Wednesday, December 31, 2014

WAZEE ZAIDI YA 300 WAPATIWA MATIBABU MAALUMU

Na John Gagarini, Kibaha
JUMLA ya Wazee zaidi ya 300 kati ya wazee 2,500 kwenye kata ya Kibaha katika halmashauri ya mji wa Kibaha mkoani Pwani wamepatiwa matibabu ya maradhi mbalimbali.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mkurugenzi wa Shirika lisilo la Kiserikali la Msamaria Mwema Huduma za Jamii (GSSST), Elisha Sibale alipozungumza na waandishi wa habari juu ya huduma walizotoa kwa wazee.
Sibale alisema kuwa wazee hao ambao wanahudumiwa na shirika lake ni wale wenye umri kuanzia miaka 60 walitibiwa magonjwa mbalimbali kama vile Kisukari, Macho, Wingi wa damu, Uoni hafifu na ugonjwa wa Ukimwi.
“Lengo la mradi huu ni kuwawezesha wazee kupata matibabu kwa wakati kwani wengi wao wamekuwa hawapati huduma hizo kutokana na jamii kutowathamini hivyo kujikuta wakiwa na changamoto za kuumwa maradhi mengi,” alisema Sibale.
Naye mtaalamu wa maabara kwenye zahanati ya Mwendapole Hans Amon alisema kuwa wazee hao wameanza kujiamini kwenda kupata matibabu ambapo awali walikuwa na woga kutokana na jamii kutowapeleka hospitali na kuwaacha.  
Kwa upande wake moja ya wazee walionufaika na mradi huo Hadija Mbwambo alisema kuwa wameweza kujua afya zao na kujitambua na kuona umuhimu wa kuwahi kupata matibabu.
 Mradi huo wa miaka miwili unatekelezwa kwenye mitaa ya Kwa Mfipa, Simbani, Mwendapole A na B kwa Kibaha Mjini na Kibaha Vijijini Mwanabwito na Kikongo na matibabu hayo yalifadhiliwa na shirika hilo kwa kushirikiana na Help Age International na Pfizer Pharmaceuticals kuanzia Oktoba Mosi siku ya wazee duniani hadi Desemba mwaka jana na litakuwa endelevu.

Mwisho.  

No comments:

Post a Comment