Tuesday, August 30, 2016

MADARASA YAUNGUA MOTO

Na John Gagarini, Kibaha

MADARASA matatu na ofisi ya Mwalimu Mkuu shule ya Msingi Kongowe wilayani Kibaha mkoani Pwani zimeungua na moto ambao ulitokea juzi usiku na kusababisha hasara kubwa.

Akizungumza na Patapata mwenyekiti wa mtaa wa Kongowe Maimuna Jamhuri alisema kuwa moto huo ulitokea Agosti 28 majira ya saa nne usiku ambapo chanzo chake bado hakijafahamika mara moja.

Jamhuri alisema kuwa moto huo ulianzia kwenye ofisi hiyo ambayo ni ya mwalimu mkuu na kuenea kwenye madarasa pamoja na chumba cha kuhifadhia vitabu ambavyo navyo vimeteketea kwa moto huo ambao ulikuwa mkali.

“Moto huo ulizimwa na wananchi ambao walijitokeza kwa wingi ambapo gari la zimamoto lilifika kwa kuchelewa kutokana na kuwa kwenye harakati za kuzima moto sehemu nyingine”, alisema Jamhuri.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Kongowe Iddi Kanyalu alisema kuwa baada ya kutokea moto huo viongozi kadhaa walifika akiwemo mkurugenzi, Mwenyekiti na Injinia wa Halmashauri kwa ajili ya kuangalia athari za moto huo.

Kanyalu alisema kuwa kutokana na makisio ya harakaharaka zinahitajika zaidi ya milioni 50 kwa ajili ya kujenga upya madarasa hayo na ofisi kwani madarasa hayo yameharibika sana na hayafai kwa matumizi wala kufanyiwa ukarabati.

Alisema kuwa kutokana na hali hiyo leo kamati ya maenedeleo ya kata ina kaa kuangalia namna ya kukabiliana na tatizo hilo ambalo limewakumba wanafunzi 200 waliokuwa wanatumia madarasa hayo.

Naye mtendaji wa kata hiyo ya Kongowe Said Kayangu alisema kuwa mwalimu mkuu wa shule hiyo Beatus Lingumbuka alitapa athari kidogo kichwani na mikononi kwani alikuwa kwenye harakati za kujaribu kuokoa baadhi ya vitu wenye ofisi yake.

Kayangu alisema kuwa kutokana na jitihada za wananchi wameweza kuokoa madawati kwenye madarasa hayo ambayo yalikuwa hatarini kuungua lakini hata hivyo waliweza kuyatoa na hakuna dawati hata moja lililoungua

Mwisho.


No comments:

Post a Comment