Tuesday, August 30, 2016

PANGANI WALILIA ZAHANATI


Na John Gagarini, Kibaha

KATA ya Pangani wilayani Kibaha inatarajia kubadilisha ofisi za Mtaa wa Kidimu kuwa Zahanati ili kukabiliana na changamoto ya mtaa huo kutokuwa na zahanati hivyo kufanya huduma za matibabu kupatikana kwa ugumu.

Akizungumza na waandishi wa habari diwani wa kata hiyo Agustino Mdachi alisema kuwa gharama za kufuata matibabu kwa wakazi wa mtaa huo ni kubwa na kuwafanya wagonjwa kuwahatarini pale wanapokuwa wamepatwa au kuzidiwa na ugonjwa.

Mdachi alisema kuwa tegemeo kubwa ni hospitali ya wilaya ya Kibaha ya Mkoani ambayo iko umbali wa kilometa 18 na ile ya jirani ya Mpiji Magohe ambayo iko kata ya Mbezi wilaya ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam ambapo usafiri wa pikipiki ni shilingi 5,000.

“Mgonjwa anapotaka kwenda Mkoani humbidi kuwa na shilingi 50,000 hasa nyakati za usiku na mchana ni 40,000 au 30,000 gharama hizi kwa ajili ya kwenda kupata matibabu ni kubwa sana na kwa mwananchi wa kawaida kumudu ni ngumu sana,” alisema Mdachi.

Alisema kuwa katika kukabiliana na changamoto hiyo wameamua kuibadili ofisi hiyo na kuwa zahanati ya mtaa ambapo wananchi watapa huduma karibu.

“Kwa sasa tuko kwenye mchakato kwa kuwaomba Halmashauri ya Mji kuturuhusu na kuleta wataalamu wa afya ili waangalie namna ya kulifanya jengo hilo kuwa zahanati na tunaamini ombi letu litakubaliwa,” alisema Mdachi.

Aidha alisema kuwa kutokana na ukubwa wa jengo hilo la serikali ya mtaa kuwa vyumba vingi wanaamini kuwa litafaa kwa ajili ya kuanzia huduma za kiafya wakati wanafanya mipango ya kujenga sehemu nyingine.

“Kwa kuwa ya kata ina ofisi nyingi tunaweza kutoa chuma kimoja kwa ajili ya ofisi ya mtaa ili kufanikisha zoezi hilo ambalo litawafanya wananchi wa mtaa na kata hiyo kupata huduma za afya karibu,” alisema Mdachi.

Aliwataka wananchi kuunga mkono jitihada za serikali kwa kujitolea katika masuala mbalimbali ya maenedeleo ikiwa ni pamoja na kufanikisha zoezi hilo la ujenzi wa zahanati hiyo.


Mwisho.

No comments:

Post a Comment