Monday, October 13, 2014

WAZIRI KAIRUKI ALITAKA KANISA KUOMBEA AMANI YA NCHI


Na John Gagarini, Kibaha

NAIBU Waziri wa Sheria na Katiba Angella Kairuki amewataka waumini wa Kanisa la Sabato Maili Moja Kibaha mkoani Pwani na wananchi kuendelea kuiombea nchi isiingie kwenye machafuko .

Waziri Kairuki aliyasema hayo mjini Kibaha katika kanisa hilo alipokuwa mgeni rasmi kwenye hafla ya kuchangia fedha za kununulia vifaa vya mawasiliano na kurekodia vya kwaya ya kanisa hilo na kusema kuwa wasikubali kutumiwa na baadhi ya watu kwa mambo ambayo ni kinyume na sheria za nchi.

Alisema nchi imekuwa na amani kwa miaka mingi sasa ikiwa ni mfano wa kuigwa na nchi nyingine hivyo haina budi kila mmoja akasali kuliombea taifa ambalo pia likielekea kwenye chaguzi mbalimbali.

“Msiwakubali watu ambao wamekuwa wakitumia wananchi ili kuvuruga amani ya nchi na wamekuwa wakitaka kuungwa mkono lakini wanaokuja kupata matatizo ni wananchi na siyo wao hivyo msikubali kufuata mkumbo,” alisema Waziri Kairuki.
Aidha Waziri Kairuki alisema hakuna haja ya kuendelezwa kwa mijadala ya katiba inayopendekezwa ama kuibua hoja zisizo na tija kwa maslahi ya taifa kwani muda wake umekamilika na hatua inayosubiriwa ni tamko kutoka kwa Mh Rais litakaloeleza wakati wa kupiga kura ya maoni kwa wananchi.

Kwa upande wake Mchungaji wa Kanisa la Sabato Maili Moja Eliasi Timasi alimshukuru Waziri Kairuki kwa nasaha zake na kusema wataendelea kuhimiza amani kwa kufanya mawasiliano ya karibu na serikali pamoja na kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili waumini wa kanisa hilo.

Katika shughuli hiyo ya kuchangia vifaa vya mawasiliano ya kanisa na kurekodia  kwaya kulipatikana zaidi ya sh m 22 ambapo ahadi zilizotolewa ni zaidi ya m 19.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment