Monday, December 8, 2014

AFA KWA KUCHOMWA KISU NA WATU WASIOFAHAMIKA

Na John Gagarini, Kibaha
MTU mmoja aliyefahamika kwa jina la Juma Abdala (65) mkulima wa Kitongoji cha Kwa Mwaleni kijiji cha Mbwewe kata ya Mbwewe wilayani Bagamoyo mkoani Pwani amekufa kwa kuchomwa kwa visu na watu wasiofahamika.
Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo walisema kuwa mzee huyo aliitwa na vijana wawili waliofika nyumbani kwake na kumwita pembezoni mwa nyumba yake kisha kumshambulia na kumwua.
Akizungumza kwa njia ya simu na mwandishi wa habari hizi ofisa mtendaji wa kijiji cha Mbwewe Ramadhan Mwanaagonile alisema kuwa tukio hilo lilitokea Novemba 6 mwaka huu majira ya saa 1:30 usiku Kitongojini hapo.
Mwanaagonile alisema kuwa siku ya tukio vijana hao ambao hawafahamiki walifika nyumbani kwa marehemu na kumtaka waongee naye wakati huo marehemu alikwenda kwenye kibanda jirani kwa ajili ya kunywa kahawa.
“Watu hao walipomuulizia marehemu walijibiwa kuwa hayupo walitaka aitwe ili waongee naye ndipo alipoitwa na kumtaka wakazungumze pembeni na ndipo walipokwenda kwenye ua wa nyumba yake na kuanza kuongea,” alisema Mwanaagonile.
Alisema baada ya muda walisikia marehemu akipiga kelele kuomba msaada huku akisema kuwa anakufa na walipokwenda walikutwa kachomwa kisu kitovuni na kifuani na mkononi.
“Marehemu alijaribu kukimbia kwenda waliko watu lakini alishindwa na kuanguka na watu walipofika walimkuta akiwa anatokwa na damu nyingi ambazo zilisababisha kifo chake huku wale watu wakiwa hawaonekani kwani walikimbia kusikojulikana,” alisema Mwanaagonile.
Aidha alisema taarifa zilitolewa kituo cha Polisi cha Mbwewe ambao walifika na kuuchukua mwili wa marehemu na baadaye mwili ulichunguzwa na daktari kisha kukabidhiwa ndugu kwa ajili ya mazishi.
“Tulijaribu kuwatafuta vijana hao bila ya mafanikio na hatukukuta chochote pale palikotokea tukio watu hao hawakumchukulia kitu chochote kwnai alikuwa na simu na vitu vingine lakini waliviacha,” alisema Mwanaagonile.
Kwa upande wake kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alipoulizwa kuhusiana na tukio hilo alisema bado halijafikishwa ofisini kwake na kusema kuwa atafuatilia na kulitolea taarifa.
Mwisho.



No comments:

Post a Comment