Tuesday, August 30, 2016

KAMPUNI YA UUNGANISHAJI MAGARI YAZIMAMOTO MBIONI KUANZA USZALISHAJI

Na John Gagarini, Kibaha

KAMPUNI ya Equator Suma Jkt inatarajia kuanza kuunganisha magari ya zimamoto na matrekata mwishoni mwa mwaka huu ikiwa ni moja ya njia ya kukabiliana na majanga ya moto pamoja na kuinua kilimo cha Tanzania ambacho ni uti wa mgongo wa uchumi.

Akizungumza na waandishi wa habari ambao walitembelea kiwanda hicho kilichopo Ruvu Mlandizi wilayani Kibaha mkurugenzi Robert Mangazeni alisema kuwa kwa sasa kiwanda hicho kiko kwenye hatua za mwishi ikiwa ni pamoja na uunganishaji wa mitambo na mashine.

Mangazeni alisema kuwa teknolojia ya uunganishaji wa magari ya zimamoto ambapo watatumia magari ya kawaida kwa kuyabadilisha na kuwa ya zimamoto wameitoa nchi ya Urusi kutoka kwenye makampuni ya St Auto na Ural huku ile ya matekta wakiitoa kwenye kampuni za Escort kutoka nchini India na Farmtrac kutoka nchini Poland.

“Tukizungumzia kuhusu uunganishaji wa magari ya zimamoto ni teknolojia ambayo imeboreshwa na kuwa ya kisasa zaidi ambapo tutakuwa na uwezo wa kuunganisha magari ya aina mbalimbali kutegemeana na mteja anavyotaka ambayo yatakuwa na ujazo wa aina tofauti tofauti kuanzia magari makubwa hadi madogo siyo lazima yawe makubwa kama tulivyozoea hivyo hata majanga haya ambayo yamezikumba shule sasa taasisi zitaweza kudhibiti moto,” alisema Mangazeni.

Alisema kuwa ujazo huo utaanzia lita za maji 300 hadi 10,000 kutegemea na ukubwa hivyo kulinagana na miuondombinu ya barabara za mitaani wataunganisha hata magari madogo ili yaweze kufika kwenye eneo lililopata maafa ya moto.

“Ikumbukwe Tanzania itakuwa nchi ya pili kuwa na teknolojia hii ya uunganishaji wa magari ya zimamoto baada ya Afrika Kusini ambapo kwa nchi za Maziwa Makuu itakuwa ni ya kwanza na itaweza kuokoa asilimia 30 ya gharama ya kununua gari jipya la zimamoto pia watakuwa na uwezo wa kuyatengeneza magari hayo badala ya kuagiza wataalamu toka nje ya nchi mara yanapoharibika,”alisema Mangazeni.

Aidha alisema kuwa kwa upande wa matrekta wataweza kuyaunganisha ambapo kwa miaka ijayo watakuwa na uwezo wa kutengeneza trekta ambalo litakuwa ni zao la Tanzania tofauti na ilivyo sasa kuagizwa toka nje ya nchi.

“Miaka ijayo tutatengenza trekta la kwetu ambapo kwa sasa vitakuwa vinakuja vifaa vyake na kuunganishiwa hapa na tatizo la matrekta kufa haraka litakwisha kwani mafundi wa matrekta watazalishwa hapa na yatadumu kwani wengi hawana utaalamu wautengenzaji bali wanatumia uzoefu tu,” alisema Mangazeni.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kibaha Asumter Mshama alisema kuwa ujenzi wa kiwanda hicho umekuja wakati mwafaka kwa upande wa janga la moto na kilimo bora.

Mshama alisema kuwa kiwanda hicho ambacho kitafanya shghuli hizo kwa pamoja itakuwa mwarobaini wa changamoto hizo ambazo ni kubwa na pia ni kutekeleza sera ya Rais John Magufuli ya kutaka Tanzania kuwa nchi ya viwanda ili baada ya miaka ijayo nchi kuwa na uchumi wa kati.

Ujenzi wa kiwanda hicho ulianza ulianza 2011 ambacho hadi kukamilika kwake kitakuwa na thamani ya shilingi bilioni tatu kitaajiri wafanyakazi 100 na kamapuni hiyo imeingia ubia na Suma Jkt na inaundwa na wanajeshi wastaafu.
 

Mwisho. 

No comments:

Post a Comment