Thursday, October 2, 2014

WANAFUNZI WAASWA KUHUSU TEKNOLOJIA

Na John Gagarini, Kibaha
WAZAZI wilayani Kibaha mkoani Pwani wametakiwa kuwalinda watoto wao waepukane na matumizi mabaya ya Teknolojia ya mawasiliano ili wasifuate tamaduni mbaya za nchi za Magharibi ambazo zimewaharibu vijana Tanzania.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha,  Jenifa Omollo wakati wa mahafali ya tisa ya darasa la saba ya shule ya awali na Msingi ya Kibaha Independent (KIPS).
Omollo alisema kuwa teknolojia ya mawasiliano ni nzuri endapo inatumiwa vizuri lakini ina athari endapo itatumiwa vibaya hasa kwa vijana kuiga tamaduni za nje zinazohamasisha vitendo viovu.
“Tuko kwenye utandawazi ambao unatumia teknolojia ya mawasiliano na kuifanya dunia kuwa Kijiji na kumekuwa na muingiliano mkubwa wa tamaduni ambazo nyingine ni mbaya zinazokinzana na maadili ya kitanzania ikiwa ni pamoja na mavazi, ngono, matumizi ya dawa za kulevya na matumizi mabaya ya mitandao ya kuangalia picha za ngono,” alisema Omollo.
Alisema kuwa kundi la vijana limeathiriwa kwa kiasi kikubwa na tamaduni hizo mbaya ambapo vijana hao wanafikiri ndiyo kwenda na wakati kumbe wanajiharibia maisha yao ya baadaye.
“Kwa sasa kuna matumizi mabaya ya teknolojia kupitia njia za simu, kompyuta na televisheni hivyo lazima wazazi wawaelekeze matumizi sahihi ya vifaa hivyo ambavyo endapo vitatumiwa vizuri vinaweza kuwa na manufaa mazuri kwa watumiaji,” alisema Omollo.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi mkurugenzi wa shule hiyo Said Mfinanga alisema kuwa shule yao moja ya vitu inavyozingatia ni maadili mazuri ya Kitanzania ili wanafunzi wanapotoka hapo wawe na tabia njema.
Mfinanga alisema kuwa licha ya shule kufundisha masomo ya mawasiliano ya Kompyuta lakini wanazingatia maadili ili kuepuka na matumizi mabaya ya Teknolojia na kuzingatia kutoa elimu bora.
Shule hiyo ni ya kutwa na bweni ilianzishwa mwaka 2002 na ina jumla ya wanafunzi 480 na ni miongoni mwa shule zinazofanya vizuri kwenye wilaya hiyo pamoja na mkoa ambapo mwaka huu jumla ya wahitimu 39 walipewa vyeti vya kuhitimu darasa la saba.

Mwisho.       

No comments:

Post a Comment