Thursday, October 2, 2014

WATOTO WANUNUA SIMU KUWASILIANA NA WAPENZI WAO

Na John Gagarini, Kibaha
IMEBAINIKA kuwa baadhi ya watoto wanaojishughulisha na biashara ndogondogo wilayani Kibaha mkoani Pwani wamejiingiza kwenye mahusiano ya kimapenzi ambapo fedha wanazopata wananunulia simu za mkononi ili kuwasiliana na wapenzi wao.
Watoto hao licha ya kuwa na umri mdogo lakini tayari wanajiingiza kwenye masuala ya mapenzi jambo ambalo ni hatari na linalosababisha kuingia kwenye ngono wakiwa na umri mdogo hivyo kuongeza vitendo vya ubakajiani ndani ya jamii.
Akizungumza mjini Kibaha wakati wa mafunzo ya kupinga vitendo vya ukatili kwa watoto kwa timu za kuzuia vitendo hivyo ndani ya jamii kwenye kata ya Kibaha wilayani humo mwenyekiti wa mafunzo hayo Alkhas Katopola alisema kuwa baadhi ya watoto wanamiliki simu ambazo wanazitumia kwa ajili ya mawasiliano na wapenzi.
“Inashangaza sana kuona watoto wadogo wanamiliki simu za mkononi na kikubwa wanachokifanya na hizo simu ni masuala ya mapenzi hivyo kutokana na umri wao kuwa mdogo ni kama vile wanabakwa kwa sasabu wengi wana mahusiano ya kimapenzi na watu wazima,” alisema Katopolo.
Katopola alisema kuwa wengi wa watoto hao ni wale ambao hawakupata nafasi ya kwenda au kuacha shule kutokana na sababu mbalimbali za kimaisha au wenyewe kukataa kuendelea na masomo.
“Pia baadhi ya watoto hawa wanategemewa na familia zao kwa ajili ya mahitaji ya nyumbani hivyo wazazi au walezi wanashindwa kuwadhibiti mara wafanyapo vitendo visivyofaa ikiwa ni pamoja na kujihusisha kwenye masuala ya mahusiano ya kimapenzi,” alisema Katopola.
Kwa upande wake mratibu wa shirika lisilo la kiserikali la (KICODET) la Kibaha lililoandaa mafunzo hayo Dk Rose Mkonyi alisema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kukabiliana na vitendo vya ukatili kwa watoto kwenye Halmashauri ya Mji wa Kibaha.
“Vitendo vya ukatili kwa watoto ni vingi na ndiyo sababu ya kuandaa mafunzo hayo ili jamii iweze kujua namna ya kutoa taarifa kwenye vyombo vya sheria na si kuvifumbia macho kama baadhi ya familia zinavyofanya kwani baadhi ya wanaofanya vitendo vya ukatili ni ndugu hivyo kuhofia mahusiano kuvunjika,” alisema Dk Mkonyi.
Dk Mkonyi alisema kuwa mafunzo hayo ambayo yatatumika kuunda timu za ufuatiliaji wa matukio mbalimbali ya ukatili kwa watoto yamewajengea uwezo wa kuweza kuwa na mtandao baina yao na vyombo vya sheria kama vile viongozi wa mitaa, waalimu, jeshi la polisi, mahakimu na wadau wengine wanaohusika kukabiliana na vitendo hivyo.
Kwa upande wake mwezeshaji wa mafunzo hayo Faustina Kayombo ambaye ni ofisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha alisema kuwa tatizo kubwa ni usiri unaofanywa na umaskini imekuwa ni vyanzo chanzo vikuu vya kuendela kwa vitendo hivyo.
Mradi huo ni wa miaka miwili ambapo mafunzo hayo yamefadhiliwa na Plan International, UNICEF, Save the Children na Jumuiya ya Ulaya na serikali kwa kushirikiana na shirika hilo la KICODET.
Mwisho.

  


No comments:

Post a Comment