Tuesday, August 30, 2016

ATISHIA KUWABAKA WANAFUNZI


Na John Gagarini, Chalinze

MWENYEKITI wa Halmashauri ya mji wa Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Said Zikatimu ameutaka uongozi wa Kitongoji Cha Msanga kata ya Talawanda uhakikisha inamkamata mtu ambaye anatishia kuwabaka wanafunzi wa shule ya Msingi Msanga.

Akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Talawanda wakati wa ziara yake kuangalia shughuli za maendeleo kwenye kata ya Talawanda alisema kuwa mtu huyo hapaswi kuachwa kwani anahatarisha afya za wanafunzi hao.

Zikatimu alisema kuwa baadhi ya wanafunzi wakike wa shule hiyo tayari wameshatoa taarifa dhidi ya mtu huyo ambaye huwa anawakimbiza kwa nia ya kuwafanyia kitendo hicho na endapo hatakamatwa anaweza kutekeleza azma yake hiyo mbaya.

“Mtu huyo inasemekena yuko Kijijini hapa amekuwa akificha sura yake ili asifahamike amekuwa akijificha kwenye vichaka na kuwakimbiza wanafunzi kwa nia ya kutaka kuwabaka hivyo lazima viongozi muweke mtego ili mumkamate mtu huyo ambaye ni hatari,” alisema Zikatimu.

Alisema kuwa serikali haiwezi kukaa kimya kwa mtu wa namna hiyo ambaye ni hatari kwa wanafunzi na kuwafanya watoto wa kike wasisome kwa amani hivyo lazima hatua za haraka zichukuliwe ili kumdhibiti mapema.

“Lazima mfanye mpango wa kumkamata mtu huyo pia mnaweza kupiga kura ili kumbainisha mtu huyo ambaye baadhi ya watu wanamfahamu na wengine hawamfahamu ambapo kwa kutumia kura anaweza kufahamika kwa urahisi,” alisema Zikatimu.

Aidha alisema kuwa kamati za ulinzi na usalama ya Kijiji na Kitongoji zinapaswa kulishughulikia suala hilo na wananchi kutolifumbia macho kwani mtu huyo anaweza kufanya kweli endapo hatua hazitachukuliwa mapema.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment