Tuesday, August 30, 2016

UVUNJAJI SHERIA WASABABISHA MIGOGORO YA ARDHI

Na John Gagarini, Rufiji

IMEELEZWA kuwa kuwepo kwa migogoro ya ya wakulima na wafugaji  katika Halmashauri ya Rufiji mkoani Pwani kunatokana na  baadhi ya wafugaji kuvunja sheria na taratibu zilizowekwa na   kwenda kulisha mifugo yao katika maeneo yaliyotengwa maalumu kwa ajili ya shughuli mbali mbali za kilimo.

Hayo yalisemwa na Mbunge  wa Jimbo la Rufiji Mkoani humo Mohamed Mchengerwa alipokuwa akizungumza na viongozi wa Halmashauri Mpya ya Rufiji ambapo ameahidi kulivalia njuga suala la migogoro ya ardhi inayotokana na jamii ya wafugaji na wakulima ambao wamekuwa wakigombania maeneo ya mashamba na kusababisha kutokea kwa mapigano ambayo wakati mwingine yanapelekea uvunjifu wa amani.

Mchengerwa alisema kuwa hawezi kuwavumilia wale wote ambao wataonekana wanakwenda kinyume cha sheria za nchi, na kuhakikisha kila mfugaji na mkulima anatengewa maeneo yao rasmi kwa ajili ya kufanyia shughuli zake ili kuepukana na migogoro na  mapigano ambayo yamekuwa yakijitokeza kutokana na kugombania ardhi.

“Nitaweka mikakati kabambe ambayo itaweza kuwawasaidia wananchi wakiwemo wafugaji na wakulima kwa kushirikina na viongozi wa halmashauri katika kuwatenge maeneo yao maalumu ambayo yataweza kusaidia kuepukana na migogoro hiyo ya ardhi,” alisema Mchengerwa.

Alisema kuwa anatambua kuwepo kwa changamoto kubwa na  migogoro kati ya wakulima na wafugaji, lakini dhamira yake kubwa anataka kuona wanachi wake wa jimbo la rufiji wanakaa kwa amani bila ya kuwepo kwa mapigano yoyote na kuhakikisha kwamba sula la amani na utulivu linakuwepo.

“Natambua wananchi wengi wa Jimbo la Rufiji wanategemea sana shughuli za kilimo hivyo kwa sasa wameshaweka utaratibu wa kutenga maeneo ya wafugaji ili wasiweze kuingia katika mashamba ya wakulima na kupelekea vurugu za mara kwa mara kitu amabcho sio kizuri na kinarudisha nyuma maendeleo,” alisema Mchengerwa.

Naye Mwenyekiti mpya wa Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji Saidina Malenda mara baada ya kushinda katika uchaguzi huo  alisema  atahakikisha anasharikina bega kwa bega na viongozi wenzake kwa lengo la kuweza kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo kwa wananchi wa Rufiji.

Malenda alisema kuwa anawashukuru madiwani wenzake kwa kuweza kumchagua kuwaongoza na kubainisha kwamba atafanya kazi bidii zote na kwa kushirikina katika mambo mbali mbali ya kimaendeleo  bila ya kuwa na ubaguzi wa aina yoyote wa itikadi ya vyama  ili kuweza  kuwatumikia wananchi katika huduma mbali mbali wanazozihitaji.

Katika uchaguzi huo wa halmashauri mpya ya Wilaya ya Rufiji,uliofanyika utete nafasi ya Mwenyekiti ilikwenda kwa Saidani Malenda ambaye alipata kura 11 kati ya kura 19 zilizopigwa, ambapo nafasi ya Makamu mwenyekiti ilikwenda kwa Hawa Mtopa  ambaye aliyepata kura 10 katika ya kura 19 zilizopigwa.
     

MWISHO

No comments:

Post a Comment