo hili la stendi ya Maili Moja ambayo inatumiwa na watu wengi.

Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa wa Maili Moja Chichi Mkongota alikiri juu ya ukosefu wa umeme kwa kipindi hicho na kusema tayari alishatoa taarifa kwa mamlaka husika juu ya tatizo hilo.

Mkongota alisema kuwa alipotoa taarifa Halmashauri aliambiwa kuwa wanafanya utaratibu wa kutatua tatizo hilo ikiwa ni pamoja na kuangalia namna ya kupata taa za muda ili kukabiliana na tatizo hilo.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Jenifa Omolo alisema kuwa tatizo lililopo ni kubwa kidogo kwani taa zilizowekwa zimeharibika na wanafanya mchakato wa kupata nyingine.

Omolo alisema taa zote 16 zilizopo hapo stendi zimeharibika ambapo gharama zake pamoja na kufungwa ni kiasi cha shilingi milioni 18 ambazo wanazitafuta kwa ajili ya kuzifunga.

“Tunafikiria kwa sasa tufunge taa za kawaida kwani hizo zilizopo ziliharibika na si mara ya kwanza kuzifunga kwani kila wakati zimekuwa zikiharibika,” alisema Omolo.

Aidha alisema kuwa wanahangaika kutafuta fedha hizo ili kuondoa changamoto hiyo ambayo imekuwa kero hata kwa wakala wanaokusanya ushuru wa stendi kutokana na usalama kuwa mdogo.

Mwisho.







Monday, August 10, 2015

CCM WATAKIWA KUACHA MAKUNDI

 Na John Gagarini, Kibaha
WANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Kibaha Mjini wametakiwa kuacha tabia ya kukumbatia makundi mara baada ya uchaguzi wa ndani kumalizika kwani yanasababisha chama kushinda kwa tochi.
Hayo yalisemwa juzi na mwenyekiti wa CCM Kibaha Mjini Maulid Bundala wakati akiwanadi watia nia waliojitokeza kuwania kuchaguliwa na chama hicho kupeperusha bendera kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu.
Bundala alisema kuwa makundi hayo yanachangia kwa kiasi kikubwa chama kushindwa kutokana na mshikamano na ushirikiano kutokuwepo kwenye chaguzi mbalimbali ambazo zinahusisha vyama vingi vya siasa.
“Kipindi hichi ni kigumu sana kuwa na kundi siyo tatizo lakini mara atakapopatikana mgombea mmoja wa ubunge makundi yanatakiwa kwisha na kubakia kundi moja tu la CCM ambalo linatakiwa lipambane na wapinzani,” alisema Bundala.
Alisema kuwa kwanini chama kishindwe kwa mbinde kwa ushindi wa tochi wakati kina wanachama wengi ukilinganisha na vyama vya upinzani lakini inaonekana kushindwa kunatokana na kukumbatiwa kwa makundi hayo.
“Makundi yanatakiwa yaishe mara uteuzi wa mwanachama mmoja ambaye atawakilisha chama kwenye uchaguzi tatizo linguine ni wanachama kumpenda mtu badala ya kukipenda chama na kuachana na tabia ya kuwasema vibaya wagombea kwani wote ni Wanaccm,” alisema Bundala.
Aliwataka wanaccm ambao wanasifa ya kupiga kura za maoni za kuchagua mbunge kwenye kura za maoni wanapaswa kuwa hai kwa kulipia kadi za chama, wawe wameorodheshwa kwenye daftari la tawi na wawe na kadi ya kupigia kura.

Mwisho.   

HABARI ZA PWANI


Na John Gagarini, Bagamoyo
KATIKA kukabiliana na changamoto ya huduma ya afya kwa wananchi wa kijiji cha Kidomole Kata ya Fukayosi, wilaya ya Bagamoyo, mkoa wa Pwani, wamejenga zahanati kwa thamani ya 58.7
Akizungumzia kuhusu ujenzi huo ofisa mtendaji wa Kijiji hicho Sef Mayala alisema kuwa ujenzi wa zahanati hiyo unaondoa adha ya kufuata huduma ya afya nje ya kijiji hicho.
Mayala alisema kuwa katika kufanikisha ujenzi huo kila mwananchi wa Kijiji hicho alitoa kiasi cha shilingi 5,000 kabla ya kuungwa mkono na wadau wengine na kufanikiwa kukamilisha ujenzi huo.
“Mradi huu wa ujenzi wa zahanati uliibuliwa na wananchi kupitia mkutano ulioitishwa na uongozi wa serikali ya kijiji ambao ulianza mwaka 2009 na kukamilika mwaka huu 2015,” alisema Mayala.
Alisema kuwa kuwa katika kuhakikisha ujenzi wa zahanati hiyo unakamilika kwa wakati Halmashauri kupitia ruzuku ya maendeleo ya serikali ilichangia pia kwenye ujenzi huo.
“Ujenzi wa zahanati hii umetokana na utekelezaji wa sera ya afya ya kijiji kuwa na zahanati na pia kuwepo kwa ongezeko la watu katika kijiji cha Kidomole na uhitaji mkubwa wa huduma za afya,,” alisema Mayala.
Aidha alisema kwenye ujenzi huo nguvu za wananchi wamechangia kiasi cha shilingi milioni 45.9, wadau mbalimbali shilingi. milioni 2.8, ruzuku ya serikali shilingi milioni 10 huku Mbunge jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akichangia bati 129.
Diwani wa kata ya Fukayosi Ally Issa aliwashukuiru wananchi wa kijiji hicho na Kata kwa ujumla kwa kuwa na mwamko wa kimaendeleo kwa kuchangia ujenzi wa zahanati hiyo hadi kukamilika.
Issa alisema kuwa anawashukuru wananchi kwa kujitolea pia kwani niaba ya viongozi ngazi mbalimbali anawashukuru kwa michango yao ya hali na mali kwa kujitolea kwa ajili ya shughuli za maendeleo kwenye Kijiji na kata kwani zahanati hiyo ni faida kwa wanancho wote.
Mwisho 
Na John Gagarini, Kibaha
WAUMINI wa Kanisa la Angikana na Watanzania kwa ujumla wametakiwa kutunza vitambulisho vyao vya kupigia kura ili waweze kushiriki kikamilifu zoezi la upigaji kura kwa ajili ya kuwapata viongozi mbalimbali akiwemo Rais atakayeongoza Taifa letu kwa amani na utulivu.
Aidha kanisa linaamini kuwa kutokana na baadhi ya watu kufunga kwa ajili ya kuombea uchaguzi huo kuwa wa amani ni dhahiri Watanzania wasiwe na wasiwasi wakati wa uchaguzi kikubwa ni kuepukana na watu wanaohamasisha uvunjifu wa amani.
 Hayo yalisemwa na Mchungaji wa Kanisa la  Anglikana Tumbi wilayani Kibaha Mkoani Pwani Methew Mwela kwenye baraza  la Halmashauri  kuu ya kanisa hilo lililoketi kwaajili ya kujadili maswala ya maendeleo ya Kanisa hilo na waumini  wake ambapo alisema kuwa kinachotakiwa kufanywa na waumini hao ni kutunza  vitambulisho vyao vya mpiga kura na kushiriki zoezi hilo kikamilifu siku itakapofika.
"Nawakumbusheni waumini na Watanzania kwamba dhambi ya manung'uniko ni mbaya sana na hata kwenye vitabu vitakatifu imeandikwa kuwa iliwatafuna wana wa Israel hivyo kama mtakaa bila kwenda kupiga kura kisha akachaguliwa kiongozi  ambaye hamkupenda achaguliwe na mkaanza kunung'unika mtakuwa mnajitafutia dhambi,"alisema Mch Mwela.
Mch Mwela alisema kuwa wanachopaswa kufanya hivi sasa waumini hao ni kutunza vitambulisho vyao vya mpiga kura na siku ikifika wafike mapema kwaajili ya kupiga kura na kwamba ili kuwawezesha waumini wake kushiriki kikamilifu ibada ya siku hiyo itaanza mapema na kuisha mapema .
"Ili kuhakikisha wote mnapata haki yenu ya msingi  ya kupiga kura ibada ya tarehe hiyo ya siku ya uchaguzi itaanza mapema hapa kanisani kwetu ili waumini wangu wote wenye kadi ya mpiga kura aende akapige kura ili kuchagua viongozi anaowapenda kadri Mungu atakavyomuonyesha,”alisema Mch Mwela.

Aliwashauri waleambao kwa bahati mbaya ama kwa sababu mbalimbali walishindwa kufanikiwa kupata kadi za mpiga kura kuwa watulivu na wanayopaswa kufanya ni kumuomba Mungu ili viongozi watakaochaguliwa waiongoze nchi kwa haki na kweli pasipo na upendeleo wa aina yoyote ili taifa liendelee kuwa na amani.

“Nawaomba Watanzania kuondoa hofu na mashaka juu ya kuwepo na uwezekano wa kuzuka vurugu kabla na baada ya uchaguzi huo mkuu nchini kwani wanachopaswa kutambua ni kuwa mungu amesha mchagua Rais atakayewaongoza watu wake,” alisema Mch Mwela.

MWISHO

Na John Gagarini, Kibaha

ABIRIA wanaosafiri kutumia vyombo mbalimbali vya vya moto mkoani Pwani wametakiwa kuacha tabia kuwashabikia madereva wanaoendesha mwendo wa kasi wakati wakisafiri kwani ni hatari kwa maisha ya wasafiri.

Wito huo ulitolewa mwishoni mwa wiki na mgeni rasmi kwenye kilele cha wiki nenda kwa usalama barabarani kimkoaFlorence Mwenda iliyofanyika mjini Kibaha na kusema kuwa kuwa pamoja na juhudi zinazofanywa na Jeshi hilo kuhakikisha ajali za barabarani zinapungua bado kuna changamoto mbalimbali hususa kwa  upande wa abiria ikiwemo kuhamasisha madereva kwenda na mwendo kasi wakiwa safarini.
Mwenda ambaye ni ofisa wa jeshi la polisi alisema kuwa kikosi cha usalama barabarani kimeendelea kutoa elimu kwa watumiaji wa barabara juu ya matumizi sahihi ya barabara lakini kumekuwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na baadhi ya abiria kushangilia mwendo wa kasi.

“Vitendo kama hivi na vingine havipaswi kufumbiwa macho kwani vinahatarisha usalama wa abiria pamoja na uharibifu wa mali lakini endapo madereva watazingatia matumizi sahihi ya barabara itasaidia kupunguza ajali ambazo zimekuwa ni moja ya vyanzo vikuu vya vifo pamoja na ulemavu,” alisema Mwenda.

Aidha alisema kuwa kikosi cha usalama barabarani kimetoa  elimu ya matumizi sahihi ya   barabara  kwa wanafunzi  wa shule za msingi na sekondari  mkoani humo wapatao 1,568 lengo likiwa ni kuielimisha jamii na makundi mbalimbali   juu ya matumizi salama ya barabara ili kupunguza ajali zisizokuwa za lazima.

“Makundi mbalimbali yamepatiwa elimu hiyo ikiwa ni pamoja na madereva wa magari wapatao 905,waendesha pikipiki1,220 na abiria 16,802 wa magari  ya aina mbalimbali ambapo zoezi hilo litakuwa endelevu  hali itakayosaidia  kupunguza ajali ambazo zimekuwa zikigharimu maisha na mali,” alisema Mwenda.

Alibainisha kuwa kamati ya usalama barabarani  ya Mkoa huo pia ilifanya mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na huduma ya  upimaji wa macho bure kwa wananchi wa kawaida na madereva wa vyombo vya moto.

MWISHO











Thursday, July 30, 2015

HABARI ZA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
MGOMBEA Ubunge anayewania kuteuliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwenye Jimbo la Kibaha Mjini Abdulaziz Jad Maarufu kama Mwarabu amesema kuwa wana CCM wasichague mbunge ambaye ni sawa na mfadhili kwani atakwamisha shughuli za maendeleo katika Jimbo hilo.
Jad aliyasema hayo juzi mjini Kibaha kwenye mkutano wa wagombea wa ubunge wa CCM kuomba kura kwenye kata ya Maili Moja na kusema kuwa baadhi ya wabunge ni sawa na wafadhili ambao hutoa misaada kwa msimu.
Alisema kuwa wabunge wa namna hiyo hujitokeza wakati wa vipindi vya uchaguzi lakini wakishachaguliwa na uchaguzi ukipita hawaonekani tena kwani maendeleo yake yatakuwa ya msimu na si endelevu.
“Sisi wakazi wa Jimbo la Kibaha tunahitaji Mbunge wa kutuletea maendeleo na si mfadhili ambaye anatoa misaada kwa msimu hasa ule wa uchaguzi na mkishamchagua hamuoni tena hadi baada ya miaka mitano,” alisema Jad.
Aidha alisema kuwa wabunge wa namna hiyo wanaleta maendeleo ya msimu lakini endapo watamchagua yeye atawaletea maendeleo endelevu na si ya msimu kama wanavyofanya baadhi ya wafadhili.
“Baadhi yao ni wafadhili lakini wanavaa kofia ya uongozi hawa hawatufai lakini mkinichagua mimi nitawaletea maendeleo enedelevu na si yale ya msimu ambayo yametudumaza,” alisema Jad.
Alibainisha kuwa endapo ilani ya chama itatekelezwa kwa ufanisi basi maendeleo yatapatikana kwani inajibu changamoto zilizopo kwenye sekta zote za maendeleo pia aliahidi kuondoa makundi yaliyojitokeza katika kipindi hichi cha uchaguzi.
Mwisho.
Na John Gagarini, Bagamoyo
SERIKALI imeombwa kuajiri watu wenye taaluma ya sheria kwenye mabaraza ya ardhi ili kupunguza migogoro ya ardhi iliyopo kwenye maeneo mengi ya miji na vijiji.
Hayo yalisemwa Bagamoyo na Raya Fereji makamu mwenyekiti wa asasi isiyo ya kiserikali ya Mkombozi wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wakati wa mafunzo ya sheria ya ardhi kwa waandishi wa habari na wadau wa ardhi wilayani humo.
Fereji alisema kuwa mabaraza ya ardhi yanaendeshwa na watu wasiokuwa na taaluma ya sheria wakati masuala yenyewe ni ya kisheria hali ambayo inasababisha migogoro ishindwe kwisha.
“Mabaraza haya yanaundwa na watu maarufu kwenye maeneo yao lakini hawana taaluma ya kisheria licha ya kuwa utatuzi wa migogoro ya ardhi unakwenda kisheria,” alisema Fereji.
Alisema kuwa ili migogoro hiyo ipungue hakuna budi kuwatumia watu wenye taaluma ya sheria ili kukabiliana na migogoro hiyo am,bayo imekithiri.
“Hata kama itashindwa kuwatumia watu wenye taaluma hiyo basi iyapatie mafunzo ya sheria mabaraza hayo kwani uzoefu unaonyesha kuwa maamuzi mengi yanayotolewa ya utatuzi wa migogoro ya ardhi inakuwa na kasoro nyingi,” alisema Fereji.
Kwa upande wake mwanasheria wa Kujitegemea Boka Lyamuya alisema kuwa migogoro mingi ya ardhi inashindwa kutatuliwa kutokana na baadhi ya watendaji  kwenye maeneo hayo kupindisha sheria.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WAGOMBEA wa nafasi za Ubunge na Udiwani mkoani Pwani wametakiwa kuweka ajenda ya kuhifadhi misitu kama sehemu ya kampeni zao za kuomba nafasi za uongozi.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha ofisa Mradi wa  Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG) Yahaya Mtonda alisema kuwa misitu hiyo endapo itaundiwa sera nzuri itasaidia kurejesha uoto wa asili ambao umetoweka kutokana na uharibifu wa mazingira.
Mtonda alisema kuwa misitu hiyo imekuwa ni chanzo kikuu cha upatikanaji wa mvua pamoja na hali ya hewa nzuri pia kukabiliana na mmomonyoko wa ardhi hivyo wawania nafasi za uongozi lazima watoe kipaumbele cha jinsi gani ya kukabiliana na hali hiyo ya uharibifu wa mazingira.
“Mabadiliko ya tabianchi  yanatokana na uharibifu wa misitu hivyo wawania nafasi za uongozi lazima wabebe suala hilo kama ajenda muhimu wanaponadi sera zao ili kuokoa misitu ya asili na ile isiyo ya asili,” alisema Mtonda.
Aidha alisema kuwa moja ya misitu ya asili hasa ile iliyojirani na Jiji la Dar es Salaam ambayo ni Kazimzumbwi na msitu wa Pugu iliyopo wilayani Kisarawe ni muhimu kwani ndiyo inayochuja hali ya hewa na kuifanya iwe nzuri.
“Kama mnavyofahamu Jiji la Dar es Salaam lina zalisha hewa mbaya kutokana na magari, viwanda na shughuli mbalimbali za kimaendeleo hivyo misitu hii ni kama mapafu ya kupumulia hivyo kutufanya tupate hewa nzuri lakini endapo isingekuwepo basi athari za kiafya zingekuwa kubwa sana,” alisema Mtonda.
Aliwataka wananchi kuwauliza wagombea kuwa wameweka mikakati gani ya kuhifadhi misitu na utunzaji wa mazingira ili kukabiliana na uvunaji holela wa misitu kwenye mkoa huo.
Mwisho.   
  Na John Gagarini, Kibaha
WAKAZI wa Kijiji cha Minazimikinda kata ya Ruvu kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha mkoani Pwani wamemwomba Waziri wa Ardhi na Makazi Wliam Lukuvi kutembelea Kijiji chao ili kukabiliana na mgogoro wa muda mrefu baina yao na Kijiji cha Kwala.
Moja ya wakazi wa Kijiji hicho Mohamed Palu alisema kuwa mgogoro huo ni wa muda mrefu na umekuwa ukiwachukulia muda mrefu kuutatua bila ya mafanikio hivyo kushindwa kufanya shughuli za maendeleo.
Palu alisema kuwa mgogoro huo umesababisha shughuli za kimaendeleo katika eneo hilo kukwama kutokana na kila upande kudai eneo hilo ni la upande mwingine.
“Tumetumia njia nyingi za kusuluhisha mgogoro huu lakini hadi sasa hakuna hatua zozote zilizofikiwa kuumaliza mgogoro huo hivyo tunaona endapo waziri atakuja anaweza kuutatua,” alisema Palu.
Alisema kuwa kamati ya Bunge inayoshughulikia migogoro ya ardhi ilifika Kijijini hapo mwezi Machi mwaka huu lakini hadi sasa hakuna taarifa yoyote juu ya suluhu ya mgogoro huo.
“Mgogoro huu na mingine iliyopo Kijijini ni moja ya changamoto kubwa zinazotukabili hivyo endapo waziri atakuja atatusaidia kuitatua na hivyo itasaidia wananchi kuendelea na shughuli za maendeleo,” alisema Palu.
Aidha alisema kuwa baadhi ya viongozi wa Vijiji wamekuwa wakichangia migogoro hiyo kutokana na kutozingatia ramani za vijiji hivyo hali inayosababisha kuwa na migogoro hiyo.

 Baadhi ya wanachama wa CCM kata ya Maili Moja wakiwasikiliza watia nia wa CCM walipokuwa wakimwaga sera jana mjini Maili Moja
Mwisho.    
Wawania nafasi ya Ubunge kupitia chama cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Kibaha Mjini mkoani Pwani kuanzia kushoto Rashid Bagdela Iddi Majuto, Abdulaziz Jad, Silvestry Koka na Rutatina Rugemalila

Tuesday, July 28, 2015

LIGI NETBALL PWANI KUFANYIKA AGOSTI 3 MWAKA HUU

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA Cha Mpira wa Pete mkoani Pwani kinatarajia kufanya mashindano ya mchezo huo Agosti 3 mwaka huu ili kupata timu itakayopanda ligi daraja la pili Taifa itakayowakilisha mkoa huo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mwenyekiti wa chama hicho Fatuma Mgeni alisema kuwa jumla ya timu 14 zitachuana kwenye michuano hiyo itakayofanyika kwenye uwanja wa Bwawani maili Moja Kibaha.
Mgeni alisema kuwa wanatarajia kila wilaya itatoa timu mbili ili mashindano yawe na uhalisia wa mkoa kwa kushirikisha timu za wilaya hizo.
“Tayari tumeshawapa taarifa wilaya zote waandae timu ili ikifika wakati walete timu zao ziweze kuwakalisha wilaya zao nah ii ni moja ya kuhamasisha mchezo huo maeneo mbalimbali ya mkoa,” alisema Mgeni.
Alisema kuwa awali mashindano hayo yalikuwa yafanyike Julai 10 mwaka huu lakini kutokana na sababu ambazo zilishindwa kuzuilika ilibidi mashindano hayo yasogezwe mbele.
“Maandalizi yako vizuri na tayari timu zimeshaplekewa taarifa za kushiriki mashindano hayo ambayo yatapandisha timu moja kwenda daraja la pili Taifa japo kuna uwezekano wa kupandisha timu mbili ila hilo bado halijawa wazi sana,” alisema Mgeni.
Aidha alizitaka timu zinazotarajiwa kushiriki michuano hiyo kujiandaa kikamilifu ili kushirikia michuano hiyo ili mkoa uweze kupata timu nzuri.
Mwisho.

     

CCM JITOKEZENI KWA WINGI KWENYE KURA ZA MAONI NA UCHAGUZI MKUU

Na John Gagarini, Kibaha
WANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Kibaha Mjini wilayani Kibaha mkoani Pwani wametakiwa kujitokeza kwa wingi ili kukipigia kura chama hicho kwenye uchaguzi mkuu Oktoba mwaka huu na si kujitokeza kwa wingi kwenye kura za maoni pekee.
Hayo yalisemwa na katibu wa CCM jimbo la Kibaha Mjini Abdala Mdimu wakati akiwanadi wagombea watano wa chama wanaowania kuteuliwa Ubunge wa Jimbo hilo kwenye kata ya Picha ya Ndege na Lulanzi.
Mdimu alisema kuwa wanachama wanaotarajiwa kupiga kura za maoni watakuwa wengi ikiwa na maana kwenye uchaguzi wa ndani ya chama lakini nje ya chama yaani uchaguzi mkuu wanachama hawajitokezi kwa wingi.
“Sasa tubadilike kwani CCM ndicho chama chenye wanachama wengi ikilinganishwa na vyama vingine lakini utashangaa wapinzani wanashinda kwa kura nyingi ambazo nyingine zinatoka humuhumu huku wengine wakiwa hawajitokezi kupiga kura lakini kura ndani ya chama ni nyingi sana,” alisema Mdimu.
Alisema kuwa wanachama wote ambao wamekidhi vigezo wanapaswa kujitokeza kupiga kura kwa wingi ndani ya chama na kwenye uchaguzi mkuu kwani kutojitokeza kwenye uchaguzi mkuu utasababisha ushindi kuwa mdogo.
“Tunataka ushindi wa kishindo kama ilivyokuwa kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambapo mlijitokeza kwa wingi na chama kushinda kwa kishindo tunataka wembe huo huo muuendeleze kwani ushindi uko dhahiri,” alisema Mdimu.
Aidha alisema kuwa Wanaccm hawapaswi kuimba wimbo wa ushindi huku hawafanyi kazi kwani wanatakiwa kufanya kazi ili baadaye waje kuimba wimbo wa ushindi kwani moja wapo kati ya wanaowania nafasi ya kuwakilisha chama nafasi ya ubunge ni wazuri.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MUWANIA Ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Kibaha Mjini wilayani Kibaha mkoani Pwani Rugemalila Rutatina amesema kuwa endapo atateuliwa atakuwa kiongozi na si mtawala.
Aliyasema hayo juzi kwenye kata ya Picha ya Ndege mjini Kibaha wakati akiomba kura kwa wanachama wa matawi ya kata hiyo na kusema kuwa uongozi bora ndiyo utakaowaletea maendeleo wananchi wa Jimbo hilo.
Rutatina ambaye ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM NEC kutoka Jimbo hilo alisema kuwa nafasi hiyo ni uongozi wa kuonyesha njia na si kuwa mtawala kwani mtawala yeye ni kutumia nguvu na kuelekeza pasipo yeye kuwajibika.
“Kiongozi ni kuwajibika wewe mwenyewe na kuwaonyesha njia watu unaowaongoza lakini mtawala yeye hana muda wa kutumikia wananchi zaidi ya kuamrisha jambo ambalo halifai kwani si shirikishi kwa wananchi,” alisema Rutatina.
Alisema kuwa ilani inajibu masuala yote ya maendeleo kwani imegusa sekta zote ikiwemo afya, elimu, ardhi, barabara, umeme, maji, mawasiliano na huduma zote za kijamii.
“Endapo mtanichagua nitazingatia mambo matatu ambayo ni ushirikishaji wananchi, ardhi, siasa safi na uongozi bora naamini katika haya yatasaidia kukabiliana na changamoto zilizopo ili kuwaletea maendeleo,” alisema Rutatina.
Wagombea wengine wanaowania nafasi hiyo ya kukiwakilisha chama kwenye kinyanganyiro cha Ubunge kwenye Jimbo hilo ni Silvestry Koka anayetetea kiti hicho, Abdulaziz Jab, Rashid Bagdela na Idd Majuto.
Mwisho 

Friday, July 24, 2015

VULLU, MGALU WATESA UBUNGE VITI MAALUMU PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
 MBUNGE wa Viti Malumu Zainab Vulu ameshinda kwenye uchaguzi wa Viti Maalumu kupitia Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) mkoa wa Pwani kwenye uchaguzi kwa kupata kura 342.
Uchaguzi huo ambao ulifanyika juzi mjini Kibaha ulishuhudia Mbunge mwingine wa viti maalumu wa mkoa huo Subira Mgalu naye alifanikiwa kushinda kwa kujipatia kura 296.
Nafasi ya tatu ilichukuliwa na Nancy Mtalemwa aliyejinyakulia kura 145 huku Alice Mwangomo kura 45, Dk Zainab Gama kura 43, huku Katibu wa CCM mkoa wa Pwani Joyce Masunga na wengine watano wakiambulia kura saba kila mmoja.
Mbunge wa zamani wa Jimbo la Kibaha Mjini Dk Zainab Gama alishinda kupitia mashirika yasiyo ya Kiserikali (NGO) ambaye alijinyakulia kura 394 akifuatiwa na Elizabeth Maya 37 na Esta Juma kura 15.
Nafasi ya ubunge kupitia nafasi ya ulemavu mshindi alikuwa ni Sita Sakawa aliyepata kura 262 ambaye alimshinda Tungi Mwanjala aliyepata kura 178, kwa upande wa ubunge wafanyakazi Hawa Chakoma alishinda kwa kupata kura 354 akimshinda Julieth Mjale aliyepata kura 82.
Upande wa Vyuo vikuu mshindi alikuw ani Dk Alice Kaijage ambaye hakuwa na mpinzani alipata kura 453 ambapo jumla ya wapiga kura walikuwa zaidi ya 450.
Moja ya wasimamizi wa uchaguzi huo mkuu wa mkoa wa Pwani Evarist Ndikilo ambaye alitangaza matokeo hayo alisema kuwa uchaguzi huo umefanyika kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa na chama.
Ndikilo alisema kuwa uchaguzi ulikwenda vizuri na kutokana na ukomavu wa wagombe ahakukutokea matatizo yoyote kwani kila upande uliridhika na matokeo hayo bila ya kupinga.
Kwa upande wake Zainab Vullu aliwashukuru wapiga kura kwa kuweza kumchagua kuwa mwakilishi wao na kusem akuwa atahakikisha anakabiliana na changamoto hususan kwa akinamama kwa kuwawezesha kwa mafunzo ya ujasiriamali.
Mwisho.