Thursday, October 2, 2014

WANAFUNZI KIDATO CHA SITA WAZAWADIWA FEDHA


Na John Gagarini, Kibaha
SHIRIKA lisilo la Kiserikali la Piniel Medical Mission la Jijini Dar es Salaam limewapa fedha wanafunzi wanne wa shule ya sekondari Kilangalanga ambao wamefaulu daraja la kwanza kwenye mtihani wa Taifa wa kidato cha sita.
Waliozawadiwa fedha hizo ni pamoja na Peter Didas, Ally Makutubu, Obote Juma na Venance Peter ambao kila mmoja alikabidhiwa kiasi cha shilingi 100,000 kila mmoja.
Akiwakabidhi fedha hizo mgeni rasmi kwenye makabidhiano hayo ambayo yalifanyika shuleni hapo Mlandizi Kibaha mwakilishi wa ofisa elimu wilaya ya Kibaha Blandina Mwenura aliwapongeza wanafunzi hao na kuwataka wanafunzi watakaofanya mitihani hiyo kutoogopa masomo ya sayansi.
Mwenura alisema kuwa wanafunzi wengi wamekuwa wakifanya vibaya kutokana na kuyaogopa masomo hayo ambayo ndiyo masomo muhimu katika kupata wataalamu mbalimbali.
“Nalipongeza shirika hili kwa kujitolea kuhamasisha masomo haya ambayo wanafunzi wamekuwa wakiyakimbia na kukimbilia masomo ya Sanaa wakidhani kuwa ndiyo rahisi,” alisema Mwenura.
Aidha aliwataka wadau wengine kujitokeza zaidi kuwatia moyo wanafunzi wanaosoma masomo hayo ili kujenga nchi yenye wataalamu wenye uwezo mzuri kwani watafanya kazi kwa mapenzi kwa kile walichokisomea.
Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa shirika hilo Jaqline Ngoma alisema kuwa walitoa ahadi kwa wanafunzi wa shule hiyo kuwa endapo mwanafunzi wa kidato cha sita atapata daraja la kwanza watampatia kiasi hicho cha fedha na huo ndiyo utekelezaji wa ahadi hiyo.
“Lengo letu ni kuwatia moyo wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi wawe na ujasiri na kuondoa woga kwani wataalamu kwa sasa wanapungua mfano wataalamu wa afya hivyo lazima tutumie njia ya kuwahamasisha ili wengi wajiunge na masomo hayo,” alisema Ngoma.
Shule hiyo ya serikali ni ya kutwa ni ya wavulana na wasichana na bweni kwa wanafunzi wa kidato cha tano na sita wavulana wanaochukua masomo ya mchepuo wa Sayansi.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment