Tuesday, December 16, 2014

TATIZO LA MAJI CHALINZE KUWA HISTORIA NA KIBAHA YAENDELEA KUKIMBIZANA NA MAABARA

Na John Gagarini, Kibaha
CHANGAMOTO ya maji wilayani Bagamoyo mkoani Pwani huenda ikawa historia baada ya serikali ya India kutoa kiasi cha bilioni 800 kwa ajili ya mradi wa maji wa Wami Chalinze.
Akizungumza na waandishi wa habari mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa fedha hizo zitasaidia kukabiliana na tatizo hilo ambalo limekuwa likiwasumbua wananchi wa wilaya hiyo.
Ridhiwani alisema kuwa fedha hizo ambazo ni sehemu ya mkopo baada ya ziara ya Waziri Mkuu wa nchi ya India alipotembelea nchini hivi karibuni.
“Fedha hizi zitasaidia kwa kiasi kikubwa kukamilisha mradi huo ambao umekwama kwa baadhi ya maeneo kutokana na mkandarasi aliyepewa kazi hiyo kutotengeneza miundombinu kwa kiwango kinachotakiwa,” alisema Ridhiwani.
Alisema mbali ya kujenga miuondombinu ya kufika kwenye vijiji mbalimbali pia fedha hizo zitatumika kwa ajili ya kujenga mabwawa ya muda kwa ajili ya kuhifadhi maji na kuchujia maji.
“Wakati mwingine maji yamekuwa yakitoka machafu kutokana na maji kuingiwa na tope hasa pale mvua inaponyesha hivyo tunatarajia kuwe na matanki ambayo yatachuja maji kwani yaliyopo ni machache,” alisema Ridhiwani.
Aidha alisema pia kutajengwa vioski na matenki kwenye vitongoji na vijiji 20 kwani baadhi viko umbali mdogo  kwenye baadhi ya matenki lakini havipati maji.
Alibainisha kuwa Jimbo la Chalinze baada ya muda mfupi itaepukana na adha ya maji kwani watakuwa na uhakika wa kupata maji safi na salama kupitia mradi huo kama baadhi ya maeneo.
Na John Gagarini, Kibaha
WILAYA ya Kibaha mkoani Pwani imefikia asilimia 80 ya ujenzi wa maabara kwenye shule za sekondari na inatarajia kukamilisha ujenzi huo mwishoni mwa mwezi huu.
Kwa mujibu wa mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba alisema kuwa wilaya hiyo imeweza kujenga maabara 53 katika kipindi cha miezi miwili cha agizo la Rais Dk Jakaya Kikwete.
Kihemba alisema kuwa kulikuwa na changamoto kubwa ambazo zimechangia ujenzi huo kushindwa kukamilika kwa asilimia 100 ambapo kwa sasa zimebakia maabara 10.
“Changamoto kubwa ilikuwa ni wenyeviti wa mitaa na viji kujiuzulu kabla ya uchaguzi kwani wao ndiyo wahamasishaji wakuu wa kukusanya michango pia mwitikio wa wananchi kuchangia kuwa mdogo na suala la akaunti ya Tegeta Escrow kushusha uchangiaji kutokana na wapinzani kutumia sababu ya wananchi wasichangie,” alisema Kihemba.
Alisema kuwa wilaya yetu ina jumla ya shule 21 ambapo kila shule inatakiwa kujenga maabara 3 hivyo kufanya wilaya kuhitaji maabara 63 na thamani ya kila maabara ni shilingi milioni 60.
“Tunawashukuru wadau wetu mbalimbali wa maendeleo na wananchi ambao walitusaidia fedha kwa ajili ya kufanikisha ujenzi wa maabara hizi na tunaendelea kuwaomba watusaidie ili tuweze kukamilisha ujenzi huo kama tulivyopanga,” alisema Kihemba.
Mkuu huyo wa wilaya ya Kibaha alisema kuwa anamshukuru Rais kwa kuwapa msukumo wa ujenzi wa maabara kwani kwa kipindi kifupi maabara nyingi zimejengwa ambazo zitakuwa na manufaa makubwa kwa wanafunzi.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment