Friday, November 7, 2014

MAHIZA AKIMBIA OFISI KUKAMILISHA UJENZI WA MAABARA NA KUKU MILIONI 20 KUNUSURIKA NA KIFO

> Na John Gagarini, Bagamoyo
>
> SUALA la Maabara kwa shule za Sekondari za Kata limeingia kwenye hatua
> nzito baada ya mkuu wa Mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza kuiacha ofisi yake na
> kuhamia Wilaya ya Bagamoyo ili kuhakikisha agizo la Rais Dk Jakaya Kikwete
> la kila wilaya iwe imekamilisha ujenzi huo ifikapo Novemba 30 mwaka huu.
>
> Sambamba na hilo mkuu huyo amewataka wakuu wa idara wa Wilaya hiyo kila
> mmoja kutokaa ofisini na kuchagua kata ya kwenda ili kusimamia ujenzi huo
> hadi ujenzi wa maabara ukamilike.
>
> Akizungumza juzi kwenye kikao cha baraza la Madiwani kilichofanyika mjini
> Bagamoyo Mahiza alisema kuwa ujenzi wa maabara kwenye wilaya hiyo bado
> zoezi hilo haliko vizuri hivyo lazima itumike nguvu ya ziada kufanikisha
> zoezi hilo.
>
> “Kuanzia sasa najua nitaanzia kata gani lakini nahamia Bagamoyo na wakuu wa
> idara kila mmoja tukitoka hapa ataniambia atakuwa kata gani ili tuanze
> usimamizi kwani bila ya kufanya hivi muda utaisha na mambo yatakuwa
> magumu,” alisema Mahiza.
>
> “Kuanzia sasa vikao vya madiwani havitakuwepo kilichobaki wote tuende
> kwenye ujenzi wa maabara na kama mtu anaona hawezi kuwajibika aondoke
> mapema asije akatuharibia mipango yetu ya maendeleo kwani watoto ni wetu,”
> alisema Mahiza.
>
> Mahiza alisema kuanzia sasa hivi hakuna cha mahafali wala sherehe wimbo
> uliopo ni maabara kwa shule zetu za sekondari kwani baadhi ndo wako kwenye
> msingi je ujenzi utakamilika kwa wakati jambo ambalo linatia mashaka.
>
> “Baadhi ya watendaji hawana haraka na kusababisha shughuli kwenda taratibu
> kuanzia sasa hapa ni mwendo wa kufanya kazi kwani tusipokuwa makini muda
> utaisha hatujakamilisha itakuwa haipendezi,” alisema Mahiza.
>
> Aidha alisema kuwa wakuu wa wilaya na mikoa waliitwa Dodoma na Rais na
> kutakiwa wawe wamekamilisha ujenzi huo ifikapo Novemba 30 mwaka huu na wao
> walimwahidi kuwa watakamilisha ujenzi kipindi hicho.
>
> Kwa upande wake mwenyekiti wa Halmashauri ya Bagamoyo Shukuru Mbato alisema
> kuwa agizo hilo wamelipokea na watahakikisha wanakamilisha ujenzi wa
> maabara hizo kwa muda uliopangwa.
>
> Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

> CHANJO mpya ya ugonjwa wa Mdondo kwa kuku ya ITA NEW itasaidia kupunguza
> vifo vya kuku wa kienyeji zaidi ya milioni 20 wanaokufa kwa mwaka kutokana
> na ugonjwa huo.
>
> Tayari dawa hiyo imeshapitishwa na mamlaka ya vyakula na dawa (TFDA) kwa
> ajili ya matumizi kwa kuku ambapo Tanzania ina jumla ya kuku wapatao
> milioni 60.
>
> Akizungumza mjini Kibaha makamu mwenyekiti wa chama cha waganga waisidizi
> wa mifugo kitaifa (TAVEPA) ambaye pia ni mwakilishi wa kampuni ya madawa ya
> Laprovet Tanzania Ephrahim Massawe alisema kuwa chanjo hiyo ni ya muda
> mrefu.
>
> “Chanjo hiyo inawakinga kuku kwa kipindi cha mwaka mmoja tofauti na chanjo
> nyingine ambazo huisha nguvu kila baada ya miezi mitatu kabla ya kuchanjwa
> chanjo nyingine,” alisema Massawe.
>
> Alisema kuwa ugonjwa huo ni mbaya kwa kuku ambao unaua kuku kwa muda mfupi
> na kusababisha hasara kubwa kwa wafugaji lakini kutokana na kupatikana
> chanjo hii itasaidia kupunguza vifo vya kuku kutokana na ugonjwa huo
> maarufu kama Kideri
>
> “Ugonjwa huo ambao hutokea kwa misimu ya mvua zinapoanza na zinapoishia
> ulikuwa ni tishio kubwa kwa wafugaji kwani ulifikia hatua ya kuua hata nusu
> ya idadi ya kuku wa kienyeji hapa nchini,” alisema Massawe.
>
> Aidha alisema kuwa kupatikana kwa chanjo hiyo kutasaidia kuongeza pato,
> lishe na kukuza uchumi wa kaya ambazo zifafuga kuku hasa vijijini ambapo
> mikoa inayoongoza kwa ufugaji wa kuku hao ni Singida, Dodoma, Shinyanga na
> Morogoro.
>
> Mwisho.
>

Friday, October 24, 2014

POLISI WAKAMATA LUNDO LA SILAHA, FEDHA NA VITU MBALIMBALI

Na John Gagarini, Kibaha
WATU watatu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi wamekamatwa wakiwa na silaha aina ya Short Gun yenye namba 07019302 ikiwa na risasi nane.
Hayo yamesemwa na kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alipoongea na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Mohamed Kalipa (20) dereva wa Bajaji mkazi wa Mbagala Rangi Tatu, Salum Shekivui (20) mkazi wa Buza na Seuli Lucas (18) makazi wa Mbagala Rangi Tatu Jijini Dar es Salaam.
Kamanda Matei alisema kuwa watuhumiwa hao walikamatwa Oktoba 20 mwaka huu majira ya saa 2:30 huko Mlandizi wilaya ya Kibaha.
“Mbali ya silaha pia walikutwa na fedha taslimu kiasi cha shilingi milioni 6,611,800, vocha mbalimbali za simu zenye thamani ya shilingi milioni 2,185,500 na simu za mkononi sita za aina mbalimbali ambazo thamani yake bado hazijafahamika,” alisema Kamanda Matei.
Aaidha alisema kuwa watuhumiwa hao wanadaiwa kuwa walifanya tukio la unyanganyi wa kutumia silaha huko Kijiji cha Mbwewe wilaya ya Bagamoyo kwenye duka la Twaha Mbuta siku ya Oktoba 19 saa 1:30 usiku na kupora kiasi cha shilingi milioni 30,000,000.
“Baada ya kukamatwa walimtaja mtuhumiwa mwenzao ambaye  walikuwa wakishirikiana naye Samwel Joseph mkazi wa Kongowe Kibaha ambapo baada ya upekuzi walimkuta na risasi sita za Short Gun ambazo alikuwa akizimiliki bila ya kibali hata hivyo mtuhumiwa huyo alitoroka,” alisema Kamanda Matei.
Katika tukio lingine watu wawili walikamatwa kwa tuhuma za wizi wa ngombe 61 wenye thamani ya shilingi milioni 27,450 ,000 mali ya Keke Furaha (37) kwa kutumia silaha aina ya sime.
Alibainisha kuwa tukio hilo limetokea Oktoba Mosi mwaka huu majira ya saa 5 asubuhi huko Lulenge kata ya Ubena wilayani Bagamoyo ambapo watuhumiwa ni Sadala Lupoto (25) mkazi wa Kimamba Kilosa na Luseky Sogoyo (25) na juhudi za kuwatafuta ngombe wengine 39 zinaendelea.  
Katika tukio lingine watu wawili wanashikiliwa kwa tuhuma za kukutwa na silaha aina ya gobore bila ya kibali  huku wengine 11 walikamatwa kwenye matukio ya kukutwa na bangi gunia mbili na kete 250 pamoja na lizla zipatazo 100.
            
Mwisho.









Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei akionyesha moja ya silaha zilizokamatwa kwa watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi. 

Silaha mbalimbali ambazo jeshi la polisi mkoani Pwani limezikamata mara baada ya kufanya misako maeneo mbalimbali ya mkoa huo. 

 Redio na deki vilivyoibiwa na kukamatwa kwa watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi. 

  Bunduki, tv, simu na vifaa vingine ambavyo vilikamatwa na polisi baada ya kuibiwa kwa watu mbalimbali mkoani humo.

Silaha pamoja na kiasi kikubwa cha fedha ambazo ziliibiwa kwa mfanyabiashara Twaha Mbuta wa huko Mbwewe. 

Sehemu ya fedha, vocha na risasi zilizokamatwa na polisi baada ya kufanya masako wa kusaka majambambazi.

 Redio zilizoibiwa kwa watu mbalimbali mkoani Pwani baada ya polisi kufanya misako mkoani humo
Kamanda wa Polisi Mkoani Pwani Ulrich Matei akiongea na waandishi wa habari mjini Kibaha hawapo pichani

Sunday, October 19, 2014

GOMBO GAMBUSI




 Mtumishi wa Mungu wa kituo cha maombezi cha Gombo Gambusi kilichopo Kibamba kwa Waitara Mwalimu Allister Albano akiwa anahubiri kituoni hapo Jumapili hii. 

 Mtumishi wa Mungu Mwalimu Allister Albano kushoto akiwa na mkewe wakifanya maombi kwa waumini kituoni hapo Jumapili hii

 Mtumishi wa Mungu Mwalimu Allister Albano kushoto akimwombea mgonjwa wakati wa ibada iliyofanyika kituoni hapo Jumapili hii 

 Baadhi ya waumini wakiwa kwenye maombi kwenye ibaada iliyofanyika Jumapili hii 

 Baadhi ya waumini wakiwa wanafanyiwa maombi na mtumishi wa Mungu Mwalimu Allister Albano 

 Mmoja ya waumini akiwa ameanguka chini baada ya kufanyiwa maombi kwenye ibaada ya Jumapili iliyofanyika kituoni hapo 

 Waumini wa kituo hicho wakiwa wanamsikiliza Mwalimu Allister Albano wa kituo hicho hayupo pichani alipokuwa akihubiri Jumapili hii 

 Waumini wakiwa wanaomba wakati wa ibaada hiyo Jumapili hii.

WACHINA WAVUTIWA BAGAMOYO

Na John Gagarini, Bagamoyo
JIMBO la Jilin nchini China limekubali kuwekeza hapa nchini kwenye eneo la Uwekezaji la (EPZ) la Kamal lililopo Kijiji cha Kerege kwa Kiwete wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.
Uwekezaji huo utafanyika baada ya ujio wa baadhi ya viongozi wa Jimbo hilo kutembelea maeneo mbalimbali ya uwekezaji wilayani humo na kuonekana kuvutiwa na sehemu hiyo.
Akizungumza jana mara baada ya kutembelea maeneo kadhaa akiongozana na mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza na sekretarieti ya mkoa wa Pwani na kuvutiwa na eneo hilo la uwekezaji la EPZ, Naibu Gavana wa Jimbo hilo Zhoncheng Sui alisema ameridhika na eneo hilo.
Sui alisema kuwa kutokana na urafiki wa kihistoria uliyopo kati ya Tanzania na China toka enzi za viongozi wa mataifa hayo Mwalimu Julius Nyerere na Mao Tse Sung kumekuwa na ushirikiano ambao ni wa damu hivyo lazima udumishwe kwa ushirikiano wa kimaendeleo.
“Tumeona mambo mengi ambayo tunaweza kushirikiana ambapo moja ni pale kwenye eneo la uwekezaji ambapo tutakuja kuwekeza hapo kwani kuna miuondombinu mizuri ya barabara, maji na umeme pia waiteni na wenzetu waliopo hapa Tanzania ili nao waje wajionee na kuangalia namna wanavyoweka kuwekeza kwenye mkoa huu wa Pwani,” alisema Sui.
Awali akimkaribisha naibu gavana wa Jimbo hilo la Jilin mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza alisema kuwa mkoa wa Pwani una mambo mengi ambayo wawekezaji wanaweza kuwekeza ikiwa ni pamoja na kwenye kilimo, uvuvi, utalii na mifugo.
“Fursa zipo nyingi ndani ya mkoa wetu na hata miundombinu ya barabara, anga, bandari, uememe na reli viko vizuri kwa ajili ya kufanikisha uwekezaji ambao una hitaji uwepo wa mawasiliano mazuri,” alisema Mahiza.
Ujumbe huo ulikuwa na ziara ya siku moja wilayani Bagamoyo kutembelea  maeneo ya uwekezaji kwenye ujenzi wa soko la kimataifa la samaki, eneo itakapojengwa bandari na eneo la uwekezaji la Kamal.

Mwisho.
 Mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza katikati mwenye kilemba akiwa na ugeni toka nchini China wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa wilaya ya Bagamoyo mara baada ya kumaliza mkutano wa pamoja uliofanyika kwenye hoteli ya Oceanic bay Hotel $ Resort  

 Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza kulia akiteta jambo na kiongozi wa ujumbe  kutoka Jimbo la Jilin nchini China Zhongcheng Sui wali[potembelea wilaya Bagamoyo kuangalia maeneo ya uwekezaji 



 Mkuu wa mkoa katikati na ugeni kutoka nchini China wakiangalia bomba ambalo limetoboka na maji kumwagika, kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Ahmed Kipozi

Monday, October 13, 2014

WAIMBAJI NA KWAYA ZA INJILI ZIJIUNGE NA BASATA

Na John Gagarini, Kibaha

KWAYA na Waimbaji wa nyimbo za Injili nchini wameshauriwa kujisajili Baraza la Sanaa ili watambulike kisheria kwa lengo la kuepuka kudhulumiwa haki za kazi zao.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha mwishoni mwa wiki na Naibu Waziri wa Sheria na Katiba Angella Kairuki wakati alipokuwa mgeni rasmi katika hafla ya kuchangia fedha za kununulia vifaa vya mawasiliano na kurekodi albamu ya video ya kwaya ya kanisa la Sabato la Maili Moja Kibaha mkoani Pwani.

Waziri Kairuki alisema kuwa baadhi ya kwenye makanisa ya na waimbaji mbalimbali hawajaona umuhimu wa kujisajili ili ziweze kutambulika na kunufaika kama zilivyo kazi nyingine za sanaa.

“Kwaya na waimbaji wa nyimbo za injili nazo zinawajibu wa kujisajili katika baraza hilo ili ziweze kupata haki zao pamoja fursa mbalimbali pia kukabiliana na baadhi ya watu wanaotumia kazi zao kujinufaisha binafsi huku walengwa wakiwa hawaambulii kitu hivyo sio vyema kukaa bila kujisajili rasmi,” alisema Waziri Kairuki.

Alisema ameona ni vyema akawahimiza kwani  jambo hilo lina manufaa kwa waimbaji na kwaya za makanisa ili waweze kupiga hatua kama ilivyo kwa baadhi ya wasanii wengine wa nyimbo za injili ambao tayari wamepiga hatua.

Alibainisha kuwa muziki unachangia amani,upendo na mshikamano hivyo wajitahidi pia kuimba nyimbo za kuiombea nchi yetu kwa masuala hayo muhimu pamoja na kumtukuza mungu.

“Nawaomba wanakwaya wa nyimbo na waimbaji wa nyimbo za injili kutengeneza albamu za video zenye maadili kwa michezo na mazingira yake pasipo kwenda kinyume na maadili ya kidini na kugeuza injili kuwa biashara, kwani zipo baadhi ya kanda za wasanii wengine ambazo hazionyeshi maadili mazuri,” alisema Waziri Kairuki.

Waziri Kairuki alisema serikali ipo pamoja na wasanii wa aina zote na inatambua kazi za sanaa ,tasnia ya wasanii na ndio maana katika katiba inayopendekezwa walihakikisha wanatambua kazi za wasanii, katika hafla hiyo kulipatikana zaidi ya sh m 22 ambapo ahadi zilizotolewa ni zaidi ya Mil 19.

Mwisho



WLAC YAPONGEZWA KUSAIDIA WANANCHI MASUALA YA SHERIA BURE

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
MKUU wa wilaya ya Kibaha mkoani Pwani Halima Kihemba amekipongeza kituo cha Msaada wa Kisheria  kwa Wanawake (WLAC) kwa kujitolea kutoa huduma za kisheria bure kwa wananchi wasio na uwezo wa kumudu gharama za kuwalipa wanasheria.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati akifunga mafunzo ya wasaidizi wa Kisheria wilayani humo ya siku 25 yaliyoandaliwa na Kituo cha Msaada wa Kisheria kwa Wanawake (WLAC).
Kihemba alisema kuwa kituo hicho kimeonyesha umuhimu wa kutoa msaada wa kisheria ni muhimu kwa watu hususani wanawake na watoto ambao wamekuwa wakipoteza haki zao kutokana na baadhi ya watu kutumia unyonge wao wakutokuwa na sauti ndani ya jamii kuwadhulumu haki zao.
“Huduma ya kisehria ni muhimu ndani ya jamii lakini watu wengi wamekuwa wakishindwa kumudu gharama hizo hivyo kushindwa kupata haki zao hivyo mashirika kama haya ni ya kuigwa,” alisema Kihemba.
Aidha alisema kuwa makundi hayo mawili ndiyo yamekuwa yakidhulumiwa haki zao kwa kiasi kikubwa hivyo mashirika kama WLAC yanayojitolea lazima yaungwe mkono na wadau mbalimbali ikiwemo serikali.
Awali akimkaribisha mkuu wa wilaya mkuu wa idara ya Mafunzo ya WLAC Magdalena Mlolere alisema kuwa lengo la kituo hicho ni kuhakikisha kuwa watu wanapata haki zao ambazo ni za msingi na ziko kikatiba.
Mlolere alisema kuwa lengo la kutoa mafunzo hayo kwa wasaidizi wa kiseheria wa vituo vya KPC na KPP ni ili waweze kusaidia wananchi kutatua migogoro inayojitokeza kabla ya kufika kwenye vyombo vya kisheria ikiwemo mahakama na polisi.
“Mafunzo hayo pia yatasaidia kupunguza kesi zinazopelekwa mahakamani ambazo nyingine zimekuwa zikitumia muda mrefu kuamuliwa na kuwafanya wahusika kutumia muda mwingi kwenda mahakamani huku wakishindwa kufanya shughuli zao za maendeleo,” alisema Mlolere.
Akisoma hotuba mbele ya mgeni rasmi moja ya wahitimu wa mafunzo hayo kwa niaba ya wahitimu John Gagarini alisema kuwa changamoto zinavyovikabli vituo hivyo ni baadhi ya wanajamii kutokuwa wawazi katika kuyapeleka mashauri hayo kwenye vituo hivyo pia ni ukosefu wa usafiri wa kuweza kufika kwenye maeneo hasa yale ya vijijini, jumla ya wahitimu 32 walihitimu mafunzo hayo na kukabidhiwa vyeti na mkuu huyo wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba.
Mwisho.
  


WAZIRI KAIRUKI ALITAKA KANISA KUOMBEA AMANI YA NCHI


Na John Gagarini, Kibaha

NAIBU Waziri wa Sheria na Katiba Angella Kairuki amewataka waumini wa Kanisa la Sabato Maili Moja Kibaha mkoani Pwani na wananchi kuendelea kuiombea nchi isiingie kwenye machafuko .

Waziri Kairuki aliyasema hayo mjini Kibaha katika kanisa hilo alipokuwa mgeni rasmi kwenye hafla ya kuchangia fedha za kununulia vifaa vya mawasiliano na kurekodia vya kwaya ya kanisa hilo na kusema kuwa wasikubali kutumiwa na baadhi ya watu kwa mambo ambayo ni kinyume na sheria za nchi.

Alisema nchi imekuwa na amani kwa miaka mingi sasa ikiwa ni mfano wa kuigwa na nchi nyingine hivyo haina budi kila mmoja akasali kuliombea taifa ambalo pia likielekea kwenye chaguzi mbalimbali.

“Msiwakubali watu ambao wamekuwa wakitumia wananchi ili kuvuruga amani ya nchi na wamekuwa wakitaka kuungwa mkono lakini wanaokuja kupata matatizo ni wananchi na siyo wao hivyo msikubali kufuata mkumbo,” alisema Waziri Kairuki.
Aidha Waziri Kairuki alisema hakuna haja ya kuendelezwa kwa mijadala ya katiba inayopendekezwa ama kuibua hoja zisizo na tija kwa maslahi ya taifa kwani muda wake umekamilika na hatua inayosubiriwa ni tamko kutoka kwa Mh Rais litakaloeleza wakati wa kupiga kura ya maoni kwa wananchi.

Kwa upande wake Mchungaji wa Kanisa la Sabato Maili Moja Eliasi Timasi alimshukuru Waziri Kairuki kwa nasaha zake na kusema wataendelea kuhimiza amani kwa kufanya mawasiliano ya karibu na serikali pamoja na kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili waumini wa kanisa hilo.

Katika shughuli hiyo ya kuchangia vifaa vya mawasiliano ya kanisa na kurekodia  kwaya kulipatikana zaidi ya sh m 22 ambapo ahadi zilizotolewa ni zaidi ya m 19.

Mwisho.