Monday, August 8, 2016

WATU ZAIDI 20 WANUSURIKA KUUNGUA MOTO

Na John Gagarini, Kibaha

FAMILIA nane zenye watu zaidi ya 20 kwenye mtaa wa Mharakani kata ya Picha ya Ndege wilayani Kibaha mkoani Pwani zimenusurika kufa baada ya moto kutokea wakati wamelala.

Wakizungumza na mwandishi habari hizi wahanga wa tukio hilo la moto huo ambao ulitokea Agosti 7 usiku kuamkia Agosti 8 majira ya saa 6;30 usiku walisema kuwa watu waliokuwa jirani na nyumba yao ndiyo waliowafahamisha juu ya moto huo ambao unasadikiwa ulianzia kwenye moja ya maduka yaliyo kwenye nyumba hiyo.

Emanuel Mhina alisema kuwa wao walikuwa wamelala na ilipofika majira ya saa saba kasoro waliamshwa na watu na walipoamka walikutana na moto mkubwa ambao hawakujua ulianza saa ngapi ndipo walipoanza kujiokoa.

“Tunamshukuru mungu tumenusurika licha ya mali zetu zote kuteketea kwa moto ambao ulianzia kwenye moja ya maduka ambayo yameungana na nyumba hii ambayo tulikuwa tunaishi,” alisema Mhina.

Naye Said Juma alisema kuwa moto huo umewapa hasara kubwa kwani amepoteza vitu karibu vyote na kufanikiwa kuokoa vichache hali ambayo inamfanya aanze upya maisha.

Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa huo Yahaya Abdala alisema kuwa wananchi, Zimamoto pamoja Jeshi la polisi walifanikisha kuzimwa moto huo ambao ulisababisha vitu vote kuteketea lakini hakuna mtu aliyedhuriwa na moto huo zaidi.

Naye diwani wa kata ya Picha ya Ndege Robert Machumbe alisema kuwa wahanga hao hawakuweza kuokoa kitu kwani vitu vyote viliteketea kwa moto huo uliokuwa mkali.

Machumbe alisema kuwa baada ya tukio hilo walichangisha kwa majirani na kupata kiasi cha shilingi 80,000 ambazo ziligawanywa kwa wahanaga hao angalau wapate fedha kwa ajili ya chakula na wahanga hao wamehamia kwa ndugu jamaa na marafiki zao wakiangalia namna ya kutafuta nyumba nyingine.

Katika hatua nyingine mtoto mwenye umri kati ya miaka minne na nusu amenusurika kufa baada ya mama yake kumwacha kwenye nyumba huku akiwa amemfungia ndani na yeye kwenda kusikojulikana ambapo kati ya majirani waliounguliwa nyumba ambaye ni mwanajeshi wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) alijitosa na kumwokoa mtoto huyo.

Mwisho.   

No comments:

Post a Comment